Wakristo wa Kweli Ni Wahubiri wa Ufalme
“Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—MATHAYO 24:14, Biblia ya New World Translation.
1, 2. (a) Ni kwa sababu gani sasa ujumbe wa Ufalme unapasa kutangazwa ulimwenguni pote? (b) Ni maulizo gani ambayo kila shahidi wa Yehova anaweza kuuliza?
UNAOTANGAZA UFALME WA YEHOVA. Kwa makumi ya miaka, hilo limekuwa ndilo lengo kuu la gazeti hili. Kwa kweli, maneno hayo ni sehemu ya kichwa chalo cha kunakiliwa. Na ni jambo la maana kwamba sasa ujumbe wa Ufalme utangazwe ulimwenguni pote. Kwa sababu gani? Kwa sababu ya aliyosema Yesu Kristo baada ya kutaja sehemu nyingine zinazofanyiza “ishara” ya “kuwapo” kwake kusikoonekana na mwisho wa mfumo huu. Yesu alisema: “Habari Njema hizi za ufalme zitatangazwa kwa ulimwengu wote kuwa ushuhuda kwa mataifa yote. Na halafu mwisho utakuja.”—Mathayo 24:3, 14, The Jerusalem Bible.
2 Leo, “mwisho” umekaribia kweli kweli. Kwa hiyo, kila shahidi wa Yehova aliye wakfu angeweza kuuliza hivi kwa kufaa: Nina maoni gani kuelekea kazi ya kuhubiri Ufalme? Je! ninaishiriki kwa ukawaida? Na je, huduma yangu inatekelezwa kwa ustadi na juhudi?
Mgawo wa Kuhubiri
3. Maneno ya Yesu yaliyoandikwa katika Mathayo 5:14-16 yanaonyesha nini juu ya wafuasi wake?
3 Hakuna Mkristo ye yote wa kweli anayeweza kwa haki kuepuka pendeleo la kazi ya kutangaza “habari njema” kwa wengine. Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Ninyi ni nuru ya ulimwengu. Mji hauwezi kusitirika ukiwa juu ya mlima. Wala watu hawawashi taa na kuiweka chini ya pishi, bali juu ya kiango; nayo yawaangaza wote waliomo nyumbani. Vivyo hivyo nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni.” (Mathayo 5:14-16) Jambo hilo lilionyesha kwamba wanafunzi wa Yesu wangekuwa wahubiri wa Ufalme.
4. Ni mambo gani yamesemwa juu ya mtangazaji mkuu zaidi wa Ufalme?
4 Kuhusu mhubiri wa Ufalme mwenye kutokeza sana, imesemwa hivi: “Bwana yetu alipohubiri ufalme Yeye alianza . . . kutayarisha na kupanga Huduma yake kwa njia iliyotengenea . . . Alianza huduma ya kiunabii. . . na kuwafanya wale Kumi na Wawili na wale Sabini kuwa washiriki wa huduma hiyo. Yeye alipohubiri ufalme unaokuja na kufanyiza ‘ishara,’ aliwatuma mbele yake na ujumbe kama uo huo na uwezo kama uo huo. Kwa mwendo mzuri ajabu wa kufundisha kidogo, . . . Yeye aliwazoeza wakati huo kwa ajili ya vyeo vyenye amana kubwa zaidi ambavyo wangepewa baadaye.”—A Church History, cha Milo Mahan.
5. Kuhusu kuhubiri Ufalme, Yesu alifanya nini?
5 Yesu alitoa maagizo mazuri kwa mitume wake na wale wanafunzi 70 aliotuma. (Luka 6:12-16; 10:1-22) Zaidi ya hayo, Mfano wetu mwenyewe “alikuwa akizunguka-zunguka katika miji na vijiji akihubiri na kuitangaza habari njema ya ufalme wa Mungu.” Pamoja naye walikuwa wale mitume na wanawake fulani ‘waliokuwa wakiwahudumia kwa mali zao.’ (Luka 8:1-3) Ndiyo, Yesu alikuwa mtangazaji mwenye bidii wa habari njema na alichukua hatua za kuanzisha tengenezo la kuhubiri Ufalme.
