Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w79 12/15 kur. 8-13
  • Juhudi Kwa Ajili ya Nyumba ya Yehova

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Juhudi Kwa Ajili ya Nyumba ya Yehova
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • JUHUDI KATIKA KUSALI NA KUTENDA
  • ‘WATENDA KAZI ZAIDI KWA AJILI YA MAVUNO’
  • ‘FURAHA NA ROHO TAKATIFU’
  • ‘KUENDELEA BILA KUACHA’
  • ‘USIJIEPUSHE’
  • “Habari Njema Lazima Zihubiriwe Kwanza”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Fundisha Peupe Na Kutoka Nyumba Kwa Nyumba
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Kwa Nini Huduma ya Nyumba kwa Nyumba Ni ya Maana Sasa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Wakristo wa Kweli Ni Wahubiri wa Ufalme
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
w79 12/15 kur. 8-13

Juhudi Kwa Ajili ya Nyumba ya Yehova

“Wivu wa nyumba yako umenila.”​—Zab. 69:9.

1. Ni ujumbe gani wenye nguvu uliotangazwa katika masika ya mwaka 29 W.K.?

NI WAKATI wa masika mwaka 29 WK. Katika jangwa la Yudea kwatokea mtu mwenye kutokeza mwenye mavazi ya nywele za ngamia na mshipi wa ngozi. Yeye ni Yohana Mbatizaji. Ebu sikiliza ujumbe wake wenye kuamsha!​—“Tubuni; kwa maana ufalme wa mbinguni umekaribia.” Kati ya wale wanaokuja kubatizwa ni wengi wa Masadukayo na Mafarisayo. Yohana hafichi maneno anapowaweka wanafiki hawa wa kidini mahali pao. “Enyi wazao wa nyoka,” ndivyo anavyowaita. Na anaonyesha wazi kwamba Mfalme anayekuja atabatiza kwa roho takatifu na kwa moto​—kwamba watu wa mfano wa ngano watakusanywa kusudi wahifadhiwe, walakini watu wasiofaa wa mfano wa makapi watakusanywa kwa ajili ya hukumu yenye moto ya uharibifu wa milele.​—Mt. 3:2-12.

2. Mfalme alitambulishwaje?

2 Wakati wa vuli wafika, Mfalme mkusudiwa anatokea. Yohana ambatiza Mtu huyu mkamilifu, ambaye juu yake sasa roho ya Mungu inamshukia kwa namna ya njiwa. Sauti ya Yehova mwenyewe yasikika kutoka mbinguni, ikitangaza hivi: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye.”​—Mt. 3:13-17.

3. (a) Ni maneno ya mwito gani yaliotangazwa katika masika ya mwaka 30 W.K.? (b) Mtiwa mafuta wa Mungu alikuwa amekwisha kuonyeshaje juhudi kwa ajili ya nyumba ya Baba yake?

3 Ni wakati wa masika tena mwaka wa 30 W.K. Sikukuu ya Kupitwa imekwisha kuadhimishwa. Na kwa mara nyingine tena, katika Galilaya, maneno yale yenye kutoa mwito yanasikiwa!​—“Tubuni; kwa maana ufalme wa mbinguni umekaribia.” (Mt. 4:17) Ni nani mtangazaji wa ufalme huu? Si mwingine ila Mfalme aliyetiwa mafuta mwenyewe, ambaye sasa amekaribia. Kule Yerusalemu, wakati wa Sikukuu ya Kupitwa, alikuwa ameonyesha kupenda kwake haki kwa kuwafukuza kutoka kwa hekalu la Yehova wafanya biashara wale ambao walikuwa wakijaribu kuifanya ibada ya Mungu kuwa biashara. Ndipo wanafunzi wa mtu huyu, Yesu, walipokumbuka kwamba mtunga zaburi alikuwa ameandika juu yake hivi, “Wivu wa nyumba [ya Yehova] umenila.”​—Zab. 69:9; Yohana 2:13-17.

JUHUDI KATIKA KUSALI NA KUTENDA

4. Yesu alionyeshaje kuhangaikia kwake sana kutakaswa kwa jina la Baba yake?

4 Wakati wote Yesu alikuwa mwenye juhudi kwa ajili ya jina na sifa ya Yehova. Yeye aliwafundisha wanafunzi wake waombee jina hilo litukuzwe, au litakaswe. (Luka 11:2) Na katika sala kwa Yehova, kabla ya kutenganishwa na wanafunzi wake, yeye alisema: “Nami naliwajulisha jina lako, tena nitawajulisha hilo; ili pendo lile ulilonipenda mimi liwe ndani yao, nami niwe ndani yao.” (Yohana 17:26) Yesu alikuwa anahangaikia sana kuona jina la Baba yake likiondolewa suto kabisa​—litukuzwe.

5. (a) Utumishi wa Yesu ulikazia nini? (b) Yeye alikuwa amekuja kwa kusudi gani jingine lenye kufaidi?

5 Mhudumu huyu mwenye kupainia alikuja na ujumbe wenye kutikisa ulimwengu. (Linganisha Waebrania 2:10; 12:10; 12:2, Revised Standard Version.) Kuhubiri kwake kwa Ufalme ambao alifundisha wanafunzi wake vilevile wauombee, “Ufalme wako uje,” kulikuwa kwenye nguvu nyingi. Pindi iyo hiyo, juu ya mlima mmoja wa Galilaya, aliwashauri wasikilizaji wake wasiweke mioyo yao juu ya mambo ya kimwili walakini, mahali pake, ‘waendelee kutafuta kwanza ufalme wa Mungu na haki yake.’ (Mt. 6:9, 19-21, 24-34) Yesu alikuja kuhudumia wanadamu, ambao yeye ni mfalme wao wa wakati ujao. Vilevile, yeye alikuja “kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi.” (Mt. 20:28) Wote ambao wangeiamini dhabihu yake ya ukombozi wangepata uzima wa milele katika milki ya ufalme wake.​​—Yohana 17:3.

6. Yesu alihubiri wapi na namna gani, na akiwa na nia gani iliyo mfano bora?

6 Lo! namna hizi zilivyokuwa “habari njema” zenye utukufu! Yesu alijishughulisha kuzihubiri katika urefu na upana wa nchi ya Palestina. Pande za milima, katika nyumba za watu mmoja mmoja, katika masinagogi, katika hekalu, ufuoni mwa bahari na katika sehemu nyingine za watu wote, yeye alihubiri.a Vilevile yeye alifanya miujiza ya kuponya, hivyo kuonyesha namna, katika ufalme wake, ataponya wanadamu wote juu ya dunia hii. Hivyo atawaleta kwenye ukamilifu wa uzima katika paradiso ya duniani pote. Maandishi yasema hivi:

“Yesu alikuwa akizunguka katika miji yote na vijiji, akifundisha katika masinagogi yao, na kuihubiri habari njema ya ufalme, na kuponya magonjwa yote na udhaifu wa kila aina. Na alipowaona makutano, aliwahurumia, kwa sababu walikuwa wamechoka na kutawanyika kama kondoo wasio na mchungaji. Ndipo alipowaambia wanafunzi wake, Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache. Basi mwombeni Bwana wa mavuno, apeleke watenda kazi katika mavuno yake.” (Mt. 9:35-38)

Sala hizo za “watenda kazi” zilijibiwaje?

‘WATENDA KAZI ZAIDI KWA AJILI YA MAVUNO’

7. (a) Wale wanafunzi kumi na wawili wangeitimizaje kazi yao? (b) Wangewapata wapi watu wenye kustahili?

7 Yesu mwenyewe alianza kutimiza uhitaji huu kwa kuwaagiza na kuwatuma wale mitume kumi na wawili. Na walipaswa kuifanyaje kazi yao? Ala! kwa juhudi ile ile ambayo Bwana wao alikuwa ameonyesha! Yeye aliwaambia hivi: “Na mji wo wote au kijiji cho chote mtakachoingia, tafuteni ni nani humo [anayestahili].” Hii ingewalazimu kwenda kwenye nyumba za watu, ambako watu wenye ‘kustahili’ wangesikiza “habari njema.” Kwa njia hii, wanafunzi hao wangepata mahali pa kulala usiku huo. Walakini miji mingine haingewakaribisha. Kwa hiyo, Yesu alisema: “Na nyumba yo yote mtakayoingia kaeni humo, tokeni humo. Na wale wasiowakaribisha, mtokapo katika mji huo, yakung’uteni hata mavumbi ya miguuni mwenu, kuwa ushuhuda juu yao.”​—Mt. 10:11-15; Luka 9:1-6.

8. (a) Ni nini kinachoonyesha zaidi kwamba ziara za nyumbani zilifanywa? (b) Wakati huo, na vilevile sasa, nia yenye fadhili ya mwenye nyumba inawezaje kumtokezea baraka?

8 Wale ambao waliwapokea wale kumi na wawili kwa fadhili walijiweka upande wa kupata baraka kutoka kwa Yehova kupitia kwa Mwana wake, kama vile Yesu alivyowaambia wanafunzi wale, akisema hivi:

“Awapokeaye ninyi, anipokea mimi; naye anipokeaye mimi, ampokea yeye aliyenituma. . . . Na mtu awaye yote atakayemnywesha mmojawapo wa hawa ngaa kikombe cha maji baridi, kwa kuwa ni mwanafunzi, amin, nawaambia, haitampotea kamwe thawabu yake.” (Mt. 10:40-42)

Huko nyuma, kama ambavyo imetokea mara nyingi katika nyakati za kisasa pia, nia ya upole na ya kuhangaikia ya mwenye nyumba ingemfungulia njia ya kupata baraka za kiroho na taraja la uzima wa milele.​—Linganisha Mathayo 25:34-40.

9. Wale 70 waliufanyia wapi utendaji wao wa kuvuna, na wakiwa na kusudi gani lenye sehemu mbili?

9 Hata hivyo, watenda kazi zaidi walipaswa kuzoezwa kwa ajili ya mavuno. Kwa hiyo, “baada ya hayo Bwana aliweka na wengine, sabini, akawatuma wawili wawili wamtangulie kwenda kila mji na kila mahali alipokusudia kwenda mwenyewe.” Wawe walienda kwenye masinagogi au sehemu za soko, maandishi hayasemi. Walakini waliagizwa waende nyumbani za watu. Yesu aliwaambia hivi: “Na nyumba yo yote mtakayoingia, semeni kwanza, Amani, iwemo nyumbani humu; na akiwamo mwana wa amani, amani yenu itamkalia; la hayumo, amani yenu itarudi kwenu.” Wanafunzi hao walipaswa kukubali kwa shukrani ukaribishaji wa wenye nyumba wale ambao wangesikiliza “habari njema.” Walakini iwapo wote nyumbani, au hata katika mji mzima, walikataa kusikiliza ujumbe huo, wanafunzi hao walipaswa angaa kuwaonya watu hao wakisema: “Jueni hili, ya kuwa Ufalme wa Mungu umekaribia.” Hivyo waliweka kiolezo ambacho Mashahidi wa Yehova hujaribu kufuata leo. Walipainia kazi yenye sehemu mbili ya kufundisha watu wa nyumba zile zilizowapokea kwa furaha na ya kuwaonya waliozidharau “habari njema” juu ya hukumu za Mungu zitakazokuja.​—Luka 10:1-16.

10. Leo Mashahidi wa Yehova wanawezaje kupata furaha kama ile ya wale 70?

10 Maandishi yatuambia kwamba ‘wale sabini walirudi kwa furaha’ kwa sababu kwa kutumia jina la Yesu mashetani waliwatii. Walakini Kristo alionyesha kwamba wanafunzi wake, mahali pake, walipaswa kufurahia mataraja yao ya kimbinguni na kuelimishwa kwao kwa kiroho. (Luka 10:17-24) Vivyo hivyo leo, Wakristo wanaojitoa kufundisha na kuhubiri nyumbani mwa watu wana sababu za kuwa na furaha nyingi kwa sababu ya uhusiano wao wenyewe na Mungu, maarifa yao juu ya makusudi yake na baraka za Yehova juu ya jitihada zao za kutangaza “habari njema” kwa wengine.

‘FURAHA NA ROHO TAKATIFU’

11. Kundi jipya la Kikristo lilitendaje wakati wa mateso?

11 Tamasha inasonga mpaka Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. na baada ya hapo. Daraka la kuzitangaza “habari njema” sasa lilikuwa kabisa juu kundi jipya la Kikristo lililotengezwa. Mara moja, lilielekeana na mateso. Walakini yaliamsha tu kuthamini zaidi kazi yalo katika kushikilia enzi kuu ya Yehova na katika kuhubiri ufalme wake kupitia kwa Kristo. Kwa ujasiri Petro na Yohana walitangaza hivi: “Sisi hatuwezi kuacha kuyanena mambo tuliyoyaona na kuyasikia.” Pamoja na waamini wale wengine, walimsifu Yehova na kumwomba yeye akiwa ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu, . . . Ambaye aliziumba mbingu na dunia na bahari na vyote vilivyomo.’​—Matendo 4:18-24.

12. Mitume walichukua msimamo gani ulio mfano bora walipoelekeana na mateso, nao ukatokeza nini?

12 Wakati wimbi zaidi la mateso lilipowakumba (lilipowapiga) wafuasi hao wa Kristo, walitoa ushuhuda wa ujasiri mbele ya Sanhedrin ya kidini, wakisema:

“Inatupasa kumtii Mungu [kama matawala] kuliko wanadamu. Mungu wa baba zetu alimfufua Yesu, ambaye ninyi mlimwua mkimtundika katika mti. Mtu huyo Mungu amemtukuza kwa mkono wake wa kuume, awe [Wakili] Mkuu na Mwokozi, awape Waisraeli toba na msamaha wa dhambi. Na sisi tu mashahidi wa mambo haya, pamoja na [roho takatifu] ambay[o] Mungu amewapa wote wamtiio [kama mtawala].” (Matendo 5:29-32)

Mradi mitume hao waliendelea bila kusita kuunga mkono Mwenye Enzi Kuu Bwana Yehova na Wakili Mkuu wake, Yesu Kristo, wangepata roho takatifu ili kuwasaidia katika kazi ya kuhubiri na kufundisha kwao.

13. Kufikia siku hizi Wakristo wanawezaje kuendeleza ‘furaha na roho takatifu’?

13 Wakati wa kipindi hicho chenye hatari, hakukuwa na wakati wa kubishania chakula na mambo mengine madogo madogo. Walipaswa kusahau vyeo na kumwelekea kwa umoja adui wa kutoka nje. Kwa kufanya hivyo, walikiona ambacho mtume Paulo aliandika habari zake baadaye, akisema hivi: ‘Maana ya ufalme wa Mungu . . . ni haki na amani na furaha katika roho takatifu.’ (Rum. 14:17) Mpaka siku hizi, Wakristo ambao hutangaza kwa ujasiri enzi kuu ya Yehova na ufalme, huku wakishikilia kanuni za haki katika umoja na ndugu zao, wanahakikishiwa msaada wa roho takatifu na furaha katika kazi yao.​—Linganisha Mathayo 25:21.

‘KUENDELEA BILA KUACHA’

14. Ingawa waliagizwa ‘waache kunena,’ wanafunzi hao waliendelezaje mgawo wao wa kimungu?

14 “Habari njema” zilikuwa zikienea kama moto usiozuilika. Hakukuwa cha kupunguza furaha na juhudi ya mitume hao. Wakati shauri lenye hekima la mwana-sheria Gamalieli “waacheni” liliposikiwa, walitoka katika ile Sanhedrin, “wakifurahi kwa sababu wamehesabiwa kuwa wamestahili kuaibishwa kwa ajili ya jina la [Yesu].” Na waliitikiaje amri ya Sanhedrin ya ‘kuacha kunena kwa jina lake Yesu’? Masimulizi yanatuambia kwamba “kila siku, ndani ya hekalu na nyumbani mwao, hawakuacha kufundisha na kuhubiri habari njema za Yesu kwamba ni Kristo.”​—Matendo 5:38-42.

15. Ingawa sehemu fulani za kazi yetu zaweza kuwa tofauti, ni utendaji gani wa msingi tunaoweza kuendeleza, kwa kufuata kiolezo cha mitume?

15 Kama vile mitume hao, tuliko na uhuru tunatafuta “nyumba kwa nyumba” wale ambao wanastahili kuzipokea “habari njema.” Tunapowapata, twaweza kuwatembelea tena na kuwasaidia kupitia kwa funzo la Biblia la nyumbani bila malipo. Bila shaka, sehemu fulani za kazi yetu ni tofauti leo, kwa kuwa hatuendi katika mahekalu au katika masinagogi kuhubiri. Vilevile, sasa tuna msaada wa karatasi zilizopigwa chapa, magari na namna nyingine za kusafiria ili kuwezesha kazi yetu. Hivyo ziara za nyumbani ni njia yenye kuvutia ya kutawanya ujumbe uliopigwa chapa na kurudi kufundisha Neno la Mungu wale ambao huziitikia “habari njema.”

‘USIJIEPUSHE’

16. (a) Paulo alitoa ushuhuda na kufundishia wapi? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba Paulo alifanya ziara za nyumbani zinazofanana na utendaji wetu wa nyumba kwa nyumba leo?

16 Mtume Paulo pia aliweka mfano mzuri katika kuhubiri waziwazi. Katika masinagogi, katika sehemu za soko, kando ya mto​—po pote ambapo angepata Wayahudi na wengine wa kuzungumzia—​Paulo alitoa ushuhuda. Kwa miaka miwili, katika jumba la shule katika Efeso, alitoa hotuba za kila siku kwa “wanafunzi wapya.” (Matendo 16:13; 18:4; 19:9) Na Baadaye, kwa wale ambao walikuwa wamekuwa katika kundi huko Efeso, Paulo alisema hivi: “Tangu siku ya kwanza nilipokanyaga hapa Asia, . . . sikujiepusha katika kuwatangazia neno lo lote liwezalo kuwafaa, bali naliwafundisha waziwazi, na nyumba kwa nyumba, nikawashuhudia [kikamilifu].” Kwa nani? Je! kwa wale tu ambao baadaye walipata kuwa wazee? Sivyo, kwa kuwa Paulo anaongeza kwamba aliwashuhudia “Wayahudi na [Wagiriki] wamtubie Mungu, na kumwamini Bwana wetu Yesu Kristo.” Kwa hiyo, watu wapya waliohitaji kufahamu mafundisho ya msingi juu ya toba na imani walikuwa kati ya wale ambao walifundishwa “waziwazi na nyumba kwa nyumba” tangu mwanzoni kabisa mwa utumishi wa Paulo wa misionari katika Efeso.​—Matendo 20:18-21; 18:19; 19:1-7; linganisha Waebrania 6:1.

17. (a) Ni nini msingi wa tafsiri nyingi za Biblia zinazolitumia neno la Kigiriki kat oikous “nyumba kwa nyumba”? (b) ‘Kutoa ushuhuda kikamilifu’ kwa Paulo kunaonyesha kutoa ushuhuda kwa Kikristo kungetia nini?

17 Usemi huu “nyumba kwa nyumba” unatafsiriwa kutoka kwa neno la Kigiriki kat oikous. Ingawa kuna matumizi mengine, tafsiri nyingi za Biblia zenye kujulikana sana zinatumia usemi huu​​—⁠“nyumba kwa nyumba.”b Hii ni kwa sababu preposition (neno lionyeshalo uhusiano uliopo kati ya tendo moja na jingine) ya Kigiriki kata iko katika maana ya “kugawa.” (Linganisha matumizi ya kata yanayofanana na hayo katika Luka 8:1, NW,​—‘mji kwa mji,’ ‘kijiji kwa kijiji’; na katika Matendo 15:21, HNWW, “katika kila mji”) Kwa hiyo inaweza kusemwa kwamba ‘kushuhudia kikamilifu’ kwa Paulo kuligawa nyumba baada ya nyumba. Mwanafunzi wa Biblia Dakt. A. T. Robertson anaeleza kama ifuatavyo juu ya Matendo 20:20:

“Kwa (kulingana na) nyumba. Inafaa kuona kwamba mhubiri huyu mkubwa zaidi ya wahubiri wote alihubiri nyumba kwa nyumba na ziara zake hazikufanywa kuwa matembezi ya kirafiki.”

Kama vile Paulo ‘alivyoshuhudia kikamilifu,’ Wakristo leo hutafuta wenye nyumba wenye uelekevu wa kiroho, wakifanya ziara za kurudia kwenye nyumba hizo na kujifunza na watu wenye kupendezwa. Baadaye kulingana na uhitaji, ziara za uchungaji zinafanywa na waangalizi waaminifu.c

18. Ni kwa sababu gani Paulo na wenzake wasingejiepusha kuhubiri na kufundisha nyumba kwa nyumba?

18 Kulikuwa na sababu za kutosha kwa nini Paulo na Wakristo wengine wa siku zake hawakupaswa ‘kujiepusha’ katika kuhubiri na kufundisha kwao nyumba kwa nyumba. Hizo zilikuwa nyakati zenye hatari. Taratibu ya mambo ya Kiyahudi ilikuwa ikikaribia kuharibiwa kwa haraka sana. Wafalme wa Rumi walikuwa wakitilia moyo kuabudu sanamu. Kwa watu ambao walikuwa ‘wakiogopa miungu hiyo,’ kulikuwako na uhitaji wa haraka sana kutafuta “Mungu aliyeufanya ulimwengu na vitu vyote vilivyomo,” Ambaye wakati huo alikuwa “anawaagiza watu wote wa kila mahali watubu.”​—Matendo 17:22-31.

19. (a) Kwa sababu gani uhitaji wa kutoa ushuhuda nyumba kwa nyumba, pamoja na utendaji mwingine wa kutoa ushuhuda, ni wenye uharaka mwingi leo? (b) ‘Kuendelea kwetu katika imani’ kutatokeza nini?

19 Uhitaji wa ‘kushuhudia kikamilifu’​—nyumba kwa nyumba, kwa ushuhuda wa vivi hivi, katika sehemu za, soko, kwa kufanya ziara za kurudia, kwa kuongoza mafunzo ya Biblia ya kawaida nyumbani​​—⁠ni wenye uharaka leo. Ni kweli, kama ilivyokuwa katika siku za mitume Paulo, “habari njema” zimehubiriwa “katika kuumba kote kuliko chini ya mbingu.” Walakini kuna uhitaji wa jitihada ya kikamili zaidi kabla ya “dhiki kuu” kuanza. Kama ambavyo mtume Paulo alivyowaambia Wakristo hao wa Kolosai, ni jambo la lazima kwetu sote ‘tuendelee katika imani tukijengwa katika msingi na kuwa imara bila kuondoshwa katika tumaini la habari njema zile.’​—⁠Kol. 1:23, NW; Mt. 24:21.

20. Kuhubiri nyumba kwa nyumba kwa nafsi yote kwawezaje kuwa ulinzi leo?

20 Kama ilivyokuwa katika siku za kufanikiwa za Milki ya Rumi, ndivyo ilivyo leo, mkazo wa ulimwengu unaelekezwa kwa Wakristo ili kuwafanya wajiachilie kwa anasa, kile kinachoitwa “tafrija” na uasherati wa watu wasiomwogopa Mungu​—“wao wasiomjua Mungu, na wao wasioitii Injili ya Bwana wetu Yesu”​—wale wale ambao karibuni ‘wataadhibiwa kwa maangamizi ya milele.’ (2 The. 1:6-9) Ulinzi wetu unategemea kufanya kazi kama alivyofanya Paulo na Wakristo wengine wote wenye juhudi wa wakati wake, ‘wakati wote kuwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana,’ katika kufanya kazi ‘kwa nafsi yote, kama kwa Bwana, wala si kwa wanadamu.’ (1 Kor. 15:58; Kol. 3:23) Uradhi mwingi sana na furaha zitapatikana katika kufanya kazi kwa kufuata kiolezo cha mtume Paulo na wengine wa kundi la karne ya kwanza, waziwazi na ‘nyumba kwa nyumba’ na katika kutoa ‘ushuhuda kikamilifu’ ili kwamba wengine wapate kujifunza juu ya ‘kumtubia Mungu, na kumwamini Bwana wetu Yesu Kristo.’ (Matendo 20:20, 21) Tunapotumikia hivyo, wakati wote na isemwe juu yetu, kama ilivyosemwa juu ya Bwana wetu: ‘Juhudi kwa ajili ya nyumba ya Yehova ya ibada imenila.’​—Yohana 2:17.

[Maelezo ya Chini]

a Mt. 5:1; 9:10, 28, 35; 12:9; 13:54; 15:29; 21:23; Marko 1:21, 38, 39; 2:13; 3:19, 20; Luka 4:15, 16; 5:1-3; 7:36; 8:1; 13:22; 19:1-6, 47; Yohana 4:7-15; 7:14; 18:20.

b Tafsiri ya New World, Authorized Version, Revised Standard Version ya 1952, Union Version, Zaire Swahili Bible.

c Kwa mazungumzo zaidi ya habari hii, tafadhali tazama makala “Nyumba kwa Nyumba” katika The Watchtower, Agosti 15, 1961, uku. 503.

[Picha katika ukurasa wa 8]

Kama walivyofanya mitume, Wakristo wa leo hutafuta ‘nyumba kwa nyumba’ wale wanaostahili kuzipokea “habari njema”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki