Kumtolea Yehova Vilivyo Bora Zaidi
“Na alaaniwe mtu mwenye kudanganya, ambaye katika kundi lake ana mume, akaweka nadhiri, ila amtolea [Yehova] kitu kilicho na kilema; kwa maana mimi ni Mfalme mkuu, asema [Yehova] wa majeshi, na jina langu latisha katika mataifa.”—Mal. 1:14.
1. Je! kwa kweli wanadamu wanaweza kumtolea Yehova kitu cho chote?
JE! HALIONEKANI kuwa jambo la ajabu kwamba watu wasiokamilika wanaweza hata kufikiria kumtolea kitu Muumba Mkuu, Yehova? Ala! katika ulimwengu wote hakuna kitu kisichokuwa chake tayari! Katika Neno lake, yeye mwenyewe anatangaza hivi: “Fedha ni mali yangu, na dhahabu ni mali yangu.” (Hag. 2:8) “Maana kila [mnyama-mwitu] ni wangu, na makundi [ya wanyama] juu ya milima elfu. Nawajua ndege wote wa milima, na [makundi ya] wanyama wote wa mashambani ni [y]angu. Kama ningekuwa na njaa singekuambia, maana [nchi yote izaayo] ni [yangu], navyo [viijazavyo]. Je! nile nyama ya mafahali! Au ninywe damu ya mbuzi!” (Zab. 50:10-13) Bila shaka Yehova hahitaji zawadi kutoka kwa mtu, kwa kuwa yeye mwenyewe hapungukiwi na cho chote. Yeye Anajitegemea Mwenyewe kwa habari ya Uzima.
2. Daudi alikubali jambo gani juu ya kumtolea Yehova matoleo kwa hiari?
2 Akiwa kijana ambaye alikuwa amefunzwa sheria ya Musa, Daudi mwana wa Myahudi Yese alijua kwamba Yehova ndiye mwenyeji wa dunia yote. (Kut. 19:5) Katika miaka ya baadaye, wakati alipokuwa akitoa michango kwa ajili ya hekalu ambalo lingejengwa Yerusalemu, alizungumza na Aliye Juu Zaidi kwa njia ya sala kwa maneno haya: “Mimi ni nani, na watu wangu ni nani, hata tuweze kutoa kwa hiari hivi? kwani vitu vyote vyatoka kwako, na katika vitu vyako mwenyewe tumekutolea. Ee [Yehova], Mungu wetu, akiba hii yote tuliyoiweka, ili tukujengee nyumba kwa ajili ya jina lako takatifu, yatoka yote mkononi mwako, na yote ni yako wewe.”—1 Nya. 29:14, 16.
3. (a) Ni maulizo gani yanayoweza kuulizwa juu ya zawadi zinazotolewa Yehova? (b) Jibu la Kimaandiko kwa maulizo hayo ni jibu gani?
3 Kwa hiyo Daudi alikubali kwamba sisi wanadamu hatuwezi kumtajirisha Mwenye Nguvu Zote kwa njia yo yote. Kwa kweli, cho chote ambacho twaweza kumtolea kunakuwa kurudisha kisehemu kidogo tu cha vile ambavyo tumepata kutoka kwa Chanzo cha ‘kila zawadi njema na kila thawabu kamili.’ (Yak. 1:17) Walakini je! hii inamaanisha kwamba kumtolea Muumba wetu zawadi hakuna ubora wo wote? Je! yeye anadharau matoleo ya watumishi waliojitoa kwake? Jibu la Neno la Mungu ni Hasha. Yehova Mungu anawaalika waabudu wanyenyekevu walete zawadi zao. Katika Zaburi 96:8 twasoma hivi: “Mpeni [Yehova] utukufu wa jina lake, leteni [zawadi] mkaziingie nyua zake.”
4. Ni zawadi za namna gani zinazompendeza Yehova?
4 Bila shaka, Yehova alitaka matoleo mazuri ambayo yalitolewa kwa mioyo yenye kuthamini. Hizi zilikuwa zawadi ambazo zilihusu kujinyima kwa mtu mwenyewe vilevile na kujitayarisha kwa kufikiria na kwa namna ya sala. Kwa mfano, wakati sheria ya Musa ilipokuwa ingali ikifanya kazi, Mwisraeli asingeweza kuleta mnyama ye yote tu kwenye lango la ua wa hema na kutarajia kukubaliwa na Mungu. Sheria hiyo ilisema hivi: “Na mtu awaye yote atakayemtolea [Yehova] dhabihu katika sadaka za amani, ili kuondoa nadhiri, au sadaka ya moyo wa kupenda, katika ng’ombe, au katika kondoo, atakuwa mkamilifu, apate kukubaliwa; pasiwe na kilema ndani yake cho chote. Kipofu, au aliyevunjika mahali, au kiwete, au aliye na vidonda, au aliye na upele, au aliye na kikoko, hamtamtolea [Yehova] wanyama hao, wala msiwasongeze kwa [Yehova] kwa njia ya moto juu ya madhabahu.”—Law. 22:21, 22.
5. Torati ilitoa takwa gani kuhusiana na matoleo ya nafaka?
5 Juu ya matoleo ya nafaka, haya yalipaswa kuwa ya unga mwembamba. (Law. 2:1, 4; 6:14, 15; Hes. 15:4) Takwa hili halikukubalia unga wenye maganda, usiochungwa vizuri. Ndiyo, vitu vilivyofaa kutolewa Aliye Juu Zaidi, Yehova, vilikuwa vile vizuri zaidi.
6. Nia ya moyo ilihusikaje juu ya kukubaliwa kwa dhabihu za Mwisraeli?
6 Takwa jingine la muhimu katika kutoa matoleo yanayokubaliwa na Yehova lilikuwa kwamba mtu awe na nia njema ya moyo. Pasipo kutamani sana kumpendeza Muumba wake, Mwisraeli angekuwa akitoa sadaka bure. Angalia namna jambo hili linavyokaziwa katika maneno yanayofuata: “Huu wingi wa sadaka zenu mnazonitolea una faida gani? asema [Yehova]. Nimejaa mafuta ya kafara za kondoo waume, na mafuta ya wanyama walionona; nami siifurahii damu ya ng’ombe wala ya wana-kondoo wala ya mbuzi waume. Mjapo ili kuonekana mbele zangu, ni nani aliyetaka neno hili mkononi mwenu, kuzikanyaga nyua zangu? Msilete tena matoleo ya ubatili; uvumba ni chukizo kwangu. . . . Sikukuu zenu za mwezi mpya na karamu zenu zilizoamriwa, nafsi yangu yazichukia; mambo hayo yananilemea; nimechoka kuyachukua. Nanyi mkunjuaapo mikono yenu, nitaficha macho yangu nisiwaone; naam, mwombapo maombi mengi, sitasikia; mikono yenu imejaa damu.” (Isa. 1:11-15) Kulipokuwa hakuna kujitoa kwa kweli na roho ya ukarimu, namna za nje-nje za ibada zingeweza kulinganishwa na hongo zenye kusudi la kununua kibali ya kimungu. Hazikukubaliwa hata kidogo.
ZAWADI YETU KWA YEHOVA
7. Ni kwa sababu gani sisi leo hatutoi dhabihu za wanyama?
7 Tofauti na walivyokuwa Waisraeli, sisi wanafunzi wa Yesu Kristo hatutoi dhabihu juu ya madhabahu halisi. Agano la Torati ambalo liliamuru kutolewa kwa matoleo hayo lilifutwa kwa msingi wa kifo cha Yesu juu ya mti. (Kol. 2:13, 14) Hii inatokeza ulizo hili, Ni dhabihu gani tunazoweza sisi kutoa?
8. Katika Warumi 12:1, mtume Paulo aliandika nini juu ya dhabihu, na inatupasa kuyafahamuje maneno yake?
8 Paulo mtume Mkristo aliwatia moyo hivi waamini waliotiwa mafuta kwa roho ambao wangeacha miili yao na kupata miili ya kiroho yenye utukufu wakati wa kufufuliwa kutoka kwa wafu: “Kwa hiyo nawasihi kwa huruma za Mungu, ndugu, mtoe miili yenu dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubaliwa kwa Mungu, utumishi mtakatifu pamoja na nguvu yenu ya akili.” (Rum. 12:1, NW) Kwa hiyo walitiwa moyo watumie nguvu na uwezo wao katika kumtumikia Muumba. Viungo vya mwili ndivyo vyombo ambavyo mtu aweza kutumia katika kusema na kutenda. Kwa hiyo, ili ‘watoe miili yao kuwa dhabihu iliyo hai,’ iliwapasa Wakristo hao wawe wenye kutenda, ‘wakifanya mambo yote kwa utukufu wa Mungu.’ (1 Kor. 10:31) Ili dhabihu hiyo iwe “takatifu,” iliwapasa kuendeleza usafi wa adili na wa kiroho. Nako kutoa huko kwa miili yao ‘kungekubaliwa na Mungu’ ikiwa tu kumeongozwa na upendo usio na unafiki. (1 Kor. 13:3) Walipofuata maisha ya kujitoa kabisa kwa Mungu katika nia, kusema na kutenda kwa sababu ya kuchagua kufanya hivyo kwa kusudi, wakithamini kwamba ni jambo linalofaa kwa sababu ya huruma ambazo amekuwa akiwaonyesha, walikuwa wakifanya utumishi mtakatifu kwa kutumia ‘nguvu ya akili zao.’ Bila kujali tumaini letu la wakati huu lilivyo, liwe la mbinguni au la duniani, je! sisi vilevile hatuwezi kumtolea Mungu utumishi wa nafsi yote?
9. Katika Waebrania 13:15, 16, tunapewa kitia-moyo gani?
9 Katika barua aliyowaandikia Waebrania, twajifunza zaidi juu ya dhabihu zinazokubaliwa na Mungu. Waebrania 13:15, 16 lasema: “Basi, kwa njia yake yeye [Kristo], na tumpe Mungu dhabihu ya sifa daima, yaani, tunda la midomo iliungamayo jina lake. Lakini msisahau kutenda mema na kushirikiana; maana sadaka kama hizi ndizo zimpendezazo Mungu.”—Linganisha Hosea 14:2.
10. “Tunda la midomo” linatia nini ndani, nasi twaweza kujiuliza maulizo gani kuhusiana na jambo hili?
10 Kutoa kwetu “tunda la midomo” kunatia ndani kushiriki katika kutimiza Mathayo 24:14, NW: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” Je! sisi tunatoa kweli kweli yaliyo bora zaidi katika kazi hii ya maana ya kuhubiri? Je! tunatazamia sana kutumia nafasi ili kutoa ushuhuda? Je! maisha yetu kama Wakristo ni ya mfano bora ili kwamba “tunda la midomo” litie ndani dhabihu ya sifa inayokubalika?—Rum. 2:21, 22.
11. Ni kwa sababu gani inafaa kuchunguza maoni yetu juu ya mikutano ya Kikristo?
11 Kusema miongoni mwa watu wote katika mikutano ya Kikristo vilevile ni sehemu ya dhabihu yetu. Kwa wazi, hiyo inatulazimu kuwapo wakati waamini wenzetu wamekusanyika kwa ibada. Je! sisi tunatamani kweli kweli kuwa pamoja na wengine wenye imani kama hiyo yenye thamani? Au sisi tunaachilia shughuli nyingine na mapendezi yachukue wakati ambao tungekuwa pamoja na ndugu zetu? Tutafanya vizuri tukiiga mfano wa mtunga zaburi ambaye aliifananisha tamaa yake nyingi ya kushirikiana na Yehova Mungu katika ushirika wa waabudu wenzake na ile tamaa ya paa jike ya kutamani sana maji. Pasipo maji, paa jike asingeweza kuishi. (Zab. 42:1, 2) Je! sisi tunathamini kweli kweli kwamba hatuwezi kuishi pasipo Yehova, “chemchemi ya maji ya uzima”?—Yer. 2:13.
