Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w80 11/15 kur. 8-13
  • Kumwomba Yehova Ili Usikiwe

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kumwomba Yehova Ili Usikiwe
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • SABABU GANI UZIFIKIRIE SALA ZAKO
  • SABABU TWAWEZA KUMJIA YEHOVA KWA UHAKIKA
  • OMBA, SI KWA YESU, BAU KUPITIA KWAKE
  • KWA HESHIMA ISTAHILIYO
  • KWA IMANI NA UENDELEVU
  • PINDI ZA SALA
  • Jinsi ya Kusali na Kusikiwa na Mungu
    Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele
  • Kumjia Msikiaji wa Sala
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Uwe Imara Katika Sala
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Mkaribie Mungu Katika Sala
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
w80 11/15 kur. 8-13

Kumwomba Yehova Ili Usikiwe

“Mtu amwendeaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko, na kwamba huwapa thawabu wale wamtafutao.”​—Ebr. 11:6.

1-3. (a) Jambo lililoonwa juu ya kasichana fulani latuambia nini? (b) Katika jambo hilo kuna jambo gani la wazazi kujifunza?

JAMBO hilo lilitokea katika Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova. Kajapokuwa kalitazamwa kwa ukali na kunong’onezewa makaripio tena na tena na mamake, kasichana hako kaliendelea kukosa adabu. Kisha mama huyo akamwonyesha kwa ishara baba achukue wajibu huo, naye akafanya hivyo. Akiwa na bintiye, alitembea kuelekea kachumba upande wa nyuma wa jumba hilo. Kakiwa kanatambua jambo lililokuwa linakangojea, kasichana hako kalilia hivi: “Ee Yehova, tafadhali nisaidie!”

2 Kisa hicho kinaposimuliwa, kinatokeza vichekesho, na ndivyo ilivyo. Walakini je! kinachekesha tu, au kinatuambia jambo fulani? Hakika kinatuambia jambo fulani. Kasichana hako kalilijua jina la Mungu Muumba, lilikuwa Yehova, jambo ambalo ni tusichana tuchache tu tunatojua. Kalikuwa kamefunzwa ubora wa sala na kwamba Yehova anaweza kuombwa msaada wakati wa taabu. Ni kweli kwamba inachekesha kalimwomba Mungu akalinde kasipewe adabu kaliyohitaji. Walakini tusichana tusitojua mambo ndito tunatotoa ombi hilo tu? Sivyo kabisa. Taifa la Israeli kwa kurudia-rudia lilifanya jambo ilo hilo, sana sana katika siku za waamuzi. Kwa kurudia-rudia, walipokuwa wakipata adhabu waliyostahili, walimwomba Mungu awape faraja.​—Amu. 2:11-18; 4:1-3, 23, 24; 10:6-16; 11:32, 33.

3 Katika hilo kuna somo kwa wazazi wote Wakristo. Anzeni mapema maishani kusitawisha katika watoto wenu kumwamini Yehova Mungu. Wasaidieni kuthamini na kuelewa kwamba Yehova ni mtu wa kweli anayesikia sala na kuzijibu. Kufunza watoto sala tangu utoto kutasaidia sana kuwafanya wawe wenye kumwogopa Mungu watakapofikia umri wa kutoa hesabu.​—Linganisha Zaburi 22:9, 10; Mithali 22:6; 2 Timotheo 3:14, 15.

SABABU GANI UZIFIKIRIE SALA ZAKO

4, 5. (a) Ni maulizo gani kuhusiana na sala yanayotufaa kujiuliza? (b) Sababu gani maulizo hayo yanafaa sana wakati huu?

4 Lakini sala ina sehemu gani maishani mwako? Unaomba mara nyingi kadiri gani? Je! wakati mwingi unajiona kuwa mwenye shughuli sana usiweze kuomba? Au, je! unaomba haraka-haraka bila kufikiria, kama kwamba ni kazi, wajibu unaopaswa kutimizwa? Sala zako ni bora kadiri gani?

5 Maulizo hayo yenye kufanya mtu afikiri yanafaa sana wakati huu. Hata kati ya wale wanaojitambulisha kuwa watumishi wa Yehova kati yao kuna watu wasioomba kwa ukawaida. Wengine wanaona kwamba sala zao zinakosa mambo ya maana. Hilo ni jambo asilopaswa Mkristo kuchukua kwa wepesi, kwa kuwa ubora wa sala zake unaonyesha hali yake ya kiroho. Afya ya kiroho ya mtu nayo, yategemea sana kutambua kwake uhitaji wake wa kiroho na kufanya jambo fulani juu ya hilo. (Mt. 5:3) Wakati uo huo, akiufikiria ubora wa sala zake, mtu anaweza kufanya maendeleo katika hali yake ya kiroho.

SABABU TWAWEZA KUMJIA YEHOVA KWA UHAKIKA

6. Kwa sababu ya yale ambayo Biblia inasema katika Zaburi 65:2, Wafilipi 4:6 na 1 Wathesalonike 5:17, sababu gani twaweza kumwomba Mungu kwa uhakika?

6 Sababu gani twaweza kumjia Yehova kwa uhakika, tukimtazamia asikilize sala zetu? Kwanza kabisa, kwa sababu yeye anajitambulisha kuwa ‘Msikiaji wa Sala’ naye kwa kurudia-rudia anatuamuru tuombe. (Zab. 65:2, NW) Neno lake lina amri kama hizi: “Mwombe, msije mkaingia majaribuni.” (Mt. 26:41) ‘Ombeaneni.’ (Yak. 5:16) ‘Salini daima.’ (Rum. 12:12, HNWW) “Ombeni bila kukoma.” (1 The. 5:17) “Msijisumbue kwa neno lo lote; bali katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu.”​—Flp. 4:6.

7. Ni nani waliokuwa watu wa sala walio mfano mzuri?

7 Vilevile Biblia inatoa mifano, kuhusiana na jambo hilo, amri zisizokuwa za moja kwa moja za kutuamuru tuombe. Tangu Mwanzo mpaka Ufunuo, maandishi yaliyoongozwa na Mungu yamejaa mifano ya watu wa sala. Twasoma juu ya Abrahamu akimwomba Yehova. (Mwa. 21:8) Tangu wakati wa kubatizwa kwake katika Yordani mpaka kutundikwa kwake juu ya mti wa kufisha, Yesu Kristo alimwomba Baba yake mara nyingi. (Luka 3:21; 23:46) Mtume Paulo anazungumza juu ya sala kwa wazi mara nyingi sana katika barua zake. Kwa kurudia-rudia anasema juu ya kuombea wengine, anatoa vitia-moyo juu ya kuomba, au awauliza wengine wamwombee. (Flp. 1:9-11; Efe. 6:​18, 19) Kitabu cha Ufunuo kilichoandikwa na mtume Yohana chamalizia kwa sala mbili.​—Ufu. 22:20, 21.

8. Twaweza kumfikia Mungu kwa uhakika kwa sababu ya suala gani?

8 Sababu ya pili ya kuweza kumfikia Mungu kwa uhakika katika sala ni kwamba jina lake linahusika. Hiyo inatia ndani jina lake au sifa kama ‘Msikiaji wa sala.’ Vilevile, kwa kuwa jina lake limeshikamanishwa na watu wake, unaoelekea kuwa ushuhuda wa yeye kuwaacha ungeweza kufasiriwa vibaya na watazamaji kuwa unaonyesha kushindwa kwa Yehova kusaidia watumishi wake wapotovu. Jambo hilo laweza kuletea jina lake suto. Kwa hiyo, katika Zaburi 79:9, twasoma hivi: “Ee Mungu wa wokovu wetu, utusaidie, kwa ajili ya utukufu wa jina lako. Utuokoe, [ufunike] dhambi zetu, kwa ajili ya jina lako.” Musa, Yoshua, Daudi na Hezekia wote waliomba kwa sababu iyo hiyo. (Kut. 32:11, 12; Yos. 7:8, 9; 2 Fal. 19:15-19; Zab. 25:11) Naye nabii Danieli alitoa mwito wake kwa maneno haya: ‘Ee [Yehova], usikilize, ukatende, usikawie; kwa sababu mji wako na watu wako wanaitwa kwa jina lako.’ (Dan. 9:19) Ndiyo, iwapo tunalichukua jina la Yehova kweli kweli, twaweza kumwomba kwa msingi huo.

9. Sababu gani twaweza kumwomba Mungu kwa uhakika atupe rehema na kutusamehe?

9 Sababu ya tatu ya kutazamia Yehova asikilize sala zetu ni kwamba ajua kadiri ya uwezo wetu naye ataka kutusaidia. Mtunga zaburi Daudi alisema jambo hilo hivi: “Kama mashariki ilivyo mbali na magharibi, ndivyo alivyoweka dhambi zetu mbali nasi. Kama vile baba awahurumiavyo watoto wake, ndivyo [Yehova] anavyowahurumia wamchao. Kwa maana Yeye anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.” (Zab. 103:12-14; tazama pia Zaburi 51:5.) Hivyo, tunapoingia katika kosa, tunapoharibu mambo au tunapofanya kosa zito, twaweza kumwomba Yehova Mungu juu ya msingi wa udhaifu na kutokamilika kwetu.

10. Kama inavyoonyeshwa na habari ya Ayubu na ya Paulo na wengine, sababu gani twaweza kumfikia Mungu kwa uhakika?

10 Sababu nyingine kubwa ya kuweza kumjia Yehova kwa uhakika ni kwamba atasikia sala zetu juu ya msingi wa sisi kuendelea kuwa wakamilifu. Ayubu alitoa ombi lenye kuvutia kuhusiana na jambo hilo, kwa kusema hivi: “Mungu na anipime katika mizani ya haki ya hukumu, naye atajua kwamba mimi sina hatia!” (Ayubu 31:6, The New English Bible) Vivyo hivyo, Paulo aliwauliza waamini wenzake hivi: “Tuombeeni; maana tunaamini kwamba tuna dhamiri njema, tukitaka kuwa na mwenendo mwema katika mambo yote.” (Ebr. 13:18) Vilevile kuonyesha kwamba tunapaswa kuwa wanyofu kwa maoni ya Mungu inaonyeshwa waziwazi na yale aliyoandika mtume Yohana: “Wapenzi, mioyo yetu isipotuhukumu, tuna ujasiri kwa Mungu; na lo lote tuombalo, twalipokea kwake, kwa kuwa twazishika amri zake, na kuyatenda yapendezayo machoni pake.”​—1 Yohana 3:21, 22.

OMBA, SI KWA YESU, BAU KUPITIA KWAKE

11. Twaweza kumfikia Mungu katika sala kupitia kwa nani?

11 Twaweza kumfikiaje ‘Msikiaji wa sala’ mkuu? Amechagua kwamba jambo hilo liwe kupitia kwa Yesu Kristo peke yake. Kuna mpatanishi mmoja tu kati ya Mungu na wanadamu, na Kuhani Mkuu mmoja, Yesu Kristo. (1 Tim. 2:5; Ebr. 7:25, 26) Yesu mwenyewe alilisema jambo hilo waziwazi hivi: “Mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.” (Yohana 14:6) “Amin, amin, nawaambia, Mkimwomba Baba neno lo lote atawapa kwa jina langu. . . . Ombeni, nanyi mtapata; furaha yenu iwe timilifu.”​—Yohana 16:23, 24.

12, 13. (a) Kwa sababu ya yale aliyofanya mtume Yohana na Stefano, ni maulizo gani yawezayo kuulizwa? (b) Lakini sababu gani mifano ya Stefano na mtume Yohana haiwezi kuchukuliwa kuwa ni sababu ya kumwomba Yesu moja kwa moja?

12 Hata hivyo, watu wengine huuliza hivi: ‘Je! hatuwezi pia kumwomba Yesu vitu moja kwa moja? Je! mwanafunzi Stefano katika sala hakuzungumza na Yesu moja kwa moja, naye mtume Yohana akafanya vivyo hivyo?’ Ni kweli, Stefano, muda mfupi kabla ya kufa, alisema hivi: “Bwana Yesu, pokea roho yangu.” (Matendo 7:59) Naye mtume Yohana aliomba hivi: “Amina; na uje, Bwana Yesu.”​—Ufu. 22:20.

13 Walakini, twafanya vema kufikiria hali hizo. Kwa mfano, Stefano, alipata njozi, kwa kuwa alisema hivi: “Tazama! naona mbingu zimefunguka, na Mwana wa Adamu amesimama mkono wa kuume wa Mungu.” (Matendo 7:56) Mtume Yohana pia alipata njozi ya mambo ya kimbinguni. (Ufu. 1:1, 10; 4:1, 2) Alipokuwa akiona njozi hiyo, mtume huyo alimwona Yesu na kumsikia akisema hivi: “Yeye mwenye kuyashuhudia haya asema, Naam; naja upesi.” (Ufu. 22:20) Kwa kulingana na hayo, Yohana alijibu mambo hayo aliyokuwa amesikia Yesu akisema. Visa hivyo vyaweza kulinganishwa na yaliyotukia wakati mtesi Sauli wa Tarso alipokuwa akielekea Damesiki. Yesu Kristo alijifunua kwa Sauli, akasema hivi: “Sauli, Sauli, mbona waniudhi?” Kama ilivyokuwa kwa habari ya mtume Yohana na ya Stefano, Sauli alimjibu Yesu moja kwa moja: “U nani wewe, Bwana?”​—Matendo 9:4, 5.

KWA HESHIMA ISTAHILIYO

14, 15. Tunapoomba, maoni, maneno na namna ya sauti inapaswa kuonyesha nini, na sababu gani?

14 Katika kumkaribia mheshimiwa Mwenye Enzi Kuu ya ulimwenguni pote katika sala, twapaswa kumjia kwa njia ifaayo. Twaweza kumfikia tu kwa heshima nyingi sana, staha na unyenyekevu mwingi sana. Uhakika wa kwamba Neno la Mungu latuambia kwamba twaweza kumjia Mungu kwa ‘uhuru wa kusema’ haumaanishi kwamba twaweza kumzoea Muumba mkuu isivyofaa. (Ebr. 4:16, NW; 1 Yohana 3:​21, 22) Ni jambo la upumbavu na lisilofaa kama nini kuanza sala kwa usemi huu, “Habari za alasiri, Yehova!” Twaweza kumjia kwa uhuru wa kusema kwa sababu ya imani na uhakika wetu katika nia Yake ya kusikiliza na kwa sababu ya sisi kuendelea kuwa wakamilifu. Walakini twapaswa kufanya hivyo kwa staha nyingi sana, kwa heshima ifaayo.​—Linganisha Mhubiri 5:1, 2.

15 Hatupaswi kusahau wakati wo wote kwamba Yehova Mungu yuko juu sana kutupita. Kwa sababu ya kuwa hapa duniani na umbo letu la kimwili, sisi tu chini ya malaika katika uwezo na utukufu. (Ebr. 2:7) Zaidi ya hayo, hatujakamilika, tu wanadamu wenye dhambi. Kwa kufaa, basi, katika sala zetu twapaswa kutumia maneno na namna ya sauti inayoonyesha kwamba tunafahamu na kuthamini uhusiano wetu na Yehova Mungu, kwa kuwa yeye huwasikiliza wanyenyekevu peke yao ‘watetemekao wasikiapo neno lake.’ (Isa. 66:2) Yesu Kristo alikazia kanuni hiyo vizuri katika mfano wake juu ya watu wawili walioenda hekaluni katika Yerusalemu kuomba! Yehova Mungu hakumsikia Farisayo mwenye kiburi, mwenye kujiona kuwa mwenye haki, bali kwa wazi alisikia na kujibu sala ya mtoza ushuru mnyenyekevu na mwenye majuto.​—Luka 18:9-14.

KWA IMANI NA UENDELEVU

16. Ni maandiko gani yanayoonyesha maana ya imani katika kusali?

16 Takwa jingine la maana ili kusikiwa na Yehova ni kumjia kwa imani. Kwa kurudiwa-rudiwa, takwa hilo la sala linavutwa kwenye fikira zetu katika Neno la Mungu. Yesu alisema hivi: “Mkiwa na imani kiasi cha punje ya haradali . . . halitakuwako neno lisilowezekana kwenu.” (Mt. 17:20) Katika Waebrania 11:6 twaambiwa kwamba ili kumpendeza Mungu twapaswa kuwa na imani ya kwamba yeye yupo na zaidi kwamba “huwapa thawabu wale wamtafutao.” Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: ‘Endeleeni kuomba kwa imani, bila kuwa na shaka kabisa, kwa kuwa yeye mwenye shaka hatapata cho chote kutoka kwa Yehova.’​—Yak. 1:6, 7, NW.

17. Maandiko yanatupa shauri gani juu ya kuendelea katika sala?

17 Ili maombi yetu yajibiwe, twapaswa pia kuendelea katika sala. Twapaswa kutaka kufanya sala iwe zoea. Biblia inashauri hivi: “Kwa uthabiti endelezeni zoea la sala.” (Rum. 12:​12, The New Testament in Modern English, ya J. B. Philips) Mara nyingi Yesu alikazia sehemu hiyo ya sala. Katika Mahubiri yake ya Mlimani, alisema hivi: “Endeleeni kuomba, nanyi mtapewa; endeleeni kutafuta, nanyi mtapata; endeleeni kubisha, nanyi mtafunguliwa.” (Mt. 7:7, NW) Katika mfano wake juu ya mjane aliyetendewa haki na hakimu ambaye hakumwogopa Mungu wala kuheshimu wanadamu, Yesu pia alikazia maana ya kuendelea katika sala. (Luka 18:1-8) Iwapo kweli kweli tuna nia ya kupata mambo tunayomwomba Yehova Mungu, ‘tutasali daima’ na ‘kuomba bila kukoma.’​—Rum. 12:12, HNWW; 1 The. 5:17.

18. Ni mambo gani tusiyopaswa kuyaruhusu yatuzuie tukose wakati wa kusali?

18 Jambo linalohusiana na kuendelea katika kusali ni kuchukua wakati wa kuomba. Hatupaswi kamwe kuwa wenye shughuli sana tusiweze kuomba. Ni kweli kwamba kuna mambo ya lazima maishani​—shughuli zetu za kila siku, kula, kujipamba, kulala​—ambayo huchukua nyingi za saa zetu 24 za kila siku. Walakini je! hakuna pia mambo mengine mengi yanayozuia wakati wetu yasivyopaswa? Mambo hayo yaweza kuwa kusoma magazeti ya ulimwengu, kutazama televisheni, kushiriki michezo na namna nyingine za tafrija au starehe. Tusipothamini pendeleo kubwa sana la sala, twaweza kujikuta tukiipuza kwa sababu ya mambo hayo kuimalizia wakati.

PINDI ZA SALA

19. Baadhi ya pindi nyingi tulizo nazo za kusali ni zipi?

19 Tuna pindi nyingi au nafasi za kuomba. ‘Kuomba bila kukoma’ kunatia ndani kuomba katika pindi zote​—baada ya kuamka asubuhi, tunapoenda kulala usiku, kabla ya chakula na wakati wa saa za usiku tunapokuwa macho. (Tazama Zaburi 5:3; 92:1, 2; 119:147-149, 164; 1 Timotheo 4:4, 5.) Huenda tukapata matatizo makubwa au nyakati za wasiwasi, tukalazimika kubeba madaraka mazito; tukatakiwa tuseme mbele ya wasikilizaji Wakristo au kutetea imani yetu mbele ya wakuu wa kiserikali. Hakika, hizo ni nyakati za kumpa Yehova mahangaiko yetu. Ndiyo, “katika njia zako zote mkiri [Mungu], naye atanyosha mapito yako.” (Mit. 3:6) Zaidi ya hayo, wakati wo wote tunapopata baraka za pekee, sana sana ikiwa hatukuwa tunatazamia au tulikuwa tunatamani sana, mioyo yetu yapaswa kujawa na shukrani kwa Yehova. Lakini, bila shaka, hatuhitaji sababu za pekee. Mioyo na akili zetu zaweza kutuchochea tuonyeshe shukrani wakati mwingine wo wote.

20. Ni jambo gani linaloweza kusemwa juu ya kikao cha mwili wetu katika kusali?

20 Kwa kuwa wakati wo wote na nyakati zote zafaa kwa sala, je! hiyo maana yake ni kwamba hatupaswi kufikiria hata kidogo kikao cha mwili wetu wakati wa kuomba? Kweli, Biblia haiagizi kuweka mwili katika hali fulani, kama vile kupiga magoti na kukunja mikono wakati wa kuomba. Walakini twasoma juu ya watu wakiomba hali wamesimama, wamepiga magoti au wakiwa wamelala chini, na kwa mikono iliyonyoshwa. (Tazama Mwanzo 24:26, 48; 1 Wafalme 8:​22, 42, 44, 54; Nehemia 2:1-4; Marko 11:25.) Jambo hilo laonyesha kwamba inafaa, wakati inapowezekana, kuwa na kikao fulani cha mwili kinachoonyesha heshima wakati wa kuomba. Kwa mfano, katika kundi twaweza kusimama na kuinamisha vichwa vyetu. Badiliko hilo katika kikao cha mwili laweza pia kutusaidia tukaze fikira juu ya sala inayotolewa kwa ajili yetu. Inaelekea kwamba kupiga magoti kunafaa sana katika kusali kibinafsi. (Linganisha Danieli 6:10; Wafilipi 2:9, 10.) Hata ikiwa lazima tulale kitandani tunapoomba kabla ya kulala, twapaswa kuwa waangalifu kutii agizo la kimtume ‘kukesha,’ kuwa macho, tukiwa tumeamka wakati wa kuomba.​—Efe. 6:18.

21. Katika kumjia Mungu ili tusikiwe, twapaswa kuomba namna gani?

21 Kweli, kweli, kumwomba Yehova Mungu ni jambo tunalopaswa kulichukua kwa uzito. Twapaswa kuwa wenye shukrani kwamba twaweza kumfikia Baba yetu wa kimbinguni, tukiwa na hakika kwamba atatusikiliza wakati wo wote! Bila shaka, jambo hilo linategemea sisi kumfikia kwa imani, kupitia kwa njia inayofaa, tukiwa katika hali ifaayo ya akili, na kisha kustahimili katika sala, tusiwe wenye shughuli mno hata tusiweze kuomba. Na, ikiwa una watoto, kwa subira wafunze maana ya sala kwa maneno na kwa mfano mwema.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki