Kusitawisha Roho ya Kujinyima
“Ndugu zangu, nawasihi, kwa huruma zake Mungu, itoeni miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, ya kumpendeza Mungu, ndiyo ibada yenu yenye maana.”—Rum. 12:1.
1. Sababu gani Yehova anastahili mambo yote tunayoweza kujinyima kwa ajili yake?
ILI wanadamu wawe na nia ya kutoa dhabihu lazima kile kinachotolewa dhabihu hizo kiwe kinastahili, kiwe kinaheshimiwa. Pasipo shaka lo lote, Yehova Mungu anastahili kutolewa dhabihu zo zote tunazomtolea. Yeye ndiye Muumba wa ulimwengu wote wa ajabu, na ulio mkubwa sana, tena yeye ndiye chanzo cha vitu vyote vilivyo hai. Vilevile yeye ndiye Muumba wa taratibu mpya yenye haki itakayomaliza magumu yote ya wanadamu. Kwa kufaa, Biblia inasema hivi: “Umestahili wewe, Bwana wetu na Mungu wetu, kuupokea utukufu na heshima na uweza; kwa kuwa wewe ndiwe uliyeviumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako, navyo vikaumbwa.” (Ufu. 4:11) Kwa kuwa Yehova anastahili sana hivyo, tunasihiwa ‘tumtolee miili yetu iwe dhabihu iliyo hai.’—Rum. 12:1.
2. Ni mambo gani yanayotiwa ndani katika neno “dhabihu”? (Soma Waebrania 13:15, 16.)
2 Kuwa dhabihu iliyo hai kwa Yehova kunapasa nini? Ufafanuzi mmoja wa neno “dhabihu” ni “kutoa kitu chenye thamani au kinachotamaniwa kwa kitu kinachoonwa kuwa na haki kubwa zaidi.” Maana nyingine ya “dhabihu” ni “kutolea mungu uhai.” Kwa kuwa Yehova hataki tuuawe , katika njia halisi juu ya madhabahu fulani, tunaweza kumtolea uhai wetu kwa kumtumikia. Alipokuwa akisema juu ya uharibifu unaokuja wa taratibu hii, mtume Petro aliwasihi Wakristo wawe watu wanaojulikana kwa “mwenendo mtakatifu na utauwa.” (2 Pet. 3:11) Kwa hiyo, dhabihu inayokubaliwa na Mungu inapasa matendo yanayofaa, pamoja na kuacha mazoea yasiyokubaliwa na Yehova au yanayoweza kutuzuia tumtumikie.
3. Je! Yehova anakubali kujinyima kote kunakofanywa kuhusiana na Ibada?
3 Je! mwendo wa kujinyima una maana ya kwamba Mungu anataka watu wafuate dini kwa shauku sana kupita kiasi, hata wafanye mambo yasiyo ya akili? Kwa mfano, watu wengine wanajikokota umbali mkubwa kwenda mahali patakatifu ya kanisa huku magoti yao yakitoka damu, wakifikiri kwamba Mungu anapendezwa na dhabihu kama hizo. Wengine huenda wakaishi maisha ya umaskini na kuomba-omba. Wengine wanakataa kula chakula cha namna fulani kama sehemu ya ibada yao. Lakini Yehova hataki watumishi wake wajitie katika magumu kama hayo. Yeye anakataa sheria za wanadamu ambazo ‘huonekana kana kwamba zina hekima, katika namna ya ibada waliyojitungia wenyewe, na katika kunyenyekea, na katika kutawala mwili kwa ukali.’—Kol. 2:23.
4. Kujinyima kwa ajili ya faida za Yehova kunamaanisha nini leo?
4 Namna ya kujinyima kwenye akili ambako Yehova anataka ni kwamba tuwe na kiasi katika tamaa zetu ili tuweze kutumikia mapenzi yake kwa ukamilifu zaidi. Mapenzi hayo yanakamatana na serikali ya Mungu inayokuja juu ya dunia yote, ufalme wake wa kimbinguni mikononi mwa Kristo. Kwa kuwa karibuni serikali hiyo ndiyo itakayokuwa mamlaka peke yake inayotawala dunia, wote wanaotaka kuishi chini ya usimamizi wake wenye haki wanahitaji kujifunza sheria, kanuni na makusudi yake. Vilevile wanahitaji kuendeleza faida zake, ‘wakihubiri habari hizi njema za ufalme huo kati ya wanadamu leo. Hivyo, kujinyima kwa ajili ya faida za Yehova kunamaanisha tutii sheria zake na kutanguliza ufalme wake maishani mwetu: “Utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake,” akasema Yesu. Mt. 6:33.
5. Je! mwendo wa kujinyima unapaswa kuonwa kama jambo gumu sana?
5 Je! mwendo wa kujinyima ni mwepesi? Hapana, si mwepesi. Walakini Yehova Mungu na Yesu Kristo ndio wanaotualika tuuchukue. Hii inamaanisha kwamba unawezekana, kwa kuwa Baba mwenye upendo na Mwanawe, ambao ndio walioumba wanadamu, wanajua yale ambayo wanadamu wanaweza kutimiza. Zaidi ya hayo, kwa kuwa Yehova na Kristo wanawapenda wanadamu sana, tunaweza kuwa na hakika kwamba hawawezi kutuuliza tufanye jambo ambalo laweza kuharibu faida zetu. Pia, tunapokumbuka zawadi zilizo mbele, inaweza kusemwa kwa hakika kabisa kwamba kujinyima ili tumtumikie Yehova ndio mwendo wa maisha ‘unaofaa peke yake leo. Mengine yote mwisho wake ni kukatiza tamaa.—Mt. 19:26; Rum. 9:33; 1 Yohana 4:16.
6, 7. (a) Nuhu alijinyima mambo gani? (b) Je! Nuhu alivunjika moyo kwa sababu ya muda mwingi kupita?
6 Tunaweza kutiwa moyo sana katika mwendo wetu wa kujinyima tukichunguza historia ya Biblia na kuona namna wanadamu wengine wa kawaida walivyofuata mwendo kama huo, na kuona baraka walizopata kwa kufanya hivyo. Kwa mfano, Yehova alimwuliza Nuhu ajinyime mambo ili aweze kufanya kazi ambayo ulimwengu wa wakati wake uliona kuwa upumbavu. Aliagizwa ajenge chombo kikubwa sana, safina. Walakini kulikuwa hakujakuwa hata kidogo mvua yenye kunya au gharika. Zaidi ya hayo, Nuhu hakuwa mjenzi wa merikebu, tena alikuwa na madaraka ya jamaa pia.
7 Ili ajenge safina kubwa hivyo, Nuhu alihitaji kupata wakati kutokana na mambo ambayo angependa kufanya. Kwa kweli, kama angetumia wakati na jitihada izo hizo aongeze utajiri wake wa kimwili, bila shaka angepata raha zaidi. Vilevile, ilimpasa ajinyime nyingine ya sifa zake njema kati ya jirani zake, kwa kuwa kazi yake ya kujenga safina ilimfanya adhihakiwe. Je! yeye alivunjika moyo au akaiacha kwa kuwa ilichukua miaka mingi huku akingojea mwisho wa taratibu hiyo? Kinyume chake, Nuhu aliendelea na mwendo wake wa kujinyima. Hii ilitia ndani kuwa “muhubiri wa haki.” (2 Pet. 2:5, ZSB) Yeye alifahamu kwamba hakuwa akiishi katika ulimwengu wa “kawaida,” bali uliokuwa ‘umeharibika mbele za Mungu, uliojaa dhuluma,’ ambao mwishowe ungeharibiwa. Kwa hiyo, Biblia inasema hivi: “Ndivyo alivyofanya Nuhu, sawa-sawa na vyote alivyomwamuru Mungu, hivyo ndivyo alivyofanya.”—Mwa. 6:11, 22.
8. Utii wa Nuhu ulikuwa na matokeo gani kwetu sisi sote?
8 Tunapaswa kufurahi kwamba Nuhu alikataa kujiunga na watu wenye kujifurahisha anasa nyingi mno katika siku zake. Sisi tunaishi leo, kwa sababu ya utii wake, kwa kuwa sisi sote tu wazao wa Nuhu. Wale waliokuwa wakijifurahisha anasa nyingi mno walipoteza vyote—nyumba, mali, waliyokuwa wakiita njia ya “kawaida” ya maisha. Vilevile, walipoteza uhai wao wenyewe na ule wa watoto wao, kwa kuwa “dunia ile ya wakati ule iligharikishwa na maji, ikaangamia.”—2 Pet. 3:6.
9. Ibrahimu alibarikiwaje kwa sababu ya nia yake ya kujinyima?
9 Mwingine aliyejua uhitaji wa kujinyima kwa ajili ya Yehova ni Ibrahimu. Yehova alimwagiza hivi: “Toka wewe katika nchi yako, na jamaa zako, na nyumba ya baba yako, uende mpaka nchi nitakayokuonyesha.” (Mwa. 12:1) Ibrahimu hakujizuia ati kwa sababu Yehova alikuwa akimwomba aiache njia ya maisha iliyokuwa salama kwa ajili ya kitu asichokuwa na hakika nacho. Yeye alikuwa na hakika kwamba cho chote ambacho Yehova angetaka afanye kilifaa na kilikuwa kwa faida yake mwenyewe. “Basi Abramu akaenda, kama [Yehova] alivyomwamuru.” (Mwa. 12:4) Ni kweli kwamba hiyo ilimaanisha ajinyime mambo mengi sana kwa miaka mingi sana. Lakini Yehova alibariki sana nia yake ya kutumikia: Ibrahimu aliona matendo mengi ya ajabu ambayo Yehova alifanya kwa ajili yake na jamaa yake; yeye hakukosa riziki; alikuja kuitwa “rafiki wa [Yehova].” (Yak. 2:23) Vilevile, Mungu alimwahidi Ibrahimu kwamba taifa zima la watu lingetoka kwake. Ni jambo la maana kwamba Biblia inasema juu ya hili: “Kwa kuvumilia akaipata ile ahadi.” (Ebr. 6:15) Kuongezea hayo, yeye alikuwa na pendeleo la kuwa babu ya Yesu.
10. Kulikuwa na maoni gani tofauti katika karne ya kwanza, na kukawa na matokeo gani?
10 Katika kame ya kwanza ya Wakati wetu wa Kawaida, wanaume na wanawake wengi walijinyima faida fulani kwa ajili ya faida za Yehova. Ndiyo, walifanya kazi ngumu na kupatwa na magumu mengi, lakini waliridhika sana kwa kujua kwamba walikuwa wakifanya yanayofaa na kumpendeza Mungu. Vilevile, walikuwa na tumaini hakika kwamba Yehova angekumbuka imani na matendo yao waliyomfanyia na kwamba bila shaka angewapa zawadi bora sana wakati ujao. Lakini namna gani wale waliojifurahisha anasa nyingi mno, waliotaka kuendeleza njia yao ya “kawaida” ya maisha wakamkataa Yesu wakiogopa kwamba ‘Warumi wangekuja wawaondolee mahali pao na taifa lao’? (Yohana 11:48) Hata hivyo njia yao ya maisha ilimalizika katika kizazi icho hicho. Majeshi ya Rumi yaliiacha nchi yao ukiwa, yakiangamiza uhai na mali nyingi sana. Walakini, Wakristo wenye kujinyima walitii mafundisho ya Yesu, wakakimbia sehemu hiyo wakaokoa maisha zao, ijapokuwa waliacha nyuma nyumba zao na karibu mali zao zote za kimwili. Wao wanahesabiwa kuwa wenye “furaha” sana.—Luka 21:20-24; 22:28-30; Ufu. 20:4-6.
KUJINYIMA KATIKA WAKATI WETU
11. (a) Je! Wakristo leo wanatakiwa waache mali zao zote? (b) Kujinyima kwa ajili ya Yehova kunahusianaje na utendaji wetu kuelekea watu wengine?
11 Je! hii inamaanisha kwamba lazima watumishi wote wa Mungu leo waache nyumba pamoja na vitu vingine vyao vya kimwili kama sehemu ya mambo wanayojinyima kwa ajili ya Mungu? Hapana, hilo silo jambo kubwa, ingawaje kwa habari ya mifano iliyoonyeshwa ya Nuhu, Ibrahimu, na Wakristo wa karne ya kwanza, kumekuwa na nia ya kufanya hivyo ikiwa lazima. Jambo kubwa ni mtu kupenda kutanguliza faida za Mungu maishani mwake, akijinyima mambo yo yote ambayo huenda akahitaji kujinyima ili afanye hivyo. Jambo kubwa si aliyo nayo au asiyo nayo mtu, bali pale ulipo moyo wake. Je! unaelekea katika kutanguliza faida za Yehova, au unaelekea katika kutanguliza faida za mtu mwenyewe? Nayo sehemu ya faida za Yehova inatia ndani kufanyia watu wengine mambo, kama lisemavyo Neno la Mungu kwamba “kila mtu asiangalie mambo yake mwenyewe [tu], bali kila mtu aangalie mambo ya wengine,” tena “haitupasi kujipendeza wenyewe [tu],” bali “kila mtu miongoni mwetu na ampendeze jirani yake, apate wema, akajengwe.”—Flp. 2:4; Rum. 15:1, 2.
12. Sababu gani tunapaswa kuthamini mwendo wa kujinyima wa wengine katika nyakati za kisasa?
12 Je! sisi tunaona roho kama hiyo ya kujinyima katika nyakati hizi? Bila shaka. Kwa kweli, watu milioni kadha ambao sasa wanafurahia kweli pamoja na ushirika wa Kikristo katika makundi zaidi ya 40,000 ya Mashahidi wa Yehova duniani pote wanafaidika kutokana na kujinyima kwa watumishi washikamanifu wa Mungu mapema katika nyakati za kisasa. Huko nyuma katika nusu ya pili ya miaka ya 1800 na nusu ya kwanza ya miaka ya 1900 watu wengi wenye kujinyima walifanya kazi kwa bidii sana wafundishe wengine kweli za Biblia na kuweka msingi wa tengenezo la Yehova la kisasa lionekanalo, ambalo sasa tunapokea kweli juu ya Yehova kutoka kwalo, pamoja na faida nyingine nyingi.
13. Wengi wanajinyima mambo gani ili wamtumikie Yehova zaidi?
13 Hivi sasa, duniani pote, makumi mengi ya maelfu ya wanaume na wanawake waliojitoa sana wanajinyima mambo katika njia isiyo ya kawaida ili wamtumikie Mungu. Wengine wamejinyima kwa halisi nyumba na mali ili watumikie wakati wote kwa ajili ya faida za Yehova katika kazi ya umisionari, katika nyumba za Betheli, au kama wajumbe wakitumikia makundi. Wengine wanajinyima ili wafanye upainia wa pekee, wa kawaida au wa msaidizi ili waweze kufundisha wengine juu ya taratibu mpya ya Yehova inayokuja.
14. Yehova anawaonaje wale ambao utumishi wao kwake unazuiwa na hali walizo nazo?
14 Walakini, si wote ambao wamejitoa kwa Yehova wasio na madaraka hivi kwamba wanaweza kufanya utumishi kama huo wa wakati wote. Wengi wanalazimika kujitahidi sana ili walishe jamaa zao katika taratibu yenye magumu ya kiuchumi, wakijua kwamba wakikosa kufanya hivyo wangekuwa “[wabaya] kuliko mtu asiyeamini.” (1 Tim. 5:8) Pia wazazi Wakristo wana daraka linalotokana na kuwa na watoto. Wanafahamu kwamba lazima wajinyime mengine ya mambo ambayo wangependa kufanya ili waweze kutumia wakati wakilea watoto wao katika “adabu na rekebisho la moyoni la Yehova.” (Efe. 6:4, NW) Vilevile, kuna wengine ambao, kwa sababu ya afya mbaya, uzee au vizuizi vingine, wanaweza kumtolea Yehova utumishi wa moja kwa moja mdogo sana. Katika hili, wao wanafanana na yule mjane maskini aliyetoa “senti mbili” zenye thamani ndogo katika hekalu la Mungu. (Luka 21:1-4) Hata hivyo watu hawa wote wanaofanya lo lote wawezalo wawasaidie watu wajifunze juu ya Yehova bila shaka wanampendeza katika yale wanayojinyima. Yeye anawapenda kwa sababu ya nia yao ya kuvumilia hali zenye magumu huku wakimtolea utumishi fulani, kulingana na hali zao—Yak. 5:11.
JICHUNGUZE
15. Ni maulizo gani mazuri tunayoweza kujiuliza?
15 Je! wewe una roho hiyo ya kujinyima? Au, una maelekeo ya kujifurahisha anasa nyingi mno? Je! wewe unamtumikia Yehova kulingana na vile hali zako zinavyokuruhusu? Sababu gani usijichunguze uone kama unaweza kufanya maendeleo katika utumishi wako wa Kikristo unaomtolea Mungu?
16. Tunawezaje ‘kukomboa’ wakati? (Soma Warumi 10:9, 10)
16 Kwa mfano, je! unaweza kutumia wakati zaidi katika kusoma Biblia kipekee? Ikiwa una jamaa, je! unakuwa na mazungumzo ya Biblia ya kawaida nao? Unaweza kutumia wakati wako zaidi uwatembelee jirani zako useme nao juu ya “habari njema”? Au, je! unaweza kutumia wakati fulani usaidie wagonjwa, wazee, au wengine kwa kufanya matendo ya Kikristo ya fadhili na upendo? Labda unaweza kulinganisha wakati unaotumia, tuseme, katika tafrija, kama vile kutazama television, na ule unaotumia kutumikia Yehova katika’ sehemu moja ya utendaji wake au nyingine. Je! unasawazika?—Efe. 5:15.
17. Sababu gani ni jambo la maana wazazi wachunguze yale wanayowaomba watoto wao wafanye?
17 Je! wewe ni mzazi? Chunguza uhusiano wako na watoto wako. Ujue kwamba wakati unaofaa wa watoto wako kujifunza mwendo wa kujinyima ni wakati wa utoto wao. Wapo watoto wako kazi ya maana wafanye nyumbani. Wasaidie waone kwamba kazi, kujinyima kunayapasa maisha, wala si kucheza tu. Labda ulipokuwa mtoto hukuwa na mavazi mazuri, hukupata tafrija au hukuwa na chakula kizuri. Huenda ukaona kwamba hutaki mtoto wako akose mambo hayo kama ulivyoyakosa. Walakini, kwa upande mwingine, kumpa mtoto wako kila kitu anachotaka huenda kukampotezea uhai wake! Huenda kukamfanya afikiri kwamba kufanya mapenzi ya Yehova ni jambo rahisi, na kwa hiyo baadaye huenda akakosa nia ya kujinyima kwa ajili ya Yehova. Kama vile ninyi mlio watu wazima mnavyojua, maisha si mepesi, vitu havipatikani kwa urahisi, nako kufanya mapenzi ya Yehova hakutakuwa rahisi. Kwa hiyo saidia watoto wako wawe na maoni yanayosawazika juu ya maisha. Wafundishe kwamba ijapokuwa kuna wakati wa tafrija, vilevile lazima kuwe na wakati wa kufanya kazi, wa kujifunza Biblia, wa kujinyima. Warudi wana na binti zako katika mwendo wa kujinyima kwa kiasi. Matokeo ya marudia hayo huenda yakawa mojawapo la mambo yenye thamani sana ambayo wanaweza kurithi kutoka kwako. (Efe. 6:4; Ebr. 12:11) Nao mfano wako mwema utasaidia sana kutia nguvu mafundisho unayowapa.
18. Ikiwa hatuwezi kutoa wakati zaidi wa kumtumikia Yehova, bado tunaweza kufanya maendeleo gani?
18 Uwe umeoa au kuolewa au sivyo, huenda kujichunguza kwa unyofu kukaonyesha kwamba unatumia wakati mwingi uwezavyo katika kutumikia faida za ufalme. Je! bado kuna jambo zaidi unaloweza kufanya? Ndiyo, liko. Unaweza kujitahidi uwe Mkristo bora zaidi, ujifunze kuonyesha zaidi matunda ya roho ya Mungu, ambayo ni “upendo, furaha, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujiweza.” (Gal. 5:22, 23, NW) Zaidi ya hayo, unaweza kujitahidi kumtolea Mungu utumishi ulio bora zaidi.
19. Sababu gani inatupasa tusitawishe roho ya kujinyima? (Soma Waebrania 6:11; 1 Wakorintho 15:58.)
19 Wakati ujao, katika taratibu mpya ya Mungu, itaridhisha namna gani kutazama nyuma na kujua kwamba wakati kulipokuwa na uhitaji, katika wakati huu wa muhimu sana, ulijitahidi sana, ukajinyima mambo uliyohitajiwa kujinyima, ukafanya sehemu yako katika kumtumikia Yehova. Ndiyo, uwe na nia ya kuachilia faida zako mwenyewe kwa ajili ya faida za Yehova, ukitazama mbele kwenye zawadi za ajabu sana. Sitawisha roho ya mtunga zaburi aliyesema: “Kwa ukunjufu wa moyo nitakutolea dhabihu; Ee [Yehova], nitalishukuru jina lako, maana ni jema.”—Zab. 54:6.
—Kutoka The Watchtower, Aug. 1, 1978.
[Picha katika ukurasa wa 21]
Petro, Nuhu, Ibrahimu na wengine walijinyima mambo kwa ajili ya Yehova nao walibarikiwa naye