12, 13. Twaweza kufaidikaje kikamilifu kutokana na mikutano ya Kikristo?
12 Tunapokuwa mikutanoni, bila shaka tutataka kufaidika kabisa. Tunaweza kufanya hivyo kwa kutumia shauri lifuatalo lililoongozwa na Mungu. “Tukaangaliane sisi kwa sisi na kuhimizana katika upendo na kazi nzuri . . . na kuzidi kufanya hivyo, kwa kadiri mwonavyo siku ile kuwa inakaribia.” (Ebr. 10:24, 25) Kwa kuwa siku kuu ya Yehova ya kufikiliza hukumu lazima ije, je! hatuna sababu nzuri kufikiria kwa sala yale tunayoweza kufanya ili kuwatia nguvu na kuwahimiza ndugu zetu? Bila shaka tusingetaka ye yote wao apatikane katika hali isiyokubalika wakati siku hiyo ijapo. (Luka 21:34-36) Je! yale tunayosema yanaonyesha kwamba tunahangaikia kweli kweli hali yao njema ya kiroho? Kwa njia ya maelezo yetu mikutanoni, je! sisi tunaendeleza upendo, pamoja na kupendezwa kusiko na choyo katika hali njema ya milele ya wengine? Je! kusema kwetu kunatia wote moyo waendelee kufanya kazi njema, wakiwa wenye juhudi katika kutangaza “habari njema” na kuwa mifano bora katika sehemu zote za maisha ya kila siku?—Linganisha Tito 2:1-14.
13 Kwa kuwahimiza wengine “katika upendo na kazi nzuri,” tunajihimiza sisi wenyewe pia, tukikazia akilini na mioyoni mwetu umuhimu wa matendo yanayopatana na imani. Hii inaweza kuwa na matokeo yenye kutufaidi, ikitufanya tujichunguze sisi wenyewe na kufanya maendeleo katika kuishi na kutenda Kikristo. Na wakati tunaposikiliza yale yanayosemwa na wengine na kutumia vitia-moyo vya Kimaandiko, tunapata furaha inayotokana na kuwa ‘watendaji wa neno.’—Yak. 1:22-25.
14, 15. Zaidi ya kutoa kiroho, ni jambo gani jingine linalotiwa ndani ya “dhabihu” zetu?
14 Barua hiyo iliyoandikiwa Waebrania inatuhimiza tushiriki vitu, tuwasaidie wenye mahitaji. Wale walioandikiwa barua hiyo waliambiwa hivi: “Zikumbukeni siku za kwanza, ambazo, mlipokwisha kutiwa nuru, mlistahimili mashindano makubwa ya maumivu; pindi mlipotwezwa kwa mashutumu na dhiki, na pindi mliposhirikiana na wale waliotendwa hayo. Maana mliwaonea huruma wale waliokuwa katika vifungo, tena mkakubali kwa furaha kunyang’anywa mali zenu, mkijua kwamba nafsini mwenu mna mali iliyo njema zaidi, idumuyo.” (Ebr. 10:32-34) Je! sisi nasi tunawahurumia na kuwasaidia wale wanaoteseka?
15 Hali ambayo katika hiyo watu wa Mungu wanajipata ndani yake inatofautiana sana. Huenda wengine wakawa maskini. Wengine huenda wakawa wamehuzunika na kushuka moyo, wakihitaji sana kufarijiwa na kupata urafiki wa wengine. Huenda wengine wakavunjika moyo kwa sababu ya magumu makubwa ya kibinafsi. Ni kweli kwamba Yehova atahakikisha kwamba wenye haki hawaachwi kabisa. (Zab. 37:25) Walakini, je! haitupasi sisi kuona moyoni mwetu daraka la kuwa mawakili wa kutumiwa na Mungu katika kuwatendea kwa fadhili na kuwasaidia? kutojali kwetu juu ya hili ni jambo zito sana. Mtume Yohana aliandika hivi: “Lakini mtu akiwa na riziki ya dunia, kisha akamwona ndugu yake ni mhitaji, akamzuilia huruma zake, je! upendo wa Mungu wakaaje ndani yake huyo? Watoto wadogo, tusipende kwa neno, wala kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli.”—1 Yohana 3:17, 18.
SABABU TUNAALIKWA TULETE ZAWADI ZETU
16, 17. Ni kwa sababu gani Yehova anatualika tutoe “dhabihu”?
16 Ili tuwe waaminifu katika kutoa dhabihu zetu za kiroho, inatupasa kufahamu sababu gani Yehova Mungu anatualika sisi tufanye hivyo. Tayari Baba yetu wa mbinguni anajua mafikira yetu na maono yetu ya ndani. Walakini anataka tuonyeshe upendo wetu kwake kwa mema tunayofanyia wengine. Ni tamaa yake kwamba watumishi wake wawe kama yeye katika kuonyesha fadhili na ukarimu. (Mt. 5:43-48) Hii inamtolea njia ya kuvuta wanadamu kwake. Namna gani hivyo? Kwa kutazama njia yetu ya maisha yenye kusifika, wengine wanaweza kupata kufahamu kwamba furaha ya kweli inatokana na kufanya mapenzi ya Mungu.—Mt. 5:16.
17 Kwa kuwa Yehova Mungu ndiye aliyetuumba, yeye anafahamu yale yanayotufaa kabisa. Hii ndiyo sababu nyingine ya kutualika tulete zawadi zetu kwake. Roho ya ukarimu inatuwezesha kufurahia amani ya akili na ya moyoni pamoja na furaha ya kweli sasa. Biblia inasema: “Kuna furaha nyingi katika kutoa kuliko zilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35, NW) Kuongezea hayo, twaweza kuwa na hakika kwamba Baba yetu wa mbinguni atatuthawabisha sana sasa na katika wakati ujao wa milele. Mwana wa Mungu alisema: “Utoapo [zawadi zako za rehema], hata mkono wako wa kushoto usijue ufanyalo mkono wako wa kuume; [zawadi zako za rehema ziwe] kwa siri, na Baba yako aonaye sirini atakujazi.” (Mt. 6:3, 4) “Ufanyapo karamu waite maskini, vilema, viwete, vipofu, nawe utakuwa heri, kwa kuwa hao hawana cha kukulipa [nacho]; kwa maana utalipwa katika ufufuo wa wenye haki.”—Luka 14:13, 14.
18. Ni jambo gani lililo la lazima katika kutoa kwetu, na kwa sababu gani?
18 Kwa hiyo, kwa kuwa na maoni yenye ufahamu mwingi juu ya dhabihu zetu, inatupasa kukubali kwamba mikutanoni, wakati tunaposhiriki “habari njema” na wengine, na katika maoni, kusema na kutenda, ndiyo, katika sehemu zote za maisha, itatupasa kuwa tayari kutoa yale yaliyo bora zaidi tuliyo nayo. Haitupasi kuwa wenye moyo nusu-nusu juu ya mambo hayo ya maana. Kukubaliwa na Yehova na kupata uzima wa milele, ndiyo mambo yaliyo hatarini. Basi, na tuishi kulingana na hakikisho hili la Kimaandiko: “Maana Mungu si dhalimu hata aisahau kazi yenu, na pendo lile mlilolidhihirisha kwa jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu, na hata hivi sana mngali mkiwahudumia.”—Ebr. 6:10.
[Picha katika ukurasa wa 8]
WOTE WAWEZA KUSHIRIKI KATIKA:
KUTOA MAELEZO MIKUTANONI
KUHUBIRI NA KUFUNDISHA
KUWATIA MOYO WENGINE KIROHO NA KWA MAMBO YA KIMWILI
KUHIMIZA WENGINE KATIKA UPENDO NA KAZI NZURI