Kwa Kweli ni Nani Walio na Kweli?
“Uniongoze katika kweli yako, na kunifundisha. Maana Wewe ndiwe Mungu wa wokovu wangu.”—Zab. 25:5.
1. Ni nini maana ya neno kweli, na sababu gani inaweza kusemwa kwamba Yehova ndiye msingi wa kweli?
NENO kweli linafafanuliwa kuwa lile linalopatana na mambo ya hakika, mambo halisi. Hii humaanisha lile linalofaa na jema. Chanzo, au msingi wa kweli ni Muumba Mwenye Nguvu Zote wa ulimwengu wote, Yehova Mungu. Yeye anajua kweli kuhusu kila sehemu ya uumbaji wake. Yeye anajua linalofaa, lililo jema na lililo baya. Yeye anajua kweli kuhusu yale yametokea katika wakati uliopita na sababu gani, pamoja na maana ya hali zilizopo ulimwenguni. Vilevile yeye anajua kweli kuhusu wakati ujao, kwa kuwa yeye amekwisha amua utakavyokuwa.—Isa. 14:24.
2. Biblia inauelezaje ukweli wa Yehova?
2 Kwa sababu hizo mtunga zaburi humweleza Muumba kuwa “[Yehova], Mungu wa kweli.” (Zab. 31:5) Kwa hiyo Mungu asemapo, maneno yake yanaaminika sikuzote: “Neno lako ndiyo kweli.” (Yohana 17:17) Atoapo maagizo kuhusu mwenendo wa wanadamu, haya huwa yanafaa sikuzote: “Maagizo yako yote ni kweli.” (Zab. 119:151) Anapoahidi kitu, tunaweza kuitumaini: “Halikuanguka neno lo lote katika lililokuwa ni jema ambalo [Yehova] alikuwa amelinena . . . yalitimia mambo yote.” (Yos. 21:45) Hivyo, “Ni za haki, na za kweli, njia zako, Ee Mfalme wa mataifa [wa milele, NW]—.”—Ufu. 15:3.
KUTEMBEA KATIKA KWELI
3, 4. (a) Mtu anatembeaje katika kweli? (b) Yehova anataka wanadamu watembee katika kweli kwa sababu gani?
3 Ni jambo la akili kwamba Mungu wa kweli angetaka viumbe vyake vya kibinadamu vitembee katika kweli. Hii ifanyweje? Kwa kupata maarifa yaliyo sahihi juu ya Mungu ni nani na juu ya makusudi yake ni nini, kisha kwa kujifunza anayotaka tufanye, na kuyafanya. (Yohana 17:3; 1 Yohana 2:3, 4) Kwa kweli hii inamaanisha kwamba kutembea katika kweli inakuwa njia ya maisha, “Njia hii,” kama vile Biblia iitavyo.—Matendo 9:2.
4 Sababu moja ya Mungu kuwataka wanadamu watembee katika kweli ni kwa vile inamletea utukufu na furaha Muumba wakati viumbe vyake vya kibinadamu vinapoonyesha sifa zake bora. (Linganisha Mwanzo 1:26, 27; Mithali 23:24, 25.) Nyingine ni kwamba, kwa kuwa Mungu ndiye aliyewaumba wanadamu, yeye anajua yaliyo mema kwao. Kwa hiyo, wale wanaofuata maagizo yake, wanaleta faida kubwa zaidi, hata faida za milele, kwao wenyewe na kwa wengine. (Isa. 48:17) Sababu zaidi ni kwamba, kwa kutembea katika kweli, wanadamu wanaweza kuwa na pendeleo la kushirikiana na watu ambao Mungu anatumia wawajulishe wale wanaotafuta kweli makusudi yake, kwa kuwa kama vile isemavyo Biblia, “Bwana [Yehova] hatafanya neno lo lote, bila kuwafunulia watumishi wake manabii siri yake.”—Amosi 3:7.
5. Kuna sababu gani nyingine ya maana sana ya kutembea katika kweli?
5 Kuna sababu nyingine ya maana sana ya kutembea katika kweli. Mtu afanyaye hivyo anajulikana kuwa anategemeza haki ya utawala wa Yehova wa ulimwengu wote. Hilo limetiliwa mashaka na kiumbe wa kiroho aliyeasi, Shetani Ibilisi. (Mwa. 3:1-4; Ufu. 12:9) Linalotiwa katika mashaka hayo yaliyotiliwa ni lawama ya kwamba Mungu hangeweza kutokeza watu ambao wangeshikamana naye na kweli yake. (Ayubu 1:6-12) Kusimama imara kwa ajili ya kweli chini ya mikazo kunaonyesha kwamba kuna watu wenye ukamilifu ambao hawataachilia yaliyo mema. (Mit. 27:11) Kwa upande mwingine, mtu asiyetembea katika kweli anafanya zaidi ya kutembea tu katika makosa. Kwa kujua au kwa kutokujua yeye anajiachilia ajipange upande wa Shetani, “baba wa uwongo,” “mungu wa taratibu hii ya mambo” ambaye “amepofusha akili za wasioamini.”—Yohana 8:44, HNWW; 2 Kor. 4:4, NW.
6. Kweli itaimarishwaje duniani pote?
6 Walakini, Mungu wa kweli ameweka kikomo cha kuruhusiwa kwa uongo na uovu uliotokana nao. (Mit. 12:19; Mhu. 3:1) Mungu amekusudia kwamba, wakati ufikiapo kikomo chake, yeye ataponda na kuiondolea mbali hii taratibu ya Kishetani, pamoja na wale wanaoiendeleza na kuipendelea. (Dan. 2:44; Ufu. 19:17-21) “Kila pando asilolipanda Baba yangu wa mbinguni litang’olewa,” akatabiri Yesu. (Mt. 15:13) Hii itatayarisha njia kwa ajili ya taratibu mpya ya Mungu, ‘ambamo haki itakaa.’ (2 Pet. 3:13, NW) Hiyo itamaanisha jamii ya kidunia ambayo msingi wake ni kweli; dunia inayokaliwa na watu wale tu wanaopenda kweli!
7. Ikiwa tunapenda kweli, nia yetu inapaswa kuwa nini?
7 Kwa hiyo, ikiwa sisi tunapenda yaliyo mema na kutaka kuishi katika taratibu mpya ya Mungu, lazima tutembee katika kweli. Inatupasa kuwa na maoni kama ya mtunga zaburi aliyesema: “Ee [Yehova], unijulishe njia zako, unifundishe mapito yako, uniongoze katika kweli yako, na kunifundisha.” (Zab. 25:4, 5) Vilevile, inatupasa kutii shauri la nabii Samweli kWa Israeli wa kale: “Wala msigeuke upande, maana, kufuata vitu vya ubatili, visivyoweza kusaidia wala kuokoa, . . . Mcheni [Yehova] tu, mkamtumikie kwa kweli kwa mioyo yenu yote.”—1 Sam. 12:21, 22, 24.
‘MIFANO’ KWA WAKATI WETU
8, 9. (a) Israeli walifaidikaje kwa kutembea katika kweli, tofauti na yalivyokuwa mataifa yaliowazunguka? (b) Ni jambo gani lililotukia wakati Israeli waliposhindwa kuendelea kutembea katika kweli?
8 Yale ambayo Mungu alitendea watu katika wakati uliopita yatoa ‘mifano,’ au vielelezo, kwetu sisi. Kutokana nayo tunajifunza namna Mungu anavyowatendea wale wanaotembea katika kweli na wale wasiofanya hivyo. (1 Kor. 10:11; Rum. 15:4) Mfano mmoja ambao tunaweza kujifunza kutokana nao ni ule wa Israeli wa kale. Walipendelewa kwa kupewa sheria za Mungu. Maadam Waisraeli walitembea katika kweli zake, walibarikiwa sana. Kwa mfano, hawakushindwa na mataifa waliokuwa adui zao. (Kum. 28:7) Mazao yao na makundi yao yalikuwa mengi. (Kum. 11:1-13) Taratibu zao za kijamii zilikuwa zenye utaratibu sana na zenye hali ya juu sana hata kwa-mba hakukuwa na uhitaji wa gereza. (Kut. 22:1-15) Maambukizo ya magonjwa yaliyokuwa yakipiga mataifa yasiyomwogopa Mungu hayakuwapata. (Kum. 7:15) Na wakiendelea kutembea katika kweli—‘wangebarikiwa kuliko mataifa yote,’ akawaahidi Yehova. (Kum. 7:14) Kwa kutofautisha, ebu angalia hali iliyoshushwa ya mataifa ya Wakanaani waliowazunguka, kama vile kinavyosema Bible Handbook cha Henry H. Halley (1955), uku. 157:
“Wakanaani waliabudu, kwa kufanya uasherati sana, kama sherehe ya kidini, mbele ya miungu yao; kisha, kwa kuua watoto wao wa-zaliwa wa kwanza, kama dhabihu kwa miungu iyo hiyo.
“Inaelekea kwamba, kwa kadiri kubwa sana, nchi ya Kanaani ilikuwa kama Sodoma na Gomora katika taifa zima . . . Je! utamaduni wenye ukatili mchafu na wenye kuchukiza namna hiyo ulikuwa na haki tena ya kuendelea kuwako? . . .
“Wachimbuzi wa mambo ya kale ambao huchimbua magofu ya miji ya Wakanaani wanashangaa kwamba Mungu hakuwaangamiza mapema kuliko wakati aliofanya hivyo.”
9 Walakini, Israeli walishindwa kuendelea kutembea katika kweli. Na kama matokeo, Mungu aliondoa msaada wake kwa taifa hilo. Ndiyo sababu Yesu aliwaambia Waisraeli katika , hekalu hivi: “Angalieni, nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.” (Mt. 23:38) Vilevile alitangaza hivi: “Ufalme wa Mungu utaondolewa kwenu, nao watapewa [taifa] lingine lenye kuzaa matunda yake.” (Mt. 21:43) Hawangeendelea tena kuwa taifa lililopendelewa na Mungu, mashahidi wake.
10. Taifa jipya la kiroho lilijitokezaje katika karne ya kwanza?
10 Katika karne ya kwanza ya wakati wetu wa kawaida, Mungu aliunda taifa jipya la kiroho. Hili lilikuwa lile kundi la Kikristo, tengenezo ambalo washiriki wake walikuwa watu wa mataifa mengi mbalimbali. (Matendo 10:34, 35; 13:46) Mnenaji wa Mungu aliyewekwa, Yesu, ndiye aliyeweka msingi wake na kusema: “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima.” (Yohana 14:6) Kwa yale aliyofundisha na kutimiza, yeye alithibitisha kwamba kwa kweli alikuwa na kweli, na kuungwa mkono na Mungu. (Mt. 3:16, 17; 15:30, 31; Matendo 2:22) Wakristo wa karne ya kwanza walithibitisha vivyo hivyo, wakitambulishwa waziwazi kuwa mashahidi wa Mungu wa Kikristo. (Matendo 1:8; 2:1-4, 43) Kwa habari ya kweli zilizotiririka sasa kupita kwa Wakristo hawa, mtume Paulo alisema hivi: “Mungu ametufunulia sisi kwa [r]oho.” Kwa kutofautisha, yeye alisema hivi: “Wenye kuitawala dunia hii hawaijui hata mmoja.” (1 Kor. 2:8, 10) Ilitukia sawasawa na alivyosema Yesu: “Kwa kuwa mambo haya [wewe Mungu] uliwaficha wenye hekima na akili, ukawafunulia watoto wachanga.”—Mt. 11:25.
11, 12. (a) Biblia ilitabirije kurudishwa kwa ibada ya kweli katika wakati wetu? (b) Kurudishwa huku kulifanywa kwa sababu gani?
11 Kufikia mwisho wa karne ya kwanza, Mungu alikuwa ametimiza jambo jingine. Alikuwa amemaliza kuandikwa kwa maandishi yenye kuongozwa na roho yake ambayo yangetumiwa baadaye kama msingi wa kuamulia yaliyo kweli. (2 Tim. 3:16, 17) Uliotiwa ndani ya Maandiko hayo yaliyokamilishwa ulikuwa unabii mwingi, historia iliyoandikwa kimbele. (2 Pet. 1:21) Unabii huo ulionyesha kwamba baada ya kifo cha mitume, kipindi cha kuacha kufuata kweli kingeanza. (Matendo 20:29) Lakini yalionyesha vilevile kwamba baadaye, Katika “siku za mwisho” kabla tu ya mwisho wa taratibu hii, kungekuwako kurudishwa kwa ibada ya kweli. (Isa. 2:1-4; Mika 3:12 mpaka 4:5) Yesu alionyesha kwamba watu wangekusanywa katika vikundi viwili: wale wanaofanyia ndugu za Kristo mema na kutembea katika kweli wangethawabishwa na “uzima wa milele”; wale wasiofanya hivyo ‘wangekatiliwa mbali milele.’—Mt. 25:31-46; 2 Yohana 4; 3 Yohana 3, 4.
12 Kukusanywa na kutengenezwa upya kwa kundi la Kikristo katika nyakati za kisasa kungekuwa na sababu kadha. Kwanza, lingepokea maagizo ya kuliunganisha kutoka kwa Mungu: “Naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake,” wasema unabii wa Isaya 2:3; Mika 4:2, pia. Kwa kutembea katika kweli, watumishi hawa wa Mungu wangetegemeza haki ya utawala wake wa ulimwengu wote, na kumletea utukufu na furaha, na faida nyingi kwao wenyewe. (Mit. 12:22) Kisha Mungu angewatumia kama mashahidi wake wa nyakati za kisasa, na kuwawezesha kukipelekea kizazi kilichopo ujumbe wake.
13. Je! Yehova amepata kutumia zaidi ya tengenezo moja duniani katika wakati wo wote mmoja?
13 Je! Mungu angetumia zaidi ya tengenezo moja katika kutoa kweli zake katika hizi “siku za mwisho”? Basi, je! Mungu amepata kutumia zaidi ya tengenezo moja katika kipindi kingine cho chote cha hukumu? Katika siku za Nuhu, je! merikebu nyingine zo zote zikiwa na watu ndani yazo, isipokuwa safina ya Nuhu zilipata ulinzi wa Mungu na kuiokoka gharika? Hapana, safina peke yake pamoja na waliokuwamo ndiyo iliokoka. (1 Pet. 3:20) Je! kulikuwako matengenezo mawili ya Kikristo katika karne ya kwanza? Hapana, Mungu alishughulika na moja tu. Vivyo, hivyo, katika siku zetu, kungali kuna “Bwana mmoja, imani moja, ubatizo mmoja.’ (Efe. 4:5) Kwamba kungekuwa na tengenezo moja tu lililoungana maneno ya Paulo yanaonyesha wazi kwamba “nyote mnene mamoja; wala pasiwe kwenu faraka.”—1 Kor. 1:10.
“KWA MATUNDA YAO”
14. Mtu anaweza kuamuaje ni nani kwa kweli i na Kweli leo?
14 Tunaweza kuamuaje ni nani kwa kweli walio na kweli leo, hivyo wakistahili kutumiwa na Mungu kama mashahidi wake duniani? Kanuni ya msingi ya kuamua kati ya kweli na uongo iliwekwa na Yesu aliposema: “Mtawatambua kwa matunda yao. . . . Kila mti mwema huzaa matunda mazuri; na mti mwovu huzaa matunda mabaya.” (Mt. 7:16, 17) Ndiyo, lazima kungalikuwa na “matunda” au ushuhuda kuonyesha kwamba roho takatifu ya Mungu yenye nguvu ilikuwa ikiwasaidia watu hawa bila shaka. Nayo ni matunda ya namna gani yangetokezwa na nguvu hiyo ya Mungu katika watumishi wake? Neno lake lajibu hivi: “Tunda la roho ni upendo, furaha, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujiweza.”—Gal. 5:22, 23, NW.
15. Kumpenda Mungu kunahusianaje na jina lake?
15 Ebu angalia, sana sana, “tunda” linaloonyeshwa kwanza, lile la upendo. Njia moja ambayo katika hiyo lazima watumishi wa kweli wa Mungu wauonyeshe ni kama vile alivyosema Yesu: “Mpende [Yehova] Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote.” (Mt. 22:37) Kumpenda Mungu kunaonyeshwa katika njia kadha. Njia mojawapo ni kulipenda jina la Mungu. (Ebr. 6:10; Zab. 69:36; 119:132) Kwa kweli, wale Wakristo waliochukuliwa kutoka katika ulimwengu huu lazima wawe watu “kwa ajili ya jina lake.” (Matendo 15:14-18) Ni nani ambao leo hulitegemeza jina la Mungu (Yehova katika Kiswahili) na kulijulisha duniani pote?—Isa. 43:10-12.
16. Kumpenda Mungu kunaonyeshwaje kwa habari ya faida za Ufalme?
16 Kumpenda Mungu kungemaanisha pia kuamini, na kuzungumza juu ya serikali yake inayokuja kwa ajili ya dunia yote, Ufalme wake wa mbinguni. Yesu alitufundisha kusali hivi: “Ufalme wako uje, Mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.” (Mt. 6:9, 10) Ni akina nani ambao leo hufanya ufalme wa Mungu kuwa fundisho kubwa la mafundisho na mahubiri yao kama alivyofanya Yesu? Ni akina nani wanaotembelea watu nyumbani mwao na kuwaambia yale ambayo ufalme wa Mungu utatimiza duniani? Ni akina nani wanaotimiza agizo alilotaja Yesu alipotabiri: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokalikwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja”?—Mt. 24:14, NW.
17. Ni katika njia gani nyingine kumpenda Mungu kunajionyesha?
17 Kumpenda Mungu bado kunaonyeshwa katika njia nyingine—kwa kuzitii sheria zake zote. (1 Yohana 5:3) Kunapokuwa na kupingana kati ya sheria za Mungu na sheria za wanadamu, kanuni ya Mungu kwa wale walio na kweli ni kwamba: “Imetupasa kumtii Mungu kuliko wanadamu.” (Matendo 5:29) Wale wanaofanya hivyo ndio peke yao wanaosaidiwa na “[roho takatifu ambayo] Mungu amewapa wote wamtiio [kama mtawala].” (Matendo 5:32) Kwa mfano, katika kuzitii sheria za Mungu, leo Wakristo “si sehemu ya ulimwengu,” kwa kutokuwamo katika mambo ya kisiasa ya, ulimwengu huu, kama walivyokuwa Yesu na Wakristo wa karne ya kwanza. (Luka 4:5-8; Yohana 6:15; 15:19; 17:14-16) Ni akina nani ambao katika siku zetu huendelea kujiepusha hivyo na ulimwengu, pamoja na upotovu wake wa kisiasa, jeuri yake, na ufisadi wake, wakiwa na nia hata ya kutiwa gerezani au hata kufa kwa sababu ya kufuata nyayo za Yesu?—1 Pet. 2:21; angalia pia Waebrania sura ya 13.
18. Toa alama nyingine iliyo wazi ya wale ambao ndio kwa kweli walio ‘na kweli.
18 Kuna sehemu nyingine ya “tunda” hili la roho, upendo. Yesu alisema hivi: “Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.” (Yohana 13:35) Maandiko mengine mengi yanaonyesha vilevile kwamba upendo wa namna hiyo ungekuwa alama iliyo wazi ya kuwa-tambulisha watumishi wa kweli wa Mungu. Kwa mfano:
“Katika hili watoto wa Mungu ni dhahiri na watoto wa Ibilisi nao. Mtu ye yote asiyetenda haki hatokani na Mungu, wala yeye asiyependa ndugu yake. . . . tupendane sisi kwa sisi; si kama Kaini alivyokuwa wa yule mwovu, akamwua ndugu yake.”—1 Yohana 3:10-12.
“Mtu akisema, Nampenda Mungu, naye anachukia ndugu yake, ni mwongo; kwa maana asiyempenda ndugu yake ambaye amemwona, hawezi kumpenda Mungu ambaye hakumwona.”—1 Yohana 4:20, 21.
Ni kikundi gani cha watu wa mataifa yote kinachoonyesha kwamba kinapendana namna hiyo, wala si kwa maneno tu, bali pia kwa matendo? Kwa muda wa karne iliyopita, ni kikundi gani ambacho, katika wakati wa vita, kimejiepusha kuwaua waamini wenzao wa mataifa mengine, na kutoachilia chuki ya kikabila, kitaifa, kitamaduni au kiuchumi iwatenganishe?
KWA KWELI NI NANI WALIO NA KWELI LEO?
19. Ni nani kwa kweli walio na kweli leo, na sababu gani useme hivyo?
19 Ushuhuda unaonyesha nini kwa habari ya tunda hili la maana sana la roho ya Mungu, upendo? Ni nani wanaolifikia? Tunaona wapi mkutano mkubwa wa watu wa mataifa yote tofauti-tofauti na jamaa za watu wakiwa wameungana pamoja katika jina la Yehova wamtumikie kwa ushikamanifu na kuwaambia wengine habari za ufalme wake? Ndiyo, tunaona wapi udugu halisi ulimwenguni pote uliounganishwa kwa upendo? (Ufu. 7:9, 10; Kol. 3:14) Gazeti la kidini liitwalo Interpretation, la Walter Stuermann, (1956), Vol. 10, uku. 323, katika sura yenye kichwa, “Biblia na Dini za Kisasa, Mashahidi wa Yehova,” linasema yafuatayo:
“Katika tengenezo lao na kazi ya kutoa ushuhuda, wao [Mashahidi wa Yehova] wanakaribia sana kama kikundi cho chote kuwa sawasawa na jamii ya Wakristo wa kwanza.
“Kujitenga kwao na ulimwengu, juhudi katika kutoa ushuhuda, na kutojali mashambulio ya ulimwengu ni kama yale yanayowapata wale wanaoamini kabisa kwamba wao wamo kati ya wateule na wale ambao wamemtolea Mungu utii wao bila masharti.
“[Ni] vikundi vingine vichache sana ambavyo hutumia Maandiko katika ujumbe wao kwa mdomo na kwa kuandika, kama wanavyofanya. [Ni] vikundi vingine vichache sana vinavyopata kutoka kwa wale tuwaitao watu wa kawaida utumishi mwingi katika kuendeleza mbele kazi ya tengenezo kama wanavyopata.”
20. Watu wote wanaopenda kweli wanapaswa kufanya nini?
20 Uchunguzi usio wa upendeleo wa Neno la Mungu, na kuulinganisha na mafundisho na matendo ya Mashahidi wa Yehova, utatoa ushuhuda wa kwamba roho ya Mungu inawasaidia kweli kweli, na kwamba yeye anawatumia kama chombo chake cha kuitangaza kweli leo. Hata hivyo, watu wote wanaopenda kweli wanaalikwa wachunguze dai hili la Mashahidi wa Yehova kwamba ndio kwa kweli walio na kweli. Katika kufanya hivyo, wangepaswa kuiga vile wale wa karne ya kwanza waliosikiliza kuhubiri kwa mitume walivyofanya: “Walilipokea lile neno kwa uelekevu wa moyo, wakayachunguza maandiko kila siku, waone kwamba mambo hayo ndivyo yalivyo.”—Matendo 17:11.