Mahubiri ya Mlimani—“Msihukumu”
KUFUATIA shauri lake juu ya uhitaji wa kutafuta ufalme wa Mungu kwanza, Yesu aliwaonya wasikilizaji wake kwa upole waepukane na zoea lenye kuumiza sana. Yeye alisema hivi: “Msihukumu, msije mkahukumiwa.” (Mt. 7:1) Kulingana na Luka, Yesu aliongeza hivi: “Msihukumu, nanyi hamtahukumiwa; msilaumu, nanyi hamtalaumiwa; achilieni, nanyi mtaachiliwa. Wapeni watu vitu, nanyi mtapewa; kipimo cha kujaa na kushindiiliwa, na kusukwa-sukwa hata kumwagika.”—Luka 6:37, 38.
Wakati wa karne ya kwanza W.K., Mafarisayo walikuwa na maelekeo ya kuhukumu wengine vikali kwa kulingana na kanuni za uongo za mapokeo yasiyo ya Kibiblia. Wo wote wa wasikilizaji wa Yesu waliokuwa na zoea hilo walipaswa ‘kuliacha’ (NW) Mahali pa kuona makosa ya wengine wakati wote, wangepaswa ‘kuachilia,’ yaani, kusamehe na kusahau makosa ya wanadamu wenzao. (Linganisha Luka 6:37, Authorized Version.) Kwa kufanya hivyo, wangewafanya wengine wawe na nia iyo hiyo ya kusamehe.
Zaidi ya kusamehe wengine na kuwatendea kwa rehema, wanafunzi wa Yesu wangepaswa ‘kupeana vitu.’ Jambo hilo lingetokezea wanafunzi hao kupokea mapajani mwao “kipimo cha kujaa na kushindiliwa, na kusukwa-sukwa hata kumwagika.” Kulingana na kitabu Word Studies in the New Testament, neno linalotafsiriwa Kigiriki “mapaja” linamaanisha “mkunjo uliowekwa pamoja wa vazi pana la upande wa juu, lililofungaminshwa pamoja na mshipi, na hivyo kufanyiza kifuko. Katika masoko ya Mashariki (Asia) leo wauzaji wanaweza kuonekana wakimwaga vitu vingi kwenye kifua cha mnunuaji.” (Linganisha Ruthu 3:15; Isaya 65:7; Yeremia 32:18.) Kadiri mtu anavyokuwa mkarimu zaidi, ndivyo anavyowatia wengine moyo watende kwa namna hiyo.
Akitaja kanuni ya muhimu kwa wote, Yesu alisema hivi: “Kwa kuwa hukumu ile mhukumuyo, ndiyo mtakayohukumiwa; na kipimo kile [njia ya kutendea watu] mpimiacho, ndicho mtakachopimiwa.” (Mt. 7:2) Kwa habari ya kutendea kwao wengine, watu ‘huvuna wapandacho.’ Jambo hilo linakuwa hivyo, si kwa yale tu wanayovuna kutoka kwa wanadamu wenzao, bali, lililo la muhimu zaidi, yale wanayovuna kutoka kwa Mungu.—Tazama Mathayo 5:7; 6:14, 15.
Ili kukazia hatari ya kuiga Mafarisayo wenye kulaumu kupita kiasi, Yesu alitoa mfano wenye sehemu mbili: “Je aliye kipofu aweza kuongoza kipofu? Hawatatumbukia shimoni wote wawili? Mwanafunzi hawi mkuu kuliko mwalimu wake, lakini kila mtu ambaye amehitimu hulingana na mwalimu wake.”—Luka 6:39, 40.
Ungekuwa upuzi kwa mtu aliye kipofu kwa halisi kujaribu kuongoza kipofu mwingine katika nchi asiyofahamiana nayo. Iwapo kungekuwako shimo njiani, kwa hakika wote wangetumbukia. Kwa habari ya kuwahukumu wanadamu wenzao, viongozi wa kidini Wayahudi walikuwa ‘vipofu’ kwa mfano. (Linganisha Mathayo 15:14; 23:16, 24.) Walikataa kuona sifa njema katika watu maskini wa kawaida. Katika pindi moja Mafarisayo walitamka hivi: “Makutano hawa wasioifahamu torati wamelaaniwa.” (Yohana 7:49) Mtu ye yote anayeiga nia hiyo ya kulaumu anaelekea kutumbukia ndani ya shimo lenye hatari.
Vilevile, kama vile “mwanafunzi” anayetwaa njia za kuwaza za mwalimu wake anavyokuwa kama “mwalimu wake,” ndivyo wote waliokuwa wakiwaiga Mafarisayo wangekuwa kama wao—wasio na kibali ya Mungu na wakiwa katika hatari ya kupoteza maisha zao, Kwa hiyo, Yesu alisema hivi katika pindi nyingine:
“Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! kwa kuwa mnawafungia watu ufalme wa mbinguni; ninyi wenyewe hamwingii, wala wanaoingia hamwaachi waingie. Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! kwa kuwa mnazunguka katika bahari na nchi kavu ili kumfanya mtu mmoja kuwa mwongofu; na akiisha kufanyika, mnamfanya kuwa mwana wa jehanum [uharibifu wa milele] mara mbili zaidi kuliko ninyi wenyewe.”—Mt. 23:13-15.
Akiutaja upumbavu wa kulaumu kupita kiasi, Yesu aliuliza hivi: “Basi, mbona wakitazama kibanzi kilicho ndani ya jicho la ndugu yako, na boriti iliyo ndani ya jicho lako mwenyewe huiangalii? Au utamwambiaje nduguyo, Niache nikitoe kibanzi katika jicho lako; na kumbe! mna boriti ndani ya jicho lako mwenyewe?”—Mt. 7:3, 4; linganisha Luka 6:41, 42a.
Yesu hazungumzi tu juu ya watu mmoja mmoja wanaoangalia makosa ya wengine huku wao wakiwa na makubwa zaidi, ingawa huo ni udhaifu wa kawaida wa wanadamu. Mahali pake, yeye anazungumza juu ya mtu anayeona kosa dogo ndani ya “jicho” la ndugu yake. Mwenye kulaumu angedai kwamba nduguye ameharibu uwezo wa adili wa kufahamu na kuamua. Hata kama kosa hilo lingekuwa dogo, kama vile “kibanzi,” kijiti au chembe ya vumbi, yule mwenye kulaumu angelifanya liwe kubwa na kwa unafiki ajitoe ‘kukiondoa kibanzi’ yaani, kumsaidia mtu huyo ayaone mambo vizuri zaidi, kumwezesha kutoa uamuzi wenye kukubalika zaidi.
Viongozi wa kidini Wayahudi sana sana walikuwa na maelekeo ya kulaumu uamuzi wa wengine. Kwa mfano, wakati mtu mmoja ambaye Yesu alikuwa amemponya upofu aliozaliwa nao, alipotangaza kwamba bila shaka Yesu alikuwa ametoka kwa Mungu, Mafarisayo walijibu vikali hivi: “Ama! wewe ulizaliwa katika dhambi tupu, nawe unatufundisha sisi?” (Yohana 9:34) Hata hivyo, kwa habari ya kuona mambo waziwazi kiroho na kuweza kuamua, Mafarisayo walikuwa na “boriti” ndani ya macho yao. Walikuwa vipofu kabisa.
Kwa hiyo, Yesu alitangaza hivi: “Mnafiki wewe, itoe kwanza ile boriti katika jicho lako mwenyewe; ndipo utakapoona vema kukitoa kile kibanzi katika jicho la ndugu yako.”—Mt. 7:5; Luka 6:42b.
Je! hiyo ilimaanisha kwamba wanafunzi wa Yesu hawangepaswa kutumia ufahamu hata kidogo kuhusiana na watu wengine? Sivyo, kwa kuwa kufuatia hilo Yesu alisema hivi: “Msiwape mbwa kilicho kitakatifu, wala msitupe lulu zenu mbele ya nguruwe, wasije wakazikanyaga chini ya miguu yao, wakageuka na kuwararua.”—Mt. 7:6.
Kulingana na Torati ya Musa, mbwa na nguruwe walikuwa wachafu. (Law. 11:7, 27) Lilikuwa jambo lenye kukubalika kumtupia mbwa nyama ya mnyama aliyeraruliwa na mnyama-mwitu. (Kut. 22:31) Walakini mapokeo ya Kiyahudi yalikataza kuwapa mbwa nyama “takatifu,” yaani, nyama ya dhabihu za wanyama. Kitabu The Mishnah chasema hivi: “Matoleo ya wanyama [Kiebrania, qodashim: “vitu vitakatifu”] hayawezi kukombolewa ili yapewe mbwa kama chakula.” Kutupia “nguruwe” lulu lingekuwa jambo jingine lisilofaa. Inaelekea kwamba nguruwe angekosea na kufikiri kuwa ni mbaazi; mbegu au vitu vinginevyo wanavyokula. Wakiona kwamba haziliki, nguruwe wangezikanyagia chini na kwa kughadhibika, wangeweza kumwumiza aliyetupa lulu hizo.
Kwa njia ya mfano, “kilicho kitakatifu” na “lulu” maana yake ni kweli za Kimaandiko zenye thamani kuhusiana na ufalme wa Mungu wa Kimasihi. Wanafunzi wa Yesu wangepaswa kuzishiriki kweli hizo na kila mtu. (Mt. 24:14, NW; 28:19, 20, NW) Walakini watu mmoja mmoja wakijionyesha kwamba hawakuthamini mambo ya kiroho, kama vile mbwa au nguruwe, Wakristo wangetafuta watu wenye kuitikia zaidi.—Tazama Mathayo 10:14; Luka 9:5; 10:11; Matendo 13:45, 46; 18:6.