6. Kabla hajapaa kwenda mbinguni, Yesu aliwapa wafuasi wake mgawo gani?
6 Baada ya huduma ya miaka mitatu na nusu, Yesu alimaliza mwendo wake wa kidunia. Kabla hajapaa kwenda mbinguni, aliwapa wafuasi wake mgawo huu: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi. Na, tazama! mimi nipo pamoja na ninyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 28:19, 20, NW) Kweli kweli, wangekuwa wahubiri wa Ufalme.
7. Ingawa wanafunzi wa Yesu hapo kwanza hawakuwa na maarifa sahihi juu ya Ufalme, ni kwa sababu gani wangefanikiwa kuwa mashahidi wake?
7 Yesu alipokuwa karibu kuondoka duniani, wanafunzi wake walimuuliza hivi: “Bwana, unarudisha ufalme kwa Israeli wakati huu?” Katika kujibu, aliwaambia hivi: “Si shauri lenu kupata kujua nyakati au majira ambayo Baba ameweka katika mamlaka yake mwenyewe.” Hata ingawa wakati huo wanafunzi hawakuwa na maarifa sahihi juu ya Ufalme, Yesu angeweza kuwapa mgawo wawe watangazaji wa Ufalme huo, kwa maana wangekuwa na msaada uliohitajiwa ili kutekeleza mgawo wao. “Lakini ninyi mtapokea nguvu wakati roho takatifu itakapofika juu yenu ninyi,” Yesu akaongeza, “na ninyi mtakuwa mashahidi wangu mimi katika Yerusalemu na katika Yudea yote na katika Samaria na kwenye sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.” (Matendo 1:6-8, NW) Chini ya uongozi wa roho takatifu, wafuasi wa Yesu hatimaye wangetambua kwamba Ufalme huo ungekuwa serikali ya kimbingu. (Yohana 16:12,13) Na muda si muda mambo ya uhakika juu ya Ufalme huo yangetangazwa mpaka “kwenye sehemu ya mbali, zaidi sana ya dunia.”
8. Kazi ya kuhubiri ya karne ya kwanza ilifanikiwa kwa kadiri gani?
8 Mashahidi hao walifanya kazi yao vizuri sana. Bila shaka, Yehova alikuwa pamoja nao, na walikuwa na utegemezo wa Yesu Kristo aliyetukuzwa. (Matendo 8:1-8; 11:19-21) Si ajabu kwamba mapema mwaka wa 60 hadi 61 W.K. mtume Paulo aliweza kusema kwamba “habari njema” zilikuwa tayari ‘zimehubiriwa katika uumbaji wote chini ya mbingu’!—Wakolosai 1:23, NW.
9. Kama ilivyosemwa hapa, ni kazi gani iliyo kuu ya kundi la Kikristo?
9 Kuhusu kazi ya kutoa ushuhuda, imeandikwa hivi: “Kutangazwa kwa injili si. . . utendaji mmoja kati ya mwingi ambao Kanisa la Agano Jipya linashiriki, bali ndio utendaji walo wa msingi, wa lazima. . . . Angalia vizuri, Yesu hakusema [katika Matendo 1:8], Ninyi mtanishuhudia, au, Mtatoa ushuhuda wangu, bali, Ninyi mtakuwa mashahidi wangu. Matumizi ya kitenzi ‘kuwa’ hapa yana maana ambayo yapasa kuchukuliwa kwa ukamili na uzito wa uhalisi. Usemi huo [katika Kigiriki] hauonyeshi tu ambayo Kanisa lingefanya, bali ambayo Kanisa lingekuwa . . . . Kanisa la Yesu Kristo ni . . . baraza la kutoa ushuhuda.” (Pentecost and the Missionary Witness of the Church, cha Harry R. Boer, kurasa 110-14) Naam, kutoa ushuhuda ndiyo kazi kuu ya kundi la kweli la Kikristo.
Kwa Uongozi wa Kimungu
10, 11. (a) Kwa msingi, watangazaji wa Ufalme wa karne ya kwanza walikuwa wamepangwaje? (b) Ilikuwaje hali mpya zilipotokea?
10 Watangazaji wa Ufalme wa karne ya kwanza walipokea mwelekezo kutoka kwa baraza linaloongoza. Wazee wenye kusafiri walitumikia ndani ya tengenezo, na kazi za kundini zilifanywa na waangalizi na watumishi wa huduma. (Matendo 15:1, 2, 22-36; Wafilipi 1:1) Lakini ilitukiaje hali mpya zilipotokea?
11 Fikiria yaliyotukia muda mfupi baada ya Pentekoste ya 33 W.K. Wayahudi wenye kusema Kigiriki walianza kunung’unika juu ya Wayahudi wenye kusema Kiebrania “kwa sababu wajane wao walisahauliwa katika huduma ya kila siku.” Ili kumaliza tatizo hilo, mitume waliweka rasmi “wanaume wenye kustahili saba” (NW) waangalie ugawanyaji wa chakula. (Matendo 6:1-8) kuhusu hilo tunasoma hivi: “Hapo kwanza, hangaiko pekee lilikuwa kwamba vyakula vya watu wote vya kila siku havikugawanywa bila upendeleo, kama tunavyoambiwa, na ndipo wale ‘saba’ wakatengwa, lakini, bila shaka, kazi nyinginezo zingeongezwa zilipotokea, kwa maana kanuni za imani hiyo mpya zijapokuwa zisizobadilika, uendeshaji na kawaida ya kutekeleza hayo, ambayo kwayo mambo hayo yangeimarishwa na kupanuliwa kwa njia yenye matokeo, vizazi vyenye kufuata viliachwa vijifanyie kwa kufuata hekima na mambo halisi ya maishani mwao . . . Kurekebisha na kubadili kidogo mambo yasiyo ya maana . . . ni jambo la lazima katika tengenezo lo lote kubwa.”—Hours With the Bible, New Testament Series, Kitabu cha Pili, cha Cunningham Geike.
12. (a) Ni nini kilichotokeza maendeleo ya Ukristo wa kwanza? (b) Ni wapi na ni jinsi gani wafuasi wa Yesu walikuja kuitwa Wakristo?
12 Kumtegemea Mungu kwa njia ya sala, pamoja na “hekima na mambo halisi ya maishani” mwa Baraza Linaloongoza, yalitokeza maendeleo ya Ukristo wa kwanza. Na kwa hakika mambo yalikuwa yakitendeka kwa uongozi wa kimungu. Kwa mfano, wafuasi wa kwanza wa Yesu waliitwa “Ile Njia.” (Matendo 9:1, 2, NW) Lakini labda mapema mwaka wa 44 W.K. katika Antiokia, Siria, “kwa uongozi wa kimungu wanafunzi waliitwa Wakristo.” (Matendo 11:26, NW) Hilo lilikuwa jina walilopewa na Mungu ambalo walilikubali mara moja.—1 Petro 4:16.a
13. Sawa na Mashahidi wa Yehova wanavyotumia njia za kisasa za kuchapa, Wakristo wa kwanza walitumia nini katika kazi yao ya kuhubiri?
13 Kati ya Wakristo hao wa kwanza, matukio mengine pia yalifanyika kwa uongozi wa kimungu. Kwa mfano, hali moja na vile Mashahidi wa Yehova wanavyotumia sasa njia za kuchapa za kisasa, ndivyo Wakristo wa kwanza walivyotangulia kutumia kitabu cha kurasa (codex)—ambacho kilifanikisha kweli kweli kazi yao ya kuhubiri Ufalme. Katika habari hiyo, C. C. McCown aliandika: “Vitabu vya kidini vya Wakristo, Agano la kale na pia maandishi mapya . . . havikuwa vya kusomwa ili kutumbuiza wale wenye mali. Wafanyi biashara wenye kufanya kazi kwa bidii walitaka kuingiza mengi kwa kadiri ambayo wangeweza ndani ya kitabu kimoja. Wao pamoja na wamisionari Wakristo wenye bidii walitaka kuweza kuangalia kwa haraka andiko la kuthibitisha hili au hili, kulazimika kufungua futi nyingi za vitabu vya mafunjo.”—The Biblical Archaeologist Reader, ukurasa 261.
Nyumba kwa Nyumba”
14. Mitume wa Yesu walikuwa na shauku ya kuhubiri chini ya hali gani?
14 Kwa sababu ya njia za kuhubiri Ufalme zilizotumiwa na Wakristo wa kwanza, lilikuwa jambo la maana sana kuweza “kuangalia kwa haraka andiko la kuthibitisha hili au hili. Bila shaka, nyakati nyingine, walitolea watu ushuhuda wa vivi hivi, hali moja na Mashahidi wa Yehova wanavyofanya mara nyingi leo. Kuhusu hilo imesemwa hivi: “Sehemu moja maalum ya kuhubiri kwa kimtume ilikuwa ni [kuhubiri bila] kungoja kufanya hivyo kirasmi. Mtume hakungoja mpaka nafasi kubwa ijitokeze. Kipindi chake pekee alichopewa na serikali ilikuwa wakati tu, kama Paulo mbele ya Feliki, aliongozwa akiwa mfungwa mbele ya mtawala aliyevaa [vazi la] zambarau ajitetee na kujibu shtaka la kuvunja sheria. Hakukosa nafasi, lakini alizipata gerezani, njiani, na katika nyumba ya kimaskini ambayo labda angepumzika usiku. . . . Alihisi kwamba ujumbe wake kwa sehemu kubwa ulikuwa kwa watu mmoja mmoja, ingawa alikuwa tayari vivyo hivyo kuutoa kwa umati. Alijiona mwenye starehe na wasikilizaji wo wote. Hakuwa amesahau mfano wa Kristo, . . . [ambaye] jumba lake la kufanyia baraza lilikuwa ni barabara yenye vumbi, au njia yenye kujazana watu, au ufuo wenye mawe-mawe wa Galilaya ya Kiyahudi . . . [Mitume] hawakuwa wamesahau kwamba hapo mwanzoni alipokuwa pamoja nao alikuwa amewapa maagizo ya pekee juu ya njia bora zaidi za kuhubiri mafundisho yake, alikuwa amekazia masomo hayo ya kwanza kwa wengine, na, kabla tu hajapaa, akawaelekeza kwa ulimwengu kuwa ni shamba lao na kila kiumbe kuwa ni wasikilizaji wao.”—History of the Christian Church, cha John F. Hurst, Kitabu cha Kwanza, uku. 96
15. Mitume walikuwa wakitimizaje kazi ya kuhubiri katika siku zilizoifuata Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K.?
15 Katika siku zilizoifuata Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., wanafunzi wa Yesu walikuwa tayari wanatumia njia nzuri sana ya kuhubiri “habari njema.” Baada ya mitume walioteswa kuvunjiwa heshima kwa sababu ya jina la Yesu Kristo, walifanya nini? “Kila siku, ndani ya hekalu na nyumbani mwao, hawakuacha kufundisha na kuhubiri habari njema za Yesu kwamba ni Kristo”! (Matendo 5:41, 42) Ndiyo, mitume walitoa ushahidi nyumba kwa nyumba.
16. Paulo aliwapa wazee wa Efeso mazoezi katika utendaji wa kuhubiri wa aina gani?
16 Baadaye, mtume Paulo alikumbusha wazee waliowekwa rasmi kutoka Efeso hivi: “Sikujiepusha katika kuwatangazia neno lolote liwezalo kuwafaa, bali naliwafundisha waziwazi, na nyumba kwa nyumba, nikiwashuhudia Wayahudi na Wayunani wamtubie Mungu, na kumwamini Bwana wetu Yesu Kristo.” (Matendo 20:20, 21) Paulo hakumaanisha kwamba alikuwa akiwafundisha wazee waliowekwa rasmi katika nyumba zao. Badala yake, alikuwa akitolea ushuhuda Wayahudi na Wagiriki wasioamini juu ya toba kumwelekea Yehova Mungu na imani katika Yesu Kristo. Bila shaka, Paulo pia alifundisha wazee hao jinsi ya kutoa ushuhuda nyumba kwa nyumba.
17. Wanachuo mbalimbali wamesema nini juu ya huduma ya nyumba kwa nyumba ya Paulo katika Efeso?
17 Kuhusu huduma ya mtume huyo katika Efeso, imesemwa hivi: “Zoea la kawaida la Paulo lilikuwa ni kufanya kazi yake tangu mapambazuko mpaka saa 5 asubuhi (Matendo 20:34-35) saa ambayo Tirano alimaliza mafundisho yake; halafu kuanzia saa 5 asubuhi mpaka saa 10 alasiri kuhubiri katika jumba hilo, kufanya mikutano pamoja na wasaidizi na kufanya mazungumzo ya faragha pamoja na watu, kupanga kufanya upanuzi mpaka kwenye [maeneo] ya ndani ndani; halafu mwishowe kufanya kazi ya kievanjeli ya nyumba kwa nyumba iliyoendelea tangu saa 10 alasiri hadi usiku sana (Matendo 20:20-21, 31).” (A. E. Bailey) Wanachuo wengine wamesema: “Hakuridhika tu na kutoa hotuba kwenye mkusanyo wa watu wote, na kutumia njia nyingine, bali kwa bidii alifuatia kazi yake kuu faraghani, nyumba kwa nyumba, na kwa uhalisi akaupeleka nyumbani ukweli wa mbinguni kwenye makao na mioyo ya Waefeso.” (A. A. Livermore) “Peupe na nyumba kwa nyumba, katika mji na kote kote katika jimbo, alikuwa amehubiri injili.” (E. M. Blaiklock) “Inafaa kuangalia kwamba mhubiri mkuu zaidi kati ya wahubiri alihubiri nyumba kwa nyumba wala hakufanya ziara zake kuwa matembezi ya kirafiki tu.”—A. T. Robertson.
18. (a) Ni kwa sababu gani ungesema kwamba kuna msingi imara wa Kimaandiko wa huduma ya nyumba kwa nyumba ya Mashahidi wa Yehova? (b) Kama Yesu na wanafunzi wake wa kwanza, ni wapi na ni jinsi gani Mashahidi wa Yehova wanahubiri ujumbe wa Ufalme?
18 Utoaji wa ushuhuda nyumba kwa nyumba ulifanywa na mitume wa Yesu mwaka wa 33 W.K. Ulikuwa sehemu ya huduma ya Paulo katika Efeso na bila shaka kwingineko. Kwa hiyo kuna msingi imara wa Kimaandiko wa huduma ya nyumba kwa nyumba ya Mashahidi wa Yehova. Na ndivyo ilivyo na njia nyingine wanazotumia kueneza ujumbe wa Ufalme. Kwa kupendeza, Cyclopedia ya McClintock na Strong inasema: “Bwana yetu na mitume wake walipata mahali pa kuhubiri po pote ambapo watu waliweza kukusanywa. Kando-kando za mlima, fuo za bahari na mito, barabara za watu wote, nyumba za faragha, ukumbi wa Hekalu, sinagogi la Kiyahudi, na sehemu nyingine mbali-mbali zilizokuwa tayari kutangaziwa Injili.” (Kitabu cha 8, ukurasa 483) Kama Yesu na wanafunzi wake wa kwanza, Mashahidi wa Yehova wanahubiri ujumbe wa Ufalme katika “barabara za watu wote, nyumba za faragha, . . . na sehemu nyingine mbalimbali.” Kwa mfano, wanashiriki kazi ya barabarani ya magazeti (wakiwa na gazeti hili pamoja na gazeti jenzi lake Amkeni!) na wanajulikana hasa kwa ajili ya kutoa kwao ushuhuda nyumba kwa nyumba.
19. Maamuzi yanafanywaje kuhusu njia za kuhubiri zinazotumiwa sasa na Mashahidi wa Yehova?
19 Namna za kawaida za huduma zinazotumiwa sasa na Mashahidi wa Yehova ziliimarishwa sana katika karne ya kwanza, na, licha ya hayo, inafaa kwa Baraza Linaloongoza la kisasa la Wakristo wapakwa mafuta kuamua ni njia gani za kuhubiri zinazofaa wakati huu. Maamuzi hayo kwa sehemu yanaweza kutegemezwa juu ya “hekima na mambo yenye mafaa” ambayo wanaume hao wamejionea maishani. Hata hivyo, wanafanya maamuzi hasa, kama baraza linaloongoza la Kikristo la karne ya kwanza lilivyofanya. Mwelekezo wa Mungu na uongozi wa roho takatifu yake vinatafutwa katika sala, na vielelezo vya Kimaandiko vinafuatwa wakati wa kuamua ni njia zipi za kuhubiri zinazofaa zaidi katika hizi “siku za mwisho.”—2 Timotheo 3:1; Matendo 15:23, 28.
20. (a) Ni kwa sababu gani tunaweza kuwa na uhakika kwamba njia za kuhubiri wanazotumia Mashahidi wa Yehova zina kibali ya kimungu? (b) Ni nia gani wanayopaswa kuwa nayo watumishi wa Yehova wote kuelekea kazi ya kuhubiri Ufalme?
20 Ni wazi kwamba njia za kuhubiri zinazotumiwa na Mashahidi wa Yehova zina uongozi wa kimungu, kwa maana Mungu amezifanikisha na kuzibariki jitihada hizo kwa utele. (Mithali 10:22) Halaiki ya watu wanaikubali ibada ya kweli na kujiunga na mabaki wa wafuasi wa Yesu waliopakwa mafuta kuwa sehemu ya tengenezo pekee linaloheshimu jina takatifu la Yehova na kutangaza bila woga habari njema za Ufalme wa kimbingu uliosimamishwa. Kwa hiyo watumishi wote wa Yehova na waendelee kujikaza kwa bidii katika kazi ya kufanya wanafunzi kwa kadiri mfumo huu unavyokaribia mwisho wake. Tunapaswa kufanya hilo kwa uaminifu, kwa maana Wakristo wa kweli bila shaka ni wahubiri wa Ufalme.
[Maelezo ya Chini]
a Ona ukurasa wa 316 wa kitabu Aid to Bible Understanding, kilichochapishwa na Sosaiti yetu.
Unaelewaje?
◻ Ni kwa sababu gani ujumbe wa Ufalme sasa unapasa kutangazwa duniani pote?
◻ Kazi kuu ya Wakristo wote wa kweli ni kazi gani?
◻ Ni kwa sababu gani inaweza kusemwa kwamba kati ya watumishi wa Yehova mambo yanafanywa kwa uongozi wa kimungu?
◻ Kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba ya Mashahidi wa Yehova ina msingi gani imara?
[Picha katika ukurasa wa 9]
Yesu aliwaambia wafuasi wake hivi: ‘Nendeni, mkafanye wanafunzi.’ Je! wewe unafanya kazi kuu hiyo ya Wakristo wote wa kweli kwa bidii?
[Picha katika ukurasa wa 11]
Je! wewe unatoa ushuhuda kwa ukawaida nyumba kwa nyumba? Mitume wa kwanza wa Yesu walifanya hivyo. Ni hali moja na mtangazaji wa Ufalme mwenye juhudi, Paulo