“Mtembee kama Anavyostahili Yehova”
“Sisi . . . hatujaacha kutoa sala kwa ajili yenu na kuomba kwamba mjawe na maarifa sahihi ya mapenzi yake katika hekima yote na ufahamu wa kiroho, ili mtembee kama anavyostahili Yehova.”—Kol. 1:9, 10, NW.
1. (a) Ni uhusiano (urafiki) gani mzuri kujifurahisha pamoja na Yehova? (b) Hivyo, basi, nia yetu kuhusu amri zake inapaswa kuwa nia gani?
YEHOVA MUNGU ndiye rafiki bora zaidi ambaye ye yote anaweza kuwa naye. Kwa sababu mzee wa ukoo “Ibrahimu alimwamini [Yehova], ikahesabiwa kwake kuwa ni haki; naye aliitwa rafiki wa [Yehova].” (Yak. 2:23) Lo! uhusiano (urafiki) mwema namna gani? Lakini Yehova anapenda kwamba watu wote walio na imani kama hiyo watembee katika jina lake wakiwa rafiki zake. Bila shaka, ikiwa watu mmoja mmoja watampendeza Mungu na kufurahia uhusiano wa kirafiki pamoja naye, ni lazima watii maneno ya Mhubiri, aliyetangaza karne nyingi zilizopita hivi: “[Mwogope] Mungu, nawe uzishike amri zake, maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu.”—Mhu. 12:13.
2. Ni jambo gani linalohitajiwa ili ‘tutembee kama anavyostahili Yehova’?
2 Maarifa sahihi ni ya maana sana ili tuwe rafiki za Mungu, tuzishike amri zake na kutembea katika jina lake. Hivyo, basi, mtume Mkristo Paulo aliwaambia waamini wenzake Wakolosai kwa kufaa hivi: “Sisi . . . hatujaacha kutoa sala kwa ajili yenu na kuomba mjawe na maarifa sahihi ya mapenzi yake katika hekima yote na ufahamu wa kiroho, ili mtembee kama anavyostahili Yehova ili mmpendeze kabisa mnapoendelea kuzaa matunda katika kila kazi njema na kuzidi katika maarifa ya Mungu.”—Kol. 1:9, 10, NW.
KUWA MACHO KWA WAJIBU WETU
3. Tunapaswa kuishije ikiwa tutatembea kama inavyostahili katika jina la Yehova?
3 Urafiki pamoja na mwanadamu mwingine hauwezi kuendelea ikiwa tunamwakilisha vibaya katika njia fulani au kusema uongo juu yake. Vivyo hivyo, ikiwa twataka Yehova awe rafiki yetu, lazima tujue kwamba kutembea inavyostahili katika jina lake kunapasa kuishi kulingana na mambo yote yanayowakilishwa na jina hilo. Hili linahitaji kujifunza Maandiko Matakatifu kwa bidii na kwa ukawaida na kutumia kipekee yale yanayosema. Watu wanapotuona, wanatushirikisha na Mungu wetu; na, sisi tukiwa Mashahidi wa Yehova, ni jambo la maana sana tumwakilishe Mungu inavyofaa, tukitenda kulingana na Neno lake.
4. Kwa habari ya kuwakilisha jina la Mungu, Mashahidi wa Yehova wana daraka gani?
4 Mashahidi wa Yehova vilevile wanajua kwamba kutembea inavyostahili katika jina lake kunapasa kila sehemu ya maisha yao. Wao wana wajibu wa kuliwakilisha jina la Mungu mbele ya wanadamu katika njia inayofaa. Bila shaka, wao si kama wale wa Jumuiya ya Wakristo leo ambao wanajiepusha kutumia jina la Yehova wakiogopa kwamba mtu fulani ataudhika. Yehova anataka jina lake lijulikane duniani pote. (Kut. 9:16) Na kwa kweli ni pendeleo kubwa sana kuwajulisha watu kwamba Yehova ndiye Mungu aliye Juu Zaidi.
5. Maoni ya Mkristo juu ya mambo ya kisiasa ni maoni gani, na kwa sababu gani?
5 Walakini, wajibu wa Mkristo unapasa mengi zaidi ya kusema tu juu ya jina la Mungu. Yehova, Rafiki tunayempenda Sana, ndiye Mfalme mkuu wa ulimwengu wote. Jina lake linashikamanishwa na ufalme wake ambao Yesu Kristo ndiye Mtawala wa Kimasihi chini yake Mungu. Kwa kweli, basi, wale wanaotembea kama inavyostahili katika jina la Yehova lazima wautangaze ufalme huo. Kwa hiyo, wao hawana sehemu yo yote katika mambo ya kisiasa ya ulimwengu huu. Mahali pake, wanachukua msimamo kama ule wa Yesu Kristo, aliyetangaza hivi: “Ufalme wangu sio wa ulimwengu huu.”—Yohana 18:36.
6. Wale wanaotembea kama inavyostahili katika jina la Yehova wana maoni gani juu ya dhambi?
6 Ulimwengu wenyewe unajaa udhalimu. Kwa hiyo, wale wanaotembea kama inavyostahili katika jina la Yehova lazima wajiepushe na ulimwengu na kila namna ya uovu uliomo ndani yake. Wao wanaiona dhambi kama anavyoiona Yehova Mungu, ambaye “ni mwenye haki katika njia zake zote, na mwenye fadhili juu ya kazi zake zote.” (Zab. 145:17) Wakristo wanajua kwamba wakiiba, wafanye uzinzi au waihalifu sheria ya Mungu katika njia nyingine yo yote, jina la Yehova lingepatwa na lawama. Sisi hatungetaka hata kidogo jambo hilo litukie! Mahali pake, tunataka mwenendo wetu umtukuze Mungu, kama alivyoandika mtume Petro: “Mwe na mwenendo mzuri kati ya Mataifa, ili, iwapo huwasingizia kuwa watenda mabaya, wayatazamapo matendo yenu mazuri, wamtukuze Mungu siku ya kujiliwa.”—1 Pet. 2:12; Rum. 2:21-24.
“WAIGAJI WA MUNGU”
7. Inawezekanaje kumwiga Mungu?
7 Mtu anaweza kupatwa na matokeo mema ama mabaya kwa sababu ya rafiki zake, kwa sababu huenda mtu akawa na maelekeo ya kuiga washiriki wake. Basi, wale wanaotembea kama inavyostahili katika jina la Yehova wakiwa rafiki zake wanaweza kuwa na hakika kwamba urafiki pamoja naye utakuwa na matokeo mema kwao. Kujaribu kumwiga Yehova kuna faida nyingi. Mtume Paulo alisihi hivi: “Iweni waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa.” (Efe. 5:1, NW) Mtu anaweza kumwiga Mungu, ijapokuwa si mkamilifu, kwa kukubali uongozi unaotolewa katika Neno la Yehova na kwa kutii maongozi ya roho takatifu au nguvu ya utendaji ya Mungu.
8. Wakristo wanapaswa kusitawisha nini? Namna gani?
8 Kwa kweli, mashahidi Wakristo wa Yehova wanatamani kusitawisha na kuyaonyesha matunda ya roho takatifu ya Mungu—upendo, furaha, amani, ustahimilifu, fadhili, wema, imani, upole na kujiweza. (Gal. 5:22, 23, NW) Watumishi wa Mungu wanapoendelea kuonyesha matunda haya, watu wengine wataongozwa wafikiri juu ya sifa hizi wanapokumbushwa juu ya Yehova Mungu. Bila shaka, hilo lawahitaji Wakristo wayaonyeshe matunda ya roho ya Mungu po pote, mbele ya watu wote. Kwa hiyo mtumishi wa Yehova anaweza kujiuliza hivi kwa faida: Je! mimi nafanya hivyo nyumbani, kazini, shuleni, ninapoendesha motokaa, wakati wa utendaji wa tafrija, na vivyo hivyo? Hayo yote yanatiwa ndani katika kutembea kama inavyostahili katika jina la Yehova. Na kwa kweli matunda haya ya roho yanapaswa kuonyeshwa ndugu na dada zetu walio na imani moja nasi. Ndipo sisi sote tunapoweza kufurahi kwa sababu ya kuwa kati ya watu wa Yehova.—Zab. 144:15.
9. Sala inalipasaje hili?
9 Kusali kwa bidii kwa Yehova ili tupate roho takatifu yake na msaada wake katika kusitawisha na kuonyesha tunda lake katika maisha kutajibiwa. (Luka 11:13; Rum. 5:5) Sasa tafadhali fikiria kifupi nyingine za faida za matunda haya ya roho. Itaonekana wazi kwamba yanaleta matokeo mema, si kwa wale wanaoonyesha sifa hizi tu, bali pia na kwa waabudu wenzao wa Yehova na kwa wengine.
10. (a) Upendo kati ya Wakristo ni wa maana kadiri gani? Eleza. (b) Kulingana na 1 Wakorintho 13:4-8, upendo ukoje?
10 Upendo ndilo tunda la kwanza katika matunda haya yaliyotajwa na Paulo. “Mungu ni upendo,” akaandika mtume Yohana. (1 Yohana 4:8) Kwa hiyo, mtu anayemwogopa Mungu ambaye huonyesha upendo anamwiga Yehova katika jambo hilo. Zaidi ya hayo, “wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu,” akasema Yesu Kristo, “mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.” (Yohana 13:35) Upendo ulioko kati ya Wakristo unavuta fikira sasa, kama ulivyofanya katika siku zilizopita. Akitaja juu ya yale yaliyosemwa na walimwengu juu ya Wakristo wa kwanza, Tertullian aliandika hivi: “‘Tazama,’ wanasema, ‘namna wanavyopendana . . . na namna wanavyokuwa tayari kufa mmoja kwa ajili ya mwenzake.’ “Kuongezea hayo, upendo ndio “kifungo cha ukamilifu.” (Kol. 3:14) Na si ajabu! Upendo ni wenye kustahimili na wenye fadhili. Haujivuni, hautakabari, haukosi kuwa na adabu, hautafuti mambo yake wenyewe, hauoni uchungu, hauhesabu mabaya, au kufurahia udhalimu. Mahali pake, unafurahi pamoja na kweli nao husubiri, huamini, hutumaini na kuvumilia yote. Kwa kweli, “upendo haupungui neno wakati wo wote.”—1 Kor. 13:4-8.
11. Furaha ni nini, na kwa sababu gani imetupasa kuwa na furaha?
11 Furaha, ni tunda jingine la roho ya Mungu. Nao uso wenye furaha wa mtangazaji wa Ufalme umefanya nyuso za wasikilizaji wengi kung’aa. Na je! hatuna sababu nzuri ya kufurahi ikiwa tunatembea kama inavyostahili katika jina la Yehova? Ndiyo, kwa kuwa tunatangaza “habari njema tukufu za Mungu wa furaha” (1 Tim. 1:11, NW) Zaidi ya hayo, tuna matazamio yenye furaha, tumaini imara la baraka za wakati ujao, ikiwa tutaendelea kutembea kama inavyostahili katika jina la Yehova. Unapokutana na magumu ya maisha fikiria hayo. Jitahidi kueneza furaha kati ya washiriki wako Wakristo pia, kwa kuwa watu ambao wamejiweka wakf kwa Mungu wanatazamiwa ‘wamtumikie Yehova kwa moyo wa furaha.’—Kum. 28:46, 47.
12. Amani kati ya Wakristo ina faida gani?
12 Amani, tunda jingine la roho, ni sifa yenye kutokeza ya Yehova. Yeye ni “Mungu wa amani.” (Ebr. 13:20) Wakristo wa kweli “[wanatafuta] kuwa na amani na watu wote.” (Ebr. 12:14) Kwa mfano: Katika Mapenzi ya Kimungu Kusanyiko la Mataifa Yote katika mwaka 1958, Mashahidi wa Yehova waliazimia: “KWAMBA, kusema kwa namna ya mfano, sisi tumezifua panga zetu ziwe majembe na mikuki yetu iwe miundu na, tujapokuwa watu wa mataifa mengi sana, sisi hatutainua upanga ili tupigane sisi kwa sisi kwa sababu sisi tu ndugu za Kikristo na washiriki wa jamaa moja ya Mungu, wala sisi hatutajifunza tena kupigana vita sisi kwa sisi, bali sisi tutatembea katika mapito ya Mungu katika amani, umoja na upendano wa udugu.” Watu wa Yehova wemeishi kulingana na azimio hilo, nayo amani inayopatikana kati yao inavuta fikira za watu wanaopenda amani katika Ukristo wa kweli. Isa. 2:2-4) Zaidi ya hayo, ‘Yehova anawabariki watu wake kwa amani.’ (Zab. 29:11) Wao hawajisumbui kwa jambo lo lote, bali kwa kusali wanamjulisha haja zao zote na kama matokeo, ‘amani ya Mungu ipitayo akili zote inahifadhi mioyo na nia zao katika Kristo Yesu.’—Flp. 4:6, 7.
13. Ustahimilifu unaipasa nini, nao unaleta faida gani?
13 Ustahimilifu, jingine la matunda ya roho, haumaanishi ‘kutaabika kwa muda mrefu.” Kunapasa mtu kutokuwa mwepesi wa hasira nao huvumilia uchungu au makosa kwa subira, unashirikishwa na mtu kutokata tumaini kwamba mambo yatakuwa nafuu katika uhusiano usio mzuri. Yehova ‘si mwepesi wa hasira,’ na ni mwenye kustahimili. (Kut. 34:6) Subira ya Mungu huwapa watu muda wa kutubu na kuokoka uharibifu. (2 Pet. 3:8-18) Wakati Mungu anapoonyesha ustahimilivu, anawakusanya “watu kwa ajili ya jina lake” na kujipatia sifa duniani pote kupitia kwao. (Matendo 15:14; Rum. 9:22-24) Watu wa jina la Yehova wanajitahidi ‘kuwastahimili watu wote.’ (1 The. 5:14, NW) Si kwamba tu jambo hilo linasaidia kusitawisha uhusiano mwema na waamini wenzetu. Ustahimilivu unawawezesha Wakristo kuwasaidia wengine kwa subira wajifunze juu ya Yehova, ili wafanye mapenzi yake na kupata uzima wa milele. (1 Tim. 4:16; Ebr. 6:11-15) Vilevile, kwa kutembea kama anavyostahili Yehova hivyo, watu wa Mungu wanaridhika kwa kujua kwamba wanampendeza sasa, wakiwa na taraja la kupata baraka za milele.
14. Fadhili ni nini, nayo inaleta matokeo gani?
14 Fadhili ni tunda la roho ya Mungu vilevile. Inapasa kupendezwa na wengine na kuwatendea mambo. Yehova “huwafadhili wasiomshukuru na waovu,” akiwatia moyo watubu. (Luka 6:35, NW; Rum. 2:4) Kwa hiyo, wakiwa “waigaji wa Mungu,” Wakristo wanapaswa kujivika fadhili. (Efe. 5:1, NW; Kol. 3:12) Wanafuata shauri la Maandiko “iweni wafadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma, mkasemeheane” kama Mungu kupitia kwa Kristo alivyowasamehe. (Efe. 4:32) Fadhili hutokeza fadhili, nayo huvutia. Kwa hiyo, inamfaidi mwenye kuionyesha, mwenye kuipokea, pamoja na yeye anayevutwa kwa watu wa Mungu kwa sababu ya kuona fadhili ikitenda kazi kati yao.
15. Wema unaonyesha nini, nao unawezaje kusitawishwa?
15 Wema, tunda jingine la roho huonyesha ubora wa adili au usafi. “[Yehova] yu mwema mwenye adili.” (Zab. 25:8) Kama msaada wa kusitawisha wema, Wakristo watafanya vyema wakimwomba Mungu hivi: “Unifundishe [wema na] akili na maarifa, maana nimeyashika maagizo yako.” (Zab. 119:66) Vilevile, wema unasitawishwa kwa kutii amri za Yehova. Inaridhisha kujua kwamba mtu anamwiga Yehova kwa kuwaonyesha waamini wenzetu wema pamoja na wengine wote. Wema kama huo huenda ukawavuta watu kwenye Ukristo wa kweli.—Gal. 6:10.
16. (a) Imani inafafanuliwaje? (b) Tukilionyesha tunda hili la roho huenda kukawa na matokeo gani katika wengine?
16 Imani, tunda la saba la roho, ni la maana sana kwa wale wanaotaka ‘kutembea kama anavyostahili Yehova.’ Ni jambo lisilowezekana kuwa na urafiki wenye kuendelea pamoja na Yehova na kumpendeza Mungu pasipo sifa hii. (Ebr. 11:6) “Imani ni taraja lililohakikishwa la mambo yanayotumainiwa, onyesho dhahiri la mambo ya hakika ijapokuwa hayaonwi.” (Ebr.11:1, NW) Si tumaini tu lisilo na msingi, bali ni taraja lenye msingi mzuri. Zaidi ya hayo, imani ndiyo ushuhuda unaotakikana ili kuamini mambo ya hakika yasiyoonekana. Kwa mfano, vitu vilivyoumbwa kama vile jua, mwezi na nyota humhakikishia mtu mwenye kufikiri kwamba Mungu Muumba yupo. (Rum. 1:20-23; Ebr. 11:3) Mtu anapomwamini Yehova, anatoa mfano mzuri kwa Wakristo wenzake. Imani yao inaweza kutiwa nguvu wanapoona namna anavyomwamini Yehova sana. Nayo imani kama hiyo yenye matendo inaweza kuwasukuma wasioamini waanze kumtumaini Yehova Mungu.
17. Upole ni nini, nako kunakuwa na matokeo gani Wakati wale wanaomwiga Yehova wanapouonyesha?
17 Upole, tunda jingine la roho, laweza kuelezwa kuwa utulivu, neema yenye nguvu. Yesu Kristo alisema hivi: “Mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo.” (Mt. 11:29) Yehova ambaye ametoa njia ya kuweza kufikiwa kupitia kwa Kristo, ni mpole, si mkatili na mkali. Kwa hiyo, wale wanaotaka kutembea kama inavyostahili katika jina la Mungu hawana sababu ya kuogopa kumkaribia katika sala. (Ebr. 4:16; 1 Yohana 4:17, 18) Kama waigaji wa Yehova na Mwanawe, Wakristo wanaonyesha upole wanaposhughulika na wengine, nalo hili ni jambo lenye faida sana. Kati ya mambo mengine, “roho ya upole na utulivu” ya mke Mkristo inaweza kumvuta mume asiyeamini katika imani ya kweli. (1 Pet. 3:1-4) Vilevile, upole unastawisha uhusiano wenye furaha kati ya watu hata wakati kunapotokea magumu, kwa kuwa “jawabu la upole hugeuza hasira.”—Mit. 15:1.
18. Kujiweza kunapasa nini, nako kunaweza kuwa na matokeo gani?
18 Kujiweza, tunda la mwisho la roho linalotajwa, linapasa mtu azuie mwili wake, msemo na matendo. Yehova ‘aliendelea kujizuia’ mpaka wakati ufaao wa kuwaadhibu Wababeli waliouacha Yerusalemu ukiwa ukafika. (Isa. 42:14, 15) Kama “waigaji wa Mungu,” Wakristo wanajitahidi kujiweza katika mambo yote nao wanaweza kumwomba Yehova msaada katika kusitawisha sifa hii wakiwa na matumaini. (1 Kor. 9:25) Kujiweza ni baraka kwa yeye anayekuwa nako na kwa wote wanaoshirikiana naye. Kama vile matunda mengine ya roho, sifa hii inaweza kuwavuta watazamaji kwenye Ukristo.
ANAYOTAKA MUNGU
19. Yehova anataka kiasi gani kutoka kwetu?
19 Wale wanaoitwa kwa jina la Yehova wanaweza kumpendeza Mungu wakitafuta msaada wake katika kusitawisha matunda ya roho. Bila shaka, tukimtumaini Yehova kweli kweli kwa uongozi na kuona wajibu wetu mbele yake kwa uzito yeye atatutia nguvu tutembee katika njia yake. Paulo alisema hivi: “Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu.” (Flp. 4:13) Katika fadhili zake za upendo, Yehova anatusaidia sana naye anataka mambo machache sana kutoka kwetu. “Ee mwanadamu, yeye amekuonyesha yaliyo mema; na [Yehova] anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako”?—Mika 6:8.
20. Kwa sababu gani tunaweza kuwa na uhakika wa ulinzi na msaada wa Yehova?
20 Kwa kutenda haki, kupenda rehema na kwa kutembea kwa unyenyekevu na Yehova, hatuachwi bila ulinzi katika taratibu hii ya mambo yenye uadui. Hapana, maana tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova Mungu atatulinda na kutusaidia sisi tulio watu wake na kutuokoa tuingie katika taratibu yake mpya aliyoiahidi, tukiendelea kutembea kama anavyostahili. Kama nabii Samweli alivyosema wakati mmoja: “[Yehova] hatawaacha watu wake kwa ajili ya jina lake kuu; kwa kuwa imempendeza [Yehova] kuwafanya ninyi kuwa watu wake mwenyewe.”—1 Sam. 12:22.
21. Wale wanaotembea sasa kama inavyostahili katika jina la Yehova wana matazamio gani mbele yao?
21 Tukichukua daraka letu mbele za Mungu kwa uzito, tutembee kweli kweli kama inavyostahili katika jina la Yehova, yeye atakuwa pamoja nasi akiwa rafiki yetu. Kwa kweli, tukiendelea kupata na kutumia maarifa ya Neno lake aliloliongoza, Yehova hatatuacha. Tukiwa Mashahidi wake, sisi tumeazimia kwamba “tutakwenda kwa jina la [Yehova], Mungu wetu.” (Mika 4:5) Na tuishi kulingana na uamuzi huo. Kwa kufanya hivyo, tutakuwa na tazamio la ajabu la kutembea kama anavyostahili Yehova milele na milele. —Kutoka The Watchtower Aug. 15, 1978,