Kudumu Katika Sala Kunathawabisha
“Hawa wote walikuwa wakidumu kwa moyo mmoja katika kusali.” —Mdo.14
1. Kudumu au kustahimili katika jambo fulani kunamaanisha nini?
“KUDUMU” au “kustahimili” katika jambo fulani kunamaanisha kufuata mwendo fulani bila kubadilika na kuendelea wakati wote mpaka lengo lifanikiwe. Viarifa hivi vinatia ndani wazo la kushinda magumu na upinzani kabla ya kufaulu.
2. Ilifaa wanafunzi wa Yesu ‘wadumu katika sala’ kwa sababu gani?
2 Kwa kufaa, Matendo 1:14, linasema kuhusu kikundi kidogo cha wafuasi wa kweli wa Yesu hivi: “Hawa wote walikuwa wakidumu kwa moyo mmoja katika kusali.” Walikuwa wakifahamu kwamba Yesu alikuwa amefufuka kutoka kwa wafu na wakati huo walikuwa wametoka kushuhudia kupaa kwake kuelekea mbinguni, lakini kuna mengi ambayo hawakufahamu. Roho takatifu na uwezo waliokuwa wameahidiwa ilikuwa bado haijaja juu yao. (Matendo 1:8) Walikuwa bado hawajafahamu kabisa sababu ya Mungu kuruhusu Kiongozi wao mpendwa apigiliwe juu ya mti wa mateso wenye kuogopesha sana. Watu waliofanya jambo hilo walikuwa wangali wanatawala na kulikuwa hakuna wonyesho wo wote wa kugeuza maoni yao. Walikuwa wanadumu katika upinzani wao usio na huruma. Kwa hiyo wafuasi wa Yesu, wakitambua uhitaji wao, walidumu katika sala kwa Yule ambaye walikuwa wanamwamini.
3. (a) Sala zao zilijibiwa wakati gani, nalo jambo hilo lilihusuje mambo waliyotanguliza? (b) Ni ushuhuda gani wenye kuenea sana uliotolewa katika siku hizo za kwanza?
3 Kuanzia na siku ya Pentekoste, sala zao zenye imani zilijibiwa. kweli kweli kuliko vile walivyokuwa wakitazamia. Walianza kuthamini maneno ya mwisho ya Yesu kwao kabla ya kupaa kwake. Mahali pa kutanguliza wakati, kama inavyoonyeshwa na ulizo lao “je! Bwana, wakati huu ndipo unapowarudishia Israeli ufalme?” sasa fikira zao zilikuwa zimekazwa juu ya mgawo wao wa kuwa “mashahidi wa [Yesu] katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi.” (Matendo 1:6-8) Lo! namna Petro alivyotoa ushuhuda wenye uhodari na ulio kamili wakati wa siku ya Pentekoste, kutia na tangazo lake “Yesu huyo Mungu alimfufua, na sisi sote tu mashahidi wake.”—Matendo 2:32; tazama pia Matendo 2:40; 3:15; 4:33; 5:32.
4. Wafuasi wa Yesu leo wanauonaje uhitaji wa kudumu katika sala?
4 Vivyo hivyo leo, inawapasa wafuasi wa kweli wa Yesu kudumu katika sala zao kwa “yeye awezaye kufanya mambo ya ajabu mno kuliko yote tuyaombeayo au tuyawazayo.” (Efe. 3:20) Ingawa wana ufahamu mwingi kuhusu kusudi la Yehova na namna linavyotimizwa, kungali na mengi wasiyofahamu kwa ukamili, juu ya wakati wenyewe wa matukio ya wakati ujao na namna maandiko mengi yanavyotimizwa kuhusiana na mwisho kamili wa taratibu ya mambo ya Shetani. Hii inatia ndani mitajo ya watu wa Yehova ya kinabii, kama ule unaopatikana katika Isaya 26:20: “Njoni, watu wangu . . ujifiche kitambo kidogo, mpaka ghadhabu hii itakapopita.”
5. (a) Ni lazima Mashahidi wa Yehova wawe na mambo gani mawili? (b) Ujumbe wa ufalme wa Mungu umekuwa na matokeo gani katika ulimwengu, nalo jambo hilo lilitabiriwaje?
5 Lililo la maana zaidi sasa ni kwamba, watumishi wa Yehova wanatambua kwamba kuna kazi kubwa ya kufanya na kuna msimamo wa kuendelezwa, kama inavyoonyeshwa na jina lao walilopewa na Mungu, Mashahidi wa Yehova. (Isa. 43:10-12) Kazi hii pamoja na msimamo wao unawahitaji wawe na ustahimilivu. Ujumbe wa ufalme wa Mungu unapasa kuhubiriwa mataifa na falme za ulimwengu. (Yer. 25:15-30) Ufalme wa Mungu “utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu.” Ujumbe huo haupendwi na watawala wa siku za leo ambao wanaonyesha roho ya utukuzaji wa taifa. Mwungano wao wa upinzani unakuwa dhahiri zaidi na zaidi. “Wanafanya shauri pamoja, juu ya [Yehova], na juu ya masihi wake [Mfalme aliyewekwa, Kristo Yesu].”—Zab. 2:2-6; Dan. 2:44.
6. (a) Ni sifa gani zinazotakiwa leo? (b) Kila hali inapaswa kuonwaje, nao uhitaji wetu umetimizwaje kuhusiana na hili?
6 Ili watumishi wa Mungu leo waweze kusema kama vile mitume wa karne ya kwanza walivyosema, “inatupasa kumtii Mungu [kama mtawala] kuliko wanadamu,” wanahitaji kuwa na ujasiri. (Matendo 5:29) Ujasiri na uhodari huo hautegemei uwezo au hali bora ya mwili ambayo ni wachache sana wetu wanaoweza kujivunia kuwa nayo. Ili tuweze kuonyesha sifa hizi tunahitaji kufahamu vizuri sana kusudi la Mungu, vilevile kanuni na matakwa ya Mungu ya haki yaliyowekwa katika Neno la Mungu. Kati ya wanadamu, watu hawajapata tena kujitoa sana kwa choyo, jeuri, upotovu na uchafu wa namna zote kama wanavyofanya sasa. (2 Tim. 3:1-5) Kuna mikazo mingi tofauti tofauti ya kushindana nayo katika hizi “siku za mwisho.” Hii maana yake ni kwamba inatupasa kujifunza namna ya kuona kila hali na kila tatizo kama vile Mungu alionavyo. Tutaweza kupata ufahamu wa kweli kupitia kwa Neno lake na kwa msaada wa roho yake na tengenezo lake ikiwa tu tutamtegemea yeye. (Zab. 36:9) Kwa hiyo, tunahitaji kudumu katika sala na kusitawisha imani ya kweli na yenye nguvu, imani ishindayo. Yehova akiyajua mahitaji yetu, ametupa kwa fadhili na kwa wakati wake vitia-moyo vingi, mashauri na maonyo juu ya mambo haya ya maana katika Neno lake. Kwanza, kunalo ulizo juu ya ni nani anayeweza kusali na afanye hivyo chini ya matakwa au hali gani, iwapo yako.
YEHOVA—“MSIKIAJI WA SALA”
7. (a) Ni nani “Msikiaji wa sala,” na ni kwa sababu gani wakati wote Daudi alikuwa na uhitaji kuhusiana na jambo hili?
7 Yehova alimwongoza mtumishi wake Daudi aandike hivi: “Ee Msikiaji wa sala, watu wote wenye mwili watakujia wewe.” (Zab. 65:2, NW) Mara nyingi Daudi aliona uhitaji wa kudumu katika sala, kama inavyoonyeshwa katika nyingi za zaburi alizoziandika. Nyakati nyingine uhitaji ulikuwa wa uharaka kwa sababu ya mkazo usio na huruma kutoka kwa adui zake, kama vile inavyoonyeshwa katika Zaburi 70:1-5. Nyakati nyingine uhitaji ulitokea kwa sababu ya udhaifu na makosa yake, mengine yakiwa mazito sana. Iwapo wewe mwenyewe unajiona kuwa mtu asiyestahili kumfikia Mungu kwa sala kwa sababu kama hiyo, twapendekeza usome na kusoma tena na tena Zaburi 51:1-12. Maneno hayo yaliyoandikwa katika mstari wa 9 mpaka 11 yanaweza kuwa msingi mzuri wa sala yako mwenyewe.
“Usitiri uso wako usitazame dhambi zangu; [uyafute makosa yangu yote]. Ee Mungu, uniumbie moyo safi, uifanye upya roho iliyotulia ndani yangu. Usinitenge na uso wako, wala roho yako [t]akatifu usiniondolee.”
8. Katika kumkaribia Yehova, uchaguzi ni wa nani hasa, nao unakuwa chini ya matakwa gani?
8 Je! usemi huu kuja kwa “watu wote wenye mwili” kwa “Msikiaji wa sala” unamaanisha kwamba mtu ye yote yu huru kufanya hivyo wakati wo wote anapotaka? Sivyo. Kwa kweli ni kinyume cha hilo. Kama inavyotajwa baadaye katika zaburi iyo hiyo. “[Mwenye furaha ni] mtu umchaguaye [wewe yaani, Yehova], na kumkaribisha akae nyuani mwako.” (Zab. 65:4) Ijapokuwa wote wanaalikwa, ni lazima kumkaribia kuwe ni kwa unyofu wa moyo wote. Ingawa huenda imani yako isiwe yenye nguvu mwanzoni, ni lazima iwe ya kweli. “[Yehova] yu karibu na wote wamwitao . . . kwa uaminifu.”—Zab. 145:18.
9. Sababu gani lazima wakati wote sala tunazomtolea Yehova zipitishiwe katika jina la Yesu?
9 Kwa kuongozea, ni lazima sala zetu kwa Yehova ziwe kupitia kwa jina la Kristo Yesu wakati wote, njia pekee iliyowekwa na Mungu. (Yohana 14:13, 14) Kwa kushukuru sana tunatambua kazi ya Kristo ya kukomboa wanadamu wote, na kwamba sasa yeye anatumikia kama kuhani mkuu wa Mungu, ambaye kupitia kwake twaweza kukikaribia “kiti cha enzi cha fadhili zisizostahilika tukiwa na uhuru wa kusema, tupate kupokea rehema na kuona fadhili zisizostahilika za kutusaidia wakati unaofaa.”—1 Tim. 2:4-6; Ebr. 2:9; 4:14-16, NW.
10. Zaburi 15 inatoaje msaada zaidi kuhusiana na jambo hili?
10 Kwa habari zaidi juu ya namna ya mtu ambaye Mungu amchagua, twapendekeza usome, kwenye Zaburi ya 15, jibu lililoongozwa kwa roho kwa ulizo hili: “[Ee Yehova], ni nani atakayekaa katika hema yako? Ni nani atakayefanya maskani yake katika kilima chako kitakatifu?” Kanuni zinazotajwa humo lazima zikubaliwe nasi kuwa za haki; na ni lazima ziwe mradi wetu, hata ingawa nyakati nyingine huenda tukakosea katika kuzifuata.
11. Maandiko Matakatifu yaliandikwa yawafaidi nani kwanza? (b) Ni kitia-moyo gani kinachoweza kupatikana katika sala ya Sulemani katika 1 Wafalme 8:41-43?
11 Pengine wasema, na ndivyo ilivyo, kwamba Maandiko Matakatifu, kutia na yale yaliyokwisha kutajwa, yanahusu watu wa Mungu na yanatumika juu yao, sana sana kundi la Kristo ambalo washiriki wake ni Israeli wa kiroho, “Israeli wa Mungu.” (Rum. 15:4; 1 Kor. 10:11; Gal. 6:16) Kwa kujilinganisha nao, labda unajiona kuwa mtu wa nje au mgeni, kwa sababu ya njia yako ya maisha ya wakati uliopita na kwa kukosa kupendezwa na dini kabisa. Wengi wamo katika hali hiyo leo. Hata hivyo, usijiachilie ushindwe upesi. Kumbuka kwamba kati ya maombi mengi ambayo Sulemani alimtolea Yehova wakati wa kuzindua hekalu la Yehova, aliombea “hata mgeni naye, asiyekuwa mmoja wa watu wako Israeli, atakapokuja kutoka nchi iliyo mbali sana kwa ajili ya jina lako.” Yeye aliomba kwamba “basi, usikie [Yehova] huko mbinguni, makao yako, ukatende kwa kadiri ya yote atakayokuomba mgeni huyo; ili watu wote wa dunia wapate kulijua jina lako, na kukucha wewe kama watu wako Israeli.”—1 Fal. 8:41-43.
12, 13. (a) Isaya aliongozwa aandikeje juu ya “wageni”? (b) Mitajo hii ni kwa ajili ya nani nayo yaweza kutumiwaje?
12 Ufahamu zaidi na kutiwa moyo kunakotolewa “wageni” hawa unapatikana katika Isaya 56:6-8:
“Na wageni, walioandamana na [Yehova] ili wamhudumu, na kulipenda jina la [Yehova], kuwa watumishi wake; kila aishikaye sabato asiivunje, na kulishika sana agano langu; nitawaleta hao nao hata mlima wangu mtakatifu, na kuwafurahisha katika nyumba yangu ya sala; makafara yao na dhabihu zao zitakubaliwa juu ya madhabahu zangu; kwa maana nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala kwa mataifa yote.”
13 Lo! namna yalivyo masimulizi yenye kukaribisha! “Wageni” hawa hawalazimishwi, walakini wanajiunga na Yehova kwa furaha kwa sababu ya kulipenda jina lake na kupenda yote linalowakilisha. Maisha yao yote ambayo yamewekwa wakf kwa Yehova (wala si siku moja tu katika siku saba), yanakuwa ya ‘kuadhimisha sabato; kwa njia hiyo wanaingia katika mapumziko Yake, kama anavyoeleza Paulo katika Waebrania 4:1-10. Vilevile mtume Paulo anaonyesha namna ‘matoleo na dhabihu za kuteketezwa’ zinavyotumika kwa Wakristo waliojiweka wakf, anapoandika hivi:
“Kwa njia yake yeye, na tumpe Mungu dhabihu ya sifa daima, yaani, tunda la midomo iliungamayo jina lake. Lakini msisahau kutenda mema na kushirikiana; maana [dhabihu] kama hizo ndizo zimpendezazo Mungu.”—Ebr. 13:15, 16.
14. Katika siku za Isaya ‘nyumba ya sala’ ilikuwa nini, nayo ilifananisha nini?
14 Katika siku za Isaya, ‘nyumba ya Yehova ya sala,’ bila shaka ilikuwa hekalu alilolijenga Sulemani. Hekalu hili lilikuwa mfano wa hekalu kuu la kiroho la Mungu. Mungu mwenyewe anakaa katika Patakatifu Zaidi pa hekalu hili la kiroho huko mbinguni. Katika chumba Kitakatifu cha hekalu hili ndimo walimo wafuasi wa Yesu Kristo waliozaliwa kwa roho ambao bado wako duniani. Vilevile wanaonyeshwa wakiwa katika nyua za kidunia zilizowekwa kwa ajili ya makuhani katika hekalu hili la kiroho.
15. (a) “Mkutano mkubwa” unatambulishwaje katika Ufunuo 7:9-17? (b) Hii inawahusuje Mashahidi wa Yehova leo?
15 Yanayolingana sawasawa na yaliyotangulia kutajwa, na baada ya kusoma Ufunuo 7:1-8 juu ya kundi la Kikristo ambalo washiriki wake ni Israeli wa kiroho, hesabu yake ikiwa 144,000, sasa twasoma juu ya “mkutano mkubwa” ambao pia wafurahia kibali ya Mungu, na kama uthibitisho wa kujiweka wakf kwake “wanamtolea utumishi mtakatifu mchana na usiku katika hekalu lake.” (Ufu. 7:15, NW) Njozi hii nzuri inauonyesha “mkutano mkubwa” wa mataifa yote kama ukimtumikia Yehova katika hekalu lake, yaani, katika nyua za kidunia ambazo zimewekwa kwa wale wasiokuwa Waisraeli wa kiroho, kana kwamba katika “nyua za watu wa mataifa.” Leo, wengi wa mashahidi wa Yehova wanajitambulisha kuwa wa huu “mkutano mkubwa,” wakiwa na tumaini la uzima wa milele katika ufalme wa Mungu kwenye dunia ya paradiso. Yesu aliwataja kuwa “kondoo wengine,” “ambao si wa zizi hili.” Kama alivyoendelea kusema Yesu, kondoo wake wote wa kweli ‘wanakuwa kundi moja, [chini] ya mchungaji mmoja.’ —Luka 12:32; Yohana 10:16.a
16. Ni mataraja gani yenye kuthawabisha yaliyowekwa mbele ya wale wanaomtafuta Yehova kwa bidii?
16 Unakaribishwa ushirikiane na kikundi hiki kilichofungamanishwa karibu karibu cha waabudu wa kweli wa Yehova. Utapata kuona hili kuwa jambo la kufurahisha. Litakuwa la kukusaidia kweli kweli na kukutia moyo katika kusitawisha ustahimilivu katika sala katika imani ya kweli. Hii inaleta matokeo, kwa kuwa Yehova “huwapa thawabu wale wamtafutao” kwa bidii. (Ebr. 11:6) Jambo hili la kudumu katika sala, linaloshikamana na imani, lilikaziwa katika njia ya kupendeza sana katika Injili ya Luka.
17. Yaliyompata Yakobo alipopigana mweleka na malaika yanatoaje mfano mzuri wa kustahimili?
17 Wakati huu tunataka kukumbusha mfano mmoja usio wa kawaida wa kustahimili na namna ulivyothawabishwa sana. Twazungumza juu ya wakati ambao Yakobo alijipata akipigana mweleka usiku kucha na malaika aliyekuwa amechukua umbo la mwanadamu. Hata ingawa malaika alitegua uvungu wa paja lake, Yakobo alizidi kumkamata, mpaka, kama alivyosema yeye mwenyewe: “Sikuachi, usiponibariki.” Kisha malaika akasema jambo ambalo lingekuwa na maana kubwa sana na yenye kudumu: “Jina lako hutaitwa tena Yakobo, ila Israeli, maana umeshindana na Mungu, na watu nawe, umeshinda.” Vilevile mwishowe alimbariki Yakobo. Kwa hakika Yakobo alifanya zaidi ya kufuatia mwendo fulani bila kubadilika na kwa kuendelea wakati wote. Ilimpasa apigane mweleka kwa halisi na kuendelea kufanya hivyo akiwa katika hali ya kulemaa mpaka alipopata kile alichokuwa akitafuta. Yeye alibarikiwa sana, kama vile alivyosema: “Nimeonana na Mungu uso kwa uso, na nafsi yangu imeokoka.” Lo! mfano bora namna gani wa kudumu katika sala!—Mwa. 32:24-30.
[Maelezo ya Chini]
a Tazama makala ‘‘Kukusanywa kwa Mataifa Yote Kwenye Hekalu Moja kwa Ibada,” katika toleo la Juni 1, 1973, la Mnara wa Mlinzi; vilevile kitabu Paradise Restored to Mankind—By Theocracy!. uku. 80, maf. 14, 15.