Tafrija Inayoburudisha Kweli Kweli
“SISI tunaiabudu miungu kwa uchangamfu, kwa karamu, nyimbo na michezo, lakini ninyi [Wakristo] mnaabudu mwanamume aliyesulibishwa ambaye hawezi kufurahishwa na wale wanaofurahia raha zote za namna hii, ambaye anadharau raha na kulaani anasa.” Hivyo ndivyo alivyonena adui wa Ukristo wa karne ya pili.a Lakini namna alivyokosea katika uamuzi wake! Wanafunzi hao wa kwanza walipata furaha ya kweli maishani.
Kiongozi wao, Yesu Kristo, mwana wa yule “Mungu mwenye furaha,” anatajwa kuwa “mwenye furaha ya kufurika,” na kuwa ‘Mwenye Uweza aliye na furaha’ ambaye alipokuwa duniani alisali kwamba wafuasi wake “wawe na furaha [yake] imetimizwa ndani yao.”—1 Timotheo 1:11; 6:15, NW; Luka 10:21; Yohana 17:13, UV.
Furaha yao haikutegemea shangwe ya muda tu ya karamu au mchezo. Wao waliijua vizuri mithali hii ya kale (14:13): “Hata wakati wa kucheka moyo huwa na huzuni; na mwisho wa furaha ni uzito wa moyo.” Jambo lililowapendeza kuliko mambo yote ni kufuata kanuni za Ukristo. Furaha hiyo iligusa mioyo yao. Sasa walikuwa na uhusiano wenye thamani kubwa pamoja na Mungu Mwenye Nguvu Zote, na walikuwa na ushirika wa Wakristo wenzao. Pia walikuwa na maono yenye kuchangamsha moyo ya kusaidia wengine wajue ukweli na ya kuweza kulea watoto ambao wangewaletea furaha.
Nafasi za Kuwa na “Wakati wa Starehe”
Saa zao zote za mchana haziwezi kumalizwa kabisa na utunzaji wa madaraka yao ya Kimaandiko na kushiriki ujumbe wa Kikristo pamoja na wengine, ingawa hayo ni mambo ya maana zaidi. Kwa mfano wake mwenyewe, Bwana wao alionyesha mafaa ya kuwa na wakati fulani wa pumziko na burudisho. Baada ya kushinda mchana kutwa wakitoa ushuhuda, Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “‘Njoni, ninyi wenyewe, kwa faragha mwingie mahali pa upweke na mpumzike kidogo.’ Kwa maana kulikuwa na wengi waliokuwa wakija na kwenda, na wao hawakuwa na wakati wa starehe hata wakaa mmoja wa chakula.”—Marko 6:31, NW.
Kitenzi icho hicho cha Kigiriki cha kusema “mpumzike” (katika hali ya mtu kujitendea mwenyewe kitendo fulani) kimetafsiriwa kwenye Filemoni 20 kuwa “uniburudishe” (katika hali ya mtu kutendewa na mwingine kitendo fulani). Kwa hiyo “wakati wa starehe” unaweza kutumiwa ili kuleta badiliko la kuacha shughuli ya ukawaida au ili kupata burudiko la kufanya mtu aweze kuendelea na kazi iliyo kawaida yake. Ingawa Wakristo hao wa kwanza walikuwa watendaji na wenye juhudi hasa katika kutangaza ujumbe wa Ufalme, mara kwa mara walitafuta wakati wa kuwa na badiliko la shughuli nalo likawaburudisha kikweli.
Bila shaka walitembeleana na wakashiriki vyakula pamoja. Tena, namna mbalimbali za tafrija inayofaa zilipatikana ambazo wanafunzi hao au watoto wao huenda wakawa waliweza kufurahia. Vijana wa kiume na wengine wanatajwa kuwa wakipiga vyombo vya muziki katika nyakati za kabla ya Ukristo. (1 Samweli 16:18; 1 Wafalme 1:40; Maombolezo 5:14; linganisha Luka 15:25.) Watoto wanatajwa kuwa wakifanya michezo na kucheza dansi. (Mathayo 11:16, 17, NW) Tofauti na namna yo yote ya “kujizoeza kupata nguvu za mwili” iliyokuwako wakati huo ikiwa na mafaa “kidogo,” utawa wenye kuonyeshwa kwa matendo ‘ulifaa kwa mambo yote, kwa kuwa unayo ahadi ya uzima wa sasa, na ya ule utakaokuwapo baadaye.’ Lo lote ambalo Wakristo walifanya lilifanywa kwa usawaziko, wala halikuonyesha tabia za kukosa kiasi na zenye makelele za wale ambao hawakuwa Wakristo. Halikufunika kamwe ‘utawa’ wao, ambao ulikuwa ndio chemchemi halisi ya furaha yao.—1 Timotheo 4:8.
Mambo Ambayo Jamaa Nyingine Zinafanya Sasa
Leo jamaa za Kikristo zinafurahia pia nyakati za kujiburudisha zikiwa pamoja. Zinapata furaha na ushirika wa kweli katika kufanya mambo pamoja—hasa, katika kujulisha wengine ufalme wa Mungu. Na bado, kuna mambo mengine ambayo zinafanya pamoja, kama vile kushiriki katika namna mbalimbali za tafrija. Namna gani? Baba mmoja aliyepata matokeo mazuri katika kulea jamaa kubwa alitaja utendaji wa namna mbalimbali unaojenga, kisha akaongeza hivi: “Namna zenye matokeo yaliyo mazuri zaidi za tafrija zinaelekea kuwa ni zile zinazotumia nishati za mtoto na kumtolea mwito wa ushindani.”
Baba Mkristo mwenye vijana-matineja wanne aliishi katika eneo lililoelekea kutokuwa na nafasi za tafrija. Aliulizwa kama alitatizwa kutafutia jamaa yake tafrija yenye ubora. Yeye alijibu hivi: “Kuwapa tafrija halijawa kamwe jambo gumu. Kipingamizi cha pekee kinachopasa kushindwa ni kuona nafasi za tafrija yenyewe na kuridhika na kile ulicho nacho. Kufurahia mambo mepesi, kama vile kuogelea, kufanya matembezi ya miguu, kustarehesha wageni kwa maongezi na mambo kama hayo, yanaelekea kuwa ndiyo mambo yenye kuridhisha zaidi. Tumejifunza kwamba ili tujiburudishe, si lazima twende kwenye majengo ya tafrija za bei kubwa wala kutumia vifaa vya anasa, bali tunaweza kujiburudisha kwa kutumia kile kilicho wazi kutumiwa na watu wote.”
Wengi wanakuta kwamba wanapokuwa wakifanya kazi ya kushiriki na wengine maarifa ya Biblia nafasi za tafrija zinajitokeza. Baba huyu mwenye watoto wanne aliandika hivi:
“Mwingi wa utendaji wetu mbalimbali wa kitafrija unahusiana sana na utendaji wetu mbalimbali wa kitheokrasi, na kwa muda ambao tunaendelea kufanya utendaji huo tafrija inajileta yenyewe. Mara nyingi kutoa ushuhuda katika eneo letu la mashambani kunatokeza nafasi ya kwenda tukiwa na chakula cha mchana cha kulia huko. Pindi nyingi tumemaliza siku ya kutoa ushuhuda kwa kujifurahisha mahali fulani katika msitu au kwenye uwanja wa kupigia mahema.”
Ni wazi kwamba hali za kila jamaa ni tofauti. Bila shaka kuna namna nyingi za mambo ambazo watu wakiwa jamaa nzima wanayaona kuwa yenye kustarehesha. Hata hivyo baba mwingine mwenye watoto wanne alisema: “Namna ya tafrija siyo inayofanya vijana waendelee kuridhika na kuwa wenye furaha, ni hali ya watu wanaowazunguka na ushirika unaohusiana nayo. Uhusiano pamoja na washiriki wa jamaa ndio unaofanya wakati unaotumiwa uwe wenye kufurahisha.” Mkristo mwingine aliongeza hivi: “Kilichofanya [tafrija] iwe jambo la pekee sana ni kwamba sisi tuliifanya tukiwa jamaa nzima.”
Ubora wa Kupendezwa kwa Wazazi
Kwa hiyo ingewapasa wazazi wawe wanajua kwamba watoto wao wanahitaji utendaji mbalimbali ulio bora wa kujaza sehemu fulani ya wakati wa starehe wa watoto. Mama mmoja, ambaye mume wake hakuwa mwamini, alisema hivi: “Ni lazima ufanye hali ya nyumbani ipendeze watoto wasitake kuondoka humo, na hata kama wataondoka kwa muda, itawafanya watake kurudi.” Baba na mama mmoja waliopata matokeo mazuri katika kulea watoto wao waliulizwa “siri” yao ilikuwa nini. Walijibu hivi: “Sikuzote tulijaribu kufanya maisha ya watoto ya kuwa pamoja nasi nyumbani yawe yenye kuwapendeza kuliko yale ya kuwa pamoja na watoto wa rika lao.”
Kufanya maisha ya nyumbani “yawe yenye kuwapendeza” watoto zaidi kunataka wazazi waonyeshe hangaikio la moyoni. “Kulea vitoto vidogo kunachosha mwili na kuusisimua, lakini vijana-matineja wanasisimua akili na kuichosha.” Ndiyo, moyo wenye hangaikio, pamoja na jitihada ya akilini, unahitajiwa na wazazi.
Ni jambo jepesi kusema kwa maneno kwamba jitihada hiyo inaweza kufanywa kwa urahisi, lakini si jambo rahisi kuifanya. “Sisi tukiwa ni wazazi wenye watoto saba, tuliona kwamba tulihitaji kujitahidi sana ndipo tuweze kuwalisha, kuwapa mavazi na makao,” ndivyo alivyoandika baba mmoja, ambaye aliongeza kusema kwamba, “kwa sababu hiyo tulifanya tafrija kwa uchache, ingawa tulikuwa tukipanga wakati fulani wa kuwa na tafrija.” Mara nyingi, kunakuwa na mzazi mmoja tu nyumbani anayelazimika kubeba furushi lote.
Inaeleweka kwamba ni vigumu kuja nyumbani baada ya kazi ngumu ya mchana na kuanza kufikiria namna ya kutolea jamaa tafrija. Wazazi wanaofaulu kutimiza madaraka yao yote ya Kimaandiko na bado wakati uo huo wanatolea jamaa tafrija bora ya namna fulani wanastahili kusifiwa kweli kweli! Ingawa ni vigumu sana kufanya hivyo, mama mmoja ambaye watoto wake wote saba walikuja kuwa Wakristo walio wakf, alisema hivi: “Mambo ya kufurahisha yanayopatikana kwa kufanya hivyo yana ubora unaopita mambo yote ambayo mtu anajinyima na kazi yote ngumu anayofanya.”
Je! watoto wanaitikia? Baba mmoja alielekeana na mwito wa ushindani wa kulea binti matineja watatu bila kuwa na mke wa kumsaidia. Wasichana wote watatu wakaja kuwa Wakristo wenye kujitoa kwa bidii. Baadaye mmoja wa binti hao alisema hivi:
“Tulifanya mambo pamoja. Nyakati nyingine tulipokuwa hatuna pesa za kujifurahisha kwa njia yo yote tulikuwa tukitembea tu, nyakati nyingine tukapiga hatua nyingi sana kupitia barabara za mji. Baba hakusitasita kutujulisha kwamba yeye alikuwa mwanadamu mwenye kupungukiwa. Ikiwa hatukuwa na mahali pa kwenda na mvua ilikuwa ikinya, yeye alikuwa akisema, ‘Twendeni nje tukatembee tukinyeshewa na mvua.’ Nasi tulikuwa tukienda tu na kutembea tukinyeshewa; hatukuwa na mahali pa kwenda lakini kule kuwa pamoja tu na yeye kulitupendeza sana. Yeye alitafuta wakati wa kuwa pamoja na sisi.”
Ni wazi kwamba si kila mtu aliye na maoni ya kwamba ni jambo la tafrija kutembea na huku ananyeshewa na mvua, lakini jambo lenyewe ni kwamba kile kinachofanywa sicho kilicho cha maana zaidi, bali kilicho cha maana zaidi ni kwamba jambo fulani lifanywe na jamaa nzima ili kuleta badiliko la shughuli ambalo litaleta burudiko la kweli.
“Jamaa” ya Kiroho
Wale wanaokuwa Wakristo wanafurahia ushirika wenye thamani kubwa ndani ya jamaa nyingine, yaani, kundi, ambalo linaweza kweli kweli kulinganishwa na jamaa yenye kujawa kabisa na ‘akina ndugu, akina dada, akina mama, akina baba na watoto.’ (Marko 10:28-30, NW) Kwa sababu hiyo ingeelekea kuwa sawa kabisa kwamba washiriki wa kundi wafurahie kutumia wakati wakiwa katika ushirika wa kujengana, si kutoa ushuhuda tu wakiwa pamoja katika vikundi-vikundi.
Vikusanyiko vya kirafiki hivyo vinaweza kuwa vyenye kuburudisha na pia vinaweza kuongeza uchangamfu wa kundi. Kijana mmoja Mkristo aliulizwa akumbuke ni kikusanyiko gani chenye kufurahika zaidi ya vyote alichopata kuhudhuria. Bila kusitasita akajibu hivi:
“Ni wakati jamaa kadha kundini, wazazi na watoto, zilipokusanyika pamoja. Baada ya kuuma vyakula vidogo-vidogo tu tukiwa pamoja, sisi sote tuliketi kwa mviringo tukaongea. Mmoja wa akina ndugu alianza kuuliza wengine wetu tueleze namna tulivyokuja kuwa Mashahidi wa Yehova au tusimulie jambo lililoonwa katika kazi yetu ya kufundisha wengine. Baada ya muda mfupi watu mbalimbali wakasimulia hadithi yao juu ya vile walivyokuja kuwa Wakristo na matatizo waliyoyashinda. Hakuna mtu aliyekuwa kidomodomo wa kutawala maongezi yote, bali wengi walishiriki. Sisi sote tulitiwa moyo na maono hayo. Ulikuwa wakati usioweza kusahauliwa.”
Kwa kutumia kanuni za Biblia, na ikiwa wazee, watumishi wa huduma au wengine waliokomaa watatumia uvutano wao kuleta faida, pindi hiyo itakuwa chanzo cha burudiko la kweli wala si tukio litakalowaacha wengi katika hali ya kuchukizwa kwa sababu ya mwenendo mbaya kutokea. Isisahauliwe kamwe kwamba agizo kuu la mgawo tuliopewa ni kuwa mashahidi kwa ajili ya jina na ufalme wa Yehova. Hata katika hali ya starehe ya kikusanyiko cha kirafiki cha Kikristo mwenendo wetu unapasa kuletea Baba Mtakatifu wetu utukufu. Ni kama vile mwandikaji Mkristo wa karne ya pili alivyosema: “Hata Mkristo awe wapi, yeye bado ni Mkristo.”—Isaya 5:12; 43:10-12; 1 Wakorintho 10:31.
Ubora wa Kiasi wa Tafrija
Tafrija inayofaa afya inaweza kuwa badiliko lenye kufurahisha. Inaweza kutuburudisha ili tuweze kusonga mbele na kazi yetu ya kawaida. Hata hivyo tafrija siyo jambo kuu maishani. Dada mmoja kijana mwenye usawaziko mzuri, ambaye ni mtangazaji wa wakati wote wa “habari njema” katika Ulaya, alisema:
“Kujifurahisha silo jambo lililokaziwa nyumbani. Kusema kweli, utumishi wa shambani ndio uliokuwa jambo kuu nyumbani kwetu. Chakula, mavazi, makao, mambo ya kiroho, mikutano, ndiyo yaliyokuwa mambo ya maana. Hata hivyo, tulipopata wakati tulikuwa tukifurahia mambo fulani ya kujifurahisha, kwenda labda kutembelea jamaa fulani-fulani kundini.
“Niliona mara nyingi watoto wakienda sehemu mbalimbali kujifurahisha na nilikuwa nikipatwa na wazo la kusema, ‘Hata mimi ningependa sana kufanya hivyo.’ Lakini, kusema kweli, kuepuka kujitia katika tafrija nyakati zote hakukuniletea kamwe hasara. Hakujanipotezea kamwe faida. Mimi si mtu wa bure kuliko vijana wale wengine wote wa rika langu.”
Kujifurahisha kukiruhusiwa kuwe sehemu kubwa ya maisha yetu, kungetuumiza kiroho na labda hata kimwili. Angalia onyo hili la wazi kutoka Mithali 21:17, NW, ambalo linasema: “Yule ambaye anapenda macheko atakuwa mtu aliye katika ukosefu; yule ambaye anapenda divai na mafuta hatapata mali.”
Wakati huo ilikuwa desturi kwenye vikusanyiko vya kirafiki au karamu kunywa divai na kumwaga mafuta na vitu vingine vyenye manukato kichwani na kwenye mavazi. (Mithali 27:9; Amosi 6:6) Baada ya muda mfupi watu waliopenda sherehe hizo wangekuta kwamba utendaji fulani-fulani katika maisha yao uliingiwa na hasara, wakajiumiza wenyewe. Matukio mengi yenye kusikitisha yameonyesha kwamba, wakati sherehe za kitafrija tu zinapofanywa kwa ukawaida, zinakuwa na maelekeo ya kuingiwa na uulimwengu. Kwa hiyo ni lazima mtu ajihadhari kabisa.
Usisahau kamwe kwamba katika sehemu mbalimbali ulimwenguni, Wakristo wengi hawawezi kupata kile ambacho wale walio katika mataifa yenye viwanda zaidi wanakiita “kujifurahisha.” Na bado wanaendelea vizuri na, kwa uhakika, kwa njia nyingi wao ndio wanaoonekana kuwa wenye furaha na wenye kuridhika kuliko wale wenye tafrija za namna mbalimbali. Mzee mmoja aliyekuwa amechunguza kwa makini hali iliyo katika mataifa yote aliandika hivi: “Watu wengi wanaona kwamba maadili yamezidi kuharibika kwa kadiri ambayo mkazo umezidi kuwekwa juu ya kujifurahisha.” Basi, ni lazima kila Mkristo ajihadhari asipatwe na hatari hiyo, kisha aweke “mkazo” huo juu ya kushiriki katika ibada ya Baba yetu wa kimbingu.
Ni lazima pia tuukubali uhakika wa kwamba wala sisi Wakristo wala watoto wetu hatutaweza kutumia wakati mwingi juu ya kujifurahisha kwa sababu tuna agizo la haraka la kutangaza ufalme wa Mungu katika “siku za mwisho” hizi. Pia, ni wazi kwamba Wakristo hawataweza kamwe kufanya mambo yote ambayo ulimwengu unayaita “kujifurahisha.” Kwa hiyo ni lazima tafrija iwekwe katika mahali panapoifaa. Ili kufanya hivyo tunahitajiwa kabisa tuendeleze daima maoni ya kiroho, si ya kimwili, kisha tujitahidi kukaza maoni ya namna hiyo ndani ya mioyo ya watoto wetu.
Kwa hiyo kila Mkristo na aendelee kuwa na maoni yaliyosawazika juu ya tafrija. Na tujenge maisha yetu kwa kuyategemea mambo yanayoleta furaha na uradhi wa kweli moyoni, na mara kwa mara tuwe tukifurahia tafrija fulani yenye kujenga. Juu ya yote, na tupate furaha yetu iliyo kubwa zaidi katika kuishi maisha safi ya Kikristo na katika kutangazia wengine kwa juhudi lile tumaini bora la Ufalme ambao hivi karibuni utasaidia wanadamu wote waishi maisha yenye usawaziko na mafaa, na hivyo Mungu wetu, Yehova, apate sifa ya milele.
[Maelezo ya Chini]
a Hivyo ndivyo hakimu mmoja alivyomwambia Epipodio mwenye kusema kwamba alikuwa ni Mkristo. Hakimu alikuwa akimwuliza maulizo na kujaribu kumfanya aache msimamo wake. Jambo hilo linasemwa kuwa lilitukia katika Ufaransa wakati wa mwaka wa 17 wa kutawala kwa Mfalme Mroma Marku Aurelio. (177 W.K.)