Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w80 9/1 kur. 16-18
  • Mahubiri ya Mlimani—“Endeleeni Kuomba”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mahubiri ya Mlimani—“Endeleeni Kuomba”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Habari Zinazolingana
  • Je, Unasali Kupatana na Maneno ya Yesu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • Mhofu Yehova, Msikiaji wa Sala
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Ile Kanuni ya Kidhahabu Ni Nini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Yehova Anawapa “Roho Takatifu Wale Wanaomwomba”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
w80 9/1 kur. 16-18

Mahubiri ya Mlimani​—“Endeleeni Kuomba”

BAADA ya kuwashauri wasikilizaji wake waepuke kuhukumu wanadamu wenzao vibaya, Yesu alisema hivi: “Endeleeni kuomba, nanyi mtapewa; endeleeni kutafuta, nanyi mtapata; endeleeni kubisha, nanyi mtafunguliwa.”​—Mt. 7:7, NWa

Mwana wa Mungu aliwasihi wanafunzi wake wadumu katika sala kwa maneno hayo. Kulikuwa na uhitaji wenye uharaka wa jambo hilo. Mahubiri ya Mlimani yalikuwa yameonyesha wazi kwamba haki machoni pa Mungu halikuwa jambo la kutenda vitendo vya kidini na vya huruma peke yake. (Mt. 5:20; 6:1) Ili yawe na maana, matendo ya ibada yapaswa kutokana na makusudi yanayofaa ya moyoni, kutia ndani kusamehe, usafi, ukweli na upendo. (Mt. 5:22, 27, 28, 33-37, 43-48) Kwa kuwa sifa hizo zinapingana na asili ya wanadamu yenye dhambi, wanafunzi hao wangepaswa kumwomba Mungu kwa ukawaida awape msaada ili kutimiza matakwa yake ya ibada ya kweli.

Kwa hiyo, walipaswa ‘kuendelea kuomba’ nguvu na hekima yenye kuhitajiwa ili kuishi maisha ya utawa. (2 Kor. 4:7; 2 Pet. 1:3) Wangepaswa ‘kuendelea kutafuta’ kama vile wangeendelea kutafuta hazina iliyofichwa. (Linganisha Mathayo 13:44.) Wangepaswa ‘kuendelea kubisha’ ili wapate kukubaliwa kabisa kwenye baraka ambazo Mungu amewekea wale wanaopata kibali yake.​—Tazama Luka 13:24, 25.

Watu ambao huomba baraka hizo kwa bidii na kufanya kazi kwa kupatana na sala zao wanaweza kupata kitiamoyo kutokana na maneno ya Yesu yaliyofuata: “Kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye atafunguliwa.” (Mt. 7:8) Hiyo haimaanishi kwamba watu wanaweza kuomba kitu cho chote wanachotaka na kupata jibu. Sala inayofaa wakati wote inapaswa kupatana na mapenzi ya Mungu. (1 Yohana 5:14) Hata hivyo, wanafunzi wa Yesu wangeweza kuwa na hakika kwamba Mungu angejibu sala zao za kutaka msaada wa kuendeleza ibada ya kweli.

Kwa habari hiyo, Mwana wa Mungu alitoa mfano: “Au kuna mtu yupi kwenu, ambaye, mwanawe akimwomba mkate, atampa jiwe? Au akiomba samaki, atampa nyoka?”​—Mt. 7:9, 10.

Katika Palestina, wakati wa karne ya kwanza W.K., mkate ulikuwa ukiokwa kwa namna ya keki pana-pana zilizofanana na mawe fulani. Vijoka fulani vidogo vilifanana na samaki ambao wakati mwingi walikuwa wakiliwa pamoja na mkate. (Angalia Yohana 6:9.) Iwapo kijana angemwomba babaye mkate, mzazi huyo asingemdanganya na kumwudhi mzao wake kwa kumpa jiwe. Iwapo mwana huyo angeomba samaki wa kula pamoja na mkate, babaye asingempa nyoka. Upendo wa asili ulioko kati ya baba na mwana ungemzuia baba asifanye jambo hilo.

“Basi,” akaendelea Yesu, “ikiwa ninyi, mlio waovu, mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! si zaidi sana Baba yenu aliye mbinguni atawapa mema wao wamwombao?”​—Mt. 7:11.

Ingawa akina baba duniani ni “waovu” kwa ajili ya dhambi iliyorithiwa, hawawapi watoto wao vitu vyenye kudhuru ambavyo vinafanana tu na vitu wanavyoomba. Mahali pake, wazazi wa kibinadamu hujitahidi kuwapa watoto wao “vipawa vyema.” “Si zaidi sana” Mungu, ambaye upendo wake ni mkamilifu, kwamba atajibu sala za waabudu wake waliojitoa. (1 Yohana 18) Yeye atawapa watumishi wake mambo “mema,” sana sana roho takatifu, ambayo inaweza kuwatia nguvu waendelee kutoa utumishi mtakatifu ambao unatimiza matakwa ya Mungu. (Linganisha Luka 11:13.) Hata hivyo, Aliye Juu Zaidi atafanya jambo hilo kwa watu wale tu wanaodumu katika ‘kumwomba.’

Halafu, Yesu aliongeza amri ya mwenendo ambayo imepata kujulikana sana: “Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo; maana hiyo ndiyo torati na manabii.”​—Mt. 7:12.

Mungu huwaonyesha watumishi wake maelekeo kama ya baba kwa kujibu sala zao. “Basi,” wao, vilevile, wanapaswa kutendea wanadamu wenzao vizuri. Ni kwa njia hiyo tu wanapoweza kujithibitisha wenyewe kuwa wana wa Mungu, yaani, watu wanaoiga maelekeo yake yenye fadhili na ambao sala zao hujibiwa na Baba wa kimbinguni bila kusita-sita.​—Linganisha Mathayo 5:44-48; 1 Petro 3:7.

Kwa habari ya hiyo “amri ya dhahabu,” kitabu A Pattern for Life kinasema hivi:

“Mambo yanayofanana na kanuni hiyo yanapatikana katika maandishi ya Kiyahudi na ya Mataifa, ikielekea kuonyesha kwamba Mungu hakuwa amewaacha wanadamu pasipo maarifa ya adili zilizo za juu zaidi kabla ya kuja kwa Kristo. Katika Tob[it, kitabu cha Aprocrypha] 4:15 twasoma hivi: “‘Unachokichukia usimtendee mwanadamu ye yote.’ Hillel [rabi mmoja aliyeishi karibu na wakati wa Yesu] alisema hivi: ‘Kinachochukiza kwako usimfanyie mtu ye yote.’ Wastoiki walikuwa na kanuni hii: ‘Usimtendee mwingine kile usichotaka kikupate wewe.’ Katika [dini ya] Confucius twapata jambo hili: ‘Usiwatendee wengine yale ambayo usingependa utendewe.’”

Hata hivyo, semi hizo zote ni juu ya kutofanya, zikitia watu moyo wasitendee watu yale ambayo wasingependa kutendewa wenyewe.

Walakini, watu ambao wangemsikiliza Mwana wa Mungu, wangepaswa kutenda zaidi ya kuepuka kutendea wengine vibaya. Wangepaswa kuchukua hatua ya kwanza kutendea wanadamu wenzao mambo mazuri, ndiyo, ‘yo yote ambayo wangetaka watu wawatendee.’ A.B. Bruce akilinganisha shauri hilo na semi zinazofanana juu ya kutofanya katika maandishi yasiyo ya Kibiblia, anasema hivi katika kitabu The Expositors Greek Testament:

“Jambo hili la kutofanya linahusu tu haki ya hukumu; hali ya kufanya inahusu ukarimu au neema, na kwa hiyo latia ndani torati na manabii. Twatazamia mengi zaidi kuliko tunayoweza kudai​—kusaidiwa tunapokuwa na uhitaji, kutiwa moyo tunapong’ang’ana na mambo, kutetewa tunaposingiziwa, kuonyeshwa urafiki tunapokazwa. Kristo angetuamuru tufanye yote hayo katika njia ya huruma na upole; si kuwa tu [wenye haki] bali [wema].”​—Tazama Warumi 5:7.

“Torati na manabii” zote zinataja Maandiko ya Kiebrania yaliyoongozwa na roho yenye maana. Wakati watu wanapowatendea wengine katika njia ambayo wangependa wengine wawatendee, wanatenda kwa kupatana na kusudi lenyewe la torati ya Mungu. “Msiwiwe na mtu cho chote.” anaandika mtume Paulo, “isipokuwa kupendana; kwa maana ampendaye mwenzake ameitimiza sheria. Maana kule kusema, Usizini, Usiue, Usiibe, Usitamani; na ikiwapo amri nyingine yo yote, inajumlishwa katika neno hili, ya kwamba, Mpende jirani yako kama nafsi yako. Pendo halimfanyii jirani neno baya; basi pendo ndilo utimilifu wa sheria.”​—Rum. 13:8-10; linganisha Mathayo 22:37-40.

[Maelezo ya Chini]

a Maneno ya Yesu katika Mathayo 7:7-11 yanapatikana pia katika Luka 11:9-13 katika kikao kilichokuwa katika Yudea wapata mwaka mmoja na nusu baada ya Mahubiri ya Mlimani. Bila shaka Yesu aliona inafaa kurudia shauri hilo.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki