Mahubiri ya Mlimani—“Basi Ninyi Salini hivi”
KUFUATA onyo lake la upole kwamba wanafunzi wake waepuke kuvuta fikira kwao wenyewe kwa unafiki wanapoomba, Yesu alitoa Sala ya Kielelezo inayojulikana sana. Alianza kwa kusema: “Basi ninyi salini hivi.”—Mt. 6:9a.
Neno “ninyi” linahusu wasikilizaji wa Yesu wakitofautishwa na wanafiki ambao alikuwa amewataja mbeleni. (Mt. 6:5) Usemi “hivi” unatokeza tofauti kwa watu waliokuwa wamezoea kusema ‘maneno yale yale kwa kurudia-rudia.’ (Mt. 6:7, NW); Hivyo, inapaswa kuwa wazi kwamba Yesu hakuwa akitia moyo wasikilizaji wake wawe wakirudia-rudia kutoka akilini sala ambayo angewafundisha.
Sala ya Kielelezo ina maombi saba. Ya kwanza matatu yanamwomba Mungu atende kuhusiana na kutakaswa kwa jina lake; yale mengine manne ni maombi yanayohusiana na mahitaji ya wanadamu. Na tuyachunguze moja moja.
(1) “Baba yetu uliye mbinguni, Jina lako litukuzwe.” (Mt. 6:9b) Kwa sababu ya kuwa Muumba wa wanadamu anayekaa juu, juu ya dunia, inafaa viumbe wamwite Mungu “Baba yetu uliye mbinguni.” (Matendo 17:24, 28; 2 Nya. 6:21; Isa. 66:1) Wakati wa karne ya kwanza W.K., usemi huu ulifaa sana, sana sana kwa Wayahudi, kwa sababu alikuwa amekuwa “baba” ya watu hao kwa kuwaweka huru kutokana na utumwa wa Misri na kwa kuwa katika uhusiano wa agano pamoja nao. (Kum 32:6, 18; Kut. 4:22; Isa. 63:16) Matumizi ya mtajo “yetu” kwa wingi, unakubali kwamba wengine licha ya anayeomba wana uhusiano wa karibu na Mungu na ni sehemu ya jamaa yake ya waabudu.
Nyakati nyingine neno “jina” huonekana katika Maandiko kama likiwa na maana sawa na mtu mwenyewe. Kwa mfano, twasoma katika Ufunuo 3:4: “Lakini unayo majina [watu] machache katika Sardi, watu wasioyatia mavazi yao uchafu.” (Linganisha Isaya 30:27; Malaki 3:16.) “Jina lako litukuzwe” inatia ndani wazo la kwamba Mungu achukue hatua ya kujitukuza kwa kuondoa kutoka kwa jina lake la ukumbusho, Yehova, suto ambalo limekuwa likiwekelewa juu yake tangu kuasi kwa wanadamu wawili wa kwanza katika bustani Edeni. (Zab. 135:13; Hos. 12:5) Katika kujibu sala hii, Mungu ataondoa uovu duniani. Kuhusu wakati huo twasoma hivi: “Nami nitajitukuza, na kujitakasa, na kujidhihirisha, mbele ya macho ya mataifa wengi; nao watajua ya kuwa mimi ndimi [Yehova].”—Eze. 38:23; pia 26:23.
(2) “Ufalme wako uje.” (Mt. 6:10a, ZSB) “Ufalme” huo ni utawala wa enzi kuu ya Mungu kama inavyoonyeshwa kupitia kwa serikali ya Kimasihi ya mbinguni mikononi mwa Kristo Yesu na “watakatifu” wanaoshirikiana naye. (Isa. 9:6, 7; 11:1-5; Dan. 7:13, 14, 18, 22, 27) Kuuomba “uje” ni kuuliza kwamba ufalme wa Mungu uje kupambana na wapinzani wote wa utawala wa Mungu wa duniani. Kulingana na kitabu cha Danieli, “ufalme [wa Mungu] . . . utavunja falme hizi zote [za kidunia] vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.” (Dan. 2:44) Baada ya hilo, utawala wa Mungu utageuza dunia iwe paradiso ya duniani pote ya amani na haki.—Zab. 72:1-15; 2 Pet. 3:13; Ufu. 21:1-5.
(3) “Mapenzi yako yatimizwe hapa duniani kama huko mbinguni.” (Mt. 6:10b, ZSB) Hili si ombi la kwamba mapenzi ya Mungu yafanywe na wanadamu kama yanavyofanywa na malaika mbinguni, ijapokuwa hilo litatokea bila shaka. (Zab. 103:19-22; 148:1-4) Mahali pake, ni ombi la kwamba Mungu mwenyewe atende kupatana na mapenzi yake juu ya dunia. Inalingana na tangazo la mtunga zaburi:
”[Yehova] amefanya kila lililompendeza, katika mbingu na katika nchi, katika bahari na katika vilindi vyote. Aliwapiga wazaliwa wa kwanza wa Misri, wa wanadamu na wa wanyama. Alipeleka ishara na maajabu kati yako, Ee Misri, juu ya Farao na watumishi wake wote. Aliwapiga mataifa mengi, akawaua wafalme wenye nguvu.”—Zab. 135:6, 8-10.
Kuomba kwamba Mungu afanye mapenzi yake duniani ni ombi la kwamba afikilize makusudi yake mema kuelekea sayari yetu, kutia na kuwaondoa wapinzani wake mara moja na kwa wakati wote, kama alivyofanya kwa kiasi kidogo katika nyakati za kale.—Ufu. 19:19-21; Zab. 83:9-18.
(4) “Utupe leo riziki yetu.” (Mt. 6:11) Katika masimulizi ya Injili ya Luka maneno ya ombi hili ni haya: “Utupe siku kwa siku riziki yetu.” (Luka 11:3) Kumwomba Mungu atupe vitu vya lazima vya “leo” kunaendeleza imani katika uwezo wake wa kuweza kuangalia mahitaji ya waabudu wake siku kwa siku. Hili si ombi la kupewa vitu vingi kupita kiasi, bali ni la mahitaji ya kila siku kama yanavyotokea. Linamkumbusha mtu juu ya amri ya Mungu kwamba Waisraeli wakusanye mana iliyoletwa kimwujiza kila mtu “sehemu ya siku,” na basi.—Kut. 16:4.
(5) “Utusamehe deni zetu, kama sisi nasi tuwasamehevyo wadeni wetu.” (Mt. 6:12) Luka anaonyesha kwamba kwa “deni” Yesu alimaanisha “dhambi.” (Luka 11:4) Watu wanaweza kupata msamaha kutoka kwa Mungu ikiwa tu wamekwisha ‘samehe’ watu wanaowakosea. (Tazama pia Marko 11:25.) Akikuza wazo hili, Yesu aliongeza hivi: “Kwa maana mkiwasamehe watu makosa yao, na Baba yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi. Bali msipowasamehe watu makosa yao, wala Baba yenu hatawasamehe ninyi makosa yenu.” (Mt. 6:14, 15) Mungu hutoa msamaha kwa wale tu wanaokuwa tayari kuwasamehe wengine.—Linganisha Waefeso 4:32; Wakolosai 3:13.
(6) “Usitutie majaribuni.” (Mt. 6:13a) Hili halikusudiwi kumaanisha kwamba Mungu hujaribu watu wafanye mabaya, kwa maana Biblia husema: “Mungu hawezi kujaribiwa na maovu, wala yeye mwenyewe hamjaribu mtu.” (Yak. 1:13) “Mjaribu” mwenyewe ambaye hujitahidi kushawishi watu wamfanyie Mungu dhambi ni Shetani Ibilisi. (Mt. 4:3; 1 The. 3:5) Hata hivyo, mara kwa mara waandikaji wa Biblia humsema Mungu kuwa akitenda au akifanya vitu ambavyo anaruhusu tu.—Ruthu 1:20, 21; Mhu. 7:13; 11:5.
Ombi, “usitutie majaribuni,” ni kumwuliza Mungu kwamba asiruhusu waabudu wake waaminifu washindwe au waanguke wanapokazwa wamwasi Mungu. Kuhusiana na hili, mtume Paulo anaandika hivi: “Jaribu halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili.”—1 Kor. 10:13.
(7) “Utuokoe na yule mwovu.” (Mt. 6:13b) Hii ni kuomba kwamba Ibilisi asiruhusiwe awashinde waabudu waaminifu wa Mungu. (Linganisha Zaburi 141:8, 9.) Wanafunzi wa Yesu wanaweza kuwa na hakika juu ya uwezo wa Mungu wa kujibu ombi hilo. Mtume Petro anaandika hivi: “[Yehova] ajua kuwaokoa watauwa na majaribu.”—2 Pet. 2:9; Linganisha Ufunuo 3:10.