Wakati Wengine Wanapojali
“MIMI sina mtu wa jamaa ya kimwili hata mmoja. . . . Najiangalia mimi mwenyewe nami sipati msaada kutoka kwa mtu ye yote, na, nakuambia hakika, kuna nyakati nyingi ambazo ungenifaa sana. . . . Kuangaliwa ko kote, hata kuwe kidogo namna gani, kunatuvutia sana. Kunathaminiwa sana kwa unyenyekevu.”
Ndivyo alivyoandika mwanamke mmoja mzee. Kama vile yeye, mara nyingi wazee wanashukuru sana wakati wengine wanapowajali.
Ndivyo ilivyo hata na kwa vijana wengi. Kijana mmoja aliwaandikia rafiki zake wapendwa hivi: “Ningependa kuwashukuru kwa kuwa wenye fadhili na wenye kunihangaikia sana, kwa kwenda ‘pamoja nasi vijana,’ kutumia wakati wenu kwa ajili yetu ili tuwe na wakati mzuri namna hiyo.” Kikundi kimoja kilikuwa kimetumia siku moja katika ushirika wenye kupendeza na wenye kujenga. Ni wazi kwamba, lilikuwa tukio lenye kukumbukwa, nayo barua hiyo fupi ilionyesha shukrani kwa wenzi hao wawili waliooana kwa “kujali sana.”
KUJALI KUNASAIDIA
Mara nyingi wanaohangaikiwa wanafaidika sana wengine wanapojali. Kwa mfano, huenda wakapata kutiwa moyo. Akimwandikia dada yake wa kiroho, kijana mwingine wa kike aliandika hivi: “Ulinitia moyo nilipokuwa na nia ya kushona, au ya kupika, na hukunilaumu hata wakati mmoja. . . . Nakupenda kweli kweli kama dada Mkristo.” Ndiyo, kutiwa moyo katika kazi zenye kujenga—sana sana katika kufuatia mambo ya kiroho—kwaweza kuwafaidi sana wengine.—Matendo 11:23; 1 Pet. 5:12.
Hata hivyo, kujali kunasaidia katika njia nyingine pia. Huenda uongozi ukahitajiwa, na bila shaka ni jambo rahisi zaidi kukubali shauri lenye kufaa wakati mwenye kulipokea anapofahamu kwamba mwenye kulitoa anajali kweli kweli. Mzee mmoja Mkristo alifurahi sana kupokea barua iliyosema hivi: “Asante kwa . . . uongozi wote na wakati uliotumia pamoja na kujali ulikoonyesha.” Bila shaka mtume Paulo aliwajali sana waamini wenzake, kwa maana aliandika hivi: “Na pamoja na maneno yale ya inje, kuna maneno yanayonisonga mimi kila siku, ndiyo masumbuko ya kulinda [makundi] yote. Nani aliye zaifu, na mimi si zaifu? Nani anayekwazwa, nami nisiumizwe?”—2 Kor. 11:28, 29, ZSB.
Walakini wengine wanapojali, kunakuwa na faida za ziada—ambazo hazionekani waziwazi sana. Kijana wa kike aliwaandikia wenzi wawili waliooana waliotangulia kutajwa akasema hivi: “Hata niwafanyie nini, isingetosha hata kidogo. Natumaini kwamba sikuwaudhi kamwe.” Ndiyo, fadhili inatokeza fadhili, nayo inavuta watu karibu zaidi. Zaidi ya hayo, unapofahamu kwamba wengine wanajali, bila shaka usingependa kuwakasirisha au kuwaudhi. Nako kujali kwako kwaweza kukutia nguvu ustahimili katika mwendo wenye upendo, wa kimungu.
KUONYESHA KWAMBA UNAJALI
Unaweza kuonyeshaje kwamba wewe unawajali wengine? Bila shaka, njia zenyewe ni nyingi sana. Walakini ebu fikiria baadhi yazo.
“Iweni wafadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma” akaandika mtume Paulo. (Efe. 4:32) Vilevile alisema: “Upendano wa ndugu na udumu. Msisahau kuwafadhili wageni.” (Ebr. 13:1, 2) Kweli kweli, wakati wote fanya jambo lililo la fadhili, la upendo, la ukarimu. Tendo kama hilo litawaonyesha wengine kwamba unajali.
Kwa mfano, katika kuonyesha ukarimu, je! si jambo lenye kutamanika kutia ndani watu wa umri mbalimbali na hali mbalimbali, wala si wale tu walio wa umri wako na cheo kama chako maishani? Wakati mmoja Yesu Kristo alisema hivi: “Ufanyapo karamu waite maskini, vilema, viwete, vipofu, nawe utakuwa heri, ,kwa kuwa hao hawana cha kukulipa [nacho]; kwa maana utalipwa katika ufufuo wa wenye haki.” (Luka 14:13, 14) Kwa vyo vyote, wakumbuke wasiojaliwa sana, miongoni mwao pengine wako wajane na waume waliofiwa na wake zao ambao wangefurahia ushirika wako.
Ni kweli kwamba huenda uwezo wako usikuruhusu kufanya karamu. Walakini hilo lisikusumbue. Mithali iliyoongozwa na Mungu inasema hivi: “Chakula cha mboga penye mapendano ni bora kuliko ng’ombe aliyenona pamoja na kuchukiana.” (Mit. 15:17) Pindi moja, wakati Yesu Kristo alipotembelea rafiki zake wema Mariamu na Martha wa Bethania, alikazia ubora wa mambo ya kiroho. Lakini namna gani chakula? “Martha, Martha,” akasema Yesu, “unasumbuka na kufadhaika kwa ajili ya vitu vingi; lakini kinatakiwa kitu kimoja tu.” (Luka 10:38-42) Ndiyo, Yesu angeridhika na namna moja tu ya chakula, kwa hiyo Martha mwenye akili zenye kutanga-tanga, pamoja na Mariamu mwenye kukaza akili zake, wangeweza kufaidika kwa njia fulani kutokana na mafundisho yake.
Wakristo wanaweza kuonyesha kwamba wanawajali wengine kwa kushirikiana nao kijamii. Pindi hizi zinafanywa kuwa zenye kukumbukwa kwa kusimulia mambo mazuri yaliyoonwa yaliyofurahiwa katika utumishi wa Mungu, au kwa kutiana moyo kupitia kwa mazungumzo yenye kujenga kiroho na yanayofaa kabisa, kusoma Biblia kama kikundi au mazungumzo ya Kimaandiko. Wazee na vijana pia wanaweza kufaidika kutokana na mambo haya, na mara nyingi wakati unaonekana ukipita upesi sana. Urafiki unatiwa nguvu na walioko huenda wakakumbuka wakati huo uliotumiwa pamoja.
Walakini namna gani wale wanaoupokea ukarimu huo au wanaofanyiwa matendo mengine ya fadhili? Lo! namna inavyofaa waonyeshe kuthamini sana! Hii inaonyesha kwamba hata nao wanajali. “Kwa sababu na nyakati tunamoishi,” kijana mmoja aliwaandikia rafiki zake wapendwa, “Sidhani kwamba sisi kama Wakristo inatupasa kukosa wakati hata kidogo wa kuambiana namna tunavyothamini urafiki wa mtu na mwenzake. Ninyi . . . mmekuwa msaada kwangu katika njia nyingi, nyingine huenda hata msizijue.”
Wale walio na kusudi zuri katika kuwahangaikia wengine hawatafuti kusifiwa kwa jitihada zao. Hata hivyo, kwa kujitoa kwao, wanathawabishwa kwa maana, kama alivyosema Yesu, “kuna furaha nyingi katika kutoa kuliko zilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35, NW) Kwa hiyo, mtoaji na mpokeaji wanafaidika kutokana na maneno na matendo ya kuhangaikiana. Lo! namna baraka zinavyotokea wakati wengine wanapojali!
‘Mtwikeni yeye magumu yenu yote, kwa kuwa yeye anawajali ninyi.’—1 Pet 5:7.