Yehova Anataka Nini Kwako?
“Ee mwanadamu, yeye amekuonyesha yaliyo mema; na [Yehova] anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako”?—Mika 6:8.
1. Ulizo linalopatikana katika Mika 6:8 lilielekezwa kwa akina nani, na kwa sababu gani?
WATU wenye mioyo minyofu huenda wakauliza hivi: ‘Tunapaswa kufanya nini ili tumpendeze Mungu?’ Walakini, nabii wa Yehova Mungu hakuelekeza maneno hayo ya Mika 6:8 kwa watu kama hao wanyofu wanaomtafuta. Mahali pake, ulizo hilo lilielekezwa kwa watu ambao Mungu Mwenye Nguvu Zote alikuwa na kesi (mateta) nao. (Mika 6:1, 2) Watu hawa, Israeli, walikuwa wamedharau wajibu wa agano lao na Aliye Juu Zaidi. Matokeo yake yakawa kuharibika sana kwa adili. Kupunja, kuoneana, matendo yasiyo ya haki, ibada ya sanamu na umwagaji wa damu ulizidi sana. Hali ilikuwa mbaya sana hivi kwamba mtu hangeweza kuwatumaini rafiki zake wakubwa hata na washiriki wa jamaa.—Mika 1:5; 2:1, 2; 3:1-3; 6:12; 7:2-6.
2. Waisraeli walitolewa nafasi gani walipotangaziwa na Yehova kwamba alikuwa na kesi nao?
2 Hivyo, alipokuwa akitangaza kesi pamoja na watu wake wasioaminika, Yehova alikuwa akiwaomba watubu. Waisraeli walikuwa wakijulishwa kwamba wangeweza kuepuka hukumu mbaya kwa kuchukua hatua inayofaa ya kupata uhusiano unaokubalika na Mungu wao. Hili lingehitaji nini? Mambo yakuonekana tu ya ibada, kutia na kutoa dhabihu zilizo bora zaidi, hayakutosha. (Mika 6:6, 7) Unabii wa Mika ulitangaza hivi: “Ee mwanadamu, yeye amekuonyesha yaliyo mema; na [Yehova] anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako”?—Mika 6:8.
‘KUONYESHWA YALIYO MEMA’
3. Kupitia kwa Musa Waisraeli walikuwa wamefundishwa nini juu ya yaliyo mema?
3 Yehova Mungu hakuwa amewaacha watu wake gizani bila kuwajulisha yaliyo mema. Karne nyingi mbele, Musa alisema kwa Waisraeli hivi: “[Yehova], Mungu wako, anataka nini kwako, ila umche [Yehova], Mungu wako, na kwenda katika njia zake zote, na kumpenda, na kumtumikia [Yehova], Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote; kuzishika amri za [Yehova] na sheria zake, ninazokuamuru leo, upate [mema]?”—Kum. 10:12, 13.
4. Waisraeli wangefaidikaje kwa kumpenda Yehova na kuzitii amri zake?
4 “Israeli wangefaidika katika kila njia ikiwa wangempenda sana Yehova Mungu na kushika amri zake kwa ushikamanifu. Kutii sheria za Mungu kungewahakikishia ulinzi wake pamoja na baraka zake zenye kuendelea katika kila jambo walitendalo. (Kum. 28:1-13) Kwa upande mwingine, kudharau sheria za Mungu kungetokeza kukosa usalama pamoja na uharibifu.—Kum. 28:15-68.
5. Ni kwa sababu gani kumtii Yehova kunaongeza hali yetu njema?
5 Vivyo hivyo, leo, watu wanaompenda Mungu kikweli na wanaojaribu kufuata maongozi yake wanafuata mwendo unaowasaidia kupata yalio mema kabisa. Sababu gani iko hivyo? Kwa kuwa Yehova ana hekima yote na ni mwenye upendo, yeye ametoa amri zile zinazoweza kuongeza hali njema ya wanadamu peke yake. (Rum. 16:27; 1 Yohana 4:8; 5:3) Msingi hasa wa sheria zote za Mungu zinazoongoza uhusiano wa kibinadamu ni upendo. Mtume Paulo alikazia jambo hili alipoandika: “Musiwe na deni ya mutu, ila kupendana tu; kwa maana mwenye kupenda mutu mwingine ametimiza sheria. Maana yake, Usizini, Usiue, Usiibe, Usishuhudu uongo, Usitamani; na kama ikiwa amri nyingine yo yote, inamlika katika neno hili, Penda jirani yako kama wewe mwenyewe. Mapendo hayafanyii mwenzake neno baya; basi mapendo ni utimilifu wa sheria.” (Rom. 13:8-10, ZSB) Kwa wazi, kama wanadamu wote kila mahali wangeonyesha upendo wa jirani, kungekuwa na furaha, amani na usalama.
6. Sababu gani ni jambo linalofaa kabisa kumpenda Yehova na kutii amri zake?
6 Zaidi ya hayo, inafaa kabisa tuonyeshe kwamba tunampenda Mungu kwa kutii amri zake. (2 Yohana 6) “[Kwa njia] yake yeye tunaishi, tunakwenda, na kuwa na uhai wetu.” (Matendo 17:28) Kwa hiyo, maoni yetu yanapaswa yawe kama ya wale wazee 24 walioonwa na mtume Yohana katika njozi. Walipaza sauti na kusema: “Umestahili wewe, [Yehova] wetu na Mungu wetu, kuupokea utukufu na heshima na uweza; kwa kuwa wewe ndiwe uliyeviumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako, navyo vikaumbwa.”—Ufu. 4:11.
‘TENDA HAKI’
7. (a) Kwa habari ya haki ya hukumu, sheria ya Yehova iliwataka Waisraeli wafanye nini? (b) Kutenda haki ya hukumu kungaliwasaidiaje watu katika siku za Mika?
7 Kwa kuwa Yehova Mungu “huzipenda haki na hukumu,” yeye aliwataka Waisraeli wamwige katika jambo hilo. (Zab. 33:5) Sheria yake ilikataza kupokea rushwa (zawadi) na ikataka watu wote matajiri na maskini wapewe haki ya hukumu pasipo upendeleo. Tunasoma hivi: “Usipotoe maamuzi; wala usipendelee uso mtu; wala usitwae rushwa; kwa kuwa rushwa hupofusha macho ya wenye akili na kugeuza daawa ya wenye haki. Yaliyo haki kabisa ndiyo utakayoyafuata, ili upate kuishi.” (Kum. 16:19, 20) “Msitende yasiyo haki katika hukumu, usimpendelee mtu maskini, wala [kumheshimu] mwenye nguvu; bali utamhukumu jirani yako kwa haki.” (Law. 19:15) Bila shaka, kama Israeli wangekubali “kutenda haki” ya hukumu katika siku za Mika kama walivyosihiwa jambo hilo lingefanya mambo kuwa bora. Dhuluma ingezuiwa. Sheria na utengamano zingalirudishwa, kuwe na amani, salama na uthabiti.
8. (a) Ni wakati gani wazee Wakristo wanapohitajiwa waonyeshe haki ya hukumu, nao wanawezaje kufanya hivyo? (b) Haki ya hukumu inahusianaje na kutii onyo la upole linalopatikana katika 2 Wathesalonike 3:11-15?
8 Vivyo hivyo, Wakristo wameamriwa ‘watende haki’ ya hukumu. Wazee huenda wakahitaji kuamua kama ndugu fulani Mkristo anastahili kutumikia kama mtumishi wa huduma au mzee. Kufuata sana Neno la Mungu kwa ushikamanifu na kwa kutegemea sana uongozi wa roho yake ndipo tu wanapoweza kufanya jambo hilo pasipo upendeleo. Vilevile, huenda wakahitajiwa kufanya uamuzi juu ya waamini wanaofanya dhambi nzito. (1 Kor. 6:1-6; 1 Tim. 5:20-22, 24 25) Vivyo hivyo, Wakristo mmoja mmoja huenda wakahitajiwa kuamua kama mwenendo usiofaa wa watu wengine wanaoshirikiana na kundi unawafanya wawe mashirika mabaya. Kuhusu jambo hili, ili tutumie haki uamuzi kama huo unapaswa uwe msingi wake ni Neno la Mungu wala si uadui wa kibinafsi au maoni yasiyopatana na Maandiko. Kusudi la kuacha kushirikiana na waamini fulani katika mashirika yetu linapaswa liwe kuwasaidia kuona uhitaji wa kubadili njia zao. Haina maana kwamba tutakosa kuonyesha fadhili, ‘tukiwatendea kama adui.’ Watu kama hao wanapaswa kuendelea ‘kuonywa kama ndugu.’ (2 The. 3:11-15) Bila shaka, vilevile jambo hili husaidia wale wanaofuata shauri la Biblia wasiongozwe vibaya.—2 Tim. 2:20-22.
9. Kulingana na Yakobo 4:11, 12, Mkristo anawezaje kushindwa kumtendea haki ya hukumu mwamini mwenzake?
9 Walakini, ikiwa Wakristo wangehukumu matendo, makusudi au njia ya maisha ya mwamini mwenzao, kwa kutumia kanuni zao wenyewe, wakikukadiri kustahili kwa mtu isivyostahili, wangekuwa na hatia kubwa ya kushindwa kuonyesha haki ya hukumu. Ebu angalia alivyoandika mwanafunzi Yakobo: “Ndugu, msisingiziane; amsingiziaye ndugu yake, au kumhukumu ndugu yake, huisingizia sheria na kuihukumu sheria. Lakini ukiihukumu sheria, huwi mtenda sheria, bali umekuwa hakimu. Mtoa sheria na mwenye kuhukumu ni mmoja tu, ndiye awezaye kuokoa na kuangamiza. U nani wewe umhukumuye mtu mwingine?” (Yak. 4:11, 12) Watu wanaohukumu hivyo wanakuwa wakidharau sheria ya upendo iliyotolewa na Mungu, wakihukumu kwamba sheria hiyo ya upendo haiwahusu. (Mt. 22:36-39; linganisha 1 Yohana 3:16.) Kwa kufanya hivyo wanakuwa wakivunja kanuni ya Yehova ya haki, ambayo msingi wake ni upendo.
10. Sababu gani ni jambo lisilo la haki kuona kikundi fulani cha watu kuwa kinastahili zaidi kusikia “habari njema” kuliko kingine?
10 Kuongezea hayo, haingepatana na haki ikiwa Mkristo anaona kundi fulani la watu kuwa linastahili zaidi kusikia “habari njema” kuliko jingine. Yesu Kristo alikufa kwa ajili ya wanadamu wote, nayo mapenzi ya Mungu ni kwamba kusiwe na upendeleo wo wote katika kuutangaza ujumbe wa wokovu. (1 Tim. 2:3-6) Kwa hiyo, katika nchi ambako inawezekana kutembelea watu nyumbani kwao kuwapelekea ujumbe wa Biblia, bila shaka lingekuwa jambo linalopatana na roho ya kutopendelea ikiwa kila nyumba ingetembelewa. Ijapokuwa huenda vikundi fulani vya watu vikawa na nia zaidi ya kusikiliza, tunahitaji kujiangalia tusipatwe na hali ya kuonyesha upendeleo.—Linganisha Yakobo 2:1-9.
‘PENDA REHEMA’
11. Usemi “kupenda rehema” au fadhili una maana gani?
11 Waisraeli waliamuriwa ‘wapende rehema,’ licha ya kutenda haki. Usemi “kupenda rehema” unaweza vilevile kufasiriwa kama “kupenda fadhili za upendo,” au, “kupenda upendo mshikamanifu.” “Fadhili za upendo” kama hizo huonyeshwa kwa kuwahangaikia wengine kwa huruma. Ni fadhili inayojionyesha katika matendo. (Linganisha Ruthu 2:8-20; 3:10.) “Kupenda rehema” au fadhili kungekuwa na maana ya kufurahia kuonyesha fadhili, kuwasaidia wengine kwa furaha.
12. Ni jambo gani linaloonyesha kwamba Yesu Kristo ‘alipenda rehema’ kweli kweli?
12 Yesu Kristo aliweka mfano bora katika jambo hili. Hata alipokuwa amechoka na faragha yake kuingiliwa, yeye aliitikia kwa huruma akatosheleza mahitaji ya wananchi wenzake. Kuhusu pindi moja, Maandiko yanaripoti hivi: ‘“Akaenda [na mitume] faraghani rnpaka mji mmoja uitwao Bethsaida. Na makutano walipojua walimfuata; akawakaribisha, akawa akisema nao habari za ufalme wa Mungu, akawaponya wale wenye haja ya kuponywa.” (Luka 9:10, 11) Yesu alifurahia sana kuonyesha fadhili kama hizo.
13. Sisi tunawezaje kuonyesha leo kwamba ‘tunapenda rehema’?
13 Ikiwa wewe ni mwanafunzi wa Yesu Kristo, je! wewe ‘unapenda fadhili’? Je’ wewe unafanya raha na tamaa zako mwenyewe kuwa jambo la pili ili uweze kuwapa watu walio na uhitaji misaada ya mambo ya kimwili na ya kiroho kwa moyo wote? Kama Yesu, je’ wewe unaona huruma unapoona hali yenye kuhuzunisha ya kiroho ya wale wasioijua kweli? (Marko 6:34) Je! wewe unawafariji wengine kiroho, kutia na rafiki zako na washiriki wa jamaa yako? Je! wewe pia unachukua wakati kila mwezi ili ushiriki kwa kadiri fulani katika kazi ya kutoa ushuhuda hadharani? (Linganisha Ufunuo 22:1, 2, 17.) Unapowaona waamini wenzako au watu wengine wakiwa na uhitaji wa mambo ya kimwili kweli kweli, je! unasukumwa na huruma uwasaidie? (Mit. 3:27, 28; 2 Kor. 8:1-4; 9:6-12) Bila shaka, inapaswa iwe hivyo ikiwa kweli sisi ‘tunapenda fadhili.’
“KWENDA KWA UNYENYEKEVU NA MUNGU WAKO”
14. Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “unyenyekevu” linamaanisha nini?
14 Vilevile unabii wa Mika uliwatia moyo Waisraeli hivi: “Kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako.” Kwa kuwa neno la Kiebrania linalotafsiriwa “unyenyekevu” katika Mika 6:8 linaonekana hapa tu na katika Mithali 11:2, maana hasa ya neno hilo haifahamiki waziwazi. Baadaye maandishi ya Kiebrania yanaonyesha kwamba neno hili la Kiebrania huleta wazo la utakatifu na adabu. Tafsiri ya Kigiriki Septuagint Version na ya Kishamu hutoa wazo la kuwa “tayari” au kuwa na “uelekevu” wa kutembea au kwenda na Mungu. Kwa hiyo, mahali pa kuwa jambo la unyenyekevu tu, kwa wazi kwenda na Yehova kunatia ndani kuwa na hali inayofaa, isiyo ya kujitanguliza na isiyo ya kujitegemea mbele zake.
15. Kama inavyoonyeshwa katika habari ya Henoko na Nuhu, ni nini linalomaanishwa na ‘kwenda na Mungu’?
15 Usemi ‘kwenda na Mungu,’ unaonekana mapema katika maandishi ya Biblia. Kwa mfano, nabii Henoko na mzee wa ukoo Nuhu wanasemekana kwamba walikwenda na Mungu. Kwa habari ya Nuhu, tunasoma hivi: “Nuhu alikuwa mtu wa haki, mkamilifu katika vizazi vyake; Nuhu alikwenda pamoja na Mungu.” (Mwa. 5:24; 6:9) Henoko, vilevile, ‘alimpendeza Mungu.’ (Ebr. 11:5) Kwa hiyo, kwenda pamoja na Mungu kunahusu kujiendesha kama kwamba tuko mbele zake, tukijipatanisha na mapenzi yake. Wote wawili Henoko na Nuhu walifurahia uhusiano (urafiki) wa pekee pamoja na Yehova Mungu kwa sababu ya imani yao na mwenendo wao mnyofu.
16. (a) Ikiwa tutakuwa wanyenyekevu katika kutembea na Mungu, mwenendo wetu unapaswa kuwaje? (b) Mfano unaostahili sifa wa maisha ya Mkristo unaweza kuleta matokeo gani mema?
16 Ili Wakristo wawe katika hali inayofaa na waendelee kufurahia uhusiano (urafiki) wa karibu na Yehova Mungu, lazima wawe wanyenyekevu katika kuenenda pamoja naye, wakiendelea kuwa watakatifu, pasipo kujitanguliza na kuwa na adabu machoni pake. Maandiko yanashauri hivi: “Mwe na mwenendo mzuri kati ya Mataifa, ili, iwapo huwasingizia kuwa watenda mabaya, wayatazamapo matendo yenu mazuri, wamtukuze Mungu siku ya kujiliwa.” (1 Pet. 2:12) Ndiyo, mfano mzuri katika maisha ya Kikristo unakupa nguvu kuhubiri kwetu “habari njema.” Unahakikisha kwamba ibada ya kweli huwa na matokeo mema katika maisha ya watu na unaweza kuwanyamazisha wale wanaowasingizia wanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo. (1 Pet. 2:13-16) Kwa kweli, huenda wasingiziaji kama hao wa Wakristo wakaja kujua makosa ya mwendo wao, na baada ya muda kupita, wao wenyewe wakaja kuwa wasifaji wa Yehova Mungu.
17, 18. (a) Kama Inavyoonekana wazi kutokana na unabii wa Mika na Yakobo 1:22-25, Yehova anataka nini kwa wale wote ambao wangependeza machoni pake? (b) Jambo ilo hilo linaonyeshwaje na namna Henoko na Nuhu walivyotembea na Mungu?
17 Maneno yaliyoongozwa na Mungu ya unabii wa Mika yanahakikisha kwamba wale wanaotaka kumpendeza Yehova Mungu wanapaswa kuwa watendaji. Jambo ilo hilo linaonyeshwa na maneno ya mwanafunzi Yakobo: “Iweni watendaji wa neno, wala si wasikiaji tu hali mkijidanganya nafsi zenu. Kwa sababu mtu akiwa ni msikiaji wa neno tu, wala si mtendaji, mtu huyo ni kama mtu anayejiangalia uso wake katika kioo. Maana hujiangalia, kisha huenda zake, mara akasahau jinsi alivyo. Lakini aliyeitazama sheria kamilifu iliyo ya uhuru, na kukaa humo, asiwe msikiaji msahaulifu, bali mtendaji wa kazi, huyo atakuwa heri katika kutenda kwake.”—Yak. 1:22-25.
18 Haitoshi kusali tu, kusoma Biblia, kuhudhuria mikutano ya Wakristo na kusikiliza kwa heshima yanayosemwa humo. Maisha zetu lazima yaonyeshe kwamba sisi tunatenda haki, tunapenda fadhili (rehema), na kwamba tu wanyenyekevu katika kutembea na Yehova. Zaidi ya kutembea kwa ukamilifu pamoja na Aliye Juu Zaidi, Henoko na Nuhu walikuwa na matendo yenye juhudi. Henoko alitabiri kwa uhodari, akawaambia watu wasiomwogopa Mungu katika siku zake kwamba Yehova angefikiliza hukumu yake kupitia kwa maelfu ya malaika. (Yuda 14, 15) Nuhu hakushiriki tu katika kujenga safina ya kuokoa jamaa yake pamoja na namna mbalimbali za wanyama, bali pia alikuwa “muhubiri wa haki,” akatoa onyo juu ya maangamizi ambayo yangekuja juu ya watu wa kizazi chake.—2 Pet. 2:5, ZSB.
19. Ni maulizo gani tunayoweza kujiuliza sisi wenyewe ili tuweze kuamua kama tunaishi kulingana na Mika 6:8?
19 Bila shaka, wanafunzi wa Yesu Kristo hawataki kujidanganya wakifikiri kwamba kuwa na utu unaopendeza pamoja na kushiriki katika ibada ya watu wote kunatosha kumpa mtu kibali ya Yehova Mungu. Lazima matendo ya kuwahangaikia wanadamu wenzetu kwa huruma yaonekane wazi. Je! wewe unayaonyesha? Je! wewe unakuwa na nia na shauku ya kukubali kutosheleza mahitaji ya mambo ya kimwili na ya kiroho ya wengine, ukifanya hivyo pasipo upendeleo? Je! wewe unatii kwa bidii amri ya kuhubiri na kufanya wanafunzi? (Mt. 28:19, 20) Je! mwenendo wako kama mtumishi wa Mungu unastahili kuigwa? Ikiwa ndivyo, unaishi kulingana na maneno yaliyoandikwa kwa uongozi wa Mungu katika Mika 6:8.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Kutembelea kila nyumba tukiwa na “habari njema” huonyesha kwamba hatuna upendeleo
[Picha katika ukurasa wa 8]
Yesu alifurahia kuonyesha fadhili kwa kuwaponya wagonjwa
[Picha katika ukurasa wa 9]
Akiwa “Muhubiri wa haki,” Nuhu alitangulia kuonya juu ya Gharika iliyokuwa ikija