Mahubiri ya Mlimani—“Ufungapo, Jipake Mafuta Kichwani”
BAADA ya kuzungumza juu ya kuwapa misaada maskini na sala, Yesu alielekeza fikira kwenye sehemu kuu ya tatu ya ibada iliyozoewa na Wayahudi, yaani, kufunga. Walakini kabla ya kutaja yale ambayo Mwana wa Mungu alisema juu ya jambo hilo, ebu tufikirie habari fulani za msingi.
Kufunga hakukutajwa waziwazi katika sheria ya Mungu kupitia kwa Musa. Walakini Torati iliamuru kwamba katika Siku ya Upatanisho Waisraeli ‘wajitese,’ jambo linalofahamika kuwa lilimaanisha kufunga. (Law. 23:27; Hes. 29:7; tazama pia Mambo ya Walawi 16:29-31; linganisha Zaburi 35:13; Isaya 58:3, 5.) Ingawa huko ndiko kufunga kwa peke yake kwa watu wote kulikohitajiwa na torati ya Musa, Waisraeli waliadhimisha kwingine kwingi. Walifunga waziwazi katika sherehe za misiba ya taifa zima na nyakati za ukame, uchache wa mazao ya shamba, tauni na vita.—Zek. 7:5; 8:19.
Pamoja na hayo, kwa hiari, watu fulani walifunga wao wenyewe kwa kusudi la kupata kibali kutoka kwa Mungu au wakati wa kuomboleza. (2 Sam. 12:16) Kufunga kungeweza kuwa siku moja au kipindi kirefu zaidi. Mapokeo ya Kiyahudi yanataja kwamba kujiepusha kwenyewe na chakula kulitokea, si kwa kipindi kamili cha saa 24, bali wakati wa saa za mchana. Mara nyingi watu mmoja mmoja walifunga kwa hiari wakati wa hali zenye msiba.
Lakini Mafarisayo walikuwa tofauti. Kulingana na mfano wa Yesu, washiriki fulani wa jamii hiyo ya kidini walijiamulia wenyewe kufunga “mara mbili kwa juma.” (Luka 18:12) Siku za kawaida za kufunga huko zilikuwa Jumatatu na Alhamisi. Kwa wazi Mafarisayo waliamini kwamba kufunga kwa hiari kukifanywa kwa ukawaida kungeleta baraka kutoka kwa Mungu na kuondoa misiba ya taifa lote. Kama wonyesho wa kupita kiasi kwa wengine, kitabu Babylonian Talmud kinasimulia hivi juu ya rabi mmoja aliyeishi wakati wa karne ya kwanza W.K.
“R[abi] Zadoki aliadhimisha kufunga kwa miaka arobaini kusudi kwamba Yerusalemu usiharibiwe, [naye akakonda sana hata kwamba] alipokula kitu cho chote chakula hicho kingeonekana [kilipokuwa kikipita kooni mwake]. Alipotaka kujirudishia nguvu walikuwa wakimletea tini, naye alikuwa akifyonza maji [ya tunda hilo] na kutupa mabaki mengine.”
SHAURI LA YESU JUU YA KUFUNGA
Yesu alianza shauri lake juu ya kujiepusha na chakula kwa kusema hivi: “Tena mfungapo, msiwe kama wanafiki wenye uso wa kukunjamana; maana hujiumbua nyuso zao, ili waonekane na watu kuwa wanafunga.”—Mt. 6:16a.
Yesu hakuwaamuru wanafunzi wake wafunge, nao walijulikana kwamba hawakufanya hivyo kwa ukawaida wo wote. (Mt. 9:14, 15) Kwa upande mwingine, Mwana wa Mungu hakuwaagiza waepuke zoea hilo kabisa. Usemi, “mfungapo,” unaonyesha kwamba wengine wa wanafunzi wake walikuwa wakifunga katika pindi za pekee.—Tazama Matendo 13:2, 3; 14:23.
Walakini hawakupaswa ‘kujiumbua nyuso zao, ili waonekane na watu kuwa wanafunga.’ Wanafiki ambao Yesu aliwataja kwa makusudi walionekana na ‘nyuso zenye huzuni.’ Hawakujali sura za nyuso zao wakati wa siku za kufunga, yawezekana kwa kutonawa au kutotunza na kwa kunyunyiza majivu vichwani mwao. Kusudi lao la kweli la kufanya hivyo lilikuwa “ili waonekane na watu kuwa wanafunga.” Walifurahia kutazamwa na kusifiwa na watu, huku wakitikisa vichwa vyao kwa kukubali wonyesho wao wa nje wa utawa.
