Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • wt sura 19 kur. 167-174
  • Endelea Kuhubiri Neno la Mungu kwa Ujasiri

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Endelea Kuhubiri Neno la Mungu kwa Ujasiri
  • Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kutotegemea Nguvu Zetu Wenyewe
  • Walihubiri kwa Ujasiri
  • Julisha Rasmi Habari Njema kwa Ujasiri
    Huduma Yetu ya Ufalme—1990
  • Kunena Neno la Yehova Kwa Ujasiri
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Mashahidi Wajasiri wa Yehova Wafanya Vitendo!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Mwige Yesu—Hubiri Kwa Ujasiri
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
Pata Habari Zaidