Uwe Imara Katika Sala
“Kila mwaminifu thabiti atasali kwako.”—Zab.32:6, NW.
1, 2. (a) Sababu gani imepasa mtu apashane habari na Mungu? (b) Mtu aonyeshaje anapendelea mapenzi ya Mungu?
KATIKA kizazi hiki cha kisasa inaelekea watu walio wengi hawana wakati wa kumfikiria Mungu. Wanatoa visababu vingi vya kutomfikiria katika maisha zao za kila siku. Walakini, ikiwa mtu anadai anamtumikia Mungu aliye hai na wa kweli, basi imempasa apashane habari naye kwa uaminifu thabiti, akimtegemea amtumikie na kumtii katika kila jambo.
2 Hasa baada ya mtu kujitoa amtumikie Yehova Mungu imempasa achukue sala kwa uzito. Badala ya kuiona kama wajibu, imempasa mtu aifurahie kama pendeleo. Kwa habari ya kufanya mapenzi ya Mungu na kuyanyenyekea kwa njia ya kitheokrasi, mtu atasali hivi: “Ee [Yehova], unijulishe njia zako, unifundishe mapito yako, uniongoze katika kweli yako, na kunifundisha. Maana Wewe ndiwe Mungu wa wokovu wangu.”—Zab. 25:4, 5.
UNYOFU KATIKA SALA
3. Twawezaje kuwa wanyofu katika maombi yetu kwa Mungu?
3 Unyofu unahusika katika kusema na Aliye Juu Zaidi ikiwa unamtazamia asikilize maombi yako. Lazima tuwe wanyofu juu ya vile tunavyojihesabu kuwa, tukifikiri kwa uzito na kuwa na akili timamu. Ili tuwe na uaminifu thabiti kwa njia za Mungu zenye haki, hatutaficha tabia zetu mbaya wala nia zetu zisizofaa. Haiwezekani kumdanganya Yeye ambaye tutatolea hesabu ya mambo tunayofanya. (Ebr. 4:12) Ungekuwa upumbavu tukisali hivi na kufanya tofauti na ombi letu.
4. Imetupasa tufanye nini ndiyo tumpendeze Msikiaji wa sala?
4 Wanaoshika amri zake kwa uaminifu thabiti wanahakikishiwa hivi: “Macho ya [Yehova] huwaelekea wenye haki, na masikio yake husikiliza maombi yao; bali uso wa [Yehova] ni juu ya watenda mabaya.” (1 Pet. 3:12) Tukiomba msamaha, lazima nasi tuzoee kusamehe kwa moyo. (Mt. 18:35) Tukiomba ufalme wa Mungu, inatupasa tuutafute kwanza katika maisha zetu. (Mt. 6:10, 33) Ikiwa tunatafuta maarifa zaidi ya Maandiko kutoka kwa Mungu, licha ya kuyaomba imetupasa tuweke kando nyakati za kawaida za kujifunza Neno lake, Biblia. Tukijawa na maarifa yaliyo sahihi, tutasaidiwa kukaza fikira juu ya mambo yaliyo ya maana zaidi, nasi tutayakumbuka tunaposali.—Flp. 1:9, 10.
KUTEGEMEZA NJIA ZA MUNGU
5. Eleza sala zisizokubalika.
5 Tunaweza kuwa na hakika kwamba sikuzote Mungu atategemeza jina lake jema na kanuni zake zenye haki. Yeye hatashusha kanuni zake kamwe zipatane na wale wanaojionyesha kuwa wasio na uaminifu thabiti au waovu. Sababu gani Mungu asikilize sala za kusingizia zinazotoka katika mioyo isiyopatana naye? Sala ya wale wanaozoea uovu inaweza “kuwa ni dhambi.” (Zab. 109:3-7) Wale wanaompa Mungu kisogo kwa unafiki na bado wanasali hawawezi kutazamia kusikiwa kwa upendeleo, kama inavyoonyeshwa katika Mithali 28:9: “Yeye aligeuzaye sikio lake asiisikie sheria, hata sala yake ni chukizo.” Sala ndefu za watu wenye kujisifu na wenye kiburi hazikubaliki nazo, kama ilivyoelezwa na aliyefundisha kusali, Kristo Yesu. (Mt. 6:5, 7; Luka 18:10-14) Tusipojifunza kufanya mema na kuitikia Neno la Mungu, huko ni kama kulikataa Neno la Mungu mwenyewe. Hiyo nayo haiwezi kusaidia sala zetu zisikiwe kwa upendeleo.
6. (a) Maneno ya mtu au matendo yake yanawezaje kuharibu sala zake kwa Mungu? (b) Ni nini kinachopaswa kuendelezwa kuwa chenye kuheshimika?
6 Ili kuendelea kuwa na uhusiano mwema na Mungu na Baba yetu, imetupasa tuendelee kushika kanuni zake bora za adili. Mtu anaweza kuonyesha anakubali au hakubali matendo ya ufisadi au maelekeo yake kwa maneno yake na/au njia yake ya kutenda mambo. “Enyi mmpendao [Yehova], uchukieni uovu; huwalinda nafsi zao watauwa wake,” ndivyo inavyoshauri Zaburi 97:10. Wale wanaokufa ganzi kwa adili wanajitenganisha na Mungu kwa kufuata mwenendo mpotovu. (Efe. 4:17-19) Mtu akizoea ufisadi au hata kuuachilia sala zake zinaweza kuwa za bure. Kama mtu wa kuheshimika, uthamini mpango wa kimungu wa ngono na ndoa na kwa uaminifu thabiti uutegemeze usije ukazuia sala zako.—Ebr. 13:4.
SALA INAWEZA KUZUIWA
7. Eleza njia kadha vile sala zinavyoweza kuzuiwa?
7 Ili kuacha wazi njia za kupashana habari na Mungu, ni lazima utembee kwa uangalifu katika taratibu hii ya mambo. Kwa njia hiyo unaweza kuwa na matumaini ambayo mtume Yohana aliandika habari zake: “Lo lote tuombalo, twalipokea kwake, kwa kuwa twazishika amri zake, na kuyatenda yapendezayo machoni pake.” (1 Yohana 3:22) Maneno ya kusema tu hayana maana kwa Mungu ikiwa matendo yetu hayapatani na maombi yetu. Mtu aweza kufanya maombi yake kwa Mungu yasiwe na matokeo asipojali. Hivyo, waume wanaonywa hivi: “Ninyi waume, kaeni na wake zenu kwa akili; na kumpa mke heshima, kama chombo kisicho na nguvu; na kama warithi pamoja wa neema ya uzima, kusudi kuomba kwenu kusizuiliwe.” (1 Pet. 3:7) Hii yaonyesha kwamba mtu aweza kufanya mambo yanayozuia sala zake kwa Mungu zisisikiwe kwa upendeleo hata katika maisha ya nyumbani. Jambo hilo limepaswa lituamshe sote tuwe wepesi zaidi kutembea katika njia ifaayo katika kila upande wa maisha, bila kudhani ati Mungu ataturehemu na kutuhurumia vyo vyote tu.
8. (a) Sababu gani lazima tupatane na ndugu zetu? (b) Ni vema kukumbuka nini?
8 Kuendeleza uhusiano wenye amani na ndugu zetu wa Kikristo kundini ni kwa lazima pia, tunapojaribu kufungamana sana na Mungu tunayetumikia. Ikiwa tu wepesi wa kufuata shauri la Yesu katika Mathayo 5:23, 24, hatutaacha tatizo lo lote, liwe kubwa au dogo, bila kulitatua pamoja na ndugu yetu. Tusiponyosha mambo kwa njia ya Maandiko, lazima tujue kwamba hiyo inaweza kufanya sala zetu na dhabihu zetu kwa Mungu zisikubalike. Ni vema sana kusimama na kufikiri kwamba inawezekana Yehova ameturehemu na kutusubiri mara nyingi sisi wenyewe, akatupa nafasi kubwa ya kusahihisha mwendo mbaya au nia isiyo ya kitheokrasi. Tukimfuata Mungu wetu katika jambo hilo, tunaweza kusaidia wengine sana, hasa wale ambao wameingia katika uhusiano wa karibu naye wakawa ndugu zetu wa kiroho. Tunapokuwa watendaji wa njia za Mungu, tutakuwa wenye furaha zaidi nazo sala zetu hazitazuiwa na tendo lo lote la kipumbavu kwa upande wetu.—1 The. 4:1.
9. Ni nini kinachoweza kuzuia sala ya kundi?
9 Sala imepaswa itolewe kwa njia safi kundini. Kusiwe na uadui wala hasira juu ya wengine. Walio na hekima na ufahamu watasitawisha upole wa hekima nao watafuata vile alivyotaka mtume Paulo: “Wanaume wasalishe kila mahali, huku wakiinua mikono iliyotakata pasipo hasira wala majadiliano.”—1 Tim. 2:8; Yak. 3:13, 17.
10. Upendo na unyenyekevu unasaidiaje kuendeleza amani kundini?
10 Ndugu mnyenyekevu hatabishana na ndugu zake wa Kikristo ili atetee au kuomba haki zake mwenyewe. Ingawa mtu anao uhuru wa kufanya jambo, imempasa ajiangalie afanye yenye kujenga peke yake. Upendo unatakiwa ili kuendeleza amani, nako kusamehe kwaweza kutokuwa na vikomo kwa upande wa kila mmoja. (Mt. 18:21, 22) Unyenyekevu unahitajiwa ili kukubali kosa na kuomba msamaha. Mwendo huo wa unyenyekevu unamletea amani mtu mwenyewe na kundi. Unafanya mtu asidhani anashushiwa heshima. Unamsitawisha mtu na kumtia nguvu katika sifa njema ya unyenyekevu, ambayo Mungu anathamini. (1 Pet. 5:5) Jioneni huru kutafuta baraka nyingi za Yehova wakati nyie Wakristo mnapoacha ‘mambo yenu yote yatendeke katika upendo.’—1 Kor. 16:14.
11. Ni nini kinachopendekezwa ili kumpendeza Mungu?
11 Kama vile jitihada inavyotakiwa ili kuendeleza uhusiano mwema na wale waliomo kundini, ndivyo inavyotupasa kujitahidi tuwezavyo tusivunje urafiki wetu wenye thamani kuu na Baba yetu aliye mbinguni. Imetupasa tuwe watakatifu katika mwenendo wetu wote ndiyo tumpendeze. (1 Pet. 1:14-16) Uaminifu thabiti utamvuta Mkristo aepuke maelekeo yo yote ya kuiacha njia ya kweli na kuwa na madoa ya ulimwengu. Mtu anapofahamu Mungu ni mwenye uwezo wote na kwamba yeye si wa kuchezewa wala wa kudhihakiwa, hiyo inamfanya aombe uongozi wa Yehova amlinde asije akajikwaa na kuingia katika ubaya wa namna yo yote. Kukosa kutembea katika njia ifaayo kwa jambo lo lote kunaweza kutokeza vizuizi hata usitoe sala kwa uhuru.—Gal. 6:7.
KUKOSA NJIA YA KUMFIKIA
12. Ni nini kinachoweza kukosesha njia ya kumfikia Mungu?
12 Ikiwa mtu anaona anakosa njia ya kumfikia Mungu, ikiwa hawezi kusali tena, basi na achunguze mwendo wake wa maisha. Huenda kukawa na kosa moja au mfululizo wa makosa unaotokana na maoni mabaya juu ya maisha, kanuni mbaya za mwenendo au hata jambo kubwa zaidi, kama vile sifa za moyo. Pengine mtu anakosa kufanya yale anayojua ni ya haki, kwa maana Neno la Mungu linasema hivi: “Basi yeye ajuaye kutenda mema, wala hayatendi, kwake huyo ni dhambi.” (Yak. 4:17) Ili tuendelee kuwa katika hali ya kuweza kusema na Mungu, lazima tuepuke kutumia maisha zetu katika utendaji unaotupinganisha naye. Tunahitaji hekima na ufahamu ili tusijitie katika jambo lo lote linaloweza kuhatirisha hali yetu na Mungu tunayependa na kuabudu.
13. Ni nini kinachoweza kufanya mtu arudi nyuma asisali?
13 Kuacha mwendo wa haki na wa kweli kwa kadiri yo yote kwaweza kufanya mtu awe na dhamiri mbaya kisha kumrudishe nyuma asiwe akisali kwa kawaida. Wale wanaokataa kunyenyekea mapenzi ya Mungu au wanaojaribu-jaribu kuyapinga hawaongozwi na hekima ya kimungu na kwa hiyo wataelekea kufanya makosa. Tunapojikuta tumepoteza kadiri yo yote ya urafiki na Yehova, ni vema kujichunguza na kurekebisha sababu za kutopashana habari. Mtu hawezi kuwa akijiwekea sheria zake mwenyewe akampendeza Mungu pia. Lakini, walio na uaminifu thabiti kwa Mungu wanaweza kumtazamia awasaidie. Tukiwa na kibali yake katika njia zetu zote tunaweza kuwa na uhakika wa kwamba atasikiliza maombi yetu na kututhawabisha katika wakati wake mwenyewe na njia yake mwenyewe.
SALA YA BIDII
14. (a) Mtu awezaje kueleza mawazo yake katika sala? (b) Unawezaje kutoa sala yako mwenyewe?
14 Kwa kweli sala si kusema na Mungu tu. Hii yatiliwa mkazo na sala nyingi zilizoandikwa katika Neno lake aliloliongoza kwa roho yake tupate uongozi. Bila shaka, sala hizo zilifaa wakati huo na pindi hiyo. Leo mwombaji hana haja ya kufuata maneno fulani kumweleza Mungu mawazo yake. Sala isiwe kawaida isiyo na maana kamwe wala haipaswi kufuatisha kabisa fungu la maneno lililowekwa kichwani. Mifano ya Biblia yaonyesha kwamba watu waliokuwa wakisali kwa kawaida walisema kwa usemi ule ule wa kawaida waliotumia walipokuwa wakizungumza na wengine. Hakuna haja ya kutumia maneno mapya ya pekee tunaposema na Mungu. Acha sala yako iwe ya maneno yanayoonyesha mawazo yanayotoka moyoni. Isitokee kamwe kamwe mtu anayeabudu Mungu kwa roho na kweli amlipe mtu mwingine amwombee wala asitumie sala za mtu mwingine zilizoandikwa katika kitabu.—Yohana 4:24.
15. Tunaweza kusali wakati gani, nayo maombi yetu yatoleweje?
15 Sala ya Kielelezo ambayo Yesu aliwapa wanafunzi wake inatusaidia tuyafahamu mambo yaliyo ya maana zaidi tuyatie katika sala zetu kwa Aliye Juu Zaidi. (Mt. 6:9-13) Sala hiyo ya mfano haina mambo magumu na ndivyo sala zetu zinavyopaswa kuwa tunapomjia Yeye awezaye kutatua tatizo lo lote tunaloweza kuwa nalo. Mgeukie akupe msaada wakati wo wote unapoona imani yako inadhoofika au unapoona maelekeo yo yote ya kutoka kidogo kidogo katika ibada safi. Mchana kutwa na usiku kucha, katika hali na shughuli zo zote, katika hatari, kishawi, biashara, safarini, katika furaha au ugonjwa, na uwe mwenye hamu ya kumjia Mungu anayesikiliza, Msikiaji wa sala. Kitumie kwa faida chanzo hicho cha nguvu unapoendelea na “sala zote na maombi.” (Efe. 6:18) Mwombe upendeleo, msaada; paza sauti yako kwa shukrani. Kumbuka kwamba mwanzilishi wa lugha hapendezwi na maneno makubwa; wewe mweleze tu yote yaliyomo moyoni mwako.—Zab. 62:8.
16, 17. (a) Je! ni vema kutafakari kabla ya kusali? Kwa sababu gani? (b) Unawezaje kutoa sala ambayo mawazo yake yanapatana sawasawa bila kwenda huku na huko?
16 Inafaidi kutafakari kabla ya kumfikia Mungu, ili useme unayotaka kusema. Kuwa na mawazo mazuri akilini kutakuzuia kupayuka-payuka, au kurudia-rudia mambo yale yale tena na tena kwa njia ya kuchosha. Husemi na jirani wala mtu ye yote yule bali na mtu aliye mkuu kupita wote katika ulimwengu wote, Yehova Mungu mwenyewe. Sala yenye kukubalika inatolewa kwake, lakini pia inatolewa juu ya mambo yanayofaa. Hivyo inafaa kabisa kufikiri kabla hujasali, ufikirie sana mambo yaliyo ya maana zaidi. Kwa njia hiyo unaweza kujizuia usiwe ukiomba mambo yale yale kila mara au maombi yako yasiwe yasiyopendeza kwa kurudiwa-rudiwa namna ile ile moja kila mara.—Mt. 6:7.
17 Huenda ikafaa utafute mahali patulivu usali. Yesu alijaribu kujiepusha na watu mambo yenye kusumbua ili atumie wakati akisali. (Marko 1:35; Luka 9:18) Unapokuwa mahali patulivu unaweza kujikumbusha mambo unayohitaji, mambo yenye kukufaidi wewe mwenyewe na wale upendao. Kufikiri kabla ya kumweleza Mungu mawazo yako kutakusaidia utoe sala ambayo mawazo yake yanapatana sawasawa bila kwenda huku na huko.
SALA YA KIPEKEE
18. (a) Ni sifa gani imepaswa ionyeshwe katika sala zetu za Pekee? (b) Twawezaje kuonyesha shukrani?
18 Katika sala zako za kipekee, mjie Mungu kwa unyenyekevu, si kujaribu kumlazimisha au kumwambia vile atakavyofanya. Imekupasa ukumbuke namna ulivyo mdogo kisha ujinyenyekeze machoni pa Yehova. (Yak. 4:10) Sala yako iwe inasemwa kwa sauti ya kusikika au kwa kimya moyoni mwako, mawazo yako ya ndani yanaweza kuwa sawasawa na ya Daudi: “Maneno ya kinywa changu, na mawazo ya moyo wangu, yapate kibali mbele zako, Ee [Yehova].” (Zab. 19:14) Si kwamba tu imetupasa kutoa sala zenye kukubalika bali pia imetupasa tupate furaha na burudisho tunapomtolea Baba yetu wa kimbinguni mawazo yetu ya ndani ndani. Tukijua kwamba sisi tu mali yake, inafaa tuikubali mipango aliyotufanyia sisi na washiriki wengine pia wa jamaa ya kibinadamu. Ko kote utazamako, waona ushuhuda wa kwamba yeye ni Muumba mwenye ukarimu mwingi na mwenye kufikiria sana. Kwa sababu tunapokea upendo na wema wa Mungu, imempasa kila mmoja wetu amwambie, ‘Asante’ kwa uaminifu thabiti na kwa kawaida. Tunatiwa moyo tufanye hivyo, tunapoambiwa hivi: “Furahini sikuzote; ombeni bila kukoma; shukuruni kwa kila jambo.”—1 The. 5:16-18.
19. Ni nini kimepaswa kiongoze yatakayosemwa katika sala? Toa mifano.
19 Sala yako ya kipekee inaweza kuhusu upande wo wote wa maisha. Nyakati nyingine pengine Neno la Mungu aliloliongoza kwa roho yake mwenyewe linaweza kueleza mawazo yako unapofikiria Maandiko fulani. Maarifa yaliyo sahihi juu ya mapenzi ya Mungu ndiyo yamepaswa yaongoze mambo yatakayosemwa katika sala, kwa maana Yehova hawezi kutenda kinyume cha makusudi yake mwenyewe, hata uombe nini. Ikiwa una uaminifu thabiti kwa enzi kuu ya Yehova, imekupasa ulitaje jina lake katika maombi yako na kuliachia nafasi katika maisha yako pia. Mambo mengine ya msingi yanayohusiana na yaliyo ya maana yamo katika sala ambayo Yesu aliwapa wanafunzi wake kwa upendo: “Ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.” Mambo mengine yanayotajwa katika sala hiyo yanahusu kutaka kwa mwombaji aishi katika upendeleo wa Mungu.—Mt. 6:9-13.
20. Kwa sababu gani ni vema kuomba roho ya Mungu?
20 Kati ya mambo unayoweza kuomba kwa kufaa ni roho ya Mungu. Nguvu hiyo ya utendaji inamvuta mtu aelekee katika njia inayofaa, njia ya Mungu. (Luka 11:13) Ikiwa kusudi lako ni kuwa mwenye mafaa zaidi kwa Mungu wako na Mwana wake Yesu Kristo, utaendelea kuomba uongozi wa kimungu utimize mengi ya faida zaidi unapotumia mali zako na nguvu zako. Kwa kweli kuishi maisha ya kujiweka wakf kuna maana ya kujikombolea wakati unaofaa. (Efe. 5:15, 16) Mwanamke mmoja Mkristo aliyejiweka wakf alisema hivi: “Mimi namwomba Yehova anijulishe wakati wo wote ninapofanya kosa au ninapoiacha njia ya Mkristo.” Yeye azijuaye siri za moyo ataona kama tunaitambua sana haja ya kumtegemea yeye kabisa ili tuweze kufanikisha njia yetu kama Kristo Yesu.—Zab. 44:21; linganisha Yoshua 1:8.
21. Taja nyingine za faida za Mungu na faida zako mwenyewe unazopaswa kuomba?
21 Ukifikiria sababu zote za kufanya iwe lazima uendelee kusali na pia ukifikiria mambo yote ya lazima kuomba utavutwa kufanya hivyo. “Dumuni sana katika kuomba, mkikesha katika kuomba huku na shukrani.” (Kol. 4:2) Endelea kusali juu ya makosa yako, matatizo yako, mahitaji ya siku, hatari inayoweza kutokea maishani mwako, mawazo yako ya moyoni, furaha zako na mambo yenye kukufisha moyo na kukufadhaisha. Sali upate nguvu zaidi za kuendelea kuwa mwabudu mwenye uaminifu thabiti wa Mungu wa kweli hata kuwe na mikazo ya maisha ya kila siku. Kwa sababu mkazo unatiwa juu ya kuhubiri habari njema za Ufalme, omba kwamba wewe pia uweze kukaza nia utende kwa juhudi. (Mt. 24:14; 1 Pet. 1:13) Ukikaza mawazo yako juu ya faida za Mungu, na juu ya zako mwenyewe pia, utakuwa macho kulisifu na kulitukuza jina lake na kupendekeza kwa uaminifu wengine wamwabudu yeye. Usisahau mambo unayoweza kufanyia wengine, na kumwomba Yehova awabariki wakati wao pia wanapojaribu kumwabudu na kumtumikia. Ebr. 13:15, 16.
KUSALI PAMOJA
22. Eleza faida za sala ya jamaa.
22 Inapendeza sana kuona jamaa ikisali pamoja nyakati za chakula na nyakati nyingine, kama wanapofurahia chakula cha kiroho. Sala ya jamaa inaweza kuwa baraka ya ajabu kwa jamaa, ikiendeleza utii, utaratibu na adabu katika maisha ya jamaa. Jamaa ni mpango wa Mungu, na uongozi wake umepaswa utafutwe juu ya mpango huo. Washiriki wote wa jamaa wanaweza kujifunza kusali. Bila shaka, Yesu alipokuwa mdogo sana alifundishwa kupiga magoti na kusali nyumbani kwao. Alipokua, aliithamini sala sana tena sana; kwa kweli, alitumika kufundisha wengine kusali sawasawa. (Mt. 21:13; Luka 11:1) Wakati watoto ni vitoto tu wanaweza kufundishwa kusema na Baba yao aliye mbinguni kwa heshima, wakimshukuru kwa uzima wanaofurahia na kwa kuwa na tumaini la kupata wakati ujao dunia ya paradiso ikiwa chini ya ufalme wa Mungu. Vijana na wazee wanaweza kuwa na mazoea ya kusali, nao wanaweza kuendeleza mazoea hayo ko kote, hata wawe chini ya hali gani.
23, 24. (a) Sala inatumiwaje nyakati za mikutano? (b) Ni mambo gani mengine yanayoweza kuombwa nyakati hizo?
23 Kwa kawaida mikutano ya Kikristo inafunguliwa na kufungwa kwa sala, ili wote wale waliokusanyika wamtegemee Mwalimu Mkuu wao kama chanzo cha mafundisho yao. Hapa tena inafaa mwenye kuwakilisha kundi mbele za Mungu afikiri kwa uangalifu kabla hajasali kwa ajili ya walioko. Baraka za kimungu zinaweza kuombwa mwanzoni mwa mkutano na mwishoni shukrani zinaweza kutolewa kwa mambo yaliyofunzwa na kufurahiwa. Imempasa mwenye kusali aseme maneno yanayofaa, akilikumbuka kusudi la sala na wakati wenyewe.
24 Mengi yaweza kusemwa kwa ufupi, kama ilivyoonyeshwa katika Sala ya Kielelezo katika Mathayo 6:9-13. Unaposali, fikiri! Kundi hili linahitaji nini? Unaweza kuomba juu ya kazi ya kutoa ushuhuda katika eneo hilo, ili akina ndugu wautoe ujumbe kwa matokeo mazuri na wawe wastadi wanapofundisha kweli ya Biblia. Ombi la watu wote linaweza kuwa na mawazo mbalimbali yenye kufaa, kama vile katika sala ya kipekee. Sala na kushirikiana kwa kawaida na wenye imani ile ile moja yenye thamani ni mpango wa kimungu kusaidia kundi lisitawi na upendo uwe mwingi. Wote waliokusanyika wamepaswa waisikie sala vizuri ndiyo waweze kusema “Amina” mwishoni.—1 Kor. 14:16.
25. Yehova anapendezwa na nini?
25 Ni vizuri sana kuona watu wa mataifa yote wakiukubali ukaribishaji wa kumjia Msikiaji wa sala. Akiwa Baba mkarimu, anapendezwa na kuthawabisha wale wanaomtumikia kwa uaminifu thabiti. Yehova “hatawanyima kitu chema hao waendao kwa ukamilifu.” (Zab. 84:11) Wote wanaoonyesha imani wakitumainia uzima wa milele wanaweza kumwita yeye Baba na kutazamia kupata kibali yake wanapomwomba sawasawa na mapenzi yake.
26. Imetupasa sote tupende nini ikiwa tunatazamia sala zetu zijibiwe?
26 Tukiwa tunatazamia kabisa kwamba Mungu atasikia mawazo yaliyomo katika sala zetu kwa huruma, lazima sisi pia tuyapende yale aliyotuandikia, yaani Biblia Takatifu. Tunapotwaa mawazo na njia za Yehova zaidi na zaidi, tutakuwa na ufahamu mwingi zaidi juu ya Yeye tunayepaswa kutumikia na kutii, nasi tutauthamini kabisa uhusiano mwema tunaoweza kuwa nao pamoja naye na Mwanawe, ambaye ndiye njia yetu ya kupashana habari. Hata uwe umefanya maendeleo ya kadiri gani katika kugeuza maisha yako yapatane na mapenzi ya Mungu, endelea kuuomba msaada na uongozi utokao juu. Uwe unapiga magoti kando ya kitanda chako au unasali unapotembea, uwe unaomba msaada asubuhi na mapema au usiku, na uwe na hakika kwamba Mfanyi wa sikio aweza kusikia sala yako.—Zab. 119:62, 147.
27. Kunaweza kuwa na furaha gani, na kwa nani?
27 Kuna furaha kubwa zaidi kweli kuliko kujibiwa sala? Kama utapata jibu la mara moja au utangojea mpaka wakati wake Mungu, usiache kamwe kuuamini uwezo wa sala. Kila mwaminifu thabiti atakuwa imara katika sala, akifurahia kila siku baraka nyingi na kushukuru akitazamia kuwa na urafiki wa milele na Msikiaji wa sala.
—Kutoka The Watchtower, July 1, 1975.
[Picha katika ukurasa wa 15]
Je! jamaa yako inasali pamoja kwa kawaida?
[Picha katika ukurasa wa 16]
Usisahau kuomba baraka ya Mungu unapojifunza Neno lake
Ni vema kumshukuru Mungu kila siku kwa ajili ya fadhili zake nyingi
[Picha katika ukurasa wa 17]
Unapokuwa katika mkazo, je! wewe unamwomba Mungu akusaidie utulie?