Yesu Alizaliwa Wakati Gani?
”SHEREHE yenye kujulikana sana wakati jua lilipokuwa kule-e-e kusini katika nyakati za kale ilikuwa ile ya Warumi,” kulingana na mwandikaji wa sayansi Isaac Asimov. Ilikuwa sikukuu ya Saturnalia iliyochukua muda wa juma moja (Desemba 17 mpaka 24), iliyosherehekewa kwa heshima ya mungu wao wa ukulima, Saturn. Dakt. Asimov anatoa maelezo haya:
‘Waabudu wa [mungu] Mithra walisherehekea kuzaliwa kwa Mithra wakati wa majira ya baridi wakati jua lilipokuwa upande wa kusini, wakati wa asili, na uliowekwa katika siku ya Desemba 25 ili kwamba [sikukuu ya] Saturnalia yenye kupendwa na watu wengi iendelee kufikia ‘Siku ya Jua’ ya waabudu wa Mithra kama upeo. . . . Muda fulani baada ya A.D. 300, Ukristo ulifanya mapinduzi ya mwisho kwa kufanya [sikukuu ya] Saturnalia kuwa sehemu yake, na kwa jambo hilo ukapata ushindi wa mwisho juu ya ibada ya Mithra. Desemba 25 ikawekwa kuwa siku ya kuzaliwa kwa Yesu, nayo sikukuu hiyo kubwa ikafanywa kuwa ya Kikristo. Hakuna mamlaka ya kibiblia hata kidogo kuwa Desemba 25 ndiyo Siku ya Kuzaliwa [ya Yesu].’
Hakika, hayo ni maelezo yenye kuvutia. Walakini yanafanya sherehe za kila mwaka za Krismas zisipendeze sana na kutokeza maulizo fulani pia. Je! inawezekana kujua mwaka wa kuzaliwa kwa Yesu Kristo? Je! ni tarehe inayoelekea kuwa inaweza kujulikana? Kweli kweli, Yesu alizaliwa wakati gani?
KUUONYESHA MWAKA WENYEWE
Njia moja ya kuujua mwaka wa kuzaliwa kwa Yesu ni kufikiria unabii ulioongozwa na Mungu wa “majuma sabini,” au “majuma sabini ya miaka,” ulioandikwa katika Danieli 9:24-27. Malaika Gabrieli alimwambia hivi nabii Mwebrania Danieli: “Tangu kuwekwa amri ya kutengeneza na kuujenga upya Yerusalemu hata zamani zile masihi aliye mkuu; kutakuwa na majuma saba; na [pia] majuma sitini na mawili [ya miaka, au miaka 483].”—Dan. 9:25; Hes. 14:34; Eze. 4:6.
Hiyo miaka 483 ilianza wakati gani? Katika vuli ya mwaka 455 K.W.K., wakati wa mwaka wa 20 wa Mfalme Artashasta, wakati mfalme huyo Mwajemi alipotoa amri kwamba Yerusalemu na kuta zake ujengwe upya. (Neh. 2:1-8) Hivyo, kipindi hicho cha “majuma” 69 (miaka 483) kilimalizika katika vuli ya mwaka 29 W.K. Wakati huo ndipo Masihi alipotokea, kwa kuwa katika mwaka huo Yesu alibatizwa na Yohana Mbatizaji naye akawa Mtiwa Mafuta au Kristo kwa kutiwa mafuta kwa roho takatifu ya Mungu. (Mt. 3:13-17) Na Luka 3:1-3 laonyesha kwamba Yohana alianza utendaji wake wa kubatiza katika “mwaka wa kumi na tano wa kutawala kwake Kaisari Tiberio,” mwaka ulioanza Agosti 17, 28 W.K., mpaka Agosti 16, 29 W.K.
Yesu alikuwa mwenye umri gani wakati wa kubatizwa? Maandiko yanajibu hivi: “Na Yesu mwenyewe, alipoanza kufundisha [mara tu alipobatizwa], alikuwa amepata umri wake kama miaka thelathini.” (Luka 3:21-23) Tukihesabu kurudi nyuma kutoka kubatizwa kwa Yesu katika mwaka 29 W.K. (na kukumbuka kwamba hakuna mwaka sufuri kati ya vipindi K.W.K. na W.K. vya kuhesabia), twapata kwamba alizaliwa katika mwaka 2 K.W.K.
Unabii wa “majuma sabini ya miaka” unaunga mkono jambo hilo. Unaonyesha kwamba Masihi angeuawa, hivyo ‘kufanya dhabihu na sadaka zikome’ kuwa zisizotakiwa tena, katikati ya “juma” la 70. Hiyo inamaanisha kwamba huduma ya Kristo ilikuwa na urefu wa miaka mitatu na nusu. Ilianza wakati wa kubatizwa kwake katika mwaka 29 W.K. na ikamalizika wakati wa kifo chake wakati wa Sikukuu ya Kupitwa katika mwaka 33 W.K. (Luka 22:7-20) Vilevile kuhesabu kurudi nyuma miaka 33| (muda wa maisha ya Yesu ya kidunia) kunatuwezesha kupiga hesabu kuwa mwaka wa kuzaliwa kwake ulikuwa 2 K.W.K.
NAMNA GANI SIKU YENYEWE?
Kama ambavyo imeonyeshwa sasa hivi, Yesu alikufa wakati wa Sikukuu ya Kupitwa, ambayo ilikuwa kama Aprili 1, 33 W.K. (Mt. 26:17-30) Kwa kuwa Kristo alikuwa na umri wa kama miaka 30 alipoanza kazi yake nayo huduma yake ilikuwa ya miaka mitatu na nusu, yeye alikuwa na miaka 33 1/2 wakati wa Sikukuu ya Kupitwa hivi, au yapata Aprili 1, 33 W.K. Kristo angekuwa na miaka 34 miezi sita baadaye, au yapata Oktoba 1. Kwa kuhesabu kurudi nyuma tena, twalazimika kukata kauli kwamba Yesu alizaliwa, si Desemba 25, bali yapata Oktoba 1, katika mwaka 2 K.W.K.
HAKUZALIWA WAKATI WA MAJIRA YA BARIDI
Hali zilizokuwa wakati wa kuzaliwa kwa Yesu miaka 30 baadaye katika Bethlehemu zisingeweza kufaa wakati wa majira ya baridi. Majira ya baridi yenye mvua ya Palestina huanza mwishoni mwa Oktoba na kuendelea kwa miezi kadha Kufikia Desemba Bethlehemu, kama vile Yerusalemu ulio jirani, unakuwa na theluji mara kwa mara wakati wa usiku. Nao ungeweza kuwa na baridi kadiri gani? Kuhusu Mfalme Yehoyakimu wa Yudea twasoma hivi: “Mfalme alikuwa ameketi katika nyumba iliyotumika wakati wa baridi, mwezi wa kenda [Kislewi, unaolingana na Novemba-Desemba] na pale palikuwa na moto wa makaa mbele yake.” (Yer. 36:22) Alihitaji joto hilo ili asipatwe na baridi. Zaidi ya hayo, katika Yerusalemu wa baada ya uhamisho, watu ambao Ezra alikusanya nje wakati wa mwezi uo huo wa majira ya baridi walikuwa “wakitetemeka kwa sababu ya neno hilo [lililokuwa likizungumzwa] na kwa sababu ya mvua kubwa.” (Ezra 10:7, 9, 13) Inafaa kuangalia kwamba mwezi uliofuata, Tebethi (Desemba-Januari), ndio wakati kulikuwa baridi nyingi zaidi mwakani, kukiwa na theluji mara kwa mara juu ya vilima.
Kaisari Augusto aliamuru kuandikishwa kufanywe ambako, kama ilivyokuwa, kulikuwa wakati ule ule wa kuzaliwa kwa Yesu. Walakini je! unafikiri kwamba mfalme huyo Mrumi angeweza kukasirisha bila lazima ya kufanya hivyo raia zake Wayahudi ambao walikuwa wakiasi wakati mwingi kwa kuamuru waende wakajiandikishe katika miji ya nyumbani kwao wakati wa mwezi wa Desemba wa majira ya baridi wenye mvua na baridi, wakati ambapo kusafiri kungekuwa ni tatizo sana? Sivyo kabisa.
Wachungaji walikuwa wakichunga mifugo yao “makondeni” wakati wa usiku ule aliozaliwa Yesu. (Luka 2:8-14) Walakini tayari katika mwezi wa vuli wa Buli (Oktoba-Novemba) majira ya mvua yalikuwa yamekwisha anza. (Kum. 11:14) Kufikia sehemu ya mwisho ya Oktoba, wakati Buli ulipoanza, wanyama wangekuwa wamekwisha rudishwa vibandani wakati wa usiku. Kwa hiyo kuwapo kwa wachungaji katika makonde wakati usiku kunapatana na ushuhuda mwingineo kuonyesha kwamba Yesu alizaliwa katika mwezi wa Ethanimu mapema katika vuli (Septemba-Oktoba).
KUSHEREHEKEA KUNAKOTAKIWA
Hivyo, ni wazi kwamba Yesu hakuzaliwa katika Desemba 25. Mahali pake, ushuhuda uliopo unaonyesha yapata Oktoba 1 wa mwaka 2 K.W.K. Kwa hiyo, kusherehekea siku yake ya kuzaliwa kwa kuadhimisha Krismas siku ya Desemba 25 hakufai kabisa kwa wale wanaoongozwa na Maandiko Matakatifu.
Hata hivyo kukosa kutajwa kwa siku yenyewe hasa ya kuzaliwa kwa Yesu hakutuhangaishi. Kwani sherehe za siku ya kuzaliwa zilizoandikwa katika Biblia ni zile za watawala wa kilimwengu.—Mwa. 40:20; Mt. 14:6; Marko 6:21-28; Yohana 18:36.
Hata hivyo, Yesu anapaswa kukumbukwa. Kwa sababu hiyo, alianzisha Ukumbusho wa kifo chake, jambo ambalo wakati mwingi linaitwa Chakula cha Bwana cha Jioni. Kristo alifanya hivyo wakati wa usiku wa mwisho wa maisha yake ya kidunia, muda mfupi kabla hajatoa “nafsi yake iwe fidia ya wengi.” (Mt. 20:28) Kwa kutumia mifano ya mwili na damu ambayo angetoa karibuni, Yesu aliwaamuru wafuasi wake waaminifu wale, na akawahimiza hivi: “Fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu.” (Luka 22:19, 20; 1 Kor. 11:23-26) Kwa hiyo, ingawa Wakristo wa kweli wanapendezwa kadiri fulani na kujua wakati Yesu alipozaliwa, ni kifo cha Yesu Kristo wanachopaswa kukumbuka kila mwaka, wala si kuzaliwa kwake.