Kwa habari ya watu waliojionyesha katika kutoa misaada kwa maskini na kuomba waziwazi kusudi waonekane na wanadamu, Yesu alisema hivi juu ya wale waliofunga kwa sababu izo hizo: “Amin, nawaambia, wamekwisha kupata thawabu yao [kamili].” (Mt. 6:16b; linganisha 6:2, 5.) Mahali pa kupata baraka kutoka kwa Mungu, kusifiwa na wanadamu wenzao ndiko kulikokuwa “thawabu” yao yote. Ilipokelewa ‘kamili’ naye Mungu asingeiongezea kitu.
“Bali wewe ufungapo,” akaendelea Yesu, “jipake mafuta kichwani, unawe uso.” (Mt. 6:17) Kusugua mwili kwa mafuta na kuusafisha ni mambo yaliyofanywa kwa ukawaida na Wayahudi. Walakini, mapokeo ya Kiyahudi yalikataza kufanya hivyo wakati wa siku za kufunga za watu wote kama vile Siku ya Upatanisho na siku ya tisa ya mwezi wa tano, Abi (sherehe ya kuharibiwa kwa hekalu la Mungu katika Yerusalemu). Mafarisayo walijiamulia kutii makatazo kama hayo wakati wa kufunga kwa hiari mara mbili kwa juma. Hata hivyo, iwapo pindi ingetokea wakati wasikilizaji wa Yesu wangetaka kufunga, wangepaswa ‘kupaka mafuta vichwa vyao na kunawa nyuso zao,’ yaani, waonekane kama kawaida.
Sababu ya jambo hilo Yesu aliisema hivi: “Ili usionekane na watu kuwa unafunga, ila na Baba yako aliye sirini” (Mt. 16:18a) Wao wanapaswa kupendeza si watu, bali Mungu, aliye “sirini,” asiyeonekana na macho ya kibinadamu hata kidogo. Hivyo, kusingekuwa na uhitaji wa kutoa wonyesho wenye kuonekana wa kufunga.
Lakini Yesu alihakikisha kwamba ingawa huenda wanadamu wasione na kumsifu mtu aliyekataa kutoa wonyesho wa waziwazi wa kufunga, “Baba yako aonaye sirini ataku[lipa].” (Mt. 6:18b) Hakika Mungu ‘anaona,’ akiangalia namna watumishi wake wanavyoendeleza ibada yao. Lililo la maana kwa Mungu, si wonyesho wa nje wa vitendo vya utawa, bali unyofu wa moyo pamoja na vitendo vya fadhili za upendo kwa mwanadamu mwenzako. (1 Sam. 16:7; 1 Nya. 28:9) Kwa habari ya kufunga Isaya aliandika hivi:
“Fahamuni, siku ya kufunga kwenu mnatafuta anasa zenu wenyewe, na kuwalemea wote watendao kazi kwenu. Tazama, ninyi mwafunga mpate kushindana na kugombana, na kupiga kwa ngumi ya uovu [kwa ajili ya kuwa wenye kukasirika-kasirika kwa sababu ya njaa]. Hamfungi siku hii ya leo hata kuisikizisha sauti yenu juu. Je! kufunga namna hii ni saumu niliyoichagua mimi? Je! ni siku ya mtu kujitaabisha nafsi yake? Ni kuinama kichwa kama unyasi, na kutanda nguo za magunia na majivu chini yake? Je! utasema ni siku ya kufunga, na ya kukubaliwa na [Yehova]. Je! saumu niliyoichagua, siyo ya namna hii? kufungua vifungo vya uovu, kuzilegeza kamba za nira, kuwaacha huru walioonewa, na kwamba mvunje kila nira? Je! siyo kuwagawia wenye njaa chakula chako, na kuwaleta maskini waliotupwa nje nyumbani kwako? umwonapo mtu aliye uchi, umvike nguo; wala usijifiche na mtu mwenye damu moja nawe?—Isa. 58:3-7.
Yesu alihakikisha kwamba Mungu ‘angelipa’ wale ambao kufunga kwao kwa mara kwa mara kulikuwa na kusudi jema. Kulipwa huko kunazidi sana kitu cho chote ambacho wanadamu wanaweza kutoa. Kwa kweli, kwa hao wasikilizaji wa Mahubiri ya Mlimani, kulikuwa na nafasi ya kupata uzima wa kutokufa mbinguni kama sehemu ya ufalme wa Mungu wa Kimasihi.—Luka 22:28-30; Yohana 14:2-4; Ufu. 20:6.