Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w79 1/1 kur. 12-17
  • Je! Wewe Unajifurahisha Ana Nyingi Mno—Ama Unajinyima?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Wewe Unajifurahisha Ana Nyingi Mno—Ama Unajinyima?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • YANAYOHUSIKA
  • UHITAJI WA KUKESHA
  • “KAMA MTEGO UNASAVYO”
  • Kusitawisha Roho ya Kujinyima
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Kumtumikia Yehova kwa Roho ya Kujidhabihu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Jinsi ya Kudumisha Roho ya Kujidhabihu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
  • Mfuate Yesu kwa Kuendelea
    Huduma Yetu ya Ufalme—1997
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
w79 1/1 kur. 12-17

Je! Wewe Unajifurahisha Ana Nyingi Mno​—Ama Unajinyima?

‘Wakati huo Yesu aliwaambia wanafunzi wake, Mtu ye yote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike [mti wake wa mateso] anifuate.”​—Mt. 16:24.

1. Ni nini yaliyo maoni ya idadi ya watu inayoendelea kuongezeka leo?

KWA watu wengi waliomo ulimwenguni leo, wazo la kujinyima wenyewe kwa ajili ya mtu mwingine, au kwa ajili ya mambo fulani, halivutii sana. Kwa kweli, maoni ya watu wanaoendelea kuwa wengi zaidi na zaidi ni kutaka mambo ya kimwili mengi zaidi na zaidi, anasa zaidi na zaidi na uhuru zaidi wa kufanya lo lote analotaka, bila kujali Mungu au mwanadamu. Hata nia ya kujinyima kwa ajili ya jamaa ya mtu mwenyewe imepungua katika miaka ya karibuni, nako kuvunjika kwa jamaa pamoja na talaka kumeongezeka sana katika taifa moja baada ya jingine.

2. Sababu gani maelekeo haya ya kujifurahisha anasa nyingi mno hayawashangazi wanafunzi wa Biblia?

2 Maelekeo haya ya kujifurahisha anasa nyingi mno, hayawashangazi wale ambao wamekuwa wakikesha kwa habari ya Neno lililoongozwa na Mungu, Biblia Takatifu. Kwa usahihi Neno hilo la unabii lilitabiri kwamba katika hizi “siku za mwisho” wengi wangekuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha,” “wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu.” Wengine wanafuata sana njia zao za kujifurahisha anasa nyingi mno hivi kwamba Biblia inawaita “wasiojizuia.” Vilevile hili linaonekana katika ongezeko kubwa la hali ya kulewa kupindukia, matumizi mabaya ya dawa za kulevya pamoja na uasherati katika miaka ya karibuni.​—2 Tim. 3:1-4.

3. Kuna maoni gani yaliyo kinyume ya haya, naye mwenye kuyapendekeza ni nani?

3 Hata hivyo, vilevile kuna maoni yaliyo kinyume ya hayo, yale ya kujinyima. Ni mwendo unaopendekezwa na Muumba Mwenye Nguvu Zote wa ulimwengu wote, Yehova Mungu mwenyewe. Lakini je! mwendo kama huo si wa kale​—usiofaa katika nyakati hizi za kisasa? Sababu gani mtu ye yote apendezwe na jambo hilo wakati watu zaidi na zaidi hawapendezwi nalo?

YANAYOHUSIKA

4, 5. Yesu alisema namna gani juu ya mwendo wa kujinyima, naye alimaanisha nini na maneno yake?

4 Ni jambo la maana sana kwetu kuwa na maoni yanayofaa juu ya jambo hili la kujinyima kuliko kujifurahisha anasa nyingi mno. Juu ya hili, Yesu Kristo alisema hivi: “Mtu ye yote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike [mti wake wa mateso] kila siku anifuate. Kwa kuwa mtu atakaye kuponya nafsi yake ataiangamiza, na mtu atakayeiangamiza nafsi yake kwa ajili yangu ndiye atakayeisalimisha. Kwa kuwa yamfaa nini mtu kuupata ulimwengu wote, kama akijiangamiza, au kujipoteza mwenyewe?”​—Luka 9:23-25.

5 Hapa Yesu alikuwa akieleza mwendo wa kujinyima. Naye alitoa mfano wa kuonyesha lililomaanishwa. Alisema hivi: “Siyatafuti mapenzi yangu mimi, bali mapenzi yake aliyenipeleka.” (Yohana 5:30) Kwa hiyo, Yesu alichukua mwendo wa kujinyima ili aweze kuyatimiza kabisa mapenzi ya Baba yake wa kimbinguni, Yehova. Huo ndio mwendo ambao Yesu alipendekeza kwa wafuasi wake. Yeye alisema kwamba wanapaswa kuwa na nia ya ‘kujikana’ wenyewe, maana yake ni kwamba wazuie tamaa zao wenyewe na kufanya mapenzi ya Mungu liwe ndilo jambo kubwa maishani mwao.

6. (a) Ni mambo gani yanayopasa mwendo wa kujinyima? (b) Mtu anawezaje ‘kuponya nafsi yake’ kwa kufanya mapenzi ya Mungu?

6 Kweli, maisha kama hayo ya kujinyima si mepesi. Yanahusu kutumia wakati na jitihada. Nyakati nyingine hata yanaweza kumfanya mtu apoteze uhai wake mikononi ya wale wanaotesa watumishi wa Mungu. Walakini, kama alivyoonyesha Yesu, yeye anayefanya mapenzi ya Mungu angeokoa ‘nafsi yake,’ au uhai. Katika njia gani? Kwa kuwa angepata kibali ya Yehova na zawadi ya baadaye ambayo Mungu huwaahidi wote wanaomtumikia, kwa kuwa yeye anawapa “thawabu wale wamtafutao.” (Ebr. 11:6) Kwa wengi wa watumishi washikamanifu wa Mungu, thawabu hiyo ni uzima wa milele katika taratibu yenye haki hapa duniani: “Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.” (Zab. 37:29) Tena, “watajifurahisha kwa wingi wa amani.” (Zab. 37:11) Hata mauti haiwezi kuzuia thawabu hii, kwa kuwa Yehova anatuhakikishia kwamba kutakuwako “ufufuo wa uzima.”​—Yohana 5:29.

7. Sababu gani wakati ujao unaoahidiwa na Yehova unastahili yote tunayoweza kujinyima?

7 Ndiyo, maisha yamo hatarini katika jambo hili la kujinyima likilinganishwa na lile la kujifurahisha anasa nyingi mno! Nayo ni maisha mazuri namna gani​—kuishi milele katika hali za kiparadiso ambazo zitafanya kila siku iwe ‘furaha’ tupu! Kweli, hayo yatakuwa maisha kweli kweli. Hakuna mwendo wa maisha unaoweza kuchagua sasa katika ulimwengu huu, hakuna kiasi cho chote cha kazi ngumu katika biashara ya namna yo yote au ufundi, hakuna matendo yo yote ya ushikamanifu kwa mwanadamu ye yote au tengenezo la ulimwengu huu yanayoweza kutoa wakati ujao kama ule unaoahidiwa na Yehova kwa wale wanaomtumikia. Hivyo, basi, mambo yo yote tunayoweza kujinyima yanastahili tujinyime.

UHITAJI WA KUKESHA

8, 9. Sababu gani tunahitaji kuongeza jitihada zetu za kukesha na kujinyima?

8 Tunapozidi kuingia zaidi na zaidi katika hizi “siku za mwisho” kunakuwa na uhitaji mkubwa zaidi wa kukesha kiroho na wa kuzidisha upendo wetu wa kujinyima mambo ili tumtumikie Mungu katika njia anayoikubali. Sababu moja ni kwamba Shetani Ibilisi anajua kwamba ana “wakati mchache tu” unaobaki kabla hajaondolewa kabisa. (Ufu. 12:12; 20:1-3) Kwa kuwa sasa wakati wake ni mfupi sana, tunaweza kutazamia azidishe jitihada zake zenye wazimu za kupotoza na kuharibu. Yeye angependa sana kuwapumbaza watumishi wa Yehova ili ufahamu wao wa kiroho utiwe giza na ili wapoteze ufahamu wao juu ya haraka ya nyakati hizi za hatari. Naye bila shaka anaweza kufurahi sana ikiwa wangeweza kupunguza, au waache kabisa kuwatangazia wengine “habari njema za ufalme” wa Mungu.​—Mt. 24:14, NW.

9 Hatupaswi kufikiri kwamba uwezo wa Shetani wa kudanganya na kuharibu ni mdogo. Neno la Yehova lililoongozwa naye linaonya hivi: “Mwe na kiasi na kukesha; kwa kuwa mshitaki wenu Ibilisi, kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze. Nanyi mpingeni huyo, mkiwa thabiti katika imani.” (1 Pet. 5:8, 9) Mtu mwenye hekima akijua kwamba simba mwenye wazimu anazunguka-zunguka mtaani, anaweza kuchukua hatua yo yote ajilinde yeye mwenyewe pamoja na jamaa yake, au sivyo?

10, 11. (a) Yesu alitoa onyo gani juu ya kujifurahisha anasa nyingi mno? (b) Sababu gani maneno ya Yesu yanatumika hata kwa wengine katika tengenezo la Yehova leo?

10 Yesu alisema juu ya uhitaji wa kuwa macho aliposema hivi juu ya uharibifu unaokuja juu ya taratibu hii mbovu ya mambo iliyopo: “Jiangalieni, mioyo yenu isije ikalemewa na ulafi, na ulevi, na masumbufu ya maisha haya; siku ile ikawajia ghafula, kama mtego unasavyo; kwa kuwa ndivyo itakavyowajilia watu wote wakaao juu ya uso wa dunia nzima. Basi, kesheni ninyi kila wakati, mkiomba, ili mpate kuokoka katika hayo yote yatakayotokea, na kusimama mbele za Mwana wa Adamu.”​—Luka 21:34-36.

11 Yesu alikuwa akisema na nani? Kwa habari hii alikuwa akisema na wafuasi wake. Hata hivyo yeye aliwaonya kwamba, ikiwa hawangekesha, hata wengine wao wangejiliwa na siku ya Yehova yenye uharibifu bila kujua. Ni jambo gani lingefanya wajiliwe bila kujua? Wangekuwa na kazi nyingi mno wakisumbukia mambo ya kila siku ya maisha haya, au wangekuwa wakijifurahisha anasa nyingi mno. Maneno hayo ya Yesu ni onyo kweli kweli leo. Kwa sababu mwisho wa taratibu hii haujaja bado, wengine wanaomtumikia Yehova huenda wakajaribiwa walegeze tamaa yao ya kujinyima kwa ajili yake. Huenda wakafikiri kwamba taratibu yake mpya iko mbali sana katika wakati ujao hivi kwamba hali hii ya sasa haipaswi kuonwa kuwa ya haraka sana. Huenda wakaona kwamba wanapaswa kuhangaikia zaidi kuishi yale yanayoitwa maisha ya “kawaida.”

12. Je! ni jambo la akili kujaribu kutafuta maisha ya “kawaida” katika taratibu hii?

12 Walakini je! kuna njia yo yote ye maisha inayoweza kuitwa ya “kawaida” kulingana na maoni ya Mungu? Ulimwengu huu uko chini ya uongozi wa Shetani na mashetani wake, na kutawaliwa na taratibu za kisiasa zenye uonevu, taratibu za kibiashara zenye pupa pamoja na taratibu za kidini zenye choyo. Inajaa hofu (woga), chuki, jeuri, uasherati, ufisadi, magumu ya uchumi, magonjwa na mauti. Yote haya yanatofautiana sana na maisha ya kawaida ambayo Yehova anakusudia wanadamu wawe nayo, yanayotia ndani afya kamili, usalama kamili pamoja na furaha, kutia na uzima wa milele, yote haya katika dunia ya paradiso. Kwa hiyo, maisha ya sasa si ya kawaida hata kidogo. Nayo yataendelea kuwa hivyo mpaka Yehova atakapoiponda na kuiondolea mbali taratibu hii yote mbovu, na kutayarisha njia kwa ajili ya taratibu yake mpya yenye utukufu. Kwa hiyo tunajidanganya sisi wenyewe tukitafuta ukawaida katika ulimwengu usio na ukawaida.

13. Kuna mifano gani ya watu walionaswa na Shetani kwa sababu za kujifurahisha anasa nyingi mno’

13 Ungekuwa msiba mkubwa namna gani, katika wakati huu ambao umesonga mbele sana, ikiwa Mkristo angekosa kujali onyo la Yesu, alegeze kinga yake na kuhatirisha uhusiano (urafiki) wake na Yehova! Mtu kama huyo angejiachilia aingie katika “mtego wa Ibilisi . . . [awe ametegwa] naye, hata kufanya mapenzi yake.” (2 Tim. 2:26) Ndivyo ilivyokuwa kwa Dema katika karne ya kwanza, ambaye hapo kwanza alikuwa Mkristo. Kwa habari yake, mtume Paulo alisema: “Dema aliniacha, akiupenda ulimwengu huu wa sasa.” (2 Tim. 4:10) Mkewe Lutu vilevile alianguka katika mtego wa Shetani. Kwa kutokutii yeye aliangalia nyuma Sodoma ulipokuwa ukiharibiwa ‘akapoteza nafsi yake.’ Kwa hiyo, Yesu alikuwa na sababu nzuri ya kusema: “Mkumbukeni mkewe Lutu.” (Luka 17:32) Tena alikuwapo Esau, aliyetoa haki yake ya uzaliwa wa kwanza kwa ajili ya faida ya kitambo tu ya mambo ya kimwili. Lo! namna huo ulivyokuwa uamuzi wenye makosa! (Mwa. 25:29-34) Mwingine alikuwa Akani aliyefikiri zaidi juu ya fedha na mavazi mazuri kuliko kusudi la Yehova. (Yos. 7:1, 20-25) Kwa huzuni, wote hawa walipoteza mengi kwa kuwa na roho ya kujifurahisha anasa nyingi mno mahali pa roho ya kujinyima. Hapana, kudanganywa na roho ya kujifurahisha anasa nyingi mno si jambo lisilo la kawaida. Liliwapata wengine wa watumishi wa zamani wa Mungu, na limewapata wengine katika nyakati za kisasa. Linaweza kutukia tena.

“KAMA MTEGO UNASAVYO”

14. Uharibifu wa ulimwengu unaokuja unafananishwaje na mtego?

14 Yesu aliposema juu ya kuja kwa siku ya Yehova yenye kuharibu, alisema kwamba ingekuja “kama mtego unasavyo.” (Luka 21:35) Mtego humnasa mnyama bila kujua wakati anapopitia mahali penye hatari bila kujiangalia. Vivyo hivyo, mwisho wa taratibu hii utakuja ghafula, wakati usipotazamiwa na watu wengi. Watu hao huenda wakatia ndani wengine wa wale waliokuwa wameanza kutembea katika “njia” “iendayo uzimani,” lakini wakajiachilia wafuate sana mambo ya ulimwengu huu, wakaendelea sana katika upande mbaya.​—Mt. 7:14.

15. Hali isiyoogopesha sana ya ulimwengu ni ushuhuda wa kwamba lazima mwisho uwe mbali sana?

15 Lakini je! hali isiyoogopesha sana ya ulimwengu, au ufanisi wa kuonekana juu-juu tu katika mahali mbalimbali, haungetoa sababu ya kuona kwamba mwisho hauko karibu? Kwa kweli, ungekuwa na maana iliyo kinyume kabisa. Ebu angalia maneno haya ya Yesu: “Kwa maana kama vile ilivyokuwa siku za Nuhu, ndiyo kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu. Kwa kuwa kama vile siku zile zilizokuwa kabla ya Gharika watu walivyokuwa wakila, na kunywa, wakioa na kuolewa, hata siku ile aliyoingia Nuhu katika safina, wasitambue, hata Gharika ikaja, ikawachukua wote ndivyo kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu.” Ndiyo sababu Yesu alionya hivi pia: “Kwa sababu hiyo ninyi nanyi jiwekeni tayari; kwa kuwa saa msiyodhani Mwana wa Adamu yuaja.”​—Mt. 24:37-39, 44.

16. Paulo na Petro walisema nini juu ya namna mwisho wa taratibu hii utakavyokuja kwa ghafula sana?

16 Vilevile, mtume Paulo alionyesha namna hii taratibu ingeisha kwa ghafula sana, bila kutazamiwa na watu wengi. Alisema hivi: “Maana ninyi wenyewe mnajua yakini ya kuwa siku ya [Yehova] yaja kama vile mwivi ajavyo usiku. Wakati wasemapo, Kuna amani na salama ndipo uharibifu uwajiapo kwa ghafula.” (1 The. 5:2, 3) Vilevile mtume Petro alisema juu ya uhakika wa kwamba “siku ya [Yehova] itakuja kama mwivi,” bila kutazamiwa na wale wasiokesha kiroho. (2 Pet. 3:10) Ndiyo sababu Paulo alishauri hivi: “Basi tusilale usingizi kama wengine, bali tukeshe, na kuwa na kiasi.”​—1 The. 5:6.

17. Sababu gani hatupaswi kuona kwamba Yehova amekawiza siku ya hasira yake?

17 Siku ya hasira ya Yehova juu ya uovu itakuja barabara kama alivyoipangia. Haitachelewa hata nukta moja. Kwa hiyo, hakuna mtu ye yote anayempenda Yehova anayepaswa kujiachilia aanze kufikiri na kuishi katika njia inayoonyesha kutoamini kusudi la Yehova la kuiondolea dunia hii uovu na kusimamisha taratibu mpya ya haki. Ikiwa mtu angechukua maoni kama hayo yasiyofaa, angekuwa kama wale wanaotajwa katika 2 Petro 3:3, 4 panaposema hivi: “Katika siku za mwisho watakuja na dhihaka zao watu wenye kudhihaki, wafuatao tamaa zao wenyewe, na kusema, Iko wapi ahadi ile ya kuja kwake? kwa maana, tangu hapo babu zetu walipolala, vitu vyote vinakaa hali iyo hiyo, tangu mwanzo wa kuumbwa.”

18. (a) Kuna ushuhuda gani unaoonyesha kwamba siku zetu ni tofauti kabisa na “mwanzo wa kuumbwa”? (b) Sababu gani jitihada zetu kubwa zapaswa kutumiwa katika kufanya mapenzi ya Yehova?

18 Ni kweli, mpango ule wa kwanza wa uhai umeendelea mpaka sasa. Walakini, katika karne hii ya 20, tuna ushuhuda kamili wa “siku za mwisho.” Mingi ya misiba mikubwa zaidi ya historia imefanyika katika karne hii. Naye mwanadamu ana uwezo wa kuangamiza uhai wote duniani sasa. Bila shaka, ushuhuda wote unaotimiza unabii wa Biblia unaonyesha kwamba ulimwengu huu unasonga mbele kuelekea mwisho wake. Nao ufikapo, utamaanisha kipindi cha taabu isiyo na mfano kwa wanadamu. Yesu aliuita “dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe.” (Mt. 24:21) Katika kipindi hicho taratibu zote za kisiasa, kiuchumi na za dini ya uongo za ulimwengu huu zitabomolewa. Kwa hiyo, wakati wote, jitihada na gharama zilizotumiwa kuendeleza taratibu hizo zitakuwa zimekuwa za bure. Bila shaka Wakristo hawatataka kutumia jitihada zao kubwa katika mambo hayo yasiyodumu. Ushikamanifu wao mkubwa pamoja na kujinyima kwao kunapaswa kuwe kwa ajili ya mambo yenye kudumu. “Dunia inapita, pamoja na tamaa zake, bali yeye afanyaye mapenzi ya Mungu adumu hata milele.”​—1 Yohana 2:17.

19. Ni uhitaji gani wa kujinyima utakaokuwako wakati wa “dhiki kubwa,” nao ni nani watakaoelekea zaidi kufanya hivyo?

19 Bila shaka wakati wa “dhiki kubwa” inayokuja watumishi wa Yehova watakuwa na nafasi nyingi za kuonyesha roho ya kujinyima. Watahitaji kusaidia Wakristo wenzao katika njia nyingi, kutia na kuwagawia mambo ya lazima ya kimwili. (Ebr. 13:16) Kwa sababu ya misukosuko mikubwa itakayokuwako ya taratibu za kisiasa, kijamii na kiuchumi, hata huenda watumishi wa Mungu wakapoteza sehemu fulani ya mali zao, au hata zote. Kwa hiyo, wale ambao sasa wanatanguliza faida za Yehova maishani mwao, ambao tayari wana roho hiyo ya kujinyima, huenda ikawa vyepesi kwao kujinyima mambo watakayohitajiwa wajinyime wakati huo.

20. Jambo hili la kujinyima ni la maana kadiri gani?

20 Hatuwezi kuepuka uhakika wa kwamba ulizo hili, “Je! wewe unajifurahisha anasa nyingi mno​—ama unajinyima?” ni jambo linalopasa uzima au mauti kulingana na maoni ya Mungu. Ikiwa sisi tunapenda uzima, na tunataka kuishi maisha makamilifu katika taratibu mpya ya Mungu, basi tunahitaji kuwa na roho ya kujinyima ili tumtumikie Mungu katika njia anayoikubali sasa.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki