Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w91 12/15 kur. 14-18
  • Kaa Karibu Na Yehova

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kaa Karibu Na Yehova
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Itikio Kulingana na Kusudi la Mungu
  • Mifano ya Kukaa Karibu na Yehova
  • Yesu, Kielelezo Chetu
  • Kumtwika Yehova Mizigo Yetu
  • Sala na Tumaini Kuendelea
  • Kumwomba Yehova Ili Usikiwe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Kwa Nini Tusali Bila Kukoma?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Jinsi Unavyoweza Kumkaribia Mungu
    Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
  • Uwe Imara Katika Sala
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
w91 12/15 kur. 14-18

Kaa Karibu Na Yehova

“Katika sala, mkidumu.”—WARUMI 12:12.

1. Ni nini mapenzi ya Yehova kuhusu sala, na mtume Paulo alitoa kitia-moyo gani kuhusu kusali?

YEHOVA ni “Mungu atoaye tumaini” kwa watu wake wote waaminifu. Akiwa “Msikiaji wa sala,” yeye husikiliza sihi zao za kuomba msaada kupata tumaini la shangwe ambalo yeye huweka mbele yao. (Warumi 15:13; Zaburi 65:2, NW) Na kupitia Neno lake, Biblia, yeye huwatia moyo watumishi wake wote wamjie wakati wowote wanaotaka. Yeye yupo sikuzote, akitamani kupokea mahangaiko yao ya ndani kabisa. Kwa hakika, yeye huwatia moyo ‘wadumu katika sala’ na ‘kuomba bila kukoma.’a (Warumi 12:12, NW; 1 Wathesalonike 5:17) Ni mapenzi ya Yehova kwamba Wakristo wote wamwendee katika sala, wakimtolea yote yaliyomo mioyoni mwao na kufanya hivyo katika jina la Mwana wake mpendwa, Yesu Kristo.—Yohana 14:6, 13, 14.

2, 3. (a) Kwa nini Mungu alituhimiza ‘tudumu katika kusali’? (b) Tuna uhakikishio gani kwamba Mungu anataka tusali?

2 Ni kwa nini Mungu anatupa himizo hilo? Kwa sababu mibano na madaraka ya maisha yaweza kutulemeza sana hivi kwamba tungeweza kusahau kusali. Au huenda matatizo yakatushinda na kutufanya tuache kushangilia katika tumaini na kukoma kusali. Kwa sababu ya mambo hayo yote, tunahitaji makumbusho yanayotutia moyo tusali na kukaribia sana chanzo cha msaada na faraja, Yehova Mungu wetu.

3 Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yakobo 4:8) Naam, Mungu si mwenye fahari nyingi mno wala mwenye kuwa mbali mno asiweze kuyasikia maneno tunayomwambia, ijapokuwa hali yetu ya kibinadamu ya kutokamilika. (Matendo 17:27) Zaidi ya hayo, yeye si mwenye kutojali wala kukosa ufikirio. Mtunga zaburi asema hivi: “Macho ya BWANA [Yehova, NW] huwaelekea wenye haki, na masikio yake hukielekea kilio chao.”—Zaburi 34:15; 1 Petro 3:12.

4. Usikivu wa Yehova kwa sala waweza kutolewa kielezi gani?

4 Yehova hukaribisha sala. Twaweza kulinganisha hilo na mkusanyiko ambapo watu kadhaa wanaongea pamoja. Wewe uko huko ukisikiliza wengine wakiongea. Daraka lako ni lile la mtazamaji. Lakini mtu fulani akugeukia, asema jina lako, na kuelekeza maneno yake kwako. Hilo lavuta usikivu wako kwa njia ya pekee. Vivyo hivyo, Yehova huelekeza usikivu wake kwa watu wake sikuzote, popote wawezapo kuwa. (2 Mambo ya Nyakati 16:9; Mithali 15:3) Kwa hiyo yeye husikia maneno yetu, ikiwa kana kwamba anatutazama kwa njia ya kutulinda na kupendezwa nasi. Hata hivyo, tunapoliita jina la Mungu katika sala, usikivu wake unavutwa, na sasa anakazia fikira zake kwetu katika njia dhahiri. Kwa nguvu zake, Yehova aweza hata kuona na kufahamu maombi ya mtu yasiyosemwa yaliyofichwa katika sehemu za ndani kabisa za moyo na akili yake. Mungu anatuhakikishia kwamba atakaribia wale wote wanaoliita jina lake kwa moyo mweupe na kutafuta kukaa karibu naye.—Zaburi 145:18.

Itikio Kulingana na Kusudi la Mungu

5. (a) Shauri la ‘kudumu katika kusali’ huonyesha nini kuhusu sala zetu? (b) Mungu hujibuje sala?

5 Shauri la kudumu katika sala huonyesha kwamba huenda nyakati nyingine Yehova akaturuhusu tuendelee kusali juu ya jambo kwa kitambo fulani kabla ya itikio lake kuwa wazi. Twaweza hata kuelekea kuchoka kumwomba Mungu ili kupata kibali au fadhili-upendo ambazo huenda zikaonekana kuhitajiwa sana lakini ambazo zachelewa sana kuja. Kwa hiyo, Yehova Mungu atusihi tusijiachilie kwa mwelekeo wowote wa jinsi hiyo bali tuendelee kusali. Twapaswa kuendelea kumwomba kuhusu mahangaiko yetu, tukiwa na uhakika kwamba anastahi sala yetu na atatosheleza uhitaji wetu wa kweli, si lile tu ambalo huenda ikawa tulilifikiria. Yehova Mungu bila shaka husawazisha maombi yetu kulingana na kusudi lake. Kwa mfano, wengine huenda wakaathiriwa na ombi letu. Twaweza kufananisha jambo hilo na lile la baba ambaye aombwa na mwana wake baiskeli. Baba huyo ajua kwamba akimnunulia mwana wake baiskeli, mwana wake mkubwa angetaka moja pia. Kwa kuwa mwana mmoja huenda akawa mdogo sana kuwa na baiskeli, huenda baba huyo akaamua kutonunua moja kwa wakati huo. Katika njia iyo hiyo, kulingana na kusudi lake na kuwekwa kwa wakati wa mambo fulani, Baba yetu wa kimbingu huamua lile litakalokuwa bora zaidi kwetu sisi na kwa wengine.—Zaburi 84:8, 11; linganisha Habakuki 2:3.

6. Yesu alitoa kielezi gani kuhusu sala, na kudumu katika sala huonyesha nini?

6 Chenye kustahili kuangaliwa ni kielezi ambacho Yesu alitoa kuhusu uhitaji wa wanafunzi wake “kumwomba Mungu sikuzote, wala wasikate tamaa.” Mjane mmoja, asiyeweza kupata haki, alidumu katika ombi lake kwa hakimu wa kibinadamu mpaka alipopokea haki hatimaye. Yesu aliongeza hivi: “Na Mungu, je! hatawapatia haki wateule wake?” (Luka 18:17) Kudumu katika sala huonyesha imani yetu, tegemeo letu kwa Yehova, nia yetu kukaa karibu naye na kufanya ombi letu rasmi, tukiacha matokeo mikononi mwake.—Waebrania 11:6.

Mifano ya Kukaa Karibu na Yehova

7. Twaweza kuigaje imani ya Habili katika kukaa karibu na Yehova?

7 Biblia imejaa masimulizi ya sala zilizosemwa na watumishi wa Mungu. Hayo “yaliandikwa ili kutufundisha sisi; ili kwa saburi na faraja ya maandiko tupate kuwa na tumaini.” (Warumi 15:4) Tumaini letu linaimarishwa kwa kufikiria kwetu mifano fulani ya wale waliokaa karibu na Yehova. Habili alimtolea Mungu dhabihu yenye kukubalika, na ingawa hakuna sala yoyote ambayo imerekodiwa, hapana shaka kwamba alimsihi Yehova katika sala kwamba toleo lake liweze kukubaliwa. Waebrania 11:4 husema hivi: “Kwa imani Habili alimtolea Mungu dhabihu iliyo bora kuliko Kaini; kwa hiyo alishuhudiwa kuwa ana haki.” Habili alijua juu ya ahadi ya Mungu kwenye Mwanzo 3:15, lakini kwa kulinganishwa na yale tujuayo sasa, alijua machache sana. Hata hivyo, Habili alitenda kulingana na maarifa aliyokuwa nayo. Kwa hiyo leo, wengine wa wale ambao wamependezwa hivi karibuni na kweli ya Mungu bado hawana maarifa mengi, lakini wao husali na kufaidika kadiri wawezavyo na maarifa walio nayo, kama Habili alivyofanya. Naam, wao hutenda katika imani.

8. Ni kwa nini twaweza kuwa na hakika kwamba Abrahamu alikaa karibu na Yehova, na twapaswa kujiuliza swali gani?

8 Mtumishi wa Mungu mwingine mwaminifu alikuwa Abrahamu, “baba yao wote waaminio.” (Warumi 4:11) Leo, zaidi ya wakati mwingine wowote, tunahitaji imani imara, nasi tunahitaji kusali katika imani, kama Abrahamu alivyofanya. Mwanzo 12:8 husema kwamba “akamjengea BWANA [Yehova, NW] madhabahu huko, akaliitia jina la BWANA [Yehova, NW].” Abrahamu alijua jina la Mungu na akalitumia katika sala. Mara kwa mara alidumu katika sala kwa moyo mweupe, akiliitia “jina la BWANA [Yehova, NW], Mungu wa milele.” (Mwanzo 13:4; 21:33) Abrahamu alikuwa akimwitia Mungu katika imani iliyompa sifa nzuri. (Waebrania 11:17-19) Sala ilimsaidia Abrahamu aendelee kushangilia sana katika tumaini la Ufalme. Je! tunaufuata mfano wa Abrahamu wa kudumu katika sala?

9. (a) Kwa nini sala za Daudi ni zenye manufaa sana kwa watu wa Mungu leo? (b) Tokeo laweza kuwa nini tukisali kama Daudi alivyosali kukaa karibu na Yehova?

9 Daudi alitokeza kwa habari ya kudumu katika sala, na zaburi zake huonyesha mambo ambayo yapasa kuwa katika sala. kwa mfano, watumishi wa Mungu waweza kwa kufaa kusali kuomba mambo kama vile wokovu au ukombozi (3:7, 8; 60:5), mwongozo (25:4, 5), ulinzi (17:8), msamaha wa dhambi (25:7, 11, 18), moyo ulio safi (51:10). Daudi alipohisi kuhuzunika, alisali hivi: “Uifurahishe nafsi ya mtumishi wako.” (86:4) Twaweza kusali vivyo hivyo kupata shangwe ya moyoni, tukijua kwamba Yehova hutamani sisi tushangilie katika tumaini letu. Daudi alikaa karibu na Yehova na akasali hivi: “Nafsi yangu inakuandama sana; mkono wako wa kuume unanitegemeza.” (63:8) Je! tutakaa karibu na Yehova, kama Daudi alivyofanya? Tukifanya hivyo, yeye atatutegemeza pia.

10. Mtunga zaburi Asafu alikuwa na mawazo gani mabaya wakati fulani, lakini alikuja kutambua nini?

10 Ikiwa tutakaa karibu na Yehova, tunahitaji kuepuka kuonea wivu hali ya waovu kwa sababu ya maisha zao za kutojali mambo na zenye kufuatia mambo ya kimwili. Wakati mmoja mtunga zaburi Asafu aliona kwamba kumtumikia Yehova hakukuwa na faida yoyote, kwani waovu ‘hustarehe sikuzote.’ Bado alifahamu kwamba kusababu kwake hakukufaa na kwamba waovu wapo “penye utelezi.” Alitambua kwamba hakukuwa jambo lililo bora zaidi ya kukaa karibu na Yehova, naye alijieleza mwenyewe kwa Mungu kwa njia hii: “Mimi ni pamoja nawe daima, umenishika mkono wa kuume. Maana wajitengao nawe watapotea . . . Nami kumkaribia Mungu ni kwema kwangu; nimefanya kimbilio kwa Bwana MUNGU [Yehova, NW], niyahubiri matendo yako yote.” (Zaburi 73:12, 13, 18, 23, 27, 28) Badala ya kuonea wivu maisha ya kutojali mambo ya waovu, wale watu wasio na tumaini, acheni tumwige Asafu katika kukaa karibu na Yehova.

11. Kwa nini Danieli ni mfano mwema wa kukaa karibu na Yehova, na sisi twaweza kumwigaje?

11 Danieli alidumu kwa uthabiti katika sala, hata alipokabili hatari ya kuwa katika tundu la simba kwa sababu ya kutotii vizuio rasmi vya sala. Lakini Yehova ‘alimtuma malaika wake, naye aliyafumba makanwa ya simba,’ akimwokoa Danieli. (Danieli 6:7-10, 22, 27) Danieli alibarikiwa sana kwa kudumu kwake katika sala. Je! sisi pia hudumu katika sala, hasa wakati tunapokabili upinzani kwa kuhubiri kwetu Ufalme?

Yesu, Kielelezo Chetu

12. (a) Mwanzoni mwa huduma yake, Yesu aliweka mfano gani kuhusu sala, na hilo laweza kuwanufaishaje Wakristo? (b) Sala ya Yesu ya kielelezo inafunua nini juu ya sala?

12 Rekodi huonyesha kwamba kutoka mwanzoni kabisa mwa huduma yake ya kidunia, Yesu alikuwa akisali. Mwelekeo wake wa kusali alipokuwa akibatizwa uliwawekea mfano mwema wale wanaopata ubatizo wa maji katika nyakati za kisasa. (Luka 3:21, 22) Mtu angeweza kusali kuomba msaada wa Mungu ili atekeleze lile lililofananishwa na ubatizo wa maji. Yesu pia alisaidia wengine wamkaribie Yehova katika sala. Katika pindi moja wakati Yesu alipokuwa akisali mahali fulani, mmoja wa wanafunzi wake alimwambia hivi baadaye: “Bwana, tufundishe sisi kusali.” Yesu kisha akasimulia ile inayojulikana kwa kawaida kuwa sala ya kielelezo, ambayo ndani yayo mpangilio wa habari huonyesha kwamba jina na kusudi la Mungu lapasa kuwekwa kwanza. (Luka 11:1-4) Hivyo, katika sala zetu tunahitaji kudumisha hali ya kutanguliza mambo ya maana na usawaziko, kutoacha “mambo yaliyo ya maana zaidi.” (Wafilipi 1:9, 10, NW) Bila shaka, kuna nyakati za uhitaji wa pekee au wakati tatizo hususa lahitaji kuzungumziwa. Kama Yesu, Wakristo waweza kumwendea Mungu katika sala ili kutafuta imara ya kutekeleza migawo fulani au kukabili maja-ribu au hatari fulani. (Mathayo 26:36-44) Kwa hakika, sala za kibinafsi zaweza kwa kweli kutia ndani kila sehemu ya maisha.

13. Yesu alionyeshaje umaana wa kusali kwa ajili ya wengine?

13 Kwa mfano wake mwema, Yesu alionyesha umaana wa kusali kwa ajili ya wengine. Alijua kwamba wafuasi wake wangechukiwa na kunyanyaswa, kama yeye alivyofanywa. (Yohana 15:18-20; 1 Petro 5:9) Kwa hiyo, alimwomba Mungu ‘awalinde na yule mwovu.’ (Yohana 17:9, 11, 15, 20) Na akijua lile jaribu la pekee lililokuwa mbele ya Petro, alimwambia hivi: “Nimekuombea wewe ili imani yako isitindike.” (Luka 22:32) Inanufaisha kama nini sisi tukidumu pia katika sala kwa ajili ya ndugu zetu, tukiwafikiria wengine wala si matatizo na mapendezi yetu wenyewe tu!—Wafilipi 2:4; Wakolosai 1:9, 10.

14. Tunajuaje kwamba Yesu alikaa karibu sana na Yehova muda wote wa huduma yake ya kidunia, na twaweza kumwigaje?

14 Muda wote wa huduma yake, Yesu alidumu katika sala, akikaa karibu sana na Yehova. (Waebrania 5:7-10) Mtume Petro, kwenye Matendo 2:25-28, anukuu Zaburi 16:8 na kuitumia kwa Bwana Yesu Kristo: “Daudi ataja habari zake, Nalimwona Bwana [Yehova, NW] mbele yangu sikuzote, kwa kuwa yuko upande wa mkono wangu wa kuume, nisitikisike.” Twaweza kufanya hivyo pia. Twaweza kusali kumwomba Mungu akae karibu nasi, na twaweza kuonyesha uhakika wetu katika Yehova kwa kumweka mbele ya macho yetu daima kiakili. (Linganisha Zaburi 110:5; Isaya 41:10, 13.) Kisha tutaepuka matata ya aina zote, kwa kuwa Yehova atatutegemeza, nasi hatutatikisika kamwe.

15. (a) Hatupaswi kushindwa kamwe kudumu katika sala kuhusu nini? (b) Ni hadhari gani inayotolewa kuhusu ushukuru wetu?

15 Na tusishindwe kamwe kuonyesha shukrani kwa Yehova kwa wema wake wote kwetu, naam, “neema [fadhili zisizostahiliwa, NW] ya Mungu iliyozidi sana,” inayotia ndani zawadi ya Mwana wake akiwa fidia ya ukombozi kwa ajili ya dhambi zetu. (2 Wakorintho 9:14, 15; Marko 10:45; Yohana 3:16; Warumi 8:32; 1 Yohana 4:9, 10) Kwa kweli, katika jina la Yesu, kuwe “kumshukuru Mungu Baba sikuzote kwa mambo yote.” (Waefeso 5:19, 20; Wakolosai 4:2; 1 Wathesalonike 5:18) Ni lazima tuwe waangalifu tusiache shukrani yetu kwa yale tuliyo nayo ipotee kwa sababu ya kujishughulisha sana na yale ambayo hatuna au na matatizo yetu ya kibinafsi.

Kumtwika Yehova Mizigo Yetu

16. Tunaposumbuliwa na mzigo fulani, twapaswa kufanya nini?

16 Kudumu katika sala huonyesha kina cha ujitoaji wetu. Tunapomwitia Mungu, tokeo kwetu ni zuri hata kabla ya kupokea jibu kwake. Ikiwa mzigo fulani unasumbua akili zetu, twaweza kukaa karibu na Yehova kwa kufuata shauri hili: “Umtwike BWANA [Yehova, NW] mzigo wako naye atakutegemeza.” (Zaburi 55:22) Kwa kumtwika Mungu mizigo yetu yote—wasiwasi, mahangaiko, matamausho, hofu mbalimbali, na kadhalika—tukiwa na imani kamili katika yeye, tutapokea utulivu wa moyoni, “amani ya Mungu, ipitayo akili zote.”—Wafilipi 4:4, 7; Zaburi 68:19; Marko 11:24; 1 Petro 5:7.

17. Twaweza kupataje amani ya Mungu?

17 Je! amani hiyo ya Mungu inakuja papo hapo? Ingawa huenda tukapata faraja ile ile, jambo ambalo Yesu alisema kuhusu kusali ili kupata roho takatifu lathibitika kuwa kweli hapa pia: “Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa.” (Luka 11:9-13) Kwa kuwa roho takatifu ni njia ambayo tunaondolea mbali wasiwasi, tunahitaji kudumu katika kuomba ili kupata amani ya Mungu na msaada wake kwa habari ya mizigo yetu. Twaweza kuwa na uhakika kwamba kwa kudumu katika sala, tutapata faraja na utulivu wa moyoni unaotamaniwa.

18. Yehova hutufanyia nini tusipojua lile hasa la kusali katika hali fulani?

18 Lakini vipi ikiwa hatujui lile hasa la kuomba? Mauguo yetu ya ndani mara nyingi hubaki bila kusemwa kwa sababu hatuelewi hali yetu kikamili, au tunashindwa la kumwelezea Yehova. Hapo ndipo roho takatifu yawezapo kutuombea. Paulo aliandika hivi: “Maana hatujui kuomba jinsi itupasavyo; lakini Roho mwenyewe [roho yenyewe, NW] hutuombea kwa kuugua kusikoweza kutamkwa.” (Warumi 8:26) Kwa jinsi gani? Katika Neno la Mungu mna unabii mbalimbali uliopuliziwa roho na sala zinazohusu hali yetu. Ni kana kwamba yeye huruhusu hizo zituombee. Yeye hukubali hizo kuwa mambo ambayo tungeomba ikiwa tu tungejua maana yayo katika kisa chetu, na kwa hiyo anazitimiza.

Sala na Tumaini Kuendelea

19. Ni kwa nini sala na tumaini zitaendelea milele?

19 Sala kwa Baba yetu wa kimbingu itaendelea milele, hasa kwa habari ya kushukuru kwa ajili ya ulimwengu mpya na mibaraka yao yote. (Isaya 65:24; Ufunuo 21:5) Tutaendelea pia kushangilia katika tumaini, kwani tumaini la namna fulani litabaki milele. (Linganisha 1 Wakorintho 13:13.) Hatuwezi hata kuwazia yale mambo mapya ambayo Yehova ataleta, wakati ambao hatakuwa tena chini ya siku ya Sabato ya pumziko alilojiwekea mwenyewe kuelekea dunia. (Mwanzo 2:2, 3) Kwa umilele wote, atakuwa na maajabu ya upendo mbele ya watu wake, na wakati ujao una mambo matukufu kwao kwa njia ya kufanya mapenzi yake.

20. Azimio letu lapasa kuwa nini, na kwa nini?

20 Tukiwa na tumaini lenye kusisimua la jinsi hiyo mbele yetu, sisi sote na tukae karibu na Yehova kwa kudumu katika sala. Na tusiache kamwe kumshukuru Baba yetu wa kimbingu kwa mibaraka yetu yote. Wakati uwadiapo matazamio yetu yatatimizwa kwa shangwe, hata kadiri ambayo tungaliweza kuwazia au kutumainia, kwa kuwa Yehova aweza “kufanya mambo ya ajabu mno kuliko yote tuyaombayo au tuyawazayo.” (Waefeso 3:20) Kwa sababu hiyo basi, acheni tumtolee Yehova Mungu wetu, “Msikiaji wa sala,” sifa yote na utukufu na shukrani kwa umilele wote!

[Maelezo ya Chini]

a Kulingana na Webster’s New Dictionary of Synonyms, “Kudumu hudokeza sifa yenye kustahiwa karibu sikuzote; kunadokeza kukataa kuvunjika moyo kwa sababu ya kutofaulu, mashaka, au magumu, na ufuatiaji imara au thabiti kutimiza jambo au mradi fulani.”

Ungejibuje?

◻ Ni kwa nini tunahitaji kudumu katika sala?

◻ Tunajifunza nini kutokana na mifano ya sala ya kabla ya Ukristo?

◻ Mfano wa Yesu unatufunza nini juu ya sala?

◻ Twaweza kumtwikaje Yehova mizigo yetu na tokeo likiwa nini?

[Picha katika ukurasa wa 17]

Danieli alidumu katika sala lijapokuwa lile tisho la kutupwa katika tundu la simba

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki