Kunena Neno la Yehova Kwa Ujasiri
“Basi sasa, [Yehova], . . . ukawajalie watumwa wako kunena neno lako kwa ujasiri wote.”—Matendo 4:29.
1, 2. (a) Baada ya kufufuliwa, Kristo alikuwa na kupendezwa gani katika wanafunzi wake, na kwa hiyo ni maagizo gani waliyopewa? (b) Kutoa ushuhuda kulipaswa kuenee kadiri gani?
IJAPOKUWA kifo kilikuwa kimetenganisha Yesu na wanafunzi wake, wao hawakusahau mwaliko wake wa kuwa “wavuvi wa watu.” Wao walifahamu hilo lilimaanisha kunena neno la Mungu kati ya watu. Walakini wangeanzaje? Walihitaji uongozi.
2 Kwa furaha kuu ya wanafunzi hao, Yesu aliyefufuliwa aliwatokea katika pindi kadha kabla ya kupaa kwa Babaye. (1 Kor. 15:3-8; Yohana 20:20) Hivyo aliweza kuwapa maagizo zaidi kuhusiana na kazi yao ya wakati ujao. Katika Galilaya, yeye alisema hivi:
“Mamlaka yote imepewa kwangu mimi mbinguni na duniani. Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi. Na, tazama! mimi nipo pamoja na ninyi siku zote mpaka mwisho wa taratibu ya mambo.” (Mt. 28:18-20, NW)
Kazi ya Kikristo ya kufanya wanafunzi, kuwabatiza na kuwafundisha, lazima ifikie watu wa mataifa yote. Lilikuwa jambo la kutia moyo kama nini kufahamu kwamba huyo Mwana wa Mungu aliyefufuliwa angekuwa pamoja na Wakristo katika kazi yao ya Ufalme kila siku mpaka kumalizika kwa taratibu hii ya mambo!
3. Roho takatifu imekuwa na sehemu gani katika jambo hilo kuanzia Pentekoste?
3 Yesu alikuwa amewaahidi wanafunzi wake kwamba msaidizi, roho takatifu, ingekuja. (Yohana 14:16, 26) Hiyo ingekuwa nini, nayo ingetendaje kazi? Muda mfupi tu kabla ya kupaa kwa Babaye, Yesu aliwaambia wanafunzi hao hivi:
“Ninyi mtapokea nguvu wakati roho takatifu itakapofika juu yenu ninyi, na ninyi mtakuwa mashahidi wangu mimi katika Yerusalemu na katika Uyahudi wote na katika Samaria na kwenye sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.” (Matendo 1:8, NW)
Lo! taraja kubwa namna gani la ushuhuda uliopanuliwa. Wanafunzi hao walirudi Yerusalemu, nako huko walikuwa wakidumu katika sala. Siku ya 50 tangu kufufuliwa kwa Yesu ilikuwa Pentekoste, nao wanafunzi hao walikuwa wamekusanyika wote mahali pamoja. Ghafula kulikuwa na sauti “kama uvumi wa upepo wa nguvu ukienda kasi,” pamoja na vionyesho vingine vya kimwujiza. Yehova alikuwa akimwaga juu yao roho takatifu iliyoahidiwa, nguvu yake ya utendaji. Nayo roho hiyo iliwachochea kufanya nini? Iliwafanya ‘waseme . . . watamke.’—Matendo 2:1-4.
4. ‘Habari Njema” zilipokewaje wakati huo?
4 Wakati ulikuwa umefika wa kufanya kazi ya ‘kuvua watu’ kwa wingi sana. Kwa msaada wa roho takatifu, wanafunzi hao wangeweza kulizungumza neno la Mungu kwa lugha nyingi. Kwa njia hiyo, katika lugha yao ya kienyeji, watu wenye kuhudhuria sikukuu ya Pentekoste kutoka sehemu nyingi za ulimwengu waliwezeshwa kusikia juu ya “matendo makuu ya Mungu.” Watazamaji walistaajabu. Kisha Petro akasimama na kuzungumza kwa ujasiri katika kuwaelezea. Yeye alitoa ushuhuda kamili kuhusiana na ufufuo wa Yesu Kristo, akiwasihi wale waliokuwapo watubu na kuokolewa na kizazi hicho kipotovu. Matokeo yalikuwa nini? Watu wapatao 3,000 walilikubali neno hilo! Hao walibatizwa na kuongezwa katika kundi la Kikristo. Kulikuwa na furaha nyingi, kwa kadiri ‘Yehova alivyozidisha kundi kila siku kwa wale waliokuwa wakiokolewa.’—Matendo 2:5-47.
5. (a) Ni kwa kusudi gani Wakristo huja mbele ya watawala katika nyakati za upinzani? (b) Tuna kitia-moyo gani katika jambo hilo?
5 Kutoa huko kwa ushuhuda kwa uwezo wa roho takatifu kulikuwa kumetokeza wasifaji wengi wapya wa Yehova. Kisha, hao nao, walifurahia kwenda nje kila siku, na kutoa kwao kwa ushuhuda waziwazi kuliujaza Yerusalemu “habari njema.” Petro na Yohana waliongoza katika kazi hiyo, wakiwasihi watu wageuke wapate kusamehewa dhambi zao, ili wapokee burudisho la kiroho kutoka kwa Yehova. Wengi wa hawa walisikiliza “habari njema” hizo kwa furaha—lakini sivyo kuhani mkuu, akida wa hekalu na Masadukayo. Waliwakamata Petro na Yohana, na kuwatia kizuizini. Hivyo wanafunzi hao walianza kuona chuki ambayo Yesu alikuwa amewaonya kimbele juu yake, aliposema hivi:
“Angalieni, mimi nawatuma kama kondoo kati ya mbwa-mwitu; basi iweni na busara kama nyoka, na kuwa watu wapole kama hua. Jihadharini na wanadamu; kwa maana watawapeleka mabarazani, na katika masinagogi yao watawapiga; nanyi mtachukuliwa mbele ya maliwali na wafalme kwa ajili yangu, kuwa ushuhuda kwao na kwa mataifa. Lakini hapo watakapowapeleka, msifikiri-fikiri jinsi mtakavyosema; maana mtapewa saa ile mtakayosema. Kwa kuwa si ninyi msemao, bali ni [roho ya] Baba yenu [isemayo] ndani yenu.” (Mt. 10:16-20)
Hata hivyo, kufikia sasa hao “wavuvi wa watu” wangeweza kufurahia uvuaji mkubwa wa waamini wapya wapatao 5,000. Lo! namna ambavyo walimshukuru Yehova kwa ajili ya ongezeko hilo! Sisi, pia, twatiwa moyo na ripoti yao ya utumishi.—Matendo 4:1-4.
KUNENA MBELE YA WATAWALA
6. (a) Petro na Yohana walifanya nini walipoletwa mbele ya watawala? (b) Sababu gani walifaa sana kufanya jambo hilo?
6 Siku iliyofuata kulikuwako kusanyiko la watawala, nao waliwahoji Petro na Yohana juu ya utendaji wao, kutia ndani kuponya kwao mtu yule aliyelemaa. Hiyo ilikuwa nafasi nzuri ya kutoa ushuhuda zaidi wa waziwazi. Kama vile ambavyo Yesu alikuwa ameonyesha ingetokea, roho takatifu ilimpa Petro uwezo wa kusema hivi:
“Enyi wakubwa wa watu na wazee wa Israeli, kama tukiulizwa leo habari ya jambo jema alilofanyiwa yule mtu dhaifu, jinsi alivyoponywa, jueni ninyi nyote na watu wote wa Israeli ya kuwa kwa jina la Yesu Kristo wa Nazereti, ambaye ninyi [mlimtundika], na Mungu akamfufua katika wafu, kwa jina hilo mtu huyu anasimama ali mzima mbele yenu. Yeye ndiye jiwe lile lililodharauliwa na ninyi waashi, nalo limewekwa kuwa jiwe kuu la pembeni. Wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokokolewa kwalo.” (Matendo 4:8-12)
Kweli hizi za lazima zilipaswa kutangazwa! Kwa hiyo mitume hao walisema mambo kama yalivyokuwa. Hawakuficha. Petro na Yohana walikuwa wavuvi tu, walakini walikuwa wamezoezwa na Yesu kunena kwa njia yenye nguvu, kwa uhakika na kusadikishwa. Wakiwa mashahidi wa Yehova, walinena kwa kuwa walitaka wawe wakitangaza neno la Mungu.—Linganisha Yohana 7:15-18, 45, 46.
7. Twajifunza nini kutokana na masimulizi katika Matendo 4 juu ya kuwaza na makusudi ya wapinzani?
7 Lo! namna tunavyopaswa kumshukuru Yehova kwa ajili ya maandishi katika Matendo sura ya 4! Kwa kuwa si kwamba tu yanaonyesha waziwazi namna Wakristo wa kweli wanavyopaswa kunena kwa ujasiri, bali pia yanafunua kuwaza kulikopotoka kwa watawala wa kilimwengu wanaopinga kazi ya Mungu. Baada ya mitume hao kutoa ushuhuda huo wa kijasiri, watawala hao waliwapeleka nje ya jumba la Sanhedrin (mahakma kuu ya Kiyahudi) walipokuwa wakishauriana. Kusudi lao lilikuwa nini? Hawangeweza kukana kwamba ishara yenye kutokeza ilikuwa imetokea kwa jina la Yesu Kristo. Walakini kuwaza kwao kulikuwa kukomesha kuenea kwa ibada ya kweli. Waliwaza kwamba kwa vitisho wangeweza kuwaogopesha mitume hao na hivyo wakomeshe kunena kwao katika jina la Yesu.—Matendo 4:16, 17.
8. Ni jambo gani linaloonyesha kwamba wanafunzi hawakuwa na woga?
8 Walakini, je! vitisho peke yake vingeweza kuwakomesha mashahidi Wakristo hao wa Yehova? Acha Wakristo wa kweli wa leo wauangalie mfano wao usio wa woga:
”[Watawala] wakawaita, wakawaamuru wasiseme kabisa wala kufundisha kwa jina la Yesu. Petro na Yohana wakawajibu wakawaambia, Kwamba ni haki mbele za Mungu kuwasikiliza ninyi kuliko Mungu, hukumuni ninyi wenyewe; maana sisi hatuwezi kuacha kuyanena mambo tuliyoyaona na kuyasikia.” (Matendo 4:18-20)
Kwa kuogopa maoni ya watu, watawala hao waliwafungua mitume hao, baada ya kuwatisha. Kwa msaada wa roho ya Mungu, Wakristo hao walikuwa wameshinda mateso.
MSAADA WENYE KUENDELEA KUTOKA KWA YEHOVA
9, 10. (a) Watumishi wa Yehova walifuata mpango gani, nayo ni tamaa gani iliyokuwa mioyoni mwao? (b) Waliomba nini, nao walijibiwaje?
9 Baada ya kufunguliwa kwao, mitume hao walirudi kundini. Waliripoti kwa ndugu mambo yaliyokuwa yametokea, na kisha kundi hilo likafanya jambo ambalo Wakristo wanapaswa kufanya wakati wote chini ya hali kama hizo. Walizungumza na Yehova katika sala. Sala yao ilikuwa yenye imani, yenye kuonyesha tamaa yao nyingi ya kuendelea kumtumikia Mungu. Wao walisema hivi:
“[Bwana Mwenye Enzi Kuu], ndiwe uliyefanya mbingu na nchi na bahari na vitu vyote vilivyomo; nawe ulinena kwa [roho takatifu] kwa kinywa cha babaetu Daudi, mtumishi wako, Mbona mataifa wamefanya ghasia, na makabila wametafakari ubatili? Wafalme wa dunia wamejipanga, na wakuu wamefanya shauri pamoja juu ya [Yehova] na juu ya Kristo wake. Maana ni kweli, Herode na Pontio Pilato pamoja na Mataifa na watu wa Israeli, walikusanyika katika mji huu juu ya Mtumishi wako mtakatifu Yesu, uliyemtia mafuta, ili wafanye yote ambayo mkono wako na mashauri yako yamekusudia tangu zamani yatokee. Basi, sasa, [Yehova], yaangalie matisho yao; ukawajalie watumwa wako kunena neno lako kwa ujasiri wote, ukinyosha mkono wako kuponya; ishara na maajabu vifanyike kwa jina la Mtumishi wako mtakatifu Yesu.”—Matendo 4:24-30.
10 Wanafunzi hao hawakuomba kwamba waachishwe kazi au kuondolewa vitisho vya adui za kweli. Walifahamu mgawo wao kutoka kwa Yehova—kuwa mashahidi wake. Tamaa ya moyo wao ilikuwa kuendelea kunena neno la Mungu kwa ujasiri wote, nao waliomba msaada wake katika jambo hilo. Wasingejiachilia washindwe na woga kamwe. Je! Yehova alipendezwa na nia hiyo? Maandishi yanatuambia hivi:
‘‘Hata walipokwisha kumwomba Mungu, mahali pale walipokusanyika pakatikiswa, wote wakajaa [roho takatifu], wakanena neno la Mungu kwa ujasiri.”—Matendo 4:31.
11. (a) Ni jambo gani lililotokea kutokana na kusema kwao kwa ujasiri? (b) Sababu gani kuwekwa kifungoni hakukuwafanya waiache kazi hiyo?
11 Mashahidi hao wa Ufalme waliendeleza kazi yao kwa nguvu zilizofanywa upya, naye Yehova alikuwa pamoja nao. “Walioamini wakaendelea kuongezeka kwa Bwana, wengi, wanaume na wanawake.” (Matendo 5:14) Kama matokeo, viongozi wa kidini walikasirika tena na kuwaweka mitume hao kifungoni. Hata hivyo, yalikuwa mapenzi ya Yehova kwamba waendelee kutoa ushuhuda katika Yerusalemu. Kwa hiyo alimtuma malaika awafungulie mitume hao, na kuwaambia hivi:
‘‘Enendeni mkasimame hekaluni mkawaambie watu maneno yote ya Uzima huu.” (Matendo 5:20)
Kuwekwa kifungoni hakukuwaogopesha mitume hao wanyamaze kama vile visivyowaogopesha hata kidogo vitisho vya makuhani na watawala.
12. Mitume walipataje kutoa ushuhuda mbele ya mahakma hiyo baadaye, na je! waliogopeshwa?
12 Walakini, mitume walikamatwa tena na askari na kuletwa mbele ya jumba la Sanhedrin wapate kuelekeana na kuhani mkuu mwenye ghadhabu, ambaye alisema hivi:
“Je! hatukuwaamuru ninyi kwa nguvu, msifundishe kwa jina hili? nanyi, tazameni, mmeijaza Yerusalemu mafundisho yenu, na mnataka kuileta damu ya mtu yule juu yetu.” (Matendo 5:28)
Katika mahakma hiyo yenye uadui, wakiwa wanalindwa na askari wa serikali naye kuhani mkuu akinena kwa nguvu sana juu yao, je! mitume hao walishindwa? Hasha.
“Petro na mitume wakajibu, wakisema, Imetupasa kumtii Mungu [kama mtawala] kuliko wanadamu. Mungu wa baba zetu alimfufua Yesu, ambaye ninyi mlimwua mkimtundika katika mti. Mtu huyo Mungu amemtukuza kwa mkono wake wa kuume, awe [Wakili] Mkuu na Mwokozi, awape Israeli toba na msamaha wa dhambi. Na sisi tu mashahidi wa mambo haya, pamoja na [roho takatifu ambayo] Mungu amewapa wote wamtiio [kama mtawala].”—Matendo 5:29-32.
13. Shauri la Gamalieli lilikuwa nini, nayo mahakma hiyo ililionaje?
13 Hapo, tena, twapaswa kushukuru maandishi ya Maandiko yanayoonyesha kuwaza kulikopotoka kwa wale wanaopinga kazi ya Mungu. Ijapokuwa mitume walikuwa wanaume wema, mahakma hiyo ilikuwa ikifikiria kuwaua. Walakini, mwalimu wa sheria mwenye kuheshimiwa Gamalieli alisimama na kuwashauri watawala hao wa kidini kwa wakati unaofaa. Yeye alisema hivi:
‘‘Enyi waume wa Israeli, jihadharini jinsi mtakavyowatenda watu hawa. Kwa sababu kabla ya siku hizi aliondoka Theuda, akijidai ya kuwa yeye ni mtu mkuu, watu wapata mia nne wakashikamana naye; naye aliuawa na wote waliomsadiki wakatawanyika wakawa si kitu. Baada ya mtu huyo aliondoka Yuda Mgalilaya, siku zile za kuandikwa orodha, akawavuta watu kadha wa kadha nyuma yake, naye pia akapotea na wote waliomsadiki wakatawanyika. Basi sasa nawaambia, Jiepusheni na watu hawa, waacheni; kwa kuwa shauri hili au kazi hii ikiwa imetoka kwa binadamu, itavunjwa, lakini ikiwa imetoka kwa Mungu hamwezi kuivunja, msije mkaonekana kuwa mnapigana na Mungu.” (Matendo 5:34-39)
Sehemu ya shauri hilo la hekima la Gamalieli ilikubaliwa. Ijapokuwa watawala wa kidini hawakuacha kupigana na Mungu, hawakuwaua. Mahali pake, waliwapiga vikali, na kuwaamuru waache kunena juu ya Yesu, nao wakawaacha waende zao.—Matendo 5:40.
UJASIRI CHINI YA MAJARIBU
14. Nao Wakristo wakati huo walitendaje kwa ujasiri, kukawa na matokeo gani?
14 Je! mambo hayo yote yaliwavunja moyo mitume wasinene neno la Mungu kwa ujasiri? Masimulizi yanajibu hivi:
“Nao wakatoka katika ile baraza, wakifurahi kwa sababu wamehesabiwa kuwa wamestahili kuaibishwa kwa ajili ya Jina hilo. Na kila siku, ndani ya hekalu na nyumbani mwao, hawakuacha kufundisha na kuhubiri habari njema za Yesu kwamba ni Kristo.” (Matendo 5:41, 42)
Kwa ujasiri mitume na Wakristo wengine waliendelea kujishughulisha na neno la Mungu na kunena kwa ujasiri, naye Yehova akabariki kazi yao.
“Neno la Mungu likaenea; na hesabu ya wanafunzi ikazidi sana katika Yerusalemu; jamii kubwa ya makuhani wakaitii ile Imani.”—Matendo 6:7.
15. Ni baadhi ya mambo gani ambayo Stefano aliyasema kwa ujasiri, nao wanadini waliitikia kwa njia gani?
15 Sasa kwa kuwa makuhani, pia, walikuwa wakigeuka na kuwa Wakristo, upinzani wa viongozi wa kidini wenye shingo ngumu haukukoma. Muda si muda, shahidi mwenye juhudi Stefano alijikuta mbele ya Sanhedrin. Yeye alitoa ushuhuda wenye nguvu nyingi, ambao katika huo alisimulia kifupi kutimizwa kwa makusudi ya Yehova. Lakini wapinzani hao walimrukia kwa hasira na kumpiga kwa mawe mpaka kufa. Ikawa kwa Stefano kama vile Yesu alivyokuwa ametabiri: “Saa yaja atakapodhania kila mtu awauaye ya kuwa anamtolea Mungu ibada.”—Yohana 16:2; Matendo 6:8–7:60.
16. (a) Kisha ni jambo gani lililolipata kundi la Kikristo? (b) Walikuwa na maoni gani kuelekea mali zao?
16 Kufia imani kwa Stefano kulikuwa dalili ya wimbi la mateso makali.
“Siku hiyo [kundi] la Yerusalemu lilianza kuteswa vibaya. Waamini wote, isipokuwa tu wale mitume walilazimika kutawanyika katika sehemu za mashambani za Yudea na Samaria.” (Matendo 8:1, HNWW)
Walakini je! jambo hilo lingewanyamazisha mashahidi wa Yehova wa wakati huo? Hakika, hapo, palikuwa jaribio jingine la Kishetani la kuvunja utendaji wa watumishi wa Mungu. Walilazimika kuacha nyumba na mali zao. Hata hivyo, walikuwa na maoni yanayofaa juu ya mali. Katika jambo hilo, walikuwa kama Wakristo wale ambao mtume Paulo aliandikia baadaye hivi: “Maana mliwaonea huruma wale waliokuwa katika vifungo, tena mkakubali kwa furaha kunyang’anywa mali zenu, mkijua kwamba nafsini mwenu mna mali iliyo njema zaidi, idumuyo.”—Ebu. 10:34.
17, 18. (a) Tendo la Filipo na Wakristo wengine waliotawanyika linatuonyeshaje namna ya kushinda njia za Shetani? (b) Ni baraka gani zinazotoka kwa Yehova?
17 Wanafunzi hao walithamini kabisa kabisa kwamba walipaswa kuendelea kuwa mashahidi waaminifu wa Mungu na wa Kristo. Hivyo, “wale waamini waliotawanyika, walikwenda kila mahali wakihubiri ule ujumbe [wa habari njema].” (Matendo 8:4, HNWW) Filipo akaenda katika mji wa Samaria, ambapo aliendelea kuuzungumza ujumbe huo kwa ujasiri, akiletea watu furaha nyingi. Muda si muda, akawa na waamini wengine wakishirikiana naye, nao ujumbe ukatumwa Yerusalemu ukiwaarifu mitume kwamba Samaria ulikuwa umelikubali neno la Mungu. Petro na Yohana wakaenda huko, roho takatifu ikawashukia Wasamaria hao, nalo kundi la Kikristo likasimamishwa huko.—Matendo 8:5-8, 14-17, 25;9:31.
18 Wakristo hao wa karne ya kwanza walikuwa na maoni yanayofaa. Waliomba kwamba Yehova awaendeleze kulizungumza neno la Mungu kwa ujasiri. Hivyo ndivyo walivyofanya, kwa msaada wa roho takatifu yake, naye akawabariki. Kama vile maandishi yasemavyo, ‘mkono wa [Yehova] ulikuwa pamoja nao.’!—Matendo 11:19-21.
KUSEMA KWA UJASIRI SASA
19. Ni ushuhuda gani tulio nao kwamba Yehova Mungu na Kristo wamekuwa na mashahidi Wakristo katika nyakati za kisasa?
19 Kwa karne zote, Yesu ametimiza ahadi yake: “Mimi nipo pamoja na ninyi siku zote mpaka mwisho wa taratibu ya mambo.” (Mt. 28:20, NW) Kwa kuwa sasa tumefika katika wakati huo, tunashukuru kama nini kwamba zaidi ya mashahidi 2,000,000 ‘wanalisema neno la Yehova kwa ujasiri’! Naye Mungu wetu amebariki sana kazi ya hawa “wavuvi wa watu,” hata kwamba “habari njema hizi za ufalme” zimepata kufahamika katika bara zote zilizo juu ya uso wa dunia, hata kufikia mbali huko Antarktika (upande wa kusini sana.) Zimepenya katika sehemu zilizo peke yake za milimani na kwenye visiwa vidogo vilivyotapakaa katika zile bahari saba. (Mt. 24:14, NW) Ndiyo, kazi ya kutoa ushuhuda imefika katika kila taifa “kwenye sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia,” na yote hayo yamefanywa kwa roho ya Yehova.—Matendo 1:8, NW, Zek. 4:6.
20. Ibilisi ameonyeshaje upinzani wake kwa wenye kulichukua Neno la Mungu, na je! mawakili wake wanaweza kuikomesha kazi hiyo?
20 Kama vile Neno la Mungu lilivyotabiri, Ibilisi ameghadhibika, kwa kuwa anafahamu kwamba wakati wake ni mchache. Yeye anaendelea kuipinga kazi ya kutoa ushuhuda. (Ufu. 12:12, 17) Ibilisi na mabaradhuli (watumishi) wake wanawachukia Mashahidi wa Yehova kwa sababu Wakristo hawa ‘si sehemu ya ulimwengu.’ Wengi wao wametawanywa na mateso kutoka nyumbani mwao. Mamia wamepata kifo cha jeuri, kama vile Stefano katika karne ya kwanza ya wakati wetu. (Ufu. 17:6, NW; 20:4) Walakini kazi hiyo imejithibitisha kuwa ya Mungu. Wanadamu hawajaweza kuipindua, wakati watumwa wa kweli wa Mungu wanapoendelea kulinena neno lake kwa ujasiri. Katika njia hiyo wameshinda, ndiyo, wameziweza hila za Ibilisi.—Linganisha Waefeso 6:11, 12; Yakobo 4:7; 1 Petro 5:8, 9.
21. (a) Ni kazi gani ambayo Yehova anataka ifanywe sasa? (b) Sababu gani twataka kuimaliza kazi tuliyopewa, na twawezaje kuendelea kulinena neno hilo kwa ujasiri?
21 Leo, kazi ya ‘kuvua’ ya Ufalme inaendelea kusonga mbele, ujapokuwapo upinzani. Nayo baraka ya Yehova inaendelea kuonyeshwa juu yake. Katika mwaka wa utumishi uliopita peke yake, Mashahidi wa Yehova wamefurahia kuona watu wapya 113,672 wakibatizwa. Hawa wana furaha kama nini kulinena neno la Yehova! Hiyo ndiyo kazi Mungu aliyotupa leo, nayo yapaswa kuwa mioyoni mwa wale waliojiweka wakf kwa Yehova kuwa wenye kutenda sana katika hiyo, kwa kuwa ndio mgawo wao. (1 Kor. 9:16) Je! moyo wako unakuchochea kulisema neno la Yehova kwa ujasiri? Kadiri hali za ulimwengu zinavyozidi kuharibika zaidi, nia yetu inapaswa kuwa kuendelea kuzisema habari njema za Ufalme mpaka kazi hiyo imalizike. Wakati upinzani unapotokea, hatuchukizwi. Twakumbuka kwamba Yesu hakuanza tu kazi aliyopewa na Yehova afanye bali pia aliimaliza. (Yohana 17:4) Yeye alitutayarisha tupambane na chuki ya ulimwengu. Wakati wote na tuwe kama yeye, na kama mitume na Wakristo wengine wa karne ya kwanza, huku, kwa imani kamili, tukitafuta msaada wa Yehova kusudi tutimize mapenzi yake yanayotuhusu. Sala yetu ya umoja na iwe hii wakati wote: ‘Basi sasa, [Yehova], . . . ukawajalie watumwa wako kunena neno lako kwa ujasiri wote.”—Matendo 4:29.—Kutoka The Watchtower Dec. 15, 1979.
[Picha katika ukurasa wa 17]
Yehova Mungu anabariki kazi ya “wavuvi wa watu” wa kisasa