Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w79 2/1 uku. 12
  • Je! Wewe Unatembea katika Jina la Mungu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Wewe Unatembea katika Jina la Mungu?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • LINALOMAANISHWA NA KUTEMBEA KATIKA JINA
  • KUTEMBEA KATIKA JINA LA YEHOVA
  • UTU NA MATENDO YA KIMUNGU
  • HESHIMA KWA JINA LA KIMUNGU
  • PENDELEO LA PEKEE
  • KUSHUHUDIA KIJASIRI
  • Liheshimu Jina Kuu La Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • Kwa Nini Ni Lazima Tujue Jina la Mungu
    Jina la Mungu Litakaloendelea Milele
  • Jina la Mungu na Lako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Jina la Mungu
    Amkeni!—2017
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
w79 2/1 uku. 12

Je! Wewe Unatembea katika Jina la Mungu?

“Kwa maana mataifa yote watakwenda, kila moja kwa jina la mungu wake, na sisi tutakwenda kwa jina la [Yehova], Mungu wetu, milele na milele.”​—⁠Mika 4:5.

1. Kila mtu mwenye akili hutembea katika jina la nani? Eleza.

KILA mtu mwenye akili anatembea katika jina la mungu fulani. Ndiyo, kwamba mataifa au watu mmoja mmoja wanajua hivyo au hapana, wanatumikia mungu fulani. ‘Hilo laweza kuwaje?’ Waweza kuuliza hivyo. Basi, leo, si watu wote wanaotumikia mungu fulani aliye na jina, kama walivyofanya watu wa zamani zilizopita. Bali watu wengine wanaabudu wachezaji, wanasiasa, wachezaji wa sinema, hata wengine wanajiabudu wenyewe. Kwani, mungu wao hata huenda akawa tumbo lao! (Flp. 3:​18, 19) Wengine humwabudu Shetani Ibilisi moja kwa moja, hali wengine wanamtumikia pasipo kujua, kwa kuwa “ulimwengu mzima uko katika nguvu za yule mwovu.” (1 Yohana 5:​19, NW) Lo! namna maneno yalioandikwa na Mika nabii Mwebrania chini ya uongozi wa Mungu katika karne ya nane kabla ya Wakati wetu wa Kawaida yalivyo ya kweli! Alitangaza hivi: “Kwa maana mataifa yote watakwenda, kila moja kwa jina la mungu wake.”​—⁠Mika 4:5.

2, 3. (a) Wakristo wa kweli wanatembea katika jina la nani, Sana Sana katika wakati gani? (b) Wao wana maoni gani? (Kol. 3:​23, 24)

2 Kabla tu ya kutaja maneno hayo, alikuwa ametaja jambo ambalo lingetukia “katika siku za mwisho.” Wakati huo mlima wa nyumba ya Yehova Mungu ungeimarishwa, uinuliwe juu ya milima (kuonyesha hali iliyotukuzwa ya ibada ya kweli) mingine yote. Watu wangeuendea makundi makundi. ‘Wangefua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu, nao hawangejifunza vita tena.’​—⁠Mika 4:​1-4.

3 Wale wanaoiendea nyumba ya Yehova wanajua kwamba “hakuna Mungu ila mmoja tu.” (1 Kor. 8:4) Hivyo, wakati “mataifa wanapokwenda kwa jina la mungu wao,’ nia ya Wakristo hawa wa kweli inaonyeshwa vizuri na maneno ya Mika yanayoendelea: “Na sisi tutakwenda kwa jina la [Yehova], Mungu wetu, milele na milele.” (Mika 4:5) Maneno hayo yana maana gani kwako? Je! wewe unatembea katika jina la Mungu?

LINALOMAANISHWA NA KUTEMBEA KATIKA JINA

4. Jina ni kitu gani? Toa mfano.

4 Jina hufanya mtu au kitu kijulikane. Neno “mungu” ni jina la kawaida. Kwa upande mwingine, jina halisi linamtofautisha mtu na wale wengine wote. “Yehova” ni jina halisi. Walakini, neno “jina” vilevile linamaanisha heshima au sifa. Kwa hiyo, ‘jina la Mungu wetu’ ni jina halisi au la pekee analojulikana kwalo, nalo linashirikishwa na sifa fulani.

5, 6. (a) Katika zamani zilizopita, ni kitu gani kilichoshirikishwa na jina la mungu? (b) Ni kitu gani kinachomaanishwa na ‘kutembea katika jina la mungu’?

5 Katika nyakati zilizopita, kwa kawaida watu waliipa miungu yao majina ya kuitofautisha. Kwa mfano, kulikuwako Tamuzi, Artemi, Zeu, Baali na Marduki (Merodaki). Mwishowe, miungu hiyo mbalimbali ya kiume na ya kike iliheshimiwa; ikajipatia sifa kwa sababu ya matendo yanayodhaniwa kwamba ilifanya. Heshima na sifa kama hiyo ilishirikishwa na jina la kila mmoja wa miungu hiyo. Kwa mfano, Marduki anadhaniwa kuwa ndiye aliyeanzisha Babeli, akaheshimiwa kwa sababu hiyo.

6 ‘Kutembea katika jina’ la mungu fulani kunamaanisha kufanya mambo yanayokubaliwa au yanayofanywa na mungu huyo. Kunamaanisha kutenda kulingana na sifa ya mungu huyo na vilevile kukubali mamlaka ya mungu huyo. Kwa kweli, ‘kutembea katika jina la mungu’ kunamaanisha kujiweka wakf kwa mungu huyo, kuitwa kwa jina lake na kumwakilisha mungu huyo duniani.

KUTEMBEA KATIKA JINA LA YEHOVA

7, 8. Kutembea katika jina la Yehova kunamaanisha zaidi ya kufanya mambo gani?

7 Mungu wa kweli amejipa jina yeye mwenyewe. Wakristo wanajua sana kwamba Yehova ndiye aliye “juu, juu ya nchi yote.” (Zab. 83:18) Wanamshukuru Mungu kwa kuwafunulia jina lake la pekee. Walakini, kutembea katika jina la Yehova kunapasa mengi kuliko kuweza tu kutamka jina lake. Kunamaanisha zaidi ya kutambua (kutofautisha) jina la Mungu katika hati za Biblia.

8 Kutembea katika jina la Yehova hakumaanishi tu kusema kwamba yeye ndiye Mungu wetu. Vilevile, kunapasa mengi kuliko kuhudhuria mikutano ya Kikristo katika Jumba la Ufalme la mahali penu la Mashahidi wa Yehova. Na, bila shaka, kutembea katika jina la Yehova hakukamatani na utendaji wa kuhubiri peke yake.

9. Je! kutembea katika jina la Yehova kunapasa tu yale tunayosema sisi wenyewe?

9 Mambo haya yajapokuwa ya maana, peke yake hayaonyeshi kwamba sisi tunatembea katika “jina” la Yehova kweli kweli. Jambo linaloamua si yale tu tunayosema na kudai sisi wenyewe, bali yale tunayofanya hasa kwa mioyo yetu, akili, nafsi na nguvu. (Luka 10:27; Yak. 1:​22-27) Mtume Paulo aliuliza ulizo hili lenye kuamsha sana fikira: “Hamjui ya kuwa yeye ambaye mnajitoa nafsi zenu kuwa watumwa kwake katika kumtii, mmekuwa watumwa wake yule mnayemtii, kwamba ni utumishi wa dhambi uletao mauti, au kwamba ni utumishi wa utii uletao haki.” (Rum. 6:16) Wale wanaotembea katika jina la Mungu wamejiweka wakf kwake, nao ‘humtumikia Yehova’ kweli kweli, wakifanya hivyo kwa uaminifu na kwa utii. (Rum. 12:11) Je! wewe umechukua msimamo imara kati ya waabudu wa Yehova? Je! wewe unatembea katika jina la Mungu?

UTU NA MATENDO YA KIMUNGU

10. Tumeendeleaje kukua katika kumthamini Yehova?

10 Huenda ikawa tulifurahi sana tulipojifunza kwa mara ya kwanza kwamba Mungu Mwenye Nguvu Zote ana jina. Labda tulifurahi tulipoona jina la Mungu Yehova katika Biblia kwa mara ya kwanza. Lo! namna tulivyofurahi tulipofahamu kwamba jina la Mungu linaonekana mara elfu nyingi katika Maandiko Matakatifu! Walakini, kutembea katika jina la Yehova lilikuwa jambo jingine. Hilo halikuanza mara moja. Tuliendelea kuthamini kadiri tulivyoendelea kujifunza mengi zaidi juu ya Yeye anayeitwa kwa jina Yehova.

11. Musa aliambiwa nini juu ya sifa za Yehova?

11 Kadiri wakati ulivyopita, tukaja kuzithamini sifa za Yehova, utu wake. Kwa mfano, tulipata ufahamu huo tulipokuwa tukitafakari juu ya maelezo haya ya Mungu katika Kutoka 34:​6, 7, NW:

“Naye Yehova akaenda akipita mbele ya uso wake [Musa] na kutangaza: ‘Yehova, Yehova, Mungu mwenye rehema na, asiye mwepesi wa hasira na mwingi wa fadhili za upendo na kweli, mwenye kuhifadhi fadhili za upendo kwa ajili ya maelfu, mwenye kusamehe makosa na uasi na dhambi, lakini hatakosa kwa vyo vyote kutoa adhabu.’ “

12. Musa alimwelezaje Yehova katika wimbo?

12 Miaka mingi baadaye, Musa aliongozwa na Mungu atunge wimbo. Katika wimbo huo alisema hivi:

“Nitalitangaza jina la [Yehova]; mpeni ukuu Mungu wetu. Yeye Mwamba, kazi yake ni kamilifu; maana, njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, asiye na uovu. Yeye ndiye mwenye haki na adili.”​—⁠Kum. 32:​3, 4.

13. Ni sifa gani ambazo tumekuja kuzishirikisha na Mungu zinazotuongoza tumpende na kumtumaini?

13 Wale wanaotembea katika jina la Yehova wamejifunza pia kwamba upendo, furaha, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, na kujiweza ni matunda ya roho takatifu ya Mungu. (Gal. 5:​22, 23, NW) Kwa hiyo, hizi ni sifa zinazotoka kwa Yehova. Sasa tunazishirikisha na jina lake takatifu, nazo hutuongoza tumpende na kumtumaini Mungu tunayetembea katika jina lake.

14. (a) Wale wanaotembea katika jina la Yehova wanawezaje kuwa na hakika kwamba Mungu anaweza kutimiza kusudi lake na kushuhudia jina lake? (b) Eleza namna ushindi wa Yehova juu ya miungu ya Misri ulivyokuja kujulikana kati ya mataifa, kama inavyoelezwa katika Yoshua 2:​10, 11 na 1 Samweli 4:8.

14 Zaidi ya hayo, Wakristo wa kweli wamekuja kujua kwamba Yehova anakusudia kutengemeza enzi yake kuu ya ulimwengu wote na kulishuhudia jina lake kupitia kwa ufalme wa kimbinguni mikononi mwa Yesu Kristo. (Luka 11:2; Ufu. 11:​16-18) Kuongezea hayo, watu wanaomwogopa Mungu wanajua kwamba Mungu anaweza kutimiza kusudi lake na kushuhudia jina lake takatifu, Kwa sababu gani? Kwa sababu kuna maandishi yanayoonyesha matendo makuu aliyoyatenda Yehova. Yeye si kama miungu ya mataifa isiyofaa kitu isiyoweza kuwafanyia jambo lo lote jema wale wanaotembea katika majina yao. (Zab. 115:​1-8) Ebu angalia namna maelezo yalivyotolewa juu ya Yehova katika wimbo baada ya kuwaokoa watu wa Israeli kwa mwujiza katika Bahari ya Shamu:

“Ee [Yehova], katika mbingu ni nani aliye kama wewe? Ni nani aliye kama wewe, mtukufu katika utakatifu, mwenye kuogopwa katika sifa zako, mfanya maajabu? Ulinyosha mkono wako wa kuume, nchi ikawameza. Kwa maana farasi za Farao na magari yake na wapanda farasi wake waliingia ndani ya bahari, [Yehova] akayarudisha maji ya bahari juu yao; bali wana wa Israeli walikwenda katika nchi kavu kati-kati ya bahari.”​—⁠Kut. 15:​11, 12, 19.

15. Wale wanaotembea katika jina la Yehova wamemjua kuwa Mungu wa unabii wenye kutegemeka namna gani?

15 Wale wanaotembea katika jina la Yehova vilevile wanamjua kuwa Mungu wa unabii unaotegemeka. Unabii wa Yehova juu ya wakati ujao umeandikwa katika jina lake mwenyewe. Ni kama kwamba ameutia sahihi yake akitoa uhakikisho wake kuonyesha uhakika wake. Tunaweza kuutegemea unabii kama huo. Kwa mfano, Yehova alitoa ahadi ya kinabii ya kuwakomboa Waisraeli kutokana na utumwa wa Misri na kuwapa nchi fulani. Aliutimiza. (Kut. 3:​6-17; 14:​19-31) Miaka mingi baadaye, Mfalme Sulemani wa Israeli aliweza kusema hivi: “Na ahimidiwe [Yehova], aliyewapa watu wake Israeli kustarehe, vilevile kama yote aliyoyaahidi. Halikukosa kupatikana neno lo lote katika ahadi yake njema, aliyoahidi kwa mkono wa Musa mtumishi wake.”​—⁠1 Fal. 8:56; tazama pia Yoshua 21:45.

16. Wale wanaotembea katika jina la Yehova wamejifunza nini juu ya upendo wa Mungu kwa wanadamu?

16 Pamoja na hayo, wale wanaotembea katika jina la Yehova wamejifunza juu ya kusudi la Mungu la kuitakasa jamii nzima ya kibinadamu na dhambi kupitia kwa uwezo wenye kulipia dhambi wa dhabihu ya Mwanawe mpendwa, Yesu Kristo, ili haki ya hukumu ipate kuridhishwa. Wanafurahi kuona kwamba haki ya hukumu inashirikishwa na jina la Mungu, kama vile anavyowapenda wanadamu. “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu,” akasema Yesu, “hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.”​—⁠Yohana 3:16; 1 Kor. 15:22; 1 Yohana 4:10.

HESHIMA KWA JINA LA KIMUNGU

17. Yehova ameonyeshaje kwamba anajiheshimu?

17 Tunapaswa kupendezwa na kuliheshimu jina la Mungu mwenye upendo kama huyo. Yehova mwenyewe anapendezwa Sana jina lake, lakini si kwa uchoyo. Yeye anajiheshimu mwenyewe naye hajafanya hata kidogo jambo lo lote ambalo limeshusha heshima ya jina lake takatifu. Sikuzote matendo yake yameshirikisha jina lake na kweli, haki ya hukumu na haki. Matendo ya Mungu yamepamba jina lake kwa heshima, utukufu, uzuri na ukuu. Basi, akiwa na sababu nzuri, Daudi aliyekuwa amezeeka aliweza kumhimidi Yehova na kusema hivi: “Ee [Yehova], ukuu ni wako, na uweza, na utukufu.” (1 Nya. 29:11) Namna lilivyo jambo la maana kwa wale waliojiweka wakf kwa Yehova leo kuliheshimu inavyofaa jina la Mungu!

18. Kwa habari ya sheria za Yehova, kanuni za adili na mipango yake ya wokovu, tu aweza kuonyeshaje kwamba tunatembea katika jina lake?

18 Watu wanaotembea katika jina la Yehova wanamkubali yeye kuwa Mfanya-Sheria wao, Hakimu na Mfalme. (Isa. 33:22) Kwa kuwa Yehova Mungu ndiye Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote, bila shaka yeye ana haki ya kufanya na kufikiliza sheria, na kuweka kanuni za adili pamoja na mipango ya kuwafaidi viumbe wake wenye akili milele. Ebu fikiria hili: Tukiheshimu sheria za Yehova na kutii kanuni za adili za Mungu, tukishukuru mipango yake kwa ajili ya hali yetu njema pamoja na wokovu wetu wa milele​—⁠hayo yote yanaonyesha ushuhuda wa kwamba sisi tunatembea katika jina la Yehova.

19. (a) Yehova ameahidi kuchukua tendo gani, na kwa sababu gani? (b) Kwa hiyo, tunatazamia mbele kwenye utimizo wa sala gani?

19 Bila shaka, wale wanaotembea katika jina la Yehova kweli kweli wanangojea kwa shauku nyingi wakati atakapochukua hatua juu ya wale wanaolitukana jina lake, atende kwa faida ya wote wanaopenda haki. (Eze. 20:9; 39:7) Kwa kweli, wanaompenda Yehova wanatazamia kutimizwa kwa Sala ya Kielelezo aliyofundisha Yesu Kristo: “Baba yetu uliye katika mbingu, jina lako na litakaswe. Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatukie, kama mbinguni, pia duniani.” (Mt. 6:​9, 10, NW) Kuongezea hayo, watu wanaotembea katika jina la Yehova wanatazamia pia siku ambayo kila mtu aliye hai atakapoheshimu jina la Mungu lililo takatifu zaidi.

PENDELEO LA PEKEE

20. Tofauti na dini za Jumuiya ya Wakristo, watu wa Yehova ‘wanatembeaje katika jina lake’?

20 Wale wanaotembea katika jina la Yehova wana daraka kubwa. Ili tutembee katika jina lake tunapaswa kuwa tumejiweka wakfu kabisa kwake. Kunatuhitaji tuishi kulingana na jina la Mungu, tukiwakilisha kila kitu kinachowakilishwa na jina la Yehova. Ndiyo, kunamaanisha kuwakilisha jina la Mungu mbele ya ulimwengu katika njia sahihi. Ni wazi kwamba, kutembea katika jina la Yehova hakutoi ruhusa yo yote ya kulidharau, kupigana nalo, kuliondoa katika tafsiri za Biblia na kujaribu kulificha, kama vile wanadini wa Jumuiya ya Wakristo wamefanya au walivyojaribu kufanya. Mahali pake, kutembea katika jina la Mungu wetu kunamaanisha kuheshimu jina Yehova, kulipigania kiroho, na kulipa mahali panapofaa katika Maandiko Matakatifu na kulitangaza bila woga.​—⁠Zab. 9:​1, 2.

21, 22. Ni nani peke yao wanaowakilisha jina la Mungu leo, nalo pendeleo lao la pekee mbele ya wanadamu wote ni pendeleo gani?

21 Katika karne ya kwanza ya Wakati wa Kawaida, Yehova Mungu alikuwa na watu kwa ajili ya jina lake. Wanafunzi hao wa Yesu Kristo waliotiwa mafuta walitegemeza jina na enzi kuu ya Yehova. Kwa kufaa, katika baraza ya mitume na wazee katika Yerusalemu katika mwaka 49 W.K., mwanafunzi Yakobo alitangaza hivi: “Ndugu zangu, nisikilizeni. Simeoni [mtume Petro] ametueleza jinsi Mungu hapo kwanza alivyowaangalia Mataifa ili achague watu katika hao kwa ajili ya jina lake.” (Matendo 15:​13,14) Vivyo hivyo leo, Yehova ana watu kwa ajili ya jina lake. Wao si sehemu ya dini za Jumuiya ya Wakristo, bali wao ni washiriki wa mabaki ya wafuasi wa Yesu waliotiwa mafuta. “Mkutano mkubwa” walio na tumaini la uzima wa milele duniani wanashirikiana na mabaki haya. (Yohana 10:​14-16; Ufu. 7:​4-9) Kati ya vikundi vyote vya dini vinavyopatikana duniani leo, mashahidi hawa wa Yehova ndio peke yao wanaowakilisha jina la Mungu.

22 Lao ni pendeleo na cheo cha pekee mbele ya ulimwengu wote wa wanadamu. Katika karne ya nane K.W.K., kupitia kwa nabii Isaya, Yehova Mungu aliiuliza miungu yote ya mataifa watoe mashahidi wao, washuhudie juu ya uungu wao. Miungu hiyo yote ya uongo ilishindwa kutoa mashahidi. Walakini ebu angalia vile Mungu wa kweli alivyowaambia watu wa jina lake: “Ninyi ni mashahidi wangu, asema [Yehova], na mtumishi [wangu] niliyemchagua.” (Isa. 43:​8-10) Leo Mashahidi wa Yehova wanafurahi kuitwa kwa jina la Mungu. Wanaliona kuwa pendeleo kubwa kumwakilisha Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote kumjulisha kwa wanadamu. kumshuhudia Mungu huyu wa kweli na makusudi yake. Yakilinganishwa na pendeleo hili la ajabu, mambo mengine yote yanakuwa na maana ndogo sana.

KUSHUHUDIA KIJASIRI

23. Henoko alifanya nini alipokuwa akitembea na Mungu, naye alipata baraka gani?

23 Mara nyingi ujasiri (uhodari) mwingi unahitajiwa ili mtu aweze kutembea katika jina la Yehova akiwa shahidi wake. Lakini kufanya hivyo kunaleta baraka nyingi. Kwa mfano, “Henoko [alikwenda] pamoja na Mungu,” akatangaza ujumbe mkali kwa ujasiri. (Mwa. 5:24) “Angalia”! akasema Henoko, “[Yehova] alikuja na watakatifu wake, maelfu, ili afanye hukumu juu ya watu wote, na kuwaadhibisha wote wasiomcha Mungu, kwa ajili ya kazi zao zote za upotevu walizozitenda bila kumcha Mungu, na kwa ajili ya maneno magumu yote ambayo hao wenye dhambi wasiomcha Mungu wameyanena juu yake.” (Yuda 14, 15) Yehova “alimtwaa” shahidi huyo hodari, akifupiza maisha yake na kuzuia wapinzani wake wasimwue. “Alihamishwa” hivi kwamba kwa wazi yeye hakuona uchungu wa mauti.​—⁠Ebr. 11:5; linganisha Yohana 3:13.

24. Uaminifu wa Nuhu ulithawabishwaje, na kwa sababu gani?

24 Vilevile, Nuhu “alikwenda pamoja na Mungu.” Mwanamume huyu mwaminifu alishuhudia juu ya kusudi la Mungu la kuwaangamiza waovu kwa gharika ya duniani pote. Uaminifu wa Nuhu ulithawabishwa kweli kweli, kwa kuwa matokeo yake yalikuwa kwamba yeye pamoja na wengine saba walihifadhiwa hai wakapitia katika gharika hiyo ya duniani pote. ​—⁠Mwa. 6:9; 7:​6, 7; 8:16; 2 Pet. 2:5.

25. Mashahidi wa Yehova wanatangaza ujumbe wa namna gani leo?

25 Wanaume hao walikuwa kati ya mashahidi wa kwanza wa Yehova. (Ebr. 11:4-7; 12:1) Wao hawakuogopa kuliheshimu jina la Mungu na kulijulisha kote kote. Mashahidi Wakristo wa Yehova wa leo wana maoni ayo hayo. Wanatangaza ujumbe wa Mungu wa hukumu kwa ujasiri. Lakini pia wanahubiri “habari njema” za taratibu mpya yenye haki iliyo karibu sana. Wanatamani sana kuona utimizo kamili wa ahadi ya Yehova ya kuleta “mbingu mpya na dunia mpya” ambamo haki itakaa. (2 Pet. 3:​8-13) Lo! namna furaha itakavyoenea pote wakati huo! Hakutakuwa tena na mtu ye yote atakayekuwa akitembea katika jina la mungu mwingine. Mahali pake, viumbe wote wenye akili watatembea katika jina la Yehova Mungu milele na milele.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki