Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w79 11/15 kur. 12-17
  • Sala Katika hizi “Siku za Mwisho”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sala Katika hizi “Siku za Mwisho”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUSTAHIMILI KWA UJASIRI KUNA MATOKEO
  • ‘UHITAJI WA KUSALI WAKATI WOTE BILA KUKATA TAMAA’
  • ‘KESHENI, WAKATI WOTE MKIOMBA’
  • Yehova Anawapa “Roho Takatifu Wale Wanaomwomba”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Yehova ‘Atasababisha Haki Ifanywe’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Kudumu Katika Sala Kunathawabisha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Kumjia Msikiaji wa Sala
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
w79 11/15 kur. 12-17

Sala Katika hizi “Siku za Mwisho”

“Basi, kesheni ninyi kila wakati, [mkisali],”​​—⁠Luka 21:36.

1. (a) Luka anataja sala au ‘maombi’ kwa mara ya kwanza wapi? (b) Yesu alijibuje ombi hili: “Bwana, tufundishe sisi kusali”?

INGAWA sala inatajwa mwanzoni mwa Injili ya Luka kuhusiana na ‘maombi’ ya Zekaria kwa Mungu (sura ya 1, mstari wa 13), Yesu anazungumza jambo hili kwa urefu katika sura ya 11. Kwanza, Yesu anajibu ombi lililofanywa na mmojawapo wa wanafunzi wake: “Bwana, tufundishe sisi kusali, kama vile Yohana alivyowafundisha wanafunzi wake.” (Luka 11:1) Yesu alijibu hivi:

“Msalipo, semeni, Baba jina lako litakaswe, ufalme wako uje, utupe siku kwa siku riziki yetu. Utusamehe dhambi zetu, kwa kuwa sisi nasi tunamsamehe kila tumwiaye. Na usitutie majaribuni.”​​—⁠Luka 11:2-4.

2. (a) Kwa hiyo jina la Mungu linaheshimiwaje, na kupatana na maandiko gani? (b) Ni hali gani zenye kutofautiana zilizopo ulimwenguni, na hali hii itatengenezwaje?

2 Sawa na maandiko yaliyoko katika 1 Wafalme 8:41-43 na Isaya 56:6-8, yaliyotajwa katika makala iliyotangulia, ebu angalia namna Yesu anavyotanguliza jina la Baba yake. Bila shaka jina la Yehova halitakaswi katika ulimwengu wa leo. Roho ya utukuzaji wa taifa, kujitanguliza na kujipendekeza, kutoridhika na kuwa “wenye mfano wa utauwa, lakini wakikana nguvu zake,” na hali nyingine kama hizo zinafanya jina la Mungu lisutwe na kudharauliwa au kupuzwa kabisa. (2 Tim. 3:5) Kwa hiyo ni lazima Mungu atakase jina lake katika kujibu sala hii. (Eze. 36:23) Hali ya mambo yenye kuchukiza itatengenezwa wakati ufalme wa Mungu, mikononi mwa Kristo Yesu utakapopambana na mataifa na watawala wake, kama inavyosimuliwa vizuri katika Zaburi ya 2.

3. Kupatana na habari hii, Petro anatoa onyo na ahadi gani?

3 Mambo haya yatatukia katika siku ya Yehova, ambayo sasa imekaribia sana, kama unabii wa Biblia unaoendelea kutimizwa unavyoonyesha waziwazi. Kwa hiyo tutafanya vizuri tukitii shauri la onyo la Petro lililoongozwa na Mungu:

“Mkingojea na kuhimiza akilini kuwapo kwa siku ya Yehova, ambayo katika hiyo mbingu zikiwa zinateketea zitafunuliwa na vitu vya asili vikiwa moto kweli kweli vitayeyuka! Lakini ziko mbingu mpya na dunia mpya ambazo sisi tunangojea kulingana na ahadi yake, na katika hizi haki itakaa. Kwa hiyo, wapenzi, kwa kuwa mnangojea mambo haya, fanyeni yote mwezayo ili mwishowe mpatikane naye bila doa na bila mawaa na katika amani.”​​—⁠2 Pet. 3:12-14, NW.

4. Maombi mawili ya kwanza yamefunganishwaje karibu karibu katika Sala ya Bwana, na hii inatusaidiaje kuhusiana na maombi yetu?

4 Mambo hayo yote yatakapotimizwa, jina la Mungu litatukuzwa na kutakaswa kabisa. Hiyo ndiyo sababu maombi hayo mawili katika Luka 11:2 yamefungamanishwa karibu karibu na ndiyo ya kwanza katika Sala ya Bwana. Haya ndiyo matukio makubwa zaidi ya wakati wetu na wakati ujao. Kuyaweka sana akilini kutasaidia katika kuwa na maoni yenye kiasi zaidi juu ya mahitaji yetu ya kibinafsi ya kila siku na matatizo ambayo yanatajwa baadaye katika sala hiyo. Mahali pa kuwa wenye kufuatia mapendezi yetu, ambalo ni jambo rahisi kufanya tutajiuliza wenyewe hivi: Ni maoni gani na mwendo gani kwa upande wangu ambao utapatana na mapenzi ya Mungu, kama yanavyoonyeshwa katika Neno lake, na hivyo nitukuze jina lake?

KUSTAHIMILI KWA UJASIRI KUNA MATOKEO

5. (a) Kanuni inayoongoza mambo yote katika mifano ya Yesu kuhusiana na watu waliomo ni kanuni gani? Taja mfano. (b) Katika Luka 11:5-8, ni watu gani wanaotajwa, na wanasimamia nini?

5 Baada ya hayo yaliyotajwa hapo juu, Luka anatuambia mfano uliotolewa na Yesu, wenye sehemu isiyo ya kawaida. Kwa kawaida wakati mtu mmoja au zaidi anapotajwa katika mfano, kila mmojawapo analingana sana na wale wanaofananishwa na watu hao. Ikiwa, kwa mfano, Baba wa mbinguni anafananishwa, kama ilivyo katika mfano wa mwana mpotovu katika Luka 15:11-32, basi hatuna ugumu wa kuona namna baba wa mwana huyo, kwa aliyosema na kufanya, alivyofananisha Baba wa mbinguni. Walakini, haiwezi kusemwa hivyo kwa habari ya mfano wa Yesu unaofuata:

“Ni nani kwenu aliye na rafiki, akamwendea usiku wa manane, na kumwambia, Rafiki yangu, nikopeshe mikate mitatu, kwa sababu rafiki yangu amefika kwangu, atoka safarini, nami sina kitu cha kuweka mbele yake; na yule wa ndani amjibu akisema, Usinitaabishe; mlango umekwisha fungwa, nasi tumelala kitandani mimi na watoto wangu; siwezi kuondoka nikupe: Nawaambia ya kwamba, ijapokuwa haondoki ampe kwa kuwa ni rafiki yake, lakini kwa vile asivyoacha kumwomba, ataondoka na kumpa kadiri ya haja yake.”​​—⁠Luka 11:5-8.

6. Hapo, mtu fulani alikuwa tofauti na Yehova namna gani, napo hapo Yesu alikuwa akikazia nini?

6 Hapa twaona kwamba yule aliyekuwa na uwezo wa kutosheleza mahitaji ya mwenye kuomba alikataa kabisa hapo kwanza kufanya jambo lo lote, akisema: “Usinitaabishe.” Hakuwa na nia ya kufanya hivyo hata kidogo. Badala ya kujionyesha kuwa kama Baba Wa mbinguni, yeye anatofautiana kabisa naye. Kwa kufanya hivyo, jambo kubwa la mfano huo lilikaziwa zaidi. Ikiwa mtu huyo pamoja na jamaa yake wakiwa wamekwisha lala kitandani angekuwa na nia ya kuamka na kutoa kilichokuwa kikihitajiwa, kusingekuwa na uhitaji wa ‘kuomba bila kuacha’ kwa upande wa mwenye kuomba. Hilo ndilo jambo kubwa alilokuwa akikazia Yesu.

7, 8. Maneno ya Yesu yaliyofuata yalithibitishaje hili, nalo hili linatutia moyo sana namna gani?

7 Maneno ya Yesu yanayofuata yanakazia hili: “Nami nawaambia, Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa.” (Luka 11:9) Kisha kwa njia ya kutofautisha, yeye anamalizia hivi: “Basi, ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Baba aliye mbinguni , kuwapa [roho takatifu] hao wamwombao?”​​—⁠Luka 11:13.

8 Ebu mwazie mtu huyo ambaye, ‘kwa sababu ya kuomba bila kuacha,’ alipata kile alichokuwa akihitaji hata ijapokuwa ulikuwa usiku wa manane! Kustahimili kwake kulikuwa na matokeo. Namna kilivyo kitia-moyo kutumia maishani mfano huo wa Yesu: ‘Ombeni​—⁠tafuteni​—⁠bisheni.’ Usiache kuomba au kuacha imani yako idhoofike kwa sababu ya upinzani unaoendelea kwa kazi yako ya kutangaza Ufalme au kufanya wanafunzi, au kwa sababu ya kuishi katika nyumba iliyogawanyika, au kwa sababu ya kushindana na udhaifu fulani wa kibinafsi ambao ni mkubwa kuliko ulivyokuwa ukifikiria.

9. Ni mifano gani ya kudumu katika kusali na kutenda inayotajwa katika Matendo 4:24-30 na Matendo 5:41, 42?

9 Mfano mzuri wa kudumu namna hiyo katika sala kukitegemezwa na tendo lifaalo, ni ule wa siku za kwanza za kundi la Kikristo. Petro na Yohana waliporipoti juu ya upinzani ambao walikuwa wamepata kutoka kwa Sanhedrin (Baraza Kuu ya Kiyahudi), ebu angalia sala ya umoja iliyotolewa katika Matendo 4:24-30, sana sana maneno ya mstari wa 29: “Sasa, [Yehova], yaangalie matisho yao; ukawajalie watumwa wako kwa kunena neno lako kwa ujasiri.” Muda mfupi baadaye, mitume wote walipokuwa wamepigwa mijeledi baada ya kusimama mbele ya Sanhedrin, maandishi katika Matendo 5:41, 42, yasema hivi: “Nao wakatoka katika ile baraza, wakifurahi kwa sababu wamehesabiwa kuwa wamestahili kuaibishwa kwa ajili ya jina hilo. Na kila siku, ndani ya hekalu na nyumbani mwao, hawakuacha kufundisha na kuhubiri habari njema za Yesu kwamba ni Kristo.” Hakuna ye yote wa mitume alipata upinzani wenye kuendelea kuliko mtume Paulo, nayo maandishi yanamwonyesha akisema hivi: “Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu.”​​—⁠Flp. 4:13.

‘UHITAJI WA KUSALI WAKATI WOTE BILA KUKATA TAMAA’

10. Kabla ya kutaja mfano mwingine unaokazia sala, Luka anaripoti kwamba Yesu alikuwa akisema nini, ikielekeza kwenye utimizo wa unabii gani wa namna mbili?

10 Alipokuwa karibu na mwisho wa utumishi wake wa kidunia, Yesu alitoa mfano unaotokeza hata zaidi wa kutumia hali ya kutofautisha katika mfano kusudi apate kuweka mkazo, kama alivyoandika Luka: “[Ndipo Yesu] akawaambia mfano, ya kwamba imewapasa kumwomba Mungu sikuzote, wala wasikate tamaa.” (Luka 18:1) Walakini, kwanza, tutafikiria ni nini kilichotokeza mfano huu. (Linalopendeza ni kwamba, mara nyingi Luka anataja sababu ya kutolewa kwa mifano fulani, kama inavyoonyesha katika Luka 18:9 na 19:11.) Tukiangalia nyuma katika Luka 17:22-37, twaona kwamba Luka alikuwa akiripoti yale ambayo Yesu alisema kuhusiana na hali zitakazokuwapo wakati ambao ‘angekataliwa na kizazi hiki.’ (Luka 17:25) Ingawa maneno haya ya Yesu, yanayofanana sehemu fulani na ya Mathayo sura ya 24, yalitimizwa katika siku zake, na kufuatwa na mwisho wa taratibu ya mambo ya Kiyahudi, yana utimizo mkubwa zaidi katika siku zetu, “wakati wa mwisho” wa taratibu iliyopo ya mambo.​​—⁠Dan. 12:4.

11. (a) Hali leo zinafananaje na siku za Nuhu na Lutu? (b) Yesu alitaja jambo gani hasa, na je! hili lina ufanani wo wote leo?

11 Ni hali gani zilizopo kati ya kizazi hiki cha leo? Ndiyo, kila siku hali zinakuwa zaidi na zaidi kama siku za Nuhu wakati Mungu alipoiona dunia, “na tazama, imeharibika; maana kila mwenye mwili amejiharibia njia yake duniani.” (Mwa. 6:12, 13) Hata hivyo, Yesu hakutaja mambo hayo, walakini, mahali pake, alitaja jambo jingine lililo la maana hata zaidi. Jambo gani hilo? Wakati huo watu walikuwa wakijishughulisha sana na kazi zao na walikuwa wameridhika na orodha yao ya mambo ya kila siku ya ‘kula na kunywa, kuoa na kuolewa.’ Ndivyo ‘ilivyokuwa .  . . katika siku za Lutu’ wakati ambapo mambo zaidi yameonyeshwa kama vile kununua, kuuza, kupanda na kujenga. (Luka 17:26-29) Mahali pa kuhangaishwa na kugutushwa na uovu na jeuri iliyokuwapo, maoni yao yalikuwa ya ubaridi na ya kutojali. Kwa habari ya ushuhuda mkubwa uliotolewa na Nuhu, kwa kusema na kwa kuunda safina, ‘watu hao hawakujali.’ (Mt. 24:39; 2 Pet. 2:5) Bila shaka yaweza kusemwa vivyo hivyo juu ya maoni ya watu wa leo kwa ujumla, sana sana kuhusiana na kushuhudiwa kikamilifu ulimwenguni pote kwa ufalme wa Mungu, kama ilivyotabiriwa katika Mathayo 24:14. Wengi hawapendezwi hata kidogo; wana mambo mengine mengi ya kuchukua wakati wao na ya kukazia fikira zao. Angalia vilevile jambo kubwa lililotajwa na Yesu kuhusiana na pindi hizo mbili zilizotajwa hapo juu, kwamba kufikilizwa kwa hukumu ya mwisho kulikuja ghafula bila kutazamiwa ‘na kuwaangamiza wote. ​​—⁠Luka 17:27-29.

12. Juu ya Luka 17:31-37, twaweza kujifunza jambo gani na kulitumia katika maisha zetu?

12 Twatumaini kwamba wewe u mmoja wa wale wachache kwa kulinganisha wa-naohangaishwa na hali ulimwenguni leo na kwamba una nia ya kukaza fikira zako juu ya yale yanayosemwa na Neno la Mungu juu ya mambo haya. Iwapo, kama inavyoonyeshwa katika Luka 17:31-37, unaona uhitaji wa kuacha kuwa sehemu ya taratibu iliyopo ya mambo na kuacha kuitegemeza nawe hutaki tena ‘kusalimisha nafsi (uhai) yako’ kwa ajili yako mwenyewe, basi usipoteze wakati. Chukua msimamo wako upande wa Yehova na ufalme wake. Weka mataraja yako yote ya maisha, ya wakati huu na ya ule ujao kwa Yehova, kwa kujiweka wakf kwake ufanye mapenzi yake. Usitamani yale ambayo umeacha nyuma. “Mkumbuke mke wa Lutu.” (Luka 17:32) Mahali pake, jitambulishe na wale ambao, Yesu alisema kuwa “si [sehemu ya] ulimwengu, kama [vile] mimi nisivyo [sehemu ya] ulimwengu.”​​—⁠Yohana 17:14-17.

13. Mambo ya muhimu katika mfano wa Luka 18:2-5 ni mambo gani?

13 Sasa tukirudi kwenye mfano ulioko katika Luka 18:2-5, kuna mwingine anayeomba, wakati huu yeye ni mjane, na vilevile kuna mwanamume aliye na uwezo wa kutimiza mahitaji yake, akifananishwa na ‘hakimu asiyemcha Mungu, wala kujali wanadamu.’ Mwishowe ilimlazimu kuona kwamba mjane huyo amepata haki hata bila ya yeye kutaka, kama vile alivyosema yeye, ‘kwa sababu ya mjane huyu kuendelea kunisumbua.’ Hakukuwa na shaka juu ya kustahimili kwa mjane huyu, kuonyesha namna ‘itupasavyo kusali wakati wote na bila kukoma.’

14. (a) Tofauti na Hakimu ‘asiye mwenye haki,’ Yesu alisema Mungu atafanya nini? (b) Twaweza kujifunza nini juu ya hili kuhusiana na wakati?

14 Hakimu huyu anafanana na yule mwanamume katika Luka 11:7, kwa sababu twaona tena tofauti kabisa na namna Mungu alivyo hasa. Angalia, vilevile, maelezo zaidi ya Yesu juu ya atakayofanya Mungu, ikimtofautisha kabisa na Hakimu huyo ‘asiye mwenye haki.’ “Na Mungu, je! hatawapatia haki wateule wake . . . [ajapokuwa] ni mvumilivu kwao?” Atafanya hivyo “upesi.” (Luka 18:6-8) Twaweza kujifunza mengi kutokana na maelezo haya. Ndiyo sababu inatupasa kujaribu kuona mambo yote kama anavyoyaona Mungu, liwe ni jambo la kibinafsi au katika kutimiza kusudi lake. Kama vile alivyoeleza Petro: “[Yehova] hakawii kuitimiza ahadi yake, kama wengine wanavyokudhani kukawia, bali huvumilia kwenu [watu wa Mungu], maana hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikie toba.” Na kama vile nabii alivyoyaripoti maneno ya Yehova kwa habari ya utimizo wa ile njozi: “Ijapokawia, ingojee; kwa kuwa haina budi kuja, haitakawia.”​​—⁠2 Pet. 3:9; Hab. 2:3; tazama pia Ufunuo 6:10, 11.

15. Hii inahusuje matatizo ya kibinafsi, na ni nini kinachopaswa kuepukwa?

15 Katika magumu ya kibinafsi, twaweza kuwa na hakika kwamba ko kote kunakoelekea kuwa kukawia katika kujibu maombi yetu si kwa sababu ya Mungu kutoweza au kutotaka kujibu. Ikiwa, kama vile yule mjane tunaonewa au kuteswa, sisi twaonyeshaje imani kwamba haki itafikilizwa? Haitupasi kuendelea kusali tu, bali vilevile kuendeleza mwendo wa uaminifu. Tukishindwa kufanya hivyo kusudi tuepuke mateso, basi, hakutakuwa na haja ya kuendelea kusali. Hii isingeonyesha kukosa imani tu, bali pia tungepoteza ushuhuda wa kuwa watumishi Wakristo wa Mungu.​​—⁠2 Kor. 11:23-27; 2 Tim. 3:12.

16. Ulizo katika Luka 18:8 lawezaje kuonwa kama jambo la kushindana nalo kwa kujifaidi sisi wenyewe?

16 Huenda likaonekana kuwa jambo la kushangaza kuona kwamba Yesu alimalizia kwa ulizo hili: “Walakini, atakapokuja Mwana wa Adamu, je! ataiona imani duniani?” (Luka 18:8) Aliliacha bila kujibiwa. Ingawa hii ingeelekea kuonyesha kwamba imani haingekuwa nyingi wakati huo, hatuwezi kukata shauri kwamba hakungepatikana imani ya kweli yo yote mahali po pote duniani. Badala yake, twaweza kuliona kuwa jambo la kupambana nalo sisi binafsi. Haitupasi sisi mmoja mmoja kujitumaini, hata tuwe tumekuwa watumishi wa Yehova walio wakf kwa muda gani. (1 Kor. 10:12, 13) Si kwamba tu inatupasa kutii onyo la upole katika Luka 11:9 la kuendelea ‘kuomba​​—⁠kutafuta​—⁠​kubisha,’ bali vilevile, kama Yesu alivyokazia, uhitaji ulio wa lazima leo ni ule wa kuendelea ‘kuangalia, kukesha . . . kuwa macho.’ Hii inatuhitaji tustahimili wakati wote, kushinda mikazo ya ubaridi na upinzani wa kutoka nje, na vilevile kushinda udhaifu wetu sisi wenyewe.​​—⁠Marko 13:32-37; 14:38.

17. Zaidi ya yote, inatupasa kusali kupatana na mambo , gani, tukifuata mfano wa nani?

17 Endelea kuomba kwa imani ili kwamba uwe mwaminifu na kwamba usirudi nyuma. (Ebr. 10:39) Katika wakati wa majaribu makali, endelea kuomba, kama vile alivyofanya Yesu wakati alipokuwa na uhitaji mkubwa sana, kwamba zaidi ya yote mapenzi ya Mungu yatendeke. (Mt. 26:38-44) Mungu anapendezwa sana na sala kama hizo. Yeye anaturuhusu kama waombaji tuonyeshe kwamba twajali sana, kwamba tuna tamaa nyingi sana na kwamba tuna makusudi manyofu. Yeye ajapokuwa mvumilivu, atafikiliza haki upesi katika wakati ufaao.​​—⁠Zab. 55:16, 17; Rum. 1:9-12.

‘KESHENI, WAKATI WOTE MKIOMBA’

18. (a) Yesu alisihi na kutoa onyo gani la waziwazi mwishoni mwa unabii wake? (b) Twaweza kuepukaje “yote yatakayotokea”?

18 Kupatana na yaliyotangulia kutajwa, Injili ya Luka inaonyesha namna Yesu, akimalizia unabii wake uliohusu siku zake na zetu, alivyoonya juu ya kujifurahisha sana na mambo na mioyo yetu “[kuwa imelemewa] na ulafi, na ulevi, na masumbufu ya maisha haya; siku ile [siku ya hukumu ya mwisho ikatujia sisi] ghafula, kama mtego unasavyo.” Kisha akataja hivi: “Basi, kesheni ninyi kila wakati, mkiomba, [kusudi gani?] ili mpate kuokoka hayo yote yatakayotokea, na kusimama mbele za Mwana wa Adamu.” (Luka 21:34-36) Hii haimaanishi kwamba tunaondolewa mahali ambapo mambo yanatendekea, bali, badala yake, kwamba inatupasa kuepuka ‘tusinaswe,’ kama katika mtego, au kupatikana katika upande usiofaa. Mahali pake, inatupasa kuomba kwa bidii nyakati zote na kujitahidi kutenda kwa kupatana na sala zetu ili kwamba tupatwe tukiwa na ‘msimamo [unaokubalika] mbele za Mwana wa Adamu.’

19. Twaweza kujiuliza maulizo gani kwa kujifaidi kuhusiana na sala, nao mfano wa Nehemia unawezaje kutusaidia?

19 Kwa sababu ya kukumbushwa mara nyingi hivyo juu ya kustahimili katika sala na kutoacha kamwe, je! wewe unaomba mara nyingi kadiri gani? Je! ni nyakati zilizowekwa tu kama vile wakati wa chakula au kwenye mikutano? Je! sala zako zatoka akilini tu na kusemwa kwa kinywa, au wewe unaendelea ‘kuomba’ na kusali kwa bidii kutoka moyoni, pengine hata nyakati nyingine kwa “kuugua kusikoweza kutamkwa”? (Rum. 8:26) Hata uhitaji uwe nini, waweza kufanya kama Nehemia alivyofanya bila kuonekana alipokuwa mbele ya mfalme: ‘Mara moja nikamwomba Mungu wa mbinguni.’ (Neh. 2:4) Sala yake yenye imani ilijibiwa. Vilevile, kumbuka kwamba, ijapokuwa unaweza kusaidiwa na sala za wengine, kwa kweli hakuna ye yote awezaye kuwa mahali pako katika kutoa sala zako mwenyewe.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki