Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w79 5/1 kur. 3-7
  • Ukombozi! Kujifanya Wenyewe Kuwa Watu wa Kushukuru

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ukombozi! Kujifanya Wenyewe Kuwa Watu wa Kushukuru
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • BUCHENWALD
  • KUOKOKA MATESO YA CHAMA CHA NAZI
  • KUUNGANA TENA NA UVUMILIVU
  • “Ee, Yehova, Msaidie Msichana Wangu Mchanga Aendelee Kuwa Mwaminifu!”
    Amkeni!—1993
  • Kuendeleza Imani Pamoja na Mume Wangu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Kwa Msaada wa Yehova, Tuliokoka Serikali za Kimabavu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Ni Shangwe Kama Nini Kuketi Kwenye Meza Ya Yehova!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
w79 5/1 kur. 3-7

Ukombozi! Kujifanya Wenyewe Kuwa Watu wa Kushukuru

Kama ilivyosimuliwa na Max Liebster

NILIMLILIA Mungu wa Ibrahimu katika taabu yangu wakati, nikiwa mwenye umri wa miaka 24, nikaona nimenyimwa uhuru wangu kwa sababu tu ya kwamba mimi nilikuwa Myahudi. Nikiwa katika chumba changu katika gereza la Pfortzheim katika Black Forest, Ujeremani, nilijiuliza mwenyewe namna zote za maulizo juu ya kuuawa kwa taifa la Wayahudi, mauaji yaliyokuwa yakienea Ujeremani wote uliokuwa chini ya utawala wa chama cha Nazi.

Kisha ukafika mwezi Januari 1940. Wafungwa wenzangu na mimi tulipelekwa kwa garimoshi kwenye kambi ya mauaji ya Sachsenhausen-oranienburg. Tulifungiwa katika mabehewa yaliyogeuzwa kuwa vyumba vingi vilivyo vidogo sana vya kutosha watu wawili. Nilipoingizwa katika kimojawapo, nikamwona mfungwa mmoja ambaye macho yake yalionyesha hali ya utulivu. Alikuwa amefungwa kwa sababu aliheshimu sheria ya Mungu, akichagua kifungo na hata kifo badala ya kumwaga damu ya watu wengine. Alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Watoto wake walikuwa wameondolewa kwake, naye mke wake alikuwa ameuawa. Alikuwa akitazamia kushiriki yaliyompata mke wake.

Safari yenye siku 14 ilinipa majibu ya sala zangu, kwani ni wakati wa safari hiyo ya kuelekea kuuawa nilipolipata tumaini la uzima wa milele. Lakini niliokoka kama kwa mwujiza nisife! Wakati wa miaka mitano na miezi minne iliyofuata, niliokoka mateso ya kambi mbalimbali tano za mauaji, kutia na ile kambi mbaya sana ya Auschwitz katika Poland.

Kwa vile vyumba vyenye hewa ya sumu na tanuru za Auschwitz zilivyokuwa zikifanya kazi mchana na usiku; ziliua na kumaliza watu zaidi ya 10,000 kila siku! Inakadiriwa kwamba watu kufika 4,000000 au zaidi, wengi wao wakiwa Wayahudi waliuawa katika muda mfupi wa kuwapo kwa kambi hiyo ya mateso. Nilipofika katika Auschwitz mwaka wa 1943, ilikuwa imekwisha anza kutumiwa kuwa kambi ya mauaji.

Zilikuwako kambi za kazi 30 zilizokuwa zikitumiwa kwa kusimamiwa na kambi kubwa ya Auschwitz. Siku fulani wakati wafungwa walipofika, makachero (polisi wa chama cha Nazi) walichagua vijana ili wajazie tena kambi hizo wafungwa. Mimi nilichaguliwa nikatumwa Buna mahali kilipokuwa kikijengwa kiwanda cha kufanyizia mipira. Katika kambi hiyo ya kazi, kila asubuhi wale walioshindwa kufanya kazi walipelekwa kwenye vyumba vyenye hewa ya sumu wakauawe huko.

BUCHENWALD

Mwishowe, katika Januari 1945 nikapelekwa Buchenwald, kambi iliyokuwa msituni mwendo wa maili tatu (kilometres 5) upande wa magharibi-kaskazini ya Weimar, Ujeremani. Wakati askari jeshi wa Kiamerika walipokaribia, mkuu wa kambi aliamua kuwaangamiza Wayahudi wote. Walikuwa wamekusudiwa kusafirishwa kwa njia ya reli mpaka kwenye kaburi la umati wa watu, kisha wapigwe risasi wafe, wakiisha kuchimba kaburi hilo la jumla. Katika msafara wangu wenye walinzi, alikuwako Myahudi mwingine jina lake Heikorn, aliyekuwa amepokea kweli za Biblia zinazofundishwa na Mashahidi wa Yehova wakati alipokuwa katika Buchenwald.

Katika msukosuko uliotokea katika jukwaa ya kituo cha garimoshi, tulikwenda nyuma ya chungu ya kuni ili tusome na kutafakari (kufikiria) kurasa chache za kitabu cha Biblia cha Ufunuo alizokuwa nazo Heikorn. Halafu, kwa sababu ya haraka-haraka iliyokuwako, askari wetu walinzi wakatusahau! Ilikuwa ajabu!

Tukashinda hapo mpaka kucha. Kisha kwa ghafula ukatolewa mwito katika kipaza-sauti: ‘Mashahidi wa Yehova wote nendeni kwenye Nyumba Na. 1.’ Tukatii mwito huo, na tulipofika huko tulikuta Mashahidi 180. Siku chache baadaye tukaokolewa na majeshi ya Waamerika.

Ukombozi! Lo! tulifurahi kama nini kwa vile tulivyokombolewa! Saa hizo wakati wa kukombolewa kwetu zilikuwa saa za kukumbukwa kweli kweli. Consolation (Faraja), lililokuwa jina la zamani la gazeti linaloitwa sasa Amkeni!, linaeleza hivi katika toleo lake la Desemba 19, 1945:

“Katika Aprili 12, wakati kambi ya Buchenwald ilipotekwa, walikutwa wafungwa elfu 20 au 30 tu, wakiwa kama wafu kwa sababu ya kuteswa na njaa. Wakati wa kuingia katika kambi hiyo, jambo lililokuwa lenye kuchukiza sana hata askari wajeuri ni zile maiti lilizolundikwa kama kuni nje ya nyumba za kambi. Ndani ya vibanda hivyo vya miti mlikuwamo rafu, si vitanda, ilipolazwa miili iliyokonda ya wale waliokuwa bado wanaweza kupumua kidogo. Nyuso na miili yao ilikuwa imefinyana-finyana na kukauka, na wengi wao walikuwa dhaifu mno wasiweze lo lote zaidi ya kupindua-pindua macho yao tu. Hao walikuwa wamepata mateso ya ujeuri sana kuliko mateso yote. Harold Denny, mleta habari za gazeti la New,York Times, anasema kwamba ‘aliambiwa habari za adhabu zilizotolewa na askari wa ulinzi, ambazo ni mbaya sana na za kuchukiza mno hata sikuweza kuzisimulia isipokuwa kuwanong’onezea watu wengine.’”

Afya yangu iliharibika daima, lakini nilishukuru kwa vile niko hai. Yale mateso ya muda mrefu katika kila kambi ya mauaji yalinitia nguvu nishikamane na azimio langu nililofanya pale mwanzoni. Wakati huo nilikuwa nimeazimia hivi: ‘Mungu akinitoa katika tundu hili la simba, nitamtumikia yeye peke yake.’ Basi mara tulipokwisha kukombolewa, nikabatizwa pamoja na Fritz Heikorn tukiwa bado huko Buchenwald. Tangu wakati huo nimejaribu sana nionekane mwaminifu kwa Yehova. Tangu nilipooa mwaka 1956, nimeshiriki azimio hilo pamoja na Simone mke wangu.

KUOKOKA MATESO YA CHAMA CHA NAZI

Simone alizaliwa katika jimbo la Alsace, sehemu ya mashariki ya Ufaransa karibu na mpaka wa Ujeremani. Wazazi wake wakawa Mashahidi wa Yehova upesi kabla ya kupigwa marufuku kwa kazi ya kuhubiri huko katika mwaka 1939. Simone alibatizwa na baba yake, Adolphe, mwaka 1941, wakati alipokuwa mwenye umri wa miaka 11 tu. Wakati uliofuata, katika Septemba 4, 1941, baba yake alikamatwa na askari polisi wapelelezi mahali alipokuwa akifanya kazi, na tangu wakati huo hakuonwa tena na jamaa yake mpaka ilipokwisha karibu miaka minne, katika mwaka 1945.

Adolphe alivumilia namna zote za majaribu wakati wa kuwekwa katika kizuizi. Kwa mfano, aliambiwa kwamba ikiwa anatia sahihi yake katika barua, kuonyesha kwamba ameikana imani yake angepewa kazi bora ya kuchora ramani za nyumba, naye mke wake na binti yake wangerudishwa kwake. Lakini kama angekataa, mke wake angekamatwa na binti yake apelekwe kwenye shule ya kufundishia tabia njema. Baadaye, alipigwa kijeuri sana mpaka akapoteza fahamu na ikachukua saa nyingi apate fahamu tena.

Simone na Emma, mama yake, hawakukamatwa mara hiyo, nao waliendesha kazi ya kuhubiri kwa njia ya siri. Emma alinieleza hivi: “Nikiwa pamoja na Ndugu , Koehl, tulikuwa tukichukua Mnara wa Mlinzi katika mpaka mpya kati ya Alsace na sehemu nyingine ya Ufaransa. Ndipo ulipotafsiriwa katika Kijeremani kisha kunakiliwa. Katika njia hiyo, ndugu wasemao Kijeremani katika Alsace na katika Freiburg, huko Ujeremani, walipokea chakula cha kiroho.”

Akiisha kuwekwa kwa muda mfupi kifungoni katika Mulhouse, Adolphe alipelekwa kwenye kambi ya mateso ya Schirmeck katika Alsace kuelekea mwisho wa mwaka 1941. Kisha akapelekwa Dachau, ambayo ni kambi ya mateso iliyo mbaya sana, karibu na Munich, Ujeremani. Kuanzia mwaka 1943 hali ya wafungwa wote katika Dachau ikawa afadhali kidogo, nao wakaruhusiwa kupokea vifurushi vya chakula.

Wakati fulani Adolphe aliniambia hivi: “Siku moja nilikuwa nikila keki ndogo ambazo Emma alinipelekea. Nikaona kwamba zilikuwa tofauti sana. Mara nikafahamu kwamba kumbe nilikuwa nikitafuna karatasi; ujumbe ulifichwa katika keki hizo!”

Emma alingojea kwa uvumilivu apokee barua ambayo Adolphe alikuwa akimwandikia mara tatu, bila kuzidi mistari 12. Lo! alitulizwa wasiwasi wake na kufurahi kama nini, aliposikia kwamba alikuwa amepokea “vitamini”!

Adolphe alisema kwamba iliwezekana aokoke kwa sababu hali ya Mashahidi wa Yehova ilianza kuwa afadhali. Lakini baada ya hapo akashtushwa tena. Akapokea habari kwamba Simone na Emma wamekamatwa. Akaniambia: “Nilihangaika sana. Halafu siku moja nilipokuwa katika mstari wa kwenda kujinyunyizia maji, nikasikia sauti ikitaja Mithali 3:5, 6, andiko linalosema: ‘Mtumaini [Yehova] kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.’ Ilivuma kama sauti inayotoka mbinguni. Ndilo jambo nililokuwa nikihitaji ili nipate tena imara.” Kwa kweli, sauti hiyo ilikuwa sauti ya mfungwa mwingine aliyekuwa akitumia andiko hilo.

Ajapokuwa bado ni kijana sana, Simone alipaswa vilevile akutane na majaribu makali. Alifukuzwa katika shule kubwa kwa sababu alishikamana na kanuni za Kikristo. Alihojiwa (aliulizwa-ulizwa sana) na huku taa zenye kupofusha zikiwa zinawaka. “Wachunguzi wa akili” wawili wakajaribu kuchunguza ili wajue mahali ambako Mnara wa Mlinzi ulikuwa ukitoka na mahali ilikofichwa mashine ya kuchapia. Yeye alijua habari zote hizo, basi akasali sana na kumwomba Yehova amsaidie ili asije akawa mhaini. Alipokuwa karibu na kushindwa, mlio mkali wa simu ukakatiza kwa ghafula kuhojiwa huko.

Mwishowe, katika Julai 9, 1943, Simone alikamatwa na wafanya kazi wawili wenye kushughulika na utabibu wa jamii, akapelekwa kwenye shule ya kufundishia tabia njema ya Kinazi huko Wessenberg, katika Constance, Ujeremani. Emma, mama yake aliweza kupanda garimoshi lile lile alilosafiri nalo apate kumsindikiza. Lakini baadaye, katika Septemba 1943, yeye mama vilevile, akakamatwa.

Emma aliwekwa katika kambi ya mateso ya Schirmeck, katika Alsace. Alipofika huko, aliamriwa kutengeneza mavazi ya wanajeshi, akakataa. Aliwekwa katika kizuizi cha upweke katika chumba cha chini ya ardhi cha gereza kwa muda wa miezi saba. Alikuwa amefunguliwa kitambo kidogo tu ili aje atolee wafungwa wengine ushuhuda, kisha akarudishwa huko. Alikaa katika mahali hapo pabaya sana muda wa miezi mingine mitatu. Lakini aliendelea kuwa imara katika imani katika majaribu yote hayo.

Wakati uo huo, Eugenie, dada ya Emma aliendelea bila kukamatwa. Naye alifanya bidii sana kusaidia washiriki wengine wa jamaa kwa hatari ya uhai wake. Aliniambia hivi: “Lilikuwa pendeleo kuchukua kazi ya kupeleka vifurushi vya chakula vyenye habari fupi za Mnara wa Mlinzi katika Dachau, na kumtembelea Simone mara moja kwa mwezi katika Ujeremani. Wakuu wa shule ya kufundishia tabia njema walikuwa wamenitumaini. Kwa hiyo nikaruhusiwa kumchukua Simone aende nami katika matembezi. Jambo hilo lilinipa nafasi ya kujifunza Mnara wa Mlinzi pamoja naye. Inaonekana kama wenye mamlaka walipofushwa na Yehova, maana hawakujua kabisa kwamba ninashirikiana na Mashahidi wa Yehova. Niliweza kumtembelea Simone mara 13 katika muda wa miezi 22 ya kuwekwa kwake katika kizuizi. Nami nilimpelekea Emma habari gerezani juu ya hali ya binti yake.”

Mwishowe Adolphe alihamishwa akapelekwa kwenye kambi ya mateso ya Mauthausen, katika Austria. Kisha katika majira ya baridi ya miaka 1944 na 1945 akapelekwa Mauthausen-Ebensee. Jambo hilo likamaanisha kuacha kupashana habari na jamaa yake kutoka nje. Kwa habari hiyo, Simone anaeleza hivi:

“Sikuhuzunika wakati jamaa yetu ilipotenganishwa. Nilizidi kukaza macho yangu juu ya mfano wa ukamilifu uliowekwa na wazazi wangu. Mara nyingi niliyakumbuka maneno ya mama yangu, akiniambia: ‘Kujaribiwa kwa imani yetu ni pendeleo na ni mazoezi mazuri.’ Sikupata kuwaona wazazi wangu wakivunjika moyo wakati wo wote wa majaribu yao wala kumwona mama akilia. Ilipokuwa lazima kila mara nionekane mbele ya wenye mamlaka, nilikumbuka kwamba Wakristo wanaoteswa ni tamasha kwa wale walio nje. Ilikuwa kana kwamba niliweza kuwaona malaika wakinitia moyo. Kabla ya kumwacha mama, tulisali pamoja, kisha tukaimba wimbo wa kumsifu Yehova. Nikapata kujua sana kwamba mkono wenye nguvu wa Yehova uko juu yangu.

