Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • kl sura 16 kur. 150-159
  • Jinsi Unavyoweza Kumkaribia Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi Unavyoweza Kumkaribia Mungu
  • Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • SABABU INAYOTUPASA TUMKARIBIE MUNGU
  • MATAKWA YA KUMKARIBIA MUNGU
  • FURSA ZA KUONGEA NA MUNGU
  • SALA AMBAZO YEHOVA HUSIKIA
  • DUMU KATIKA SALA
  • UWASILIANO PAMOJA NA YEHOVA SI WA UPANDE MMOJA
  • Mkaribie Mungu Katika Sala
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Jinsi ya Kusali na Kusikiwa na Mungu
    Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele
  • Namna ya Kupata Msaada kwa Sala
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • “Maombi Yenu na Yajulishwe Mungu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
Pata Habari Zaidi
Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
kl sura 16 kur. 150-159

Sura 16

Jinsi Unavyoweza Kumkaribia Mungu

1. Ni mambo gani yenye kufanana yaliyo dhahiri katika dini nyingi?

MTALII mmoja aliyekuwa akitembelea nchi fulani ya Mashariki alistaajabia desturi za kidini alizoona kwenye hekalu la Kibuddha. Ingawa sanamu hazikuwa zile za Mariamu au Kristo, desturi zilizo nyingi zilifanana na zile za kanisa lake huko nyumbani. Kwa mfano, yeye aliona utumizi wa rosari na kuimbwa kwa sala. Wengine wamefanya malinganisho kama hayo. Iwe Mashariki au Magharibi, njia ambazo wenye kujitoa kidini hujaribu kumkaribia Mungu au kukaribia vitu wanavyoabudu zinafanana sana.

2. Sala imefafanuliwaje, na ni sababu gani watu wengi husali?

2 Wengi hasa hujaribu kumkaribia Mungu kwa kusali kwake. Sala imefafanuliwa kuwa “tendo la mwanadamu la kuwasiliana na aliye mtakatifu—Mungu, miungu, makao fulani ya hali bora zaidi, au nguvu zinazozidi zile za kibinadamu.” (The New Encyclopædia Britannica) Hata hivyo, wanapomfikia Mungu katika sala, wengine hufikiria tu kile wawezacho kujifaidi nacho. Kwa kielelezo, wakati mmoja mtu fulani alimuuliza mmoja wa Mashahidi wa Yehova hivi: “Ukisali kwa ajili yangu, je, matatizo niliyo nayo katika familia yangu, kazini kwangu, na ya afya yangu yatasuluhishwa?” Inaonekana kwamba mtu huyo alifikiri hivyo, lakini wengi husali na kuona kwamba matatizo yao yanaendelea. Kwa hiyo tunaweza kuuliza, ‘Ni kwa sababu gani hasa inatupasa kumkaribia Mungu?’

SABABU INAYOTUPASA TUMKARIBIE MUNGU

3. Sala zetu zapasa kuelekezwa kwa nani, na sababu gani?

3 Sala si desturi isiyo na maana, wala si njia tu ya kujipatia kitu fulani. Sababu kubwa ya kumfikia Mungu ni kuwa na uhusiano wa karibu naye. Kwa hiyo sala zetu zapaswa zielekezwe kwa Yehova Mungu. “BWANA yu karibu na wote wamwitao,” akasema mtunga-zaburi Daudi. (Zaburi 145:18) Yehova hutualika tuingie katika uhusiano wenye amani pamoja naye. (Isaya 1:18) Wale wanaoitikia mwaliko huo wanakubaliana na mtunga-zaburi aliyesema: “Nami kumkaribia Mungu ni kwema kwangu.” Sababu gani? Kwa sababu wale wanaomkaribia Yehova Mungu watakuwa na furaha ya kweli na amani ya akilini.—Zaburi 73:28.

4, 5. (a) Sababu gani ni jambo la maana kusali kwa Mungu? (b) Ni uhusiano wa aina gani pamoja na Mungu tunaoweza kujenga kupitia sala?

4 Sababu gani tusali kwa Mungu ili tupate msaada ikiwa ‘anajua tunayohitaji kabla sisi hatujamwomba’? (Mathayo 6:8; Zaburi 139:4) Sala inaonyesha kwamba tuna imani katika Mungu na tunamwona kuwa Chanzo cha “kila zawadi njema na kila upaji mkamilifu.” (Yakobo 1:17, NW; Waebrania 11:6, NW) Yehova hupendezwa na sala zetu. (Mithali 15:8) Anafurahi kusikia maonyesho yetu yenye maana ya uthamini na sifa, kama vile baba ashangiliavyo kusikia mtoto wake mchanga akisema maneno ya shukrani kwa moyo mweupe. (Zaburi 119:108) Kunapokuwa na uhusiano mzuri kati ya baba na mtoto kuna uwasiliano mchangamfu. Mtoto apendwaye hutaka kusema na baba yake. Ndivyo ilivyo kwa habari ya uhusiano wetu na Mungu. Tukithamini kwelikweli yale tunayojifunza juu ya Yehova na upendo ambao yeye ametuonyesha, sisi tutatamani sana kujieleza kwake katika sala.—1 Yohana 4:16-18.

5 Tunapomfikia Mungu Aliye Juu Zaidi Sana, tunapaswa kuwa wenye staha, ingawa hakuna haja ya kuhangaika mno juu ya maneno barabara tunayotumia. (Waebrania 4:16) Tunaweza kumfikia Yehova sikuzote. Na ni pendeleo lililoje kwamba tunaweza ‘kuifunua mioyo yetu’ kwa Mungu katika sala! (Zaburi 62:8) Kumthamini Yehova kunaongoza kwenye uhusiano mchangamfu pamoja naye, kama ule ambao yule mwanamume mwaminifu Abrahamu alifurahia akiwa rafiki ya Mungu. (Yakobo 2:23) Lakini tunaposali kwa Bwana Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote mzima, ni lazima tutii matakwa yake ya kumfikia.

MATAKWA YA KUMKARIBIA MUNGU

6, 7. Ingawa Mungu hadai malipo ili kusikia sala zetu, yeye hutaka nini kwetu tunaposali?

6 Je, fedha zahitajiwa ili kumfikia Mungu? Watu wengi huwalipa makasisi ili wasali kwa ajili yao. Wengine hata huamini kwamba sala zao zitasikiwa kulingana na kiasi cha upaji wanachotoa. Hata hivyo, Neno la Mungu halisemi kwamba utoaji wa kifedha wahitajiwa kwetu ili kumfikia Yehova katika sala. Maandalizi yake ya kiroho na baraka za kuwa na uhusiano pamoja naye katika sala vyapatikana bila gharama yoyote.—Isaya 55:1, 2.

7 Ni nini kinachotakiwa, basi? Kuwa na mtazamo wa moyo unaofaa ni jambo moja la muhimu. (2 Mambo ya Nyakati 6:29, 30; Mithali 15:11) Ni lazima tudhihirishe moyoni mwetu imani katika Yehova Mungu kuwa “Msikiaji wa sala” na “mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Zaburi 65:2, NW; Waebrania 11:6, NW) Ni lazima pia tuwe na moyo mnyenyekevu. (2 Wafalme 22:19; Zaburi 51:17) Katika kimojapo vielelezo vyake, Yesu Kristo alionyesha kwamba mkusanya-kodi mnyenyekevu alipokuwa akimfikia Mungu akiwa na mtazamo wa moyo wa hali ya kujishusha chini alithibitika kuwa mwadilifu zaidi kuliko Farisayo mwenye kiburi. (Luka 18:10-14) Tumfikiapo Mungu katika sala, acheni tukumbuke kwamba “kila mwenye moyo wa kiburi ni chukizo kwa BWANA.”—Mithali 16:5.

8. Ikiwa tunataka Mungu ajibu sala zetu, tunapaswa kujisafisha kutokana na nini?

8 Tukitamani Mungu ajibu sala zetu, ni lazima tujisafishe kutokana na mwenendo wenye dhambi. Mwanafunzi Yakobo alipowatia moyo wengine wamkaribie Mungu, yeye aliongeza hivi: “Itakaseni mikono yenu, enyi wenye dhambi, na kuisafisha mioyo yenu, enyi wenye nia mbili.” (Yakobo 4:8) Hata watenda-makosa wanaweza kuingia katika uhusiano wenye amani pamoja na Yehova wakitubu na kuacha njia yao ya maisha ya zamani. (Mithali 28:13) Hatuwezi kusikilizwa na Yehova tukijifanya tu kwamba tumeisafisha njia yetu. “Macho ya Bwana huwaelekea wenye haki, na masikio yake husikiliza maombi yao; bali uso wa Bwana ni juu ya watenda mabaya,” Neno la Mungu husema.—1 Petro 3:12.

9. Tunapaswa kumfikia Yehova kupitia nani, na sababu gani?

9 Biblia hutaarifu: “Hakuna mwanadamu mwenye haki hapa duniani; ambaye afanya mema, asifanye dhambi.” (Mhubiri 7:20) Kwa hiyo unaweza kuuliza hivi: ‘Tunaweza kumfikiaje Yehova Mungu basi?’ Biblia hujibu hivi: “Mtu akitenda dhambi tunaye Mwombezi kwa Baba, Yesu Kristo mwenye haki.” (1 Yohana 2:1) Ingawa sisi ni watenda-dhambi, tunaweza kumfikia Mungu tukiwa na uhuru wa usemi kupitia Yesu Kristo, aliyekufa akiwa fidia kwa ajili yetu. (Mathayo 20:28) Yeye ndiye njia pekee ambayo kupitia hiyo tunaweza kumfikia Yehova Mungu. (Yohana 14:6) Hatupaswi kupuuza thamani ya dhabihu ya fidia ya Yesu kwa kutenda dhambi kimakusudi. (Waebrania 10:26) Hata hivyo, ikiwa tunafanya kadiri tuwezavyo ili kuepuka yaliyo mabaya na hata hivyo tunakosea nyakati fulani, tunaweza kutubu na kumwomba Mungu msamaha. Tunapomfikia kwa moyo mnyenyekevu, yeye atatusikia.—Luka 11:4.

FURSA ZA KUONGEA NA MUNGU

10. Kwa habari ya sala, twaweza kumwigaje Yesu, na ni nini baadhi ya pindi za kuwa na sala ya faragha?

10 Yesu Kristo alithamini sana uhusiano wake pamoja na Yehova. Kwa hiyo, Yesu aliweka kando wakati wa kuongea na Mungu katika sala ya faragha. (Marko 1:35; Luka 22:40-46) Ingefaa tuige kielelezo cha Yesu na kusali kwa Mungu kwa ukawaida. (Warumi 12:12) Inafaa kuanza siku kwa maneno ya sala, na kabla ya kulala usingizi, twaweza kwa kufaa kumshukuru Yehova kwa utendaji wa siku hiyo. Wakati wa mchana, azimia kumfikia Mungu “kila wakati.” (Waefeso 6:18) Twaweza hata kusali kimya-kimya moyoni mwetu, tukijua kwamba Yehova aweza kutusikia. Kuongea na Mungu kwa faragha kunatusaidia kuimarisha uhusiano wetu pamoja naye, na kusali kwa Yehova kila siku kwatusaidia sisi kumkaribia hata zaidi.

11. (a) Sababu gani familia zisali pamoja? (b) Inamaanisha nini tunaposema “Ameni” kwenye mwisho wa sala?

11 Yehova husikiliza pia sala zinazotolewa kwa niaba ya vikundi vya watu. (1 Wafalme 8:22-53) Tunaweza kumkaribia Mungu tukiwa familia, kichwa cha nyumba akiwa anaongoza. Hilo linatia nguvu kifungo cha familia, na Yehova anakuwa halisi kwa wachanga wanaposikia wazazi wao wakisali kwa Mungu kwa unyenyekevu. Namna gani ikiwa mtu fulani anawakilisha kikundi katika sala, labda kwenye mkutano wa Mashahidi wa Yehova? Ikiwa tumo kati ya wasikilizaji, acheni tusikilize kwa uangalifu ili kwenye mwisho wa sala hiyo, tuweze kusema kwa moyo wote “Ameni,” linalomaanisha “Na iwe hivyo.”—1 Wakorintho 14:16, NW.

SALA AMBAZO YEHOVA HUSIKIA

12. (a) Sababu gani Mungu hajibu sala fulani-fulani? (b) Sababu gani tusikazie fikira mahitaji ya kibinafsi tu tunaposali?

12 Huenda watu fulani wakahisi kwamba Mungu hajibu sala zao hata ingawa wao husali kwake kupitia Kristo. Hata hivyo, mtume Yohana alisema hivi: “Tukiomba kitu sawasawa na mapenzi [ya Mungu], atusikia.” (1 Yohana 5:14) Kwa hiyo basi, tunahitaji kuomba kulingana na mapenzi ya Mungu. Kwa kuwa yeye apendezwa na hali njema yetu ya kiroho, jambo lolote linaloathiri hali yetu ya kiroho ni habari inayofaa sala. Ni lazima tukinze kishawishi cha kukazia fikira mahitaji ya kimwili tu. Kwa mfano, ingawa inafaa kusali ili kupata ufahamu wenye kina na imara ya kushughulika na ugonjwa, wasiwasi juu ya afya haupasi kuyasonga nje masilahi ya kiroho. (Zaburi 41:1-3) Alipopata kujua kwamba alikuwa akihangaikia sana afya yake, mwanamke Mkristo mmoja alimwomba Yehova msaada ili awe na maoni yanayofaa juu ya ugonjwa wake. Likiwa tokeo, matatizo yake ya afya yalikuja kuwa hangaiko dogo zaidi, naye alihisi kwamba alipewa “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida.” (2 Wakorintho 4:7, NW) Tamaa yake ya kuwasaidia wengine kiroho iliongezeka, naye akawa mpiga-mbiu wa Ufalme wa wakati wote.

13. Kama vile ionyeshwavyo kwenye Mathayo 6:9-13, ni nini baadhi ya habari zinazofaa ambazo tunaweza kutia ndani katika sala zetu?

13 Tunaweza kutia ndani mambo gani katika sala zetu hivi kwamba Yehova atapendezwa kuzisikia? Yesu Kristo alifundisha wanafunzi wake jinsi ya kusali. Katika sala ya kigezo iliyorekodiwa kwenye Mathayo 6:9-13, yeye aliweka kiolezo cha habari tunazoweza kuomba ifaavyo. Ni nini lipaswalo kuwa jambo kuu la kuhangaikiwa katika sala zetu? Jina la Yehova Mungu na Ufalme vyapaswa kuwa ndilo jambo kuu la kwanza. Kuomba kwa ajili ya mahitaji yetu ya kimwili kunafaa. Ni jambo la maana pia kuomba msamaha wa dhambi zetu na kuomba tukombolewe katika vishawishi na pia na yule mwovu, Shetani Ibilisi. Yesu hakutaka sisi tuimbe sala hiyo au kuirudia-rudia, tukiisema bila kufikiria maana yayo. (Mathayo 6:7) Uhusiano ungekuwa wa namna gani ikiwa mtoto angetumia maneno yaleyale kila wakati ambapo angesema na baba yake?

14. Zaidi ya maombi, tunapaswa kutoa sala zipi?

14 Zaidi ya maombi na dua za kuhisiwa moyoni, tunapaswa kutoa sala za sifa na shukrani. (Zaburi 34:1; 92:1; 1 Wathesalonike 5:18) Twaweza pia kusali kwa ajili ya wengine. Sala zinazohusu ndugu na dada zetu wa kiroho wanaoteseka au kunyanyaswa zinaonyesha kupendezwa kwetu nao, na Yehova anapendezwa kutusikia tukionyesha ufikirio wa jinsi hiyo. (Luka 22:32; Yohana 17:20; 1 Wathesalonike 5:25) Kwa kweli, mtume Paulo aliandika hivi: “Msijisumbue kwa neno lo lote; bali katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu. Na amani ya Mungu, ipitayo akili zote, itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu.”—Wafilipi 4:6, 7.

DUMU KATIKA SALA

15. Tunapaswa kukumbuka nini ikiwa inaonekana kwamba sala zetu hazijibiwi?

15 Ingawa unapata ujuzi juu ya Mungu, huenda ukahisi kwamba sala zako hazijibiwi nyakati nyingine. Hali ingeweza kuwa hivyo kwa sababu huenda usiwe wakati wa Mungu wa kujibu sala fulani hususa. (Mhubiri 3:1-9) Huenda Yehova akaruhusu hali fulani iendelee kwa muda, lakini yeye hujibu sala na ajua wakati bora zaidi wa kufanya hivyo.—2 Wakorintho 12:7-9.

16. Sababu gani tudumu katika sala, na kufanya hivyo kwaweza kuathirije uhusiano wetu na Mungu?

16 Udumifu wetu katika sala hufunua upendezi wetu wa kuhisiwa moyoni katika yale tunayomwambia Mungu. (Luka 18:1-8) Kwa kielelezo, huenda tukamwomba Yehova atusaidie tushinde udhaifu fulani. Kwa kudumu katika sala na kutenda kwa kupatana na maombi yetu, tunaonyesha moyo wetu mweupe. Tunapaswa kutaja mambo kihususa na kusema kweli katika maombi yetu. Ni jambo la maana hasa kusali sana tupatwapo na kishawishi. (Mathayo 6:13) Tunapoendelea kusali huku tukijaribu kudhibiti misukumo yetu yenye dhambi, tutaona jinsi Yehova anavyotusaidia. Hili litajenga imani yetu na kutia nguvu uhusiano wetu pamoja naye.—1 Wakorintho 10:13; Wafilipi 4:13.

17. Tutanufaikaje tukiwa na mtazamo wenye sala katika kumtumikia Mungu?

17 Kwa kusitawisha mtazamo wenye sala katika kutoa utumishi mtakatifu kwa Yehova Mungu, tutakuja kutambua kwamba sisi hatumtumikii kwa nguvu yetu wenyewe. Ni Yehova anayewezesha mambo yafanywe. (1 Wakorintho 4:7) Kukiri hili kutatusaidia tuwe wanyenyekevu na kutatajirisha uhusiano wetu pamoja naye. (1 Petro 5:5, 6) Ndiyo, sisi tuna sababu imara za kudumu katika sala. Sala zetu zenye bidii na ujuzi wetu wenye thamani wa jinsi ya kumkaribia Baba yetu wa kimbingu mwenye upendo zitafanya maisha yetu yawe yenye furaha kwelikweli.

UWASILIANO PAMOJA NA YEHOVA SI WA UPANDE MMOJA

18. Tunaweza kumsikilizaje Mungu?

18 Ikiwa tunamtaka Mungu asikie sala zetu, ni lazima tusikilize anayosema. (Zekaria 7:13) Yeye hapeleki ujumbe wake mbalimbali kupitia manabii waliopuliziwa kimungu na kwa hakika hatumii njia zinazohusiana na uwasiliani-roho. (Kumbukumbu la Torati 18:10-12) Lakini tunaweza kumsikiliza Mungu kwa kujifunza Neno lake, Biblia. (Warumi 15:4; 2 Timotheo 3:16, 17) Kama vile huenda tukahitaji kukuza hamu ya kula chakula cha kimwili ambacho ni chenye afya kwetu, tunahimizwa “[tufanyize] hamu sana ya maziwa yasiyoghushiwa yaliyo ya lile neno.” Kuza hamu ya kula chakula cha kiroho kwa kusoma Neno la Mungu kila siku.—1 Petro 2:2, 3, NW; Matendo 17:11, NW.

19. Kuna manufaa gani katika kutafakari juu ya yale unayosoma katika Biblia?

19 Tafakari juu ya yale unayosoma katika Biblia. (Zaburi 1:1-3; 77:11, 12) Hilo lamaanisha kufikiria sana habari hiyo. Unaweza kulifananisha hili na kusaga chakula tumboni. Unaweza kusaga chakula cha kiroho kwa kuhusianisha yale unayosoma na mambo unayojua tayari. Fikiria jinsi habari hiyo inavyoathiri maisha yako, au fikiria yale ambayo inafunua juu ya sifa za Yehova na mishughuliko yake. Hivyo kupitia funzo la kibinafsi, waweza kutwaa chakula cha kiroho kinachoandaliwa na Yehova. Hili litakuvuta karibu zaidi na Mungu na litakusaidia ushughulike na matatizo ya kila siku.

20. Kuhudhuria mikutano ya Kikristo kunatusaidiaje tumkaribie Mungu?

20 Unaweza kumkaribia Mungu pia kwa kusikiliza Neno lake likizungumzwa kwenye mikutano ya Kikristo, kama vile Waisraeli walivyosikiliza kwa uangalifu walipokusanyika ili kusikia usomaji wa umma wa Sheria ya Mungu. Wafunzi wa wakati huo walitia maana katika usomaji wao wa Sheria, hivyo wakisaidia wasikilizaji wao waelewe na kusukumwa watumie yale waliyosikia. Hili liliongoza kwenye shangwe kubwa. (Nehemia 8:8, 12) Kwa hiyo fanya liwe zoea lako kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova. (Waebrania 10:24, 25) Hili litakusaidia uelewe kisha utumie ujuzi juu ya Mungu maishani mwako na litakuletea furaha. Kuwa sehemu ya udugu wa Kikristo wa ulimwenguni pote kutakusaidia uendelee kuwa karibu na Yehova. Na kama tutakavyoona, unaweza kupata usalama wa kweli miongoni mwa watu wa Mungu.

TAHINI UJUZI WAKO

Sababu gani umkaribie Yehova?

Ni nini baadhi ya matakwa ya kumkaribia Mungu?

Unaweza kutia ndani mambo gani katika sala zako?

Sababu gani kudumu katika sala?

Unaweza kumsikilizaje Yehova leo?

[Picha ya ukurasa mzima katika ukurasa wa 157]

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki