Mahubiri ya Mlimani—‘Yasikieni Maneno Hayo, na Kuyafanya’
YESU aliyamalizia Mahubiri ya Mlimani kwa kutoa mfano wenye sehemu mbili: “Basi kila asikiaye hayo maneno yangu, na kuyafanya, atafananishwa na mtu mwenye akili aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile; isianguke, maana misingi yake imewekwa juu ya mwamba.”—Mt. 7:24, 25; linganisha Luka 6:47, 48.
Usemi “hayo maneno yangu” unahusu mambo yaliyofundishwa katika Mahubiri ya Mlimani. Usemi huu, “kila asikiaye hayo maneno” haumaanishi tu wale waliokuwapo wakati wa hotuba bora mno ya Yesu. Unatia ndani pia wale wote ambao baadaye wanasikia kwa kunenwa ama kwa kusoma mahubiri yake yanayojulikana sana. Hata hivyo, mwenye kupokea baraka za kudumu ni yule tu anayesikia na kuyafanya” yale aliyotia moyo Yesu.
Hiyo haimaanishi tu kufanya matendo ya kuabudu, kujinyima na huruma ambayo wengine wanaweza kuvutiwa nayo. Ni wachache wenye juhudi kama ya Mafarisayo katika mambo hayo. Hata hivyo vitendo vyao vilifanywa wa unafiki navyo havikufaa kitu kwa Mungu. (Angalia Mt. 6:1, 2, 5, 16.) Badala ya kuyakazia matendo yenye kuonekana na wanadamu, Yesu aliwasihi wasikilizaji wake wajigeuze kindani, wayasitawishe maelekeo ya akili na moyo ambayo kweli kweli yanampendeza Mungu. Kwa mfano, Mwana wa Mungu aliwaomba wasikilizaji wake wautambue umaskini wao wa kiroho na kuhitaji kwao Mungu pia. (Mt. 5:3), kukuza roho ya upole kumwelekea Mungu na kwa wanadamu wenzao (Mt. 5:5), kuwa wapenda haki, wenye rehema, moyo mweupe na wapenda amani. (Mt. 5:6-9) Watu wanaolitii shauri hilo watakuza kweli kweli utu kama wa Mungu. Hilo litajionyesha waziwazi kwa “kasi njema” zenye kung’aa sana kwa utukufu wa Mungu. Hilo linatia ndani kusukumwa kwenye utendaji, kama ilivyokuwa kwa wengi wa wasikilizaji wa Yesu wakati ule, kutangazia wengine “habari njema.”—Mt. 5:14-16; linganisha Wakolosai 3:10, 16.
Mtu “mwenye akili” (mwenye busara, mwenye kufanya uamuzi mzuri, mwangalifu) hujenga nyumba yake “juu ya mwamba,” jiwe kubwa kama vile mlima, jabali ama mwamba. Nyumba iliyojengwa imara juu ya msingi wa mwamba haiwezi kuangushwa kunapokuwa na tufani (mvua kubwa). “Mvua” na “mafuriko” (yanayotokea ghafula kwenye mabonde yanayobubujika maji kunaponyesha) hayatafagilia mbali msingi wake.a “Pepo” zinazovuma kutoka pande zote hazitasababisha kuanguka kwa nyumba ile. ‘Haitaanguka’ kunapokuwa na tufani.
Kwa njia ya mfano, mtu kujenga nyumba juu ya mwamba maana yake ni kugeuza mawazo, makusudi na kisha matendo yanayofuata kulingana na “hayo maneno yangu” yote, kama yalivyo katika Mahubiri ya Mlimani. Misiba inapotokea ghafula kama tufani huko Palestina (Mashariki ya Kati) haiwezi kufagilia mbali huo msingi imara wa mwenendo wa utawa. Ni wakati wa magumu ambapo anayefanya maneno ya Yesu “atafananishwa na” (au atajithibitisha kuwa kama) mjenzi yule mwenye akili aliyejenga juu ya msingi wa mwamba. Maelekeo na sifa za utu ambazo amesitawisha kulingana na Neno la Mungu ‘hazitaanguka’ wakati wa hali zenye kujaribu. Hataacha kumtumikia Mungu.
Kwa upande mwingine, Yesu akaendelea kusema hivi: “Na kila asikiaye hayo maneno yangu asiyafanye, atafananishwa na mtu mpumbavu, aliyejenga nyumba yake juu ya mchanga; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, ikaanguka na anguko lake lilikuwa kubwa.”—Mt. 7:26, 27, linganisha Luka 6:49.
Katika nchi ile ambayo Yesu aliifanya huduma yake, ungekuwa upumbavu kujenga nyumba juu ya mchanga. Mvua, mafuriko na pepo kali vingeweza kubomoa mjengo kama huo kwa urahisi. ‘Anguko lake lingekuwa kubwa’—kabisa na isiweze kutengezwa upya.
Jambo linalofanana na hilo litatokea kwa njia ya mfano kwa mtu “asikiaye hayo maneno yangu asiyafanye.” Mtu wa namna hiyo anayategemeza maisha yake, si kwa kutii mafundisho ya Kristo, bali juu ya kutokuyati kwa uchoyo maneno ya Yesu ambayo, kama mchanga, yanafagiliwa mbali na mafuriko. Siku za utulivu, kunapokuwa hakuna masumbuko ya maisha kwa kadiri kubwa, mtu wa namna hiyo aweza kwa urahisi kuficha kukosa kwake sifa za kimungu. Lakini mara tu magumu yanapotokea “atafananishwa” au atajithibitisha kuwa kama mpumbavu aliyejenga juu ya mchanga. Kwa habari ya kujifanya kuwa mtumishi wa Mungu, mateso kama tufani yatamfanya ayumbe-yumbe na kupatwa na “anguko kubwa.” Alipokuwa akizungumza juu ya uhitaji wa kuyaondoa mawazo na makusudi mabaya na badala yake kuwa na yaliyo sahihi, ili kuwa ‘mtendaji wa kazi ya Mungu’ mwenye furaha, mwandikaji wa Biblia Yakobo alitoa shauri linalofanana na lile la Yesu:
“Lakini iweni watendaji wa neno, wala si wasikiaji tu, hali mkijidanganya nafsi zenu. Kwa sababu mtu akiwa ni msikiaji wa neno tu, wala si mtendaji, mtu huyu ni kama mtu anayejiangalia uso wake katika kioo. Maana hujiangalia, kisha huenda zake, mara akasahau jinsi alivyo. Lakini aliyeitazama sheria kamilifu iliyo ya uhuru, na kukaa humo, asiwe msikiaji msahaulifu, bali mtendaji wa kazi, huyo atakuwa heri katika kutenda kwake.”—Yak. 1:22-25
Halafu masimulizi ya Injili ya Mathayo yanaongeza hivi: “Ikawa, Yesu alipoyamaliza maneno hayo, makutano walishangaa mno kwa [ajili ya njia yake ya kufundisha]; kwa maana alikuwa akiwafundisha kama mtu mwenye amri, wala si kama waandishi wao.”—Mt. 7:28, 29.
‘Njia ya kufundisha’ ya Yesu, yaani, jumla ya maagizo katika Mahubiri ya Mlimani yaliwashangaza wasikilizaji wake. Haikuwa namna ya mafundisho waliyozoea kupata kutoka kwa “waandishi wao,” ambao walikuwa wamejifunza sana mapokeo ya Kiyahudi yenye kunenwa. Waandishi walipofundisha jambo, walilisema “kwa jina la” mwenye amri fulani aliyetangulia. Kuhusu jambo hilo tunasoma hivi katika kitabu Theological Dictionary of the New Testament:
“Neno mish·shum [“kwa jina la”] ni la muhimu sana katika mapokea ya Kiyahudi. R[abi] Meir anasema akitoa mfano kwa jina (mish·shum) la Rabban Gamalieli, . . . Yeye aliyelisikia jambo fulani katika jumba la kufundishia naye akalipokeza alipaswa kumtaja mwenye amri aliyemwuliza ambaye kwa jina lake alipokezana naye mapokeo hayo. Mojayapo ya masharti 48 ya kuipata Torah ni kwamba “mtu alitamke kila neno kwa jina la mbuni (mwanzilishi) wake . . . ,’ Ab[oth], 6, 6; linganisha Meg[illah], 15a. Jambo hilo linaonyesha usemi ule ulikuwa na mamlaka ya namna gani na ya kadiri gani.”
Habari fulani ya Kirabi inaeleza kwamba Hillel Mkuu, aliyeishi wakati wa karne ya kwanza W.K., alifundisha mapokeo fulani kwa usahihi. “Lakini, ingawa alihutubu juu ya jambo hilo mchana kutwa, hawakulikubali fundisho lake, hadi mwishowe aliposema, Ndivyo nilivyosikia kutoka kwa Shemaia na Abatalioni [wenye amri waliomtangulia Hillel].”
Yesu hakufundisha kwa njia hiyo. Badala ya kusema kwa jina la mwanadamu mwingineyo, mara nyingi Mwana wa Mungu alitangaza “Amin [mimi] nawaambia,” “Bali mimi nawaambieni.” (Tazama, kwa mfano, Mathayo 5:18, 20, 22, 26, 28, 32, 34, 39, 44.) Alisema kama “mtu mwenye amri” ambaye alimwakilisha Mungu moja kwa moja, kama ilivyokuwa kwa habari ya manabii walioongozwa na Mungu wa nyakati zilizotangulia Ukristo (Linganisha Mt. 28:18.) Lo! namna tunavyoweza kuwa na shukrani kwamba Mungu ameona yafaa hotuba hiyo iliyo bora mno iandikwe katika Neno lake lililoongozwa kwa roho!
[Maelezo ya Chini]
a Kuhusu masimulizi ya namna mvua kubwa na mafuriko yenye kuharibu yanavyoweza kutokea katika Palestina, tazama Jambo lililoonwa. katika wakati wa kisasa lililoandikwa katika Awake! ya April 8, 1970.