Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w81 9/1 kur. 21-24
  • Kitabu cha Zaburi-Dawa ya Moyo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kitabu cha Zaburi-Dawa ya Moyo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • UTUKUFU NA ADHAMA YA MUNGU
  • UANGALIZI WAKE WA UPENDO KWA WATU WAKE
  • REHEMA YAKE
  • UDHAMBI WA MWANADAMU NA UHITAJI WA KUTUBU NA KUSAMEHEWA
  • TUMAINI NA UHAKIKA KATIKA MUNGU
  • UFALME WA KIMASIHI
  • Kitabu Cha Biblia Namba 19—Zaburi
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Nyimbo Zilizoongozwa na Roho Ambazo Zinafariji na Kufundisha
    Biblia—Ina Ujumbe Gani?
  • Mambo Makuu Katika Kitabu cha Kwanza cha Zaburi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
w81 9/1 kur. 21-24

Zaburi

Kitabu cha Zaburi-Dawa ya Moyo

KITABU cha Zaburi kilikuwa ndicho kitabu cha mashairi na nyimbo cha taifa la kale la Kiebrania. Mashairi yake yalitungiwa muziki nayo yalitumiwa katika ibada ya Yehova katika hekalu la Yerusalemu, pamoja na kuwa ndizo nyimbo ambazo sana sana ziliimbwa nyumbani na zilizokuwa katika mioyo ya Waisraeli mmoja mmoja. Msingi wa mashairi hayo haukuwa sauti yenye kufanana ya maneno, wala mistari. Mara nyingi, kunakuwa na kulingana kwa mawazo, mara nyingine yakiwa na maana inayolingana, nyakati nyingine maana inayotofautiana. Hiyo inasaidia akili na roho ya msomaji kufuatana na wazo kwa utaratibu hata kwamba matokeo yanakuwa kufahamu vizuri zaidi pamoja na kusukumwa kutenda. Kurudia-rudia, pamoja na tofauti ya maneno, hukazia kweli zinazoonyeshwa, huku kukizifanya zitokeze zaidi na kuwa wazi zaidi. Mifano hii michache kutoka kwa maelfu yanayopatikana itatoa mfano:

“Sheria ya Yehova ni kamilifu, inarudisha nafsi.

Kumbukumbu la Yehova linatumainika, linamfanya asiye na ujuzi kuwa na hekima.”​—Zab. 19:7, NW.

“Mwovu anakopa naye harudishi,

Bali mwenye haki anaonyesha kibali na kutoa zawadi.”​—Zab. 37:21, NW.

“Kama inanipasa kutembea katikati ya taabu, wewe utanihifadhi hai.

Kwa sababu ya hasira ya adui zangu wewe utanyosha mkono wako,

Nao mkono wako wa kuume utaniokoa mimi.”​—Zab. 138:7, NW.

Zaburi zinaelekezwa kwenye moyo. Uvutano mkubwa mno zinazotokeza ni kwa sababu ya uhakika wa kwamba, kupitia kwa Zaburi, Mungu huufunua wazi moyo wa kibinadamu, akigusia maono yake yenyewe na majaribu. Upendo, furaha, kushangilia, sifa, huzuni, kuvunjika moyo, toba, tumaini​—msomaji aweza kujitambulisha na hayo yote. Kushuka moyo kunakoletwa na ugonjwa, uadui mkali kwa upande wa washiriki, kuvunjwa moyo na rafiki aliyeaminiwa anapogeuka na kuwa msaliti, maono ya kusikitika na kumwogopa Mungu wakati mtu ametenda dhambi, furaha kuu mtu anapojua kwamba amesamehewa dhambi yake​—yote hayo pamoja na maelfu mengine ya maono yanayoletwa na mabadiliko ya maisha si kwamba tu msomaji anayasoma, bali anayaona pia.

Kwa sababu hizo Zaburi ni sehemu ya maana, isiyopaswa kukosekana ya Neno la Mungu, linaloweza kumfanya mtu wa Mungu kuwa “anastahili kabisa, ametayarishwa kabisa kwa ajili ya kila kazi njema.” (2 Tim. 3:16, 17, NW) Kitabu hicho kinashughulika na hali ya wanadamu kama vile ilivyo kweli kweli na kumfariji msomaji kuhusu kila tatizo la kibinadamu, na kuzifanya Zaburi kuwa zafaa nyakati zote, zikitumika katika maisha ya leo kama vile zilivyotumika miaka elfu nyingi zilizopita.

UTUKUFU NA ADHAMA YA MUNGU

Zaburi zinaonyesha kwa nguvu sana sifa za Mungu—utukufu wake na ukamilifu. Uzuri wa umilele wa Yehova, adhama na uenye-nguvu-zote ni sifa zinazoonyeshwa kwa njia kubwa sana. Kiwazo chaweza kuonwa katika mifano hii mitatu mifupi:

“Ee Yehova, wewe mwenyewe umejithibitisha kuwa makao ya kweli kwetu sisi

Wakati wa kizazi baada ya kizazi.

Kabla ya milima yenye kuzaliwa,

Au hujaanza kutokeza kama kwa maumivu ya kuzaa dunia na nchi izaayo,

Hata tangu wakati usiojulikana mpaka wakati usiojulikana wewe ndiwe Mungu. . . .

Kwa kuwa miaka elfu moja machoni pako ni kama jana tu inapopita,

Na kama kesha wakati wa usiku.”​—Zab. 90:1-4, NW.

“Zamani sana wewe uliweka misingi ya dunia yenyewe,

Nazo mbingu ni kazi ya mikono yako.

Zenyewe zitapotelea mbali, bali wewe mwenyewe utaendelea kusimama;

Na kama vile vazi zenyewe zote pamoja zitachakaa

Kama vile nguo utazibadilisha, nazo zitamaliza zamu yake.

Bali wewe ni yule yule, nayo miaka yako mwenyewe haitatimizwa.”​—Zab. 102:25-27, NW.

“Mawingu na giza zito humzunguka yeye; Haki na hukumu ndizo mahali palipoimarishwa pa kiti chake cha enzi.

Mbele yake moto wenyewe huenda,

Nao hula adui zake kuzunguka sehemu zote.

Umeme wake uliangaza nchi izaayo;

Dunia ikaona ikapatwa na maumivu makali.

Milima yenyewe ilianza kuyeyuka kama vile nta kwa sababu ya Yehova,

Kwa sababu ya Bwana wa dunia yote.”​—Zab. 97:2-5, NW.

Hali moja na hiyo, uhusiano wa karibu sana wa Mungu pamoja na watu wake unaonyeshwa kwa wingi sana katika Zaburi, kama vile hivi vichwa vidogo vichache vinavyofuata vionyeshavyo:

UANGALIZI WAKE WA UPENDO KWA WATU WAKE

“Kwa sababu ulisema: ‘Yehova ni kimbilio langu,’

Umemfanya yeye Aliye Juu Zaidi mwenyewe makao yako;

Hakuna msiba utakaokuangukia wewe,

Na hata tauni haitakaribia hema yako.

Kwa kuwa yeye atawapa malaika zake amri kuhusu wewe,

Wakulinde katika njia zako zote.

Mikononi mwao watakuchukua,

Ili mguu wako usigonge juu ya jiwe.”​—Zab. 91:9-12, NW.

REHEMA YAKE

“Kama vile baba huwaonyesha wanawe rehema,

Yehova ameonyesha rehema wale wanaomwogopa yeye.

Kwa kuwa yeye mwenyewe anajua vizuri sana umbo letu,

Akikumbuka kwamba sisi tu mavumbi.”​—Zab. 103:13, 14, NW.

“Kama makosa ndiyo unayoangalia,

Ee Yah, Ee Yehova, ni nani angeweza kusimama?

Kwa kuwa kuna msamaha wa kweli kwako wewe,

Ili upate kuogopwa.

Mimi nimetumaini, Ee Yehova, nafsi yangu imetumaini.

Na neno lake mimi nimelingojea.”​—Zab 130:3-5, NW.

UDHAMBI WA MWANADAMU NA UHITAJI WA KUTUBU NA KUSAMEHEWA

“Usiingie hukumuni pamoja na mtumishi wako,

Kwa kuwa mbele yako hakuna aliye hai anayeweza kuwa mwenye haki.”​—Zab 143:2, NW.

“Ee Yehova, katika hasira yako usinikaripie mimi,

Wala katika ghadhabu yako usinisahihishe.

Kwa kuwa mishale yako imepenya sana ndani Yangu,

Na juu yangu mkono wako umeshuka

Hakuna sehemu yenye afya katika nyama yangu kwa sababu ya malaumu yako.

Hakuna amani mifupani mwangu kwa sababu ya dhambi yangu.

Kwa kuwa makosa yangu yamepita juu ya kichwa changu;

Kama vile mzigo mzito ni mazito sana kwangu

Vidonda vyangu vimekuwa vyenye kunuka, vimeoza,

Kwa sababu ya upumbavu wangu.

Nimefadhaika, nimeinama chini sana kupita kiasi;

Mchana kutwa nimetembea huku na huku kwa huzuni.”​—Zab. 38:1-6, NW.

“Tazama! Pamoja na makosa nilitokezwa kwa maumivu ya kuzaa,

Na katika dhambi mama yangu alichukua mimba yangu.”

“Na unitakase mimi na dhambi kwa hisopo, ili nipate kuwa safi;

Na unisafishe mimi, ili nipate kuwa mweupe hata kuliko theluji.”

“Ufiche uso wako dhambi zangu,

Na kuyafuta hata makosa yangu yote.”​—Zab. 51:5, 7, 9, NW.

“Mwenye furaha ni yeye ambaye uasi wake umesamehewa, ambaye dhambi yake imefunikwa.

Mwenye furaha ni mtu yule ambaye Yehova hamhesabii kosa,

Na ambaye katika roho yake hakuna udanganyifu. . . .

Mwishowe dhambi zangu nikaungama kwako, na kosa langu sikufunika.

Nilisema: ‘Nitaungama makosa yangu kwa Yehova.’

Nawe, wewe mwenyewe ukanisamehe kosa dhambi zangu.”​—Zab. 32:1-5, NW.

TUMAINI NA UHAKIKA KATIKA MUNGU

“Abarikiwe Yehova, ambaye kila siku huchukua mzigo kwa ajili yetu,

Mungu wa kweli wa wokovu wetu.

Selah

Mungu wa kweli kwetu ni Mungu wa matendo ya kuokoa;

Na Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu ndiye mwenye njia za kutoka kwenye mauti.”​—Zab. 68:19, 20, NW.

“Mimi nina nani katika mbingu?

Na mbali na wewe mimi sina pendezi jingine duniani. 7

Mwili wangu na moyo wangu vimeshindwa.

Mungu ndiye mwamba wa moyo wangu na fungu langu mpaka wakati usiojulikana.

Kwa maana, tazama! wale wenyewe wanaokaa mbali nawe wataangamia.

Kwa hakika wewe utanyamazisha kila mmoja akuachaye isivyo adili.

Lakini kwa habari yangu mimi, kukaribia Mungu ni kwema kwangu mimi.

Katika Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova nimeweka kimbilio langu,

Kuzitangaza kazi zako zote.”​—Zab. 73:25-28, NW.

Katika Mungu nimeweka tumaini langu. Mimi sitaogopa.

Mtu wa duniani anaweza kunifanya nini?”‏​—Zab. 56:11, NW.

“Kwa kuwa huyu Mungu ni Mungu wetu mpaka wakati usiojulikana, hata milele.

Yeye mwenyewe atatuongoza mpaka tufe.”​—Zab. 48:14, NW.

UFALME WA KIMASIHI

Zaburi zina mengi ya kusema kuhusu Kristo Yesu na ufalme wa Kimasihi, si kwa kumtaja kwa jina, bali kwa kumweleza, hasa akiwa mfalme mwenye utukufu anayetawala dunia yote katika amani na haki. Zaburi nyingine zinaelekea kutabiri juu ya Masihi moja kwa moja, kwa mfano, kama vile Zaburi ya 2 na ya 110. Katika visa vingi zaburi nyingine husema juu ya Masihi, si moja kwa moja, bali kwa kumfananisha, na kwa mafumbo. Yaani, mtunga zaburi alikuwa hasa akifikiria tatizo lake mwenyewe au mambo ya taifa lake, na yale aliyosema yalihusu wakati wake mwenyewe moja kwa moja. Walakini kwa kanuni, au katika utimizo wa pili na ulio kamili au wa mwisho, yale aliyosema yanafanywa yamhusu Kristo na waandikaji wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Inawezekana sana ikawa kwamba mtunga zaburi hakuwa akimfikiria Masihi sikuzote, wala hakufahamu kabisa matumizi ya mfano, hata kama vile mtume Petro anavyosema kwamba manabii hawakufahamu kabisa maana ya mambo yote waliyotabiri.​—1 Pet. 1:10-12.

Mfano wa hili unapatikana katika Zaburi 102:25-27, iliyotangulia kutajwa. Mstari wa kwanza wa zaburi hiyo unaonyesha kwamba mtunga zaburi huyo alikuwa akisema na Yehova. Walakini katika Waebrania 1:10-12 mtume Paulo anamhesabia Yesu Kristo sifa hizo, kwa sababu Yesu ndiye aliyetumiwa na Mungu katika kazi ya kuumba na ambaye amepewa sasa mamlaka yote “katika mbingu na duniani.” (Mt. 28:18, NW; Kol. 1:15-17) Yesu anamwakilisha Mungu kwetu kwa ukamilifu katika sifa zake zote na matendo.

Zaburi 22, anayohesabiwa Daudi, inaeleza kwa sehemu, katika usemi wa mfano, baadhi ya mateso ya Kristo. (Linganisha Zaburi 22:1 na Marko 15:34; vilevile linganisha zaburi hiyo yote na yale masimulizi manne ya Injili ya kuhukumiwa kwa Yesu na kutundikwa kwake.) Maelezo ya matukio yameandikwa katika usemi unaowezesha utimizo kamili katika maisha ya Kristo.

Hata hivyo, waandikaji wa zaburi walifahamu kwa kadiri fulani kwamba maandishi yao yalimhusu Kristo. Wakati Daudi alipoandika Zaburi ya 16, aliongozwa kwa roho atabiri juu ya Masihi ambaye nafsi yake haingeachwa katika Sheol au Hadeze (kaburi) milele, wala mwili wake uliozikwa haungeoza kabisa. (Matendo 2:31, New International Version; The Jerusalem Bible; Revised Standard Version) Kwa hiyo, mtume Petro, akizungumza kwa maelfu ya Wayahudi katika siku ya Pentekoste, alionyesha kwamba Masihi ndiye aliyekuwa akitajwa, aliposema hivi: “Basi kwa kuwa [Daudi alikuwa] nabii, akijua ya kuwa Mungu amemwapia kwa kiapo, ya kwamba katika uzao wa viuno vyake atamketisha mmoja katika kiti chake cha enzi; yeye mwenyewe akitangulia kuyaona haya, alitaja habari za kufufuka kwake Kristo, ya kwamba [nafsi] yake haikuachwa [kaburini, Kiebrania, Sheʹol], wala mwili wake haukuona uharibifu.”​—Matendo 2:30, 31.

Mbele ya Wayahudi waliokusanyika, waliokubali kabisa kabisa kwamba Zaburi ziliandikwa kwa uongozi wa Mungu, Petro alitumia hoja hiyo kwa nguvu sana, pamoja na Zaburi ya 110 ya Kimasihi, kuthibitisha kwamba Kristo ndiye aliyekuwa akitajwa na ya kwamba alikuwa amefufuliwa kutoka Hadeze (Sheʹol). Alisema kwamba Daudi mwenyewe alikufa akazikwa na ya kwamba kaburi lake lilikuwamo miongoni mwa Wayahudi wakati uo huo likiwa ushuhuda wa uhakika huo. Wao walijua kwamba alikwenda katika Sheʹol, au Hadeze, na ya kwamba mwili wake ulipatwa na uharibifu, au kuoza. Ndipo walipofahamu kwamba Daudi hakuwa akisema habari zake mwenyewe. Kwa hiyo, kwa kuwa hiyo ilikuwa kweli, Daudi, akiwa nabii, alikuwa akisema juu ya mmoja wa wazao wake mwenyewe ambaye jambo hilo lingempata. Ushuhuda ulioonyeshwa na matukio kuhusiana na kifo na kufufuliwa kwa Yesu ulikuwa vilevile mbele ya Wayahudi wakati uo huo, ukithibitisha waziwazi kwamba Daudi alikuwa akisema kiunabii juu ya Kristo, mzao wa Daudi. (1 Pet. 1:10-12) Hoja hiyo ilikuwa na matokeo yenye nguvu sana juu ya Wayahudi waliokuwa wakisikiliza hotuba ya Petro.​—Matendo 2:29-36.

Katika kila njia Zaburi hutukuza Mungu na Mwanawe nazo hutusaidia tupate kujua vizuri zaidi wale wanaoambiwa hivi: “Hii ndiyo maana ya uzima wa milele, wapate maarifa ya kukujua wewe, Mungu wa kweli peke yako, na ya yeye uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3, NW) Zaburi hueleza majaribu yanayowapata wanadamu wote nazo hutuonyesha jinsi ya kusali katika wakati wa furaha na wa taabu. Hata tuwe na tatizo la namna gani, kuna zaburi ya kutusaidia na kutupa zeri yenye kufariji moyo.

Paulo alisema juu ya uhitaji wa msaada katika sala, akisema: “Hatujui kuomba kama itupasavyo.” (Rum. 8:26) Mara nyingi hiyo inakuwa kweli kwa kila Mkristo. Mara nyingi tunaweza kupata katika kitabu cha Zaburi msaada unaohitajiwa wa kumweleza Mungu kwa ukamili zaidi mawazo na tamaa zetu za ndani zaidi.​—Linganisha Waefeso 5:19; Kolosai 3:16.

Zaburi, kwa kuzungumza juu ya maono ya ndani mbalimbali ya kibinadamu, hutokeza uvutano mchangamfu wa kibinafsi. Msomaji aweza kujiona naye anaona kwamba zinazungumza naye, au kwa niaba yake. Mawazo yake ya ndani zaidi na misukumo huchochewa nao moyo wake huchunguzwa. Anasukumwa afanye mabadiliko maishani mwake. Katika kufanya hivyo anatajirishwa, naye anapata kumjua Mungu zaidi. Kila mtu apaswa kusoma Zaburi tangu mwanzo mpaka mwisho. Hakuna mtu anayeweza kuzisoma na asifaidike kibinafsi.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki