Maswali Kutoka kwa Wasomaji
■ Tunaweza kuwasaidiaje wale walio katika kundi letu ambao mtu wa ukoo wao ametengwa na ushirika?
Ni vizuri wakati wazee na wengine wanapowafikiria kwa uchangamfu na upendo Wakristo ambao wamo katika hali hiyo, kwa maana kwa kuonyesha fadhili na ufahamu wanaweza kusaidia kuzuia maumivu ya kimoyo na ya kiroho yanayoweza kutokezwa na hali hiyo. Hata hivyo Wakristo ambao mtu wa ukoo wao ametengwa na ushirika, na wanaotaka msaada, wanahitaji kuwa na maoni yanayofaa ya kufahamu waziwazi hatua ya kutenga na ushirika.
Neno la Mungu linaelekeza kundi liwaondoshe nje wale wanaozoea dhambi bila kutubu. (1 Wakorintho 5:11-13) Kufanya hivyo kunalinda kundi kwa ujumla lisichafuliwe, tena kunaiinua juu sifa yalo iliyo nzuri. Lakini Wakristo mmoja mmoja walio katika jamaa hiyo, na wengine wanaotaka kuwasaidia, wanahitaji kulindwa kibinafsi pia. Tunaweza kufahamu sababu kwa kuangalia hatua ya kutenga mtu na ushirika inafunua nini juu ya hali yake ya moyoni. Angalia hali hizi mbili zinazohusiana na kutenga na ushirika:
Kwanza, wakati mtu anapokuwa ametenda dhambi nzito ambayo inaweza kumkosesha upendeleo wa Mungu na kufanya atengwe na ushirika, halmashauri ya wazee wa kiroho inakutana pamoja naye. Huenda akawa tayari amekwisha kujua ubaya wa mwendo wake, akatubu katika moyo wake na kuanza “matendo yanayopatana na kutubu.” (Matendo 26:20) Inapokuwa hivyo, wazee watamkaripia kwa kutumia Neno la Mungu, wampe mawazo ya Kibiblia juu ya ‘kufanyia miguu yake njia za kunyoka’ kisha wasali pamoja naye na kwa ajili yake. Kwa kuwa yeye ni mwenye kutubu, hana uhitaji wa kuondoshwa nje wala kuonwa na watu wa jamaa yake au na wengine kuwa mtu aliyetengwa na ushirika.—1 Timotheo 5:20, NW; Waebrania 12:13; Yakobo 5:14-16.a
Pili, huenda ikawa kwamba wakati halmashauri inapokutana na mtenda dhambi, yeye hajatubu bado. Wakati mkutano unapoendelea wazee huenda wakaweza kugusa moyo wake, kumfanya aone wazi uzito wa dhambi yake. (Linganisha 2 Samweli 12:1-13.) Bila shaka, kwa kuwa mpaka wakati huo hajazaa ‘tunda lo lote linalopatana na kutubu,’ inawapasa wazee wajihadhari sana ili kuhakikisha kwamba yeye hasikitiki au haoni aibu kwa sababu tu anajulikana. (Luka 3:8) Kwa sababu wanahangaikia kundi, inawapasa wasadikishwe kabisa kwamba sasa yeye ametubu kikweli na yuko tayari ‘kumwelekea Mungu kwa kutenda matendo yanayopatana na kutubu.’ (Matendo 26:20) Ikiwa wanasadiki kwamba ametubu, anaweza kubaki katika kundi na kusaidiwa na wazee, watu wa jamaa yake na wengine.
Kusudi la kutaja mambo mawili hayo ni nini? Ni kuonyesha kwamba ikiwa mtu ametengwa na ushirika, lazima iwe kwamba wakati huo alikuwa na moyo mbaya kweli kweli na/au alikuwa amejikaza kabisa kufuatia mwendo unaovunjia Mungu heshima. Petro alisema kwamba hali ya mtu wa namna hiyo ni mbaya kuliko ile ya wakati alipokuwa hajawa Mkristo; yeye ni kama ‘nguruwe aliyeoshwa lakini akarudi kugaagaa matopeni.’ (2 Petro 2:20-22) Jambo hilo linapasa lisaidie watu wa ukoo walio Wakristo na pia wengine kuwa na maoni ya Mungu juu ya mtu aliyetengwa na ushirika.
Lakini maoni ya moyoni na mambo ya uhusiano wa kibinadamu yana mavutano yenye kutatiza sana, kufanya iwe vigumu watu kutenda kupatana na hukumu iliyotoa amri ya kutenga na ushirika ikiwa mtu wa ukoo ndiye anayehusika. (Linganisha Hesabu 16:16-33.) Kwa mfano, mke mwaminifu wa Kikristo anatambua kwamba hatua ya kutenga mume wake na ushirika inamaanisha kwamba sasa vifungo vya kiroho walivyokuwa navyo zamani vimekatishwa. Kwa mwenendo wake na matokeo ya mwenendo huo, yeye amevunja kifungo cha kiroho kati yake mwenyewe na Wakristo wa kweli. Mke wake ataendelea kumwonyesha upendo na heshima kwa kuwa ndiye mume na kichwa cha jamaa, sawasawa na vile wake ambao waume zao si waamini wanavyofanya. (1 Petro 3:1, 2) Lakini haitawezekana kuwa na ushirika wa kiroho pamoja naye, kushiriki katika mazungumzo ya Biblia na sala pamoja naye kama alivyokuwa akifanya hapo zamani. (Mithali 28:9) Kwa uhakika mke huyo atajisikia amepoteza ushirika huo.
Wengine wanaoweza kujisikia wamepoteza kitu ni mababu na akina nyanya Wakristo ambao ni washikamanifu, ambao watoto wao wametengwa na ushirika. Huenda ikawa walikuwa wamezoea kutembelea watoto wao kwa ukawaida, na kufanya hivyo kukawapa nafasi ya kuwafurahia wajukuu wao. Sasa wazazi wametengwa na ushirika kwa sababu ya kukataa viwango vya Yehova na njia zake. Kwa hiyo mambo hayako kama yalivyokuwa katika jamaa. Bila shaka, mababu na akina nyanya hao wanapaswa kuamua waone kama mambo fulani ya kijamaa yaliyo na uhitaji mkubwa kabisa yanawataka wawe na uhusiano mdogo pamoja na wale watoto waliotengwa na ushirika. Na huenda nyakati nyingine wakakaribisha wajukuu wao wawatembelee. Hata hivyo, ni jambo la kusikitisha sana kwamba kwa mwenendo wao usio wa Kikristo watoto wanakatiza furaha iliyo jambo la kawaida ambayo mababu na nyanya hao walikwa wakifurahia!
Mifano hiyo inaonyesha sababu gani Wakristo wale wengine wanapaswa kuwa macho waone uhitaji wa pekee unaoweza kuwapo wakati mtu wa ukoo wa mtu fulani ametengwa na ushirika. Mtume Paulo alihimiza Wakristo ‘waseme kwa kuzifariji nafsi zilizoshuka moyo,’ na huenda ikawa ndivyo ilivyo kuhusu mshiriki yule wa jamaa aliye Mkristo mshikamanifu. (1 Wathesalonike 5:14, NW) Wala hatupaswi kufariji mtu na kumtia moyo kwa maneno wakati tu mwenzake anapotengwa na ushirika, halafu mambo yanaishia hapo. Huenda kukawa na uhitaji wa kumjenga kwa muda mrefu kidogo. Kwa njia fulani, huenda uhitaji huo ukaongezeka kwa kuwa kwa muda mrefu aliye mwaminifu hana ushirika wa kiroho pamoja na mshiriki huyo wa jamaa. Bila shaka, hakuna uhitaji kuwa tukitaja-taja jambo la kutengwa na ushirika katika maongezi yetu. Tunalohitaji kufanya ni kujitokeza sisi wenyewe tukamwonyeshe urafiki kwa uchangamfu, kupendezwa naye kikweli na, juu ya yote, kuwa watu wa hali ya kiroho.—Mithali 15:23; Mhubiri 12:10.
Mema mengi yanaweza kutimizwa pia kwa kumpa ushirika wa Kikristo. Nyakati nyingine Mkristo ambaye mwenzi wake wa ndoa ametengwa na ushirika anajisikia akiwa peke yake. Kama ilivyotangulia kutajwa, yule mwenzi wa ndoa aliyeondoshwa nje amethibitisha kwamba yeye si mtu wa namna ambayo tungependa kushirikiana naye. Na tunahitaji kuwa waangalifu tusihusike katika kushirikiana na mwanamume huyo ati kwa sababu tu tunataka kutembelea au kusaidia mwenzi wa ndoa Mkristo. Kwa hiyo labda matembezi yanaweza kufanywa wakati inapojulikana kwamba yule aliyetengwa na ushirika hayuko nyumbani.
Tunahitaji kusaidia ndugu na dada zetu ambao watu wa ukoo wao wametengwa na ushirika waone ukweli wa maneno haya yaliyoongozwa na Mungu: “Yuko rafiki aambatanaye na mtu kuliko ndugu” wa kimwili, au kuliko mtu mwingine wa ukoo wa kimwili (Mithali 18:24) Huenda tusiweze kurekebisha maumizo yote au kuondoa hasara yote ambayo mtu aliyetengwa na ushirika ameletea Wakristo wa ukoo wake. Lakini, kwa kuwa macho kuyaona mahitaji ya pekee ambayo Wakristo hao wanayo huenda tukaweza “kuwafariji wale walio katika dhiki za namna zote,” kutia ndani huyu. Na kwa upendo tunaweza kuwatia nguvu wale walio na uhitaji huo wa pekee.—2 Wakorintho 1:3,4; Waebrania 12:12, 13.
[Maelezo ya Chini]
a Ili upate mazungumzo kamili zaidi juu ya mambo mbalimbali yanayopasa kufikiriwa katika kutambua toba ya kweli, na pia ili kuona ni mambo gani yanayotiwa ndani ya “matendo yanayopatana na kutubu,” ona Mnara wa Mlinzi wa Desemba 15, 1981, kurasa 16-19.