Walifanya Mapenzi ya Yehova
Maria Achagua “Fungu Jema”
WAKATI wa Yesu, mapokeo ya kirabi yaliwawekea wanawake Wayahudi vizuizi vingi. Hivyo, walizuiwa kujifunza Sheria. Kwa kweli, maoni fulani yaliyonukuliwa katika Mishnah yalisema: “Mwanamume yeyote akimfundisha binti yake Sheria ni kana kwamba anamfundisha uasherati.”—Sotah 3:4.
Kwa sababu hiyo, wanawake wengi katika Yudea ya karne ya kwanza hawakuelimishwa vizuri. “Hakuna uthibitisho kwamba kabla ya huduma ya Yesu wanawake Wayahudi waliruhusiwa wakati wowote wawe wanafunzi wa mwalimu mkuu, sembuse kutembea na mwalimu kama huyo, au kufundisha mtu yeyote ila watoto tu,” chasema kichapo The Anchor Bible Dictionary. Kwa kuwadhalilisha zaidi wanawake, viongozi fulani wa kidini hata walitoa sheria iliyomtaka mwanamume asiongee na mwanamke hadharani!
Yesu alipuuza mitazamo hiyo miovu. Aliwafundisha wanawake na wanaume vilevile, na miongoni mwa wafuasi wake walikuwemo wanaume na wanawake. (Luka 8:1-3) Wakati mmoja, Yesu alialikwa awe mgeni wa Martha na Maria. (Luka 10:38) Wanawake hao wawili walikuwa dada za Lazaro, na wote watatu walikuwa wanafunzi na rafiki wazuri wa Yesu. (Yohana 11:5) Kwa kuzingatia idadi kubwa ya watu waliokuja kumfariji Martha na Maria Lazaro alipokufa, yawezekana familia hiyo ilikuwa maarufu. Kwa vyovyote, kilichotukia nyumbani kwao Yesu alipowatembelea kiliandaa somo lenye thamani kwao na kwetu pia.
Kujifunza Miguuni pa Yesu
Haikosi Martha na Maria walikuwa na hamu ya kumwandalia Yesu karamu nono, na labda walikuwa na uwezo wa kufanya hivyo. (Linganisha Yohana 12:1-3.) Hata hivyo, mgeni wao alipofika, Maria “aliketi kwenye miguu ya Bwana na kufuliza kulisikiliza neno lake.” (Luka 10:39) Hakuna pokeo lolote la wanadamu ambalo lingeweza kumzuia Yesu asimfundishe mwanamke mnyofu, mwenye hamu nyingi ya kujifunza! Tunaweza kumwazia Maria akiwa ameketi mbele ya Yesu, kama mwanafunzi anayesikiliza kwa makini kabisa mafundisho ya Bwana-Mkubwa wake.—Linganisha Kumbukumbu la Torati 33:3; Matendo 22:3.
Tofauti na Maria, Martha “alivutwa fikira kwa kushughulikia kazi nyingi.” Kwa kutayarisha mlo mnono, alikuwa na shughuli nyingi sana za kazi zake ngumu. Muda si muda, Martha akakasirika kwa sababu ameachiwa kazi zote huku dada yake akiketi miguuni pa Yesu! Hivyo, Martha akakatiza mazungumzo ya Yesu na Maria, yamkini kwa ghafula, kwa kusema: “Bwana, si kitu kwako kwamba dada yangu ameniacha mimi peke yangu kushughulikia mambo? Kwa hiyo, mwambie ajiunge katika kunisaidia.”—Luka 10:40.
Ombi lenyewe la Martha halikuwa baya. Kwa vyovyote, ni kazi ngumu kutayarishia kikundi cha watu mlo, na daraka hilo zito halipasi kuachiwa mtu mmoja. Hata hivyo, maneno yake yalimpa Yesu fursa ya kumfundisha jambo lenye thamani. “Martha, Martha,” akasema, “wewe wahangaika na kusumbuka juu ya mambo mengi. Ingawa hivyo, mambo machache yahitajiwa, au moja tu. Kwa sehemu yake, Maria alichagua fungu jema, nalo halitaondolewa mbali naye.”—Luka 10:41, 42.
Yesu hakumaanisha kwamba Martha hapendezwi na mambo ya kiroho. Kinyume chake, alimfahamu kuwa mwanamke aliyejitoa sana kwa Mungu.a Haikosi jambo hilo hasa ndilo lililomchochea kumwalika Yesu nyumbani kwake. Hata hivyo, alipomkaripia kwa upole, Yesu alikuwa akionyesha kwamba Martha, kwa kuhangaikia sana mlo huo, alikuwa akikosa fursa ya kupokea mafundisho ya kibinafsi kutoka kwa Mwana wa Mungu.
Ni kweli kwamba utamaduni wa wakati huo huenda ikawa uliunga mkono maoni ya kwamba thamani ya mwanamke ilibainishwa vizuri zaidi kwa uhodari wake katika kazi za nyumbani. Lakini maneno ya Yesu yalionyesha kwamba wanawake, kama wanaume, wangeweza kuketi chini miguuni pa Mwana wa Mungu na kupokea maneno ya uhai! (Yohana 4:7-15; Matendo 5:14) Kwa kuzingatia hayo, ingelikuwa afadhali zaidi Martha kuandaa vyakula vichache—labda kimoja tu—ikiwa kufanya hivyo kungelimpa fursa ya kuketi miguuni pa Bwana-Mkubwa na kujifunza kutoka kwake.—Linganisha Mathayo 6:25.
Somo Kwetu
Leo, wanaume kwa wanawake wamo miongoni mwa wale wanaoitikia mwaliko wa Yesu wa ‘kuchukua maji ya uhai bure.’ (Ufunuo 22:17) Kwa kuchochewa na upendo, wengine—kama Martha—hufanya yote wawezayo kushughulikia mahitaji ya waamini wenzao. Wao hutumia busara na huchukua hatua haraka, naye Yehova huahidi kuthawabisha jitihada zao za upendo. (Waebrania 6:10; 13:16) Wengine yamkini wafanana zaidi na Maria. Wao ni wanana na wenye kutafakari. Hamu yao ya kutaka kutafakari Neno la Mungu huwasaidia kudumisha imani thabiti.—Waefeso 3:17-19.
Watu hao wa aina zote mbili hutimiza uhitaji muhimu katika kutaniko la Kikristo. Hata hivyo, hatimaye wote wapaswa ‘kuchagua fungu jema’ kwa kuzingatia zaidi mambo ya kiroho. Kwa kuhakikisha mambo yaliyo muhimu zaidi, tutapata upendeleo na baraka ya Yehova.—Wafilipi 1:9-11.
[Maelezo ya Chini]
a Uhakika wa kwamba Martha alikuwa mwanamke wa kiroho mwenye imani kubwa wathibitishwa na mazungumzo yake pamoja na Yesu baada ya kifo cha ndugu yake, Lazaro. Wakati huo, Martha ndiye aliyeonyesha hamu kubwa zaidi ya kukutana na Bwana-Mkubwa wake.—Yohana 11:19-29.