“Nikiwa peke yangu katika hali ya kudhulumiwa iliyokuwa katika shule ya kufundishia tabia njema, nilijifunza kutembea pamoja na Mungu kama tegemeo langu la pekee. Na nilipokuwa nikisali, nilifikiria vilevile sala za wazazi wangu zikipanda kwenye mbingu, nami nikaona kana kwamba sote tulikuwa tukitoa sala moja. Kisha nikajisikia kuchangamka kama wakati wa miaka yangu ya mapema, nilipokuwa nikikaa katika mapaja ya baba au nikijipasha moto karibu na mama yangu. Tangu wakati huo miaka imepita, lakini Yehova habadiliki hata kidogo. Yeye ni Mungu wa wokovu.”

KUUNGANA TENA NA UVUMILIVU

Kuungana tena kwa Simone na jamaa yake wakati wa kumalizika kwa vita, kulifurahisha kweli kweli. Kulitokea katika nyumba yao ya orofa katika Mulhouse. Nyumba hiyo ilikuwa imekaa bila kuharibiwa ijapokuwa kando zake zote zilikuwa magofu na mahame tupu.

Emma aliniambia hivi: “Shukrani inayojaa mioyo yetu kwa sababu ya ukombozi ambao hatukutazamia, zilisahaulisha hata mateso tuliyopata. Kwa vile tulivyokuwa tumepata sasa uhuru mpya wa kuhubiri ‘habari njema,’ tulijiona kana kwamba tulikuwa tukitembea​—⁠au tukipanda baisikeli​—⁠hewani, maana haikuwa ajabu kwetu kuendesha baisikeli mwendo wa zaidi ya maili 37 (kilometres 60) ili tutafute ‘kondoo’ za Yehova. Tulipungukiwa mambo ya lazima ya maisha, lakini ndugu zetu wenye upendo katika United States, walitupatia mavazi na msaada mwingine wa kimwili kupitia kwa Sosaiti. Jambo hilo likatuonyesha jinsi tengenezo la Yehova linavyotuangalia, kama mama anavyoangalia watoto wake.”

Mara walipokombolewa, Simone alipokuwa mwenye umri wa miaka 17 tu, alikataa kazi bora ya kuwa mchoraji wa ramani za ujenzi wa nyumba pamoja na baba yake, naye alifanya hivyo ili awe painia. Basi ulikuwa muda mfupi sana baada ya kuungana tena kwa jamaa hiyo kwamba tena Simone akaenda kwenye mgawo wa kuhubiri. Lo! jinsi ninavyofurahia bidii yake ya Kikristo, maana, kwa kufanya hivyo, alikaribishwa kwenye shule ya Gileadi katika mwaka 1952 na nikaweza kukutana naye na kumwoa!

Jamaa yetu imebarikiwa sana. Tumeweza kusaidia watu zaidi ya 250 waje upande wa Yehova. Wengine kati ya hao ni wazee sasa, na wengine wanatumikia katika makao ya Betheli, wengine ni waangalizi wa mizunguko, mapainia na wamisionari. Basi, pamoja na wengine wengi walio katika ulimwengu, tunaweza kusema tena maneno haya ya mtunga zaburi ya Biblia: “Nitamhimidi [Yehova] kila wakati . . . akaniponya na hofu zangu zote. . . . Mtukuzeni [Yehova] pamoja nami, na tuliadhimishe jina lake pamoja.”​—⁠Zab. 34:​1, 4, 3.

[Picha of Max Liebster katika ukurasa wa 4]

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki