Upendo Wako ni Halisi Kadiri Gani?
KUMWELEZA mtu kuwa mtu halisi au wa kweli ni kumpa sifa kubwa sana. Kwa kawaida uhalisi au ukweli wa mtu, au kitu, unaonyeshwa waziwazi na majaribu. Kwa hiyo Biblia husema juu ya dhahabu kama ikijaribiwa kwa moto, nayo inasema juu ya “dhahabu halisi,” “fedha halisi” na “nardo safi [“halisi,” NW],” marhamu ya thamani nyingi. (Yer. 52:19; Marko 14:3; 1 Pet. 1:7) Neno la Mungu vilevile husema juu ya watu wakiwa halisi, kama vile wakati ambapo mtume Paulo anapomwita Timotheo “mwanangu halisi katika imani.”—1 Tim. 1:2, HNWW.
Ulizo la kama wengine walikuwa na upendo wa kweli au halisi lilitokea kuhusiana na Wakristo Wayahudi katika Yerusalemu. Walikuwa wamepatwa na uhitaji mkubwa sana, nao waamini wenzao katika Makedonia, ‘wajapokuwa wenyewe walikuwa maskini sana,’ walikuwa wamejitaabisha sana ili watoe michango kwa ajili ya ndugu zao waliokuwa na shida. Baada ya kuwaambia Wakristo waliokuwa matajiri katika Korintho juu ya mambo hayo, mtume Paulo aliendelea kusema hivi: “Siwapi ninyi amri, lakini nataka tu kuonyesha jinsi wengine walivyo na bidii ya kusaidia ili nipate kujua jinsi mapendo yenu yalivyo ya kweli [halisi, NW].” Kwa wazi walikuwa wamedai kuwa wanawapenda waamini wenzao na sasa mtume huyo alikuwa akiwapa nafasi ya kuonyesha uhalisi wa upendo wao. Namna gani? Kwa matendo, kwa michango yao.—2 Kor. 8:8, HNWW.
Akiongozwa na Mungu, mtume Yohana, katika barua yake ya kwanza, anasema jambo ilo hilo, akisema: “Sisi tumepata kujua upendo ni nini kwani Kristo aliyatoa maisha yake kwa ajili yetu. Nasi, vile vile tunapaswa kuyatoa maisha yetu kwa ajili ya ndugu zetu. Basi, mtu akiwa na mali za hapa duniani, halafu akamwona ndugu yake ana shida, lakini akawa na moyo mgumu bila kumwonea huruma, anawezaje kusema kwamba anampenda Mungu? Watoto wangu, upendo wetu usiwe maneno matupu bali uwe upendo wa kweli na wa vitendo.”—1 Yohana 3:16-18, HNWW.
Ndiyo, upendo wa kweli, upendo halisi, unaonyeshwa si kwa maneno matupu tu, bali kwa kufanya mambo, kuwasaidia wale wanaohitaji. Muumba, Yehova Mungu mwenyewe, ndiye anayetupa mfano ulio bora zaidi juu ya jambo hili. Kwa sababu ya uasi wa wazazi wetu wa kwanza, wanadamu walipatwa na uhitaji mkubwa, na kwa sababu hiyo Mungu alimtuma Mwanawe pekee “ili kila amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” Yehova Mungu alimtuma Mwanawe ili awe na sababu ya kuwasamehe wanadamu wenye kutubu, kama vile tusomavyo: “Tukiziungama dhambi zetu, Yeye ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi zetu, na kutusafisha na udhalimu wote.”—Yohana 3:16; 1 Yohana 1:9.
Upendo huu halisi wa Yehova Mungu katika kusamehe dhambi zetu unawekwa uwe mfano wa kuigwa nasi. Neno lake linashauri hivi: “Iweni wafadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma, mkisameheana kama na Mungu katika Kristo alivyowasamehe ninyi.” (Efe. 4:32) Pengine hakuna njia nyingine ambayo katika hiyo uhalisi au ukweli wa upendo unajaribiwa au kuonyeshwa kama vile katika kuwa na nia ya kusamehe. Ni jambo rahisi kutoa zawadi za mambo ya kimwili, hata zenye bei kubwa sana, kuliko kuonyesha moyo uliokunjuka, ukarimu, kwa kusamehe.
Mtume Petro aliliona kuwa jambo gumu sana kuendelea kusamehe na kwa hiyo alimwuliza Bwana wake, Yesu, kama ilimpasa kumsamehe ndugu yake hata mara saba. Yesu alijibuje? ‘Si mpaka mara saba bali mpaka mara sabini na saba’; maana yake, hakuna kikomo cha mtu kumsamehe mwingine. (Mt. 18:21, 22, NW) Bila shaka Petro alikumbuka vizuri sana maneno haya ya Yesu kwa kuwa miaka mingi baadaye aliandika hivi: “Zaidi ya yote iweni na juhudi nyingi katika kupendana; kwa sababu upendano husitiri wingi wa dhambi.” (1 Pet. 4:8) Wingi ni hesabu kubwa, sivyo? Kwa kweli, katika Mithali 10:12 twasoma kwamba “kupendana husitiri makosa yote.”
Kati ya washiriki wa jamaa, jinsi kulivyo na nafasi nyingi kila siku za kusamehe! Wote wawili mume na mke, katika uhusiano wao wenyewe, au kama wazazi, na vilevile watoto, wanafanya makosa, mengine madogo, mengine makubwa, yakiwa na matokeo mazito. Wale wengine wa washiriki wa jamaa wapaswa kuitikiaje? Je! ni kwa kulaumu, wakionyesha maoni kama vile, ‘Kosa la upumbavu namna gani! Wawezaje kufanya jambo kama hilo?’ Au, kwa huruma, wakimhurumia yule ambaye amefanya kosa hilo na kupunguza matokeo yake au wakionyesha njia za matokeo yake? Kulikuwako na sababu nzuri ya kusema kama vile imekwisha semwa kwamba ‘ndoa yenye furaha ni mwungano wa wawili wenye kusameheana vizuri.’
Na ndivyo ilivyo katika ile jamaa kubwa ya kiroho ambayo Wakristo ni washiriki wake. Kwa kuwa hakuna aliye mkamilifu, wale wanaochukua uongozi katika kundi, au wanaochukua uongozi katika nchi fulani, huenda wakapungukiwa katika nyakati nyingine na kufanya makosa katika uamuzi. Kutokamilika kwao kunakuwa jaribu kubwa kwa wale walio chini ya uangalizi wao.
Inaweza kusemwa kwamba kama vile ‘ndoa yenye furaha ni mwungano wa wawili wenye kusameheana vizuri,’ ndivyo furaha katika kundi la Kikristo inavyotegemea nia ya ndugu na dada za kiroho ya kusameheana. Yesu alisema kwamba wafuasi wake wangejulikana kwa kupendana wao kwa wao. (Yohana 13:34, 35) Ili upendo wao uwe halisi, lazima utie ndani nia hii ya kusameheana. Kama vile “Wimbo wa Ufalme” unavyosema:
“Kweli msamaha wetu waweza Kuzuia siku za huzuni; Kwa huo twaonyesha fadhili Zatoka kweli mbinguni. . . . Msamaha wa kweli ndio wema Tupaswao tuusitawishe. Utatuepusha na hasira, Na uchungu wa hasira.”
Kwa kweli, si upendo halisi peke yake, bali hata hekima na haki ya hukumu yaweza kusemwa kwamba yatuhitaji tuwe wenye kusamehe. Tusipowasamehe wengine, Yehova Mungu hawezi kutusamehe sisi. Kuwa wenye kusamehe kunaleta furaha kwa wote wanaohusika. Je! kusamehe si namna ya kutoa inayoleta furaha zaidi? (Mt. 18:35; Matendo 20:35, NW) Haki ya hukumu vilevile yatuhitaji tuwe wenye kusamehe. Sababu gani? Kwa sababu kukosa kuwa wenye kusamehe ni kuwadhania ndugu zetu kuwa na makusudi mabaya au kuwahukumia kuwa wakosaji wasiostahili kusamehewa. Walakini, je! haki ya hukumu haitaki kwamba tuwafanyie wengine yale ambayo tungetaka watufanyie sisi? Sisi hatungetaka wengine wayahukumu vibaya au vikali makusudi yetu; badala yake, sisi tungetaka wawe wenye kusamehe. Kwa hiyo lazima si tuwe wenye kuwasamehe ndugu zetu.—Luka 6:31.
Kwa hiyo kuna kila sababu ya kuwafanya Wakristo wawe wenye kusameheana. Ndilo jambo la hekima na ndilo jambo la haki la kufanya. Na zaidi ya yote, ndilo jambo lisilo la choyo, jambo la upendo la kufanywa, lenyewe likiwa uthibitisho wa upendo wetu halisi.
[Picha katika ukurasa wa 3]
Ndoa yenye furaha ni mwungano wa wawili wenye kusameheana vizuri