Sala Ambazo Hakika Zitajibiwa
KUNA sala ambazo zitajibiwa pasipo shaka. Wazo kuu la sala hizo limo katika kiolezo ambacho Yesu Kristo aliwapa wanafunzi wake aliposema: “Basi ninyi salini hivi; Baba yetu uliye mbinguni, jina lako litukuzwe [litakaswe, NW], ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.”—Mathayo 6:9-13.
Maneno hayo ya sala ya Yesu ya kiolezo yamerudiwa mamilioni mengi ya nyakati. Ingawa Kristo hakutarajia wafuasi wake wa kweli warudie-rudie tu sala hiyo, maombi yao yenye kuonyesha mawazo kama hayo ya moyoni yatajibiwa hakika. (Mathayo 6:7, 8) Hivyo basi, yamaanisha nini kutakasisha jina la Mungu? Kwa nini kusali ili Ufalme wake uje? Na kwa nini kuomba mapenzi ya Mungu yatimizwe?
‘Jina Lako Litakaswe’
Yehova, ‘Aliye juu, juu ya nchi yote,’ Ndiye Yesu alimtaja kuwa “Baba yetu uliye mbinguni.” (Zaburi 83:18) Mungu alikuwa ‘amekuwa baba’ kwa Waisraeli kwa kuwaweka huru kutoka ufungwa wa Kimisri na kwa kuingia katika uhusiano wa agano pamoja nao. (Kumbukumbu 32:6, 18; Kutoka 4:22; Isaya 63:16) Leo, Wakristo wapakwa-mafuta wana ufikirio mwororo kwa Yehova akiwa Baba yao. (Warumi 8:15) Na washirika wao, walio na tumaini la kidunia, vilevile husali kwa Yehova Mungu akiwa Baba yao.—Yohana 10:16; Ufunuo 7:1-9.
Lakini kwa nini kusali ili jina la Mungu litakaswe? Ni kwamba, tangu uasi wa wanadamu wa kwanza wawili katika bustani ya Edeni, suto limerundikwa juu ya jina la kimungu. Katika kujibu sala ya jinsi hiyo, Yehova ataondolea mbali suto lote ambalo limepata kutupwa juu ya jina lake la ukumbusho. (Zaburi 135:13) Atafanya hivyo kwa kuondoa uovu duniani. Kwa habari ya wakati huo, Mungu alisema hivi kupitia nabii Ezekieli: “Nami nitajitukuza, na kujitakasa, na kujidhihirisha, mbele ya macho ya mataifa mengi; nao watajua ya kuwa mimi ndimi BWANA [Yehova, NW].”—Ezekieli 38:23.
Yehova Mungu ni mtakatifu na safi. Kwa hiyo jina lake lapasa kutakaswa, au kuwekwa kando kuwa takatifu. Yeye ataonyesha utakatifu wake kwa kutenda ili ajitakase mbele ya uumbaji wote. (Ezekieli 36:23) Wale wanaotamani upendelevu wake na uhai wa milele ni lazima wamfikirie Yehova kwa kicho na kutakasa jina lake kwa kulichukua kuwa lililotengeka kutoka kwenye mengine yote likiwa juu kuyapita. (Walawi 22:32; Isaya 8:13; 29:23) Kwa sababu hiyo, Yesu aliambia wafuasi wake wasali hivi: “Jina lako litukuzwe [litakaswe, NW]” au, “lichukuliwe kuwa takatifu; litendewe kuwa takatifu.” Twaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu atajibu sehemu hii ya sala ya Yesu ya kiolezo.
“Ufalme Wako Uje”
Yesu aliwaambia wafuasi wake wasali hivi pia: “Ufalme wako uje.” Pasipo shaka sala za kuomba kuja kwa Ufalme wa Mungu zitajibiwa. Ufalme ni utawala wa enzi kuu ya Yehova kama uonyeshwavyo kupitia serikali ya kimbingu ya Kimesiya ikiwa mikononi mwa Mwana wake, Yesu Kristo, na “watakatifu” walio washirika. (Danieli 7:13, 14, 18, 22, 27; Isaya 9:6, 7) Kwa muda mrefu Mashahidi wa Yehova wamethibitisha kutokana na Maandiko kwamba Yesu alitawazwa akiwa Mfalme wa kimbingu katika mwaka 1914. Basi, kwa nini impase mtu yeyote kusali ili Ufalme “uje”?
Kusali ili kuomba kuja kwa Ufalme kwa kweli humaanisha kuomba kwamba uje dhidi ya wapinzani wote wa utawala wa kimungu duniani. Karibuni sasa “ufalme [wa Mungu] . . . utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.” (Danieli 2:44) Tukio hilo litachangia utakaso wa jina takatifu la Yehova.
“Mapenzi Yako Yatimizwe”
Yesu alizidi kufundisha wanafunzi wake kusali hivi: “Mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.” Hilo ni ombi la kwamba Yehova atende kupatana na mapenzi yake kwa dunia. Lafanana na julisho la mtunga zaburi: “BWANA [Yehova, NW] amefanya kila lililompendeza, katika mbingu na katika nchi, katika bahari na katika vilindi vyote. Ndiye apandishaye mvuke toka miisho ya nchi; huifanyia mvua umeme; hutoa upepo katika hazina zake. Aliwapiga wazaliwa wa kwanza wa Misri, wa wanadamu na wa wanyama. Alipeleka ishara na maajabu kati yako, Ee Misri, juu ya Farao na watumishi wake wote. Aliwapiga mataifa mengi, akawaua wafalme wenye nguvu.”—Zaburi 135:6-10.
Kusali kwamba mapenzi ya Yehova yatimizwe duniani ni ombi la kwamba atekeleze makusudi yake kuelekea tufe hili. Hiyo yatia ndani kuondoshwa daima kwa wapinzani wake, kama vile alivyowaondoa kwa kadiri ndogo nyakati za kale. (Zaburi 83:9-18; Ufunuo 19:19-21) Sala za kuomba mapenzi ya Yehova yafanywe katika sehemu zote za dunia na katika ulimwengu wote mzima hakika zitajibiwa.
Wakati Ufalme Utawalapo
Badala ya uovu ambao sasa waienea jamii ya kibinadamu, ni jambo gani laweza kutarajiwa wakati Ufalme wa Mungu utawalapo na mapenzi ya kimungu yatimizwapo duniani kama yalivyo mbinguni? Kulingana na mtume Petro, “tunatazamia mbingu mpya na nchi [dunia, NW] mpya, ambayo haki yakaa ndani yake.” (2 Petro 3:13) “Mbingu mpya” hizo ni mamlaka za kiroho zenye uadilifu ambazo zinatawala—Yesu Kristo na warithi-washirika 144,000 katika Ufalme wa kimbingu. (Warumi 8:16, 17; Ufunuo 14:1-5; 20:4-6) ‘Dunia mpya’ si tufe jingine la kidunia. Bali, ni jamii adilifu ya watu wenye kuishi duniani.—Linganisha Zaburi 96:1.
Chini ya utawala wa Ufalme, dunia itageuzwa iwe paradiso ya tufe lote. (Luka 23:43, Zaïre Swahili Bible) Ndipo amani na ufanisi wa kweli vitakapoonewa shangwe na ainabinadamu wote watiifu. (Zaburi 72:1-15; Ufunuo 21:1-5) Wewe waweza kuwa miongoni mwa masongamano hayo ya watu yenye furaha ikiwa wewe ni mtetezi mwaminifu-mshikamanifu wa utawala wa Kimesiya juu ya raia watiifu wa kidunia. Watetezi wa utawala huo huomba kwa bidii ili jina la Yehova litakaswe, ili Ufalme wake uje, na ili mapenzi yake yatimizwe. Sala zao zenye kuhisiwa moyoni hakika zitajibiwa.