Maswali Kutoka Kwa Wasomaji
● Kwa kusema kwamba Yesu “alijaribiwa,” je! Waebrania 4:15 linaonyesha kwamba Mungu hakuwa na uhakika kama Mwanawe angekuwa mwaminifu?
Sivyo, kwa kuwa hakuna jambo lo lote katika Maandiko linaloonyesha maoni yaliyo tofauti kuliko yale ya kwamba Yehova alikuwa na uhakika kwamba Mwanawe angeendeleza ukamilifu wake. Ni jambo tofauti kabisa linaloonyeshwa katika Waebrania 4:15, ambalo lasema hivi: “Kwa kuwa hatuna kuhani mkuu asiyeweza kuchukuana nasi katika mambo yetu ya udhaifu; bali yeye alijaribiwa sawasawa na sisi katika mambo yote, bila kufanya dhambi.”
Yehova alikuwa ametabiri kwamba akiwa Masihi, Mwanawe angeendeleza ukamilifu wake ajapoteseka. (Zab. 118:22; Isa. 53:3-7, 10-12) Mungu alikuwa na sababu nzuri za kuwa na hakika kwamba Mwanawe pekee, ajapokuwa na uhuru wa kujichagulia, angekuwa mwaminifu chini ya majaribu.
Kwa kushirikiana naye kwa muda wa mileani (maelfu ya miaka) nyingi pamoja na mambo waliyofanya pamoja na Mwanawe, Yehova alipata kumfahamu kwa kadiri asiyopata mtu mwingine kumfahamu. (Mt. 11:27; Yohana 10:14, 15) Mungu alikuwa anafahamiana vizuri kabisa na nia ya akili na hali ya moyoni ya Mwanawe. (Rum. 15:5) Kwa mfano, ingawa Neno ndiye aliyetangulia kuumbwa, yeye hakutafuta kuabudiwa, kama alivyofanya kiumbe wa kiroho aliyepata kuwa Shetani. (Flp. 2:5, 6) Tofauti na malaika waasi ambao waliasi kabla ya Gharika, sikuzote Mwana huyo hutafuta kumpendeza Babaye. Hivyo, mtume Paulo anayatumia maneno ya mtunga zaburi kwake, akisema hivi: “Mungu ni kiti chako cha enzi milele, na fimbo ya ufalme wako ni fimbo ya unyofu. Ulipenda haki, na ukachukia uasi.” (Ebr. 1:8, 9, NW; Zab. 45:6, 7) Zaidi ya hayo, wakati wote amependezwa na wanadamu kwa ajili ya faida yao. (Mit. 8:30, 31) Na mara nyingi alionyesha kumtegemea Babaye, ambaye mapenzi yake alitamani sana kufanya. (Yuda 9; linganisha Yohana 12:27, 28.) Kwa hiyo hata kabla ya Yesu kuzaliwa kama mwanadamu, Yehova angeweza kuwa na uhakika kwamba angeendeleza ukamilifu wake.
Wengine wameuliza hivi: “Namna gani kama Yesu angefanya dhambi?” Lakini kwa kweli huko ni kuwazia kusikofaa. Jambo hilo linapingana na mambo ya hakika, Ukweli ni kwamba yeye hakufanya dhambi. Namna Yehova alivyomtumaini akionyesha maarifa na hekima kamili ya Mungu inaonyesha kwamba ilistahili amtumaini hivyo.
Waebrania 4:15 linakaza fikira zetu juu ya sifa za Yesu kama Kuhani Mkuu wa kimbinguni. Kwa kuwa mtu mkamilifu mwenye kulingana na Adamu na kwa kujionyesha kuwa mwaminifu mpaka kufa, Yesu alitumika kama ukombozi. (Ebr. 2:9) Walakini vilevile alipata namna ya majaribu na kushuka moyo kunakopata wanadamu wanaojitahidi kuwa waaminifu, kutia ndani na wale watakaochukuliwa mbinguni kama “ndugu” za Yesu na watawalawenzi wake. (Ebr. 2:14-17) Alipatwa na uchovu wa maumbile na kukatishwa tamaa. Na hata zaidi, alielekeana na majaribu ya kuteseka pamoja na magumu. Paulo angeweza kusema kwa kufaa kwamba Kristo ndiye ‘aliyejaribiwa sawa-sawa na sisi katika mambo yote.’ Kwa njia hiyo Yesu alikamilishwa au akastahilishwa kwa ajili ya sehemu yake kama Kuhani Mkuu anayeweza “kuchukuana nasi katika mambo yetu ya udhaifu.” Ingawa kuhani wakuu wengineo walipaswa kutoa dhabihu kwa ajili ya dhambi zao wenyewe, Kristo akiwa Kuhani Mkuu ‘hana dhambi.’ Hata hivyo, kwa kuwa na mwili na damu kama sisi, yeye anaweza ‘kuchukuliana nasi kwa upole.’—Ebr. 4:15, 16; 5:1, 2, 8; 7:28.
Kwa hiyo, Waebrania 4:15 linapaswa kututia moyo. Mahali pa kudokeza kwamba Mungu alikosa uhakika katika Mwanawe, lapaswa kujenga uhakika wetu kwamba wanadamu wanaweza kuwa waaminifu kwa Yehova. Nalo lapaswa kutufanya kuwa na uhakika kwamba katika kumkaribia Yehova tunaye Kuhani Mkuu mpole, mwenye kuhurumia na mwenye ufahamu akitumikia kwa ajili yetu.