Wakati Msiba wa Ulimwengu Ukaribiapo—‘Mfikirie Yesu’
“Ndugu watakatifu, . . . mfikirieni mtume na kuhani mkuu ambaye sisi tunaungama—Yesu.”—WAEBRANIA 3:1, NW.
1, 2. Tunaweza kufaidikaje kutokana na msiba ulioadhimishwa katika Roma?
KATIKA Roma unaweza kupata mchoro wenye kutoa ushuhuda kwamba kulikuwa na msiba—msiba unaopasa kugeuza sana maisha yako. Katika Uwanja Mkuu wa Roma wa kale wa mazungumzo ya kibaraza liko lile Tao la Tito, lenye kuadhimisha hatua ya Jemadari Tito ya kuuteka na kuuharibu Yerusalemu mwaka wa 70 W.K. Umbo lililochongwa katika tao hilo linaonyesha Wayahudi wenye pingu mikononi wakilazimishwa kuchukua nyara zilizotekwa katika mji huo.
2 Sisi Wakristo tunaweza kufaidika kutokana na msiba huo kwa kuchunguza mashauri ya Biblia yanayoufaa wakati huu, ambayo ni wazi yaliandikwa miaka tisa hivi kabla ya uharibifu huo. Yamo katika kitabu cha Waebrania, ambacho mtume Paulo aliwaandikia Wakristo Waebrania katika Yerusalemu na Yudea.
3. Ni jambo gani lililofanya hali ya Wakristo Waebrania katika Yerusalemu iwe ngumu?
3 Ndugu zetu huko nyuma walikuwa katika hali yenye ugumu mkubwa. Ingawa Yudea ilielekea kuwa imesimamiwa kwa imara na Roma, wengi wa Wayahudi walikuwa waasi. (Matendo 5:36, 37) Ebu wazia mkazo mkali ambao Wayahudi hao wangaliweka juu ya wafuasi wa Yesu ambao hawakukubali kuwa upande mmoja na Wayahudi dhidi ya (kupinga) Roma, kwa sababu ‘hawakuwa sehemu ya ulimwengu.’ (Yohana 17:16, NW) Sababu nyingine iliyofanya Wakristo Waebrania wateswe ni maoni ya Wayahudi ya kujiona kuwa wakubwa zaidi kwa sababu walikuwa wamechaguliwa na Mungu, wakaingizwa katika agano la Torati na kupewa njia ya ibada iliyohusu makuhani wa Kilawi na dhabihu.
4. (a) Kwa sababu gani ingeweza kusemwa kwamba Yesu alikuwa ametokea kwenye “umalizio wa mifumo ya mambo”? (b) Yesu alitabiri nini juu ya umalizio huo?
4 Walakini, muhula (kipindi) wa Wayahudi—pamoja na mifumo yao ya dhabihu za hekaluni, makuhani, sikukuu na Sabato zao—ulikwisha kwanza baada ya kifo cha dhabihu cha Masihi. (Wagalatia 3:24, 25; Wakolosai 2:13-17) Hivyo Paulo angeweza kuandika kwamba Mwana wa Mungu alidhihirishwa kama mwanadamu “mara moja kwa wakati wote kwenye umalizio wa mifumo ya mambo.” (Waebrania 9:26, NW; 1:2) Baada ya muda mfupi umalizio huo ungeonekana wazi kwa njia isiyoweza kukanwa, wakati wa kuharibiwa kwa hekalu. Yesu alipotabiri uharibifu huo, wanafunzi wake waliuliza, “Mambo hayo yatakuwa wakati gani?” (Mathayo 23:37–24:3, NW) Yesu alijibu kwamba kungekuwako vita, upungufu wa chakula, matetemeko ya ardhi, rnagonjwa ya kipuku na kazi yenye kuenea sana ya kuuhubiri Ufalme kabla ya mwisho kuja. (Mathayo 24:4-14; Luka 21; 10, 11, NW) Maneno hayo yalitimia katika kizazi kilichokuwa kati ya wakati ambao Yesu aliutoa unabii huo na wakati Paulo alipowaandikia Waebrania. Kristo alitabiria Yerusalemu pia ‘dhiki kubwa ambayo haikuwa imetokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu.’ (Mathayo 24:21) Dhiki yenye uharibifu iliyoujilia Yerusalemu mwaka wa 70 W.K. haikuwa na kifani wala haingeweza kutokea nyingine ya namna iyo hiyo katika mji huo. Hata hivyo huo ulikuwa utimizo mdogo tu. Kwa sababu gani? Kwa sababu wakati wa baadaye sana “dhiki kubwa” ingeupata ulimwengu wote wa wanadamu.
5. Ni kwa njia gani bado kutakuwa na “dhiki kubwa’’ kwa kadiri kubwa zaidi?
5 Mambo ya uhakika yanathibitisha kwamba maneno ya unabii wa Yesu yana utimizo mkubwa zaidi wakati wa ‘kuwapo kwake na wa umalizio wa mfumo wa mambo.’ (Mathayo 24:3, NW) Ufunuo sura ya 6, ulioandikwa miongo ya miaka baada ya dhiki ya Yerusalemu, ulitabiri pia vita, njaa kuu na magonjwa. Hayo yangepata eneo kubwa kuliko Yudea, kwa maana Ufunuo ulisema kwamba vita yenyewe ‘ingeondoa amani duniani.’ (Ufunuo 6:4, HNWW) Matukio ambayo yamekuwa yakiendelea kuonekana duniani pote tangu Vita ya Ulimwengu ya Kwanza katika mwaka wa 1914 kufikia 1918 yanaonyesha kwamba tunaishi katika umalizio wa mfumo wa mambo ya sasa, nao utafikia upeo katika “dhiki kubwa.” Dhiki hiyo itamaliza uovu duniani, itayarishe njia ya kuingia kwa Paradiso chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu.
6. Ni nini kinachoonyesha kwamba kitabu cha Waebrania kiliandikwa kwa kufikiria wakati wetu?
6 Kitabu cha Waebrania kinaelekeza mambo mpaka kwenye wakati wetu. Ndani yacho Paulo aliandika kwamba wakati huo Kristo alikuwa mbinguni “akingojea hata adui zake wawekwe kuwa chini ya miguu yake.” (Waebrania 10:13) Kitabu hicho kinataja pia wakati “ambapo [Mungu] analeta tena Mzaliwa-wa-kwanza wake ndani ya dunia inayokaliwa na watu.” (Waebrania 1:6, NW) Wakati huo ndio sasa! Ushuhuda unaonyesha kwamba Kristo amepokea uufalme na akawachukulia hatua adui za Mungu mbinguni. (Ufunuo 12:7-12) Kristo amegeuza fikira zake kuzielekeza kwenye dunia inayokaliwa na watu, akiwapo bila kuonekana. Kwa hiyo, kama Yesu alivyotabiri, karibuni sisi tutaelekeana na kuondolewa kabisa kwa adui za Mungu katika dunia yetu. Basi, je! kitabu cha Waebrania kina mashauri gani ya kutupa sisi?
‘Mfikirie Yesu’
7, 8. Kwa sababu gani ilifaa kitabu cha Waebrania kikakaza fikira juu ya Yesu hasa?
7 Paulo alielekeza fikira juu ya Yesu hasa. Aliandika hivi: “Basi, katika hayo tunayosema, neno lililo kuu ndilo hili: Tunaye kuhani mkuu wa namna hii, aliyeketi mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Ukuu mbinguni.” (Waebrania 8:1) Kwa sababu gani hilo lilikuwa shauri lenye kufaa sana hasa kwa Wakristo wenye kuishi katika umalizio wa mfumo wa mambo?
8 Kwa muda mrefu kumekuwako maoni yaliyopotoshwa kumhusu Yesu. Wayahudi wa karne ya kwanza walikuwa na kiburi cha kwamba walikuwa wazao wa Abrahamu, kwamba walifuata dini iliyopewa kupitia Musa na walikuwa na makuhani wa ukoo wa Haruni. Kwa hiyo huenda ikawa waliwaza hivi: ‘Jamaa huyu Yesu wa Nazareti ni kabwela Mgalilaya tu aliye mwana wa seremala.’ Hata walimshtakia Mwana wa Mungu kuwa ni Msamaria aliyepagawa na mashetani. (Yohana 7:52; 8:39-41, 48; 9:24, 28, 29) Kwa hiyo, kwa hekima Mungu aliwatia moyo Wakristo Waebrania ‘wamfikirie Yesu,’ kwa sababu kuwa na maoni yanayofaa, yenye usawaziko juu ya Mwana wa Mungu na kuwa na uhusiano naye kungewasaidia Wakristo hao wawe waaminifu.
9. Kwa sababu gani shauri la ‘kumfikiria Yesu’ linafaa leo, lakini tunahitaji kujihadhari na hatari gani?
9 Mashauri ya kimungu yaliyo katika Waebrania yanatusaidia sisi kwa sababu kungali na wingi wa maoni ya uongo au yaliyopotoshwa kumhusu Kristo hata sasa. Badala ya kumshushia Yesu heshima kama walivyofanya wapinzani Wayahudi, watu wengi leo wanatia chumvi kwa kukuza mno cheo chake. Makanisa yao yanashikilia sana kwamba Yesu ni sehemu ya mungu-utatu na kwamba Baba, Mwana na Roho Mtakatifu wanalingana. Hata hivyo, ni nani wanayempa heshima nyingi zaidi? Ni Yesu. Yeye anatangulizwa mbele, naye Baba anasukumiwa huko pembeni-pembeni. Jambo hilo linatokezea Wakristo wa kweli mwito wa ushindani. Kwenye Yohana 14:28 Yesu alisema kwamba Baba yake ni mkubwa zaidi, nayo Zaburi 83:18 inasema kwamba Wewe, uitwaye YEHOVA, ndiwe peke yako Uliye juu, juu ya nchi yote.” Lakini tusiyapinge kupita kiasi maoni hayo yaliyopotoshwa juu ya Yesu na bila kujua tushushe cheo kimpasacho. Kama ilivyokuwa kwa Wakristo Waebrania, kumkadiria Yesu kwa njia yenye usawaziko na usahihi kutatufaa sana sana tunapoelekeana na wakati ujao.
10. Kitabu cha Waebrania kinaonyesha Yesu ana cheo gani?
10 Kitabu cha Waebrania kinaanza kwa kukaza fikira juu ya cheo kikuu cha Kristo. Sasa yeye ni roho aliyetukuzwa, “chapa [halisi] ya nafsi yake” Mungu. Hiyo haimaanishi kwamba Baba na Mwana ni mtu mmoja wala mungu mmoja, kwa maana Waebrania 1:3 inaongezea kwamba Yesu “aliketi mkono wa kuume wa Ukuu [“wa Mungu,” Today’s English Version] huko juu.” Maandiko kama Waebrania 2:10 na 5:5, 8 pia yanaonyesha kwamba Yehova ni mkuu kuliko Mwanaye. Hata hivyo, Kristo sasa ana ‘jina [cheo au sifa] lililo tukufu kuliko lao’ malaika.—Waebrania 1:4.
11. (a) Malaika za Mungu wanamtendeaje Yesu Kristo? (b) Ni kwa njia gani Waebrania 1:6 inapasa kufahamiwa?
11 Kama vile malaika waaminifu wanavyofanya, hata sisi tunahitaji kukitambua cheo kilichotukuzwa cha Kristo. Ikitumia maneno ya Zaburi 97:7 (Tafsiri ya Septuagint ya Kigiriki), Waebrania 1:6 inasema: “Acheni malaika wote wa Mungu wamsujudie yeye.” Kama vile tafsiri nyingine zinavyofasiri andiko hilo, malaika ‘wanaanguka mbele ya,’ ‘wanainama mbele ya’ au ‘kumtolea heshima’ yule Mwana.a Habari zinazozunguka andiko hilo zinadokeza kwamba hiyo inamaanisha kwamba hata malaika wanampa Yesu heshima zao akiwa ndiye mwakilishi mkuu zaidi wa Mungu na Mwana aliyetukuzwa. Wanafahamu kwamba yeye “amevikwa taji ya utukufu na heshima” na kupewa mamlaka juu ya dunia yenye kukaliwa na watu itakayokuja.—Waebrania 2:5, 9.
12. Kwa sababu gani ni jambo la maana kwetu tutii maneno ya Yesu?
12 Hilo linapasa kuwa na matokeo gani juu yetu? Baada ya Paulo kuonyesha kwamba Yesu ni mkuu kuliko malaika, anasema hivi: “Ndiyo sababu ni lazima kwetu tuyaangalie zaidi kuliko kawaida mambo yaliyosikiwa na sisi, tusije tukapeperushwa kamwe.” (Waebrania 2;1, NW) Kama Wakristo Waebrania walivyojua, Wayahudi walielekeza fikira zao kwa muda mrefu kwenye Neno la Mungu, au Torati, iliyopewa kupitia Musa. Inahitajiwa zaidi tuelekeze fikira kwenye uongozi wa kimungu unaotolewa kupitia Yesu.
13. Wakristo wanaweza kufaidikaje kwa kumwangalia Yesu? Toa mfano.
13 Kuonyesha jambo hilo wazi, kumbuka Yesu Kristo alivyokuwa amesema juu ya kukimbia wakati Yerusalemu ungezungukwa na majeshi yenye kupiga kambi. (Luka 19:43, 44; 21:20-24) Waroma waliuzunguka Yerusalemu wenye kuasi katika mwaka wa 66 W.K. lakini kwa njia ya kifumbo wakajiondosha, na hapo Wakristo wakaukimbia mji huo. Kumtii Yesu kuliokoa maisha zao Warumi waliporudi, wakaleta msiba mwaka wa 70 W.K. Acheni tujipatie somo kutokana na jambo hili: Kwa kuwa msiba wa ulimwengu mzima upo hapa mbele tu, jiulize: ‘Je! mimi ninayafikiria kwa makini maneno ya Yesu? Kwa mfano, je! kiasi cha wakati ninachotumia katika tafrija, nia yangu kuelekea kazi au biashara yangu, au maoni yangu juu ya elimu ya kilimwengu yanaonyesha kwamba mimi nimeyatii maneno ya Yesu kwenye Luka 12:16-31?’
14. (a) Ni kwa njia gani Yesu ndiye ‘Wakili Mkuu Zaidi wa wokovu’? (b) Yesu ‘alikamilishwa’ katika maana gani?
14 Waebrania 2:10 (NW) inamwita Yesu ‘Wakili Mkuu Zaidi wa wokovu.’ Ndivyo kwanza alivyo kwa Wakristo waliotiwa mafuta ambao ni “ndugu” zake. (Waebrania 2:11-17) Lakini wote wanaotumainia uzima katika dunia-Paradiso wanamtegemea yeye pia kwa wokovu. Paulo aliandika hivi: “Ingawa ni Mwana, alijifunza kutii kwa mateso hayo yaliyompata; naye alipokwisha kukamilishwa, akawa sababu ya wokovu wa milele kwa watu wote wanaomtii; kisha ametajwa na Mungu kuwa kuhani mkuu.” (Waebrania 5:8-10) Bila shaka, Yesu alikuwa amekuwa roho mkamilifu, na alipokuwa duniani alikuwa mkamilifu kimwili. Hata hivyo, kwa sababu ya cheo chake cha kuwa kuhani wetu, Yesu alipaswa kukamilishwa katika maana nyingine. Alipokuwa duniani alipokea mazoezi—elimu, nidhamu na kujaribiwa kwa utii wake hata kwenye kifo—ili kumkamilisha awe kuhani mkuu mwenye rehema na huruma.
Kumtumaini Kuhani Mkuu Wetu
15. Kwa sababu gani tunaona mambo mengi yakiwa yamesemwa juu ya makuhani katika kitabu cha Waebrania?
15 Kwa kusoma Waebrania unaweza kuona kwamba kitabu hicho kinasema mengi juu ya makuhani. Kusudi ni kukuza ufahamu na kuthamini kwetu yule “Kuhani Mkuu wa maungamo yetu, Yesu.” (Waebrania. 3:1) Paulo anaeleza kwamba “kila kuhani mkuu aliyetwaliwa katika wanadamu amewekwa kwa ajili ya wanadamu katika mambo yamhusuyo Mungu, ili atoe matoleo na dhabihu kwa ajili ya dhambi.” (Waebrania 5:1; 8:3) Sehemu kubwa ya agano la Torati ilikazia uhakika wa kwamba wanadamu ni watenda dhambi. Ndiyo sababu dhabihu zilitolewa na makuhani kwa ajili yao, na makuhani hao walifanya matoleo ya kufunika dhambi zao wenyewe pia. Hata hivyo, dhabihu za wanyama zilizotolewa-tolewa hazikushinda dhambi nguvu wala kukamilisha wo wote wa watu hao. (Waebrania 7:11, 19, 27; 10:1-4,11) Hiyo inathibitisha kwamba agano jipya lilihitajiwa, pamoja na dhabihu mpya na kuhani mkuu mpya.—Yeremia 31:31-34.
16. Yesu akiwa kuhani anawapitaje makuhani wa Kiisraeli?
16 Mwenye kutimiza hayo ni Kristo. Akiwa ametangulia kufananishwa na Melkizedeki, ambaye ukoo wake hauonyeshwi katika Biblia, Yesu hakuwa kuhani kupitia uzao wa asili wa Lawi wala Haruni. Mungu alimweka kwenye cheo kwa njia ya moja kwa moja. (Waebrania 7:1-3, 15-17; 5:5, 6) Ikiwa kwa njia hiyo Mungu anamkubali Yesu kuwa kuhani mkuu, je! sisi hatuwezi kumtumaini huyo kabisa? Zaidi ya hilo, yeye hatakufa baada ya muda mfupi halafu ahitaji mtu wa kuchukua nafasi aliyoacha, kama ilivyokuwa ikitukia kwa makuhani chini ya ile Torati. Yeye aliweza kutoa dhabihu ya mwisho kabisa, mwili wake mwenyewe; ilikuwa kamilifu, na dhabihu hiyo haingekuwa kamwe tena na uhitaji wa kurudiwa. Kristo kuhani mkuu wetu alipeleka mbinguni ubora wa damu ya uhai wake na kuuonyesha mbele za Mungu. Yeye angali huko, akitumikia kama kuhani kwa ajili yetu.—Waebrania 9:24-28; 10:12-18.
17. Ni kwa njia gani mbalimbali sisi tunasaidika Yesu akiwa kuhani mkuu wetu?
17 Tunaweza kumtumaini kuhani mkuu wetu tunapoelekeana na msiba wa ulimwengu mzima unaokuja. Tofauti na dhabihu zilizotolewa chini ya ile Torati, dhabihu kamilifu ya Kristo inaweza kufunika kabisa dhambi zetu. Kupita hapo, inaweza ‘kusafisha dhamiri zetu ziachane na zilizokufa [shughuli mbovu tulizofuatia zamani na jitihada zo zote tulizofanya kibinafsi kutetea wenyewe haki yetu mbele za Mungu] ili tupate kumtolea utumishi mtakatifu yule Mungu aliye hai.” (Waebrania 9:14, NW; 10:1-4) Hakika tutakubali kwamba kuwa na dhamiri safi mbele za Mungu kuna ubora usiopimika wakati tunapokuwa katika hali ngumu na chini ya mkazo. (Waebrania 10:19-22) Katika njia nyingine nyingi, pia, tunaweza kufurahi kwamba Yesu ni kuhani mkuu wa kudumu katika mbingu.
18. Kwa sababu gani zamani, na hata sasa, ilikuwa vizuri kujua kwamba kuhani mkuu wetu ni mwenye kuhurumia watu?
18 Kitabu cha Waebrania kinatuhakikishia kwamba Kristo ni kuhani mwenye kuhurumia (kusikitikia). Ebu wazia maamuzi na matatizo ambayo Wakristo Waebrania walielekeana nayo katika mazingira yenye watu wenye kutukuza taifa lao huko Yerusalemu walipokuwa wakijitayarisha kukimbia, kuacha nyumba zao, watu wa ukoo wao na kazi zao za kuajiriwa. Hata hivyo hawakuwa peke yao, bila msaidizi. Paulo aliandika hivi: “Sisi tunaye kuhani mkuu, si yeye asiyeweza kusikitikia udhaifu wetu, bali yeye ambaye amejaribiwa katika mambo yote kama sisi, lakini bila dhambi.” Kuwa na mtu wa namna hiyo bila shaka kuliwafariji sana, na ndivyo kunavyopasa kuwa upande wetu pia katika siku za kumalizia za huu mfumo wa mambo! Kwa sababu ya kuwa na kuhani mkuu mwenye kuhurumia hivyo tunaweza “kupokea rehema na kuona fadhili zisizostahilika za kutusaidia wakati unaofaa.” (Waebrania 4:15, 16, NW) Hata litokee jaribu liwalo lote, yeye “aweza kuwasaidia wao wanaojaribiwa.”—Waebrania 2:17, 18.
Mkamilishaji wa Imani Yetu
19, 20. Ni kwa njia gani Yesu ndiye “Mkamilishaji wa imani yetu”?
19 Imani yetu inahusika kwa njia ya wazi ‘tunapomfikiria Yesu.’ Baada ya kuitaja “dhambi inayotutenganisha kwa wepesi,” yaani, ukosefu wa imani, Paulo anasema ‘tumkazie sana macho yule Wakili Mkuu Zaidi na Mkamilishaji wa imani yetu, Yesu.’ (Waebrania 12:1, 2, NW) Kwa sababu gani hilo ni jambo linalohitajiwa kabisa wakati wa umalizio wa mfumo wa mambo ya sasa?
20 Kuanzia unabii wayo wa kwanza katika Mwanzo 3:15, Biblia inaelekeza kwa Kristo. Yeye ndiye kielekezo kikubwa cha mambo mengi yaliyotabiriwa na ndiye Mfananishwa mkuu wa mambo yaliyotajwa katika Biblia. Nyingi za sehemu za Torati ya Musa zinazotajwa katika kitabu cha Waebrania zilikuwa “kivuli cha mema yatakayokuwa.” (Waebrania 9:23; 10:1) Lakini “uhalisi ni wa Kristo.” (Wakolosai 2:17, NW) Ndiyo, uzawa wa Yesu, huduma ya kidunia, kifo cha dhabihu chake, ufufuo na utumishi wake wa kikuhani mbinguni ndiyo mambo yanayoleta kwenye ukamilisho unabii wote, mambo yote yaliyo vifano vya mambo ya baadaye na violezo vinavyohusu mambo haya.
21. Ni katika maana gani zaidi Yesu ndiye “Mkamilishaji wa imani yetu” leo?
21 Ingawa Paulo aliweza kumtambua Kristo kuwa ndiye “Mkamilishaji wa imani yetu,” sisi tuna sababu zaidi ya kufanya hivyo leo. Sisi tunauona utimizo ulio mkubwa wa maneno ya Yesu yanayohusu ile ‘ishara ya kuwapo kwake na umalizio wa mfumo wa mambo.’ (Mathayo 24:3, NW) Kwa hiyo imani yetu ina msingi ulio imara zaidi. Wokovu wa kuingia katika “dunia yenye kukaliwa na watu itakayokuja” umekaribia zaidi pia kuliko vile ulivyokuwa siku za Paulo. Basi, acheni sisi tuendelee kumfikiria Yesu, yule Mkamilishaji wa imani yetu, tukiwa na tumaini la kuamini kwamba Mungu “huwapa thawabu wale wamtafutao [kwa bidii]” wakiwa na imani. (Waebrania 2:5; 11:6) Kama vile makala inayofuata itakavyoonyesha, kitabu cha Waebrania kinaweza kutusaidia tupate imani na maoni ya Kikristo yanayohitajiwa ili tuwe katika hali ya kuweza kuipokea ile thawabu nzuri sana.
[Maelezo ya Chini]
a Paulo alitumia neno la Kigiriki proskynéo, ambalo kamusi inayoitwa The Greek-English Lexicon of the New Testament (ya Bauer, Arndt, Gingrich) inasema “lilitumiwa kumaanisha desturi ya kujishusha chini usujudie mbele ya mtu na kupiga busu miguu yake, upindo wa vazi, ardhi.” (1 Samweli 24:8; 2 Wafalme 2:15) Linaweza pia kumaanisha “ibada,” na ndivyo Biblia nyingine zinavyosema kwenye Waebrania 1:6. Ikiwa hiyo ndiyo maana sahihi hapo, ni wazi kwamba inayomaanishwa ni ibada ya kiasi, kuabudu Yehova Mungu kwa njia ya moja kwa moja kupitia Mwanaye aliyetukuzwa,—Linganisha Ufunuo 14:7: The Watchtower la Novemba 15, 1970, kurasa 702-704.
Je! Wewe Unaweza Kueleza?
□ Hali yetu inalinganaje na ile ya Wakristo walioandikiwa kitabu cha Waebrania?
□ Kwa sababu gani tunahitaji maoni yenye usawaziko juu ya Yesu na kutii maneno yake?
□ Kwa sababu gani kitabu cha Waebrania kinasema mengi yuu ya dhabihu na makuhani?
□ Wewe una maoni gani juu ya Yesu Kuhani Mkuu na Mkamilishaji wa imani?
[Sanduku katika ukurasa wa 12]
KUSUJUDIA KWA HESHIMA au IBADA
Katika Waebrania 1:6 neno la Kigiriki proskynéo linaweza kumaanisha:
1. Kusujudia kwa njia ya heshima, kama ‘kuinama,’ kwa kumfanyia Yesu hivyo akiwa ndiye amepewa na Yehova Mungu cheo cha heshima na kutukuzwa
2. Kumwabudu Yehova Mungu kupitia au kwa njia ya mwakilishi wake aliye mkuu zaidi, Mwanaye Yesu
[Picha katika ukurasa wa 13]
Yesu alitoa dhabihu yenye ubora wa kudumu zaidi ya zile dhabihu zilizotolewa hekaluni na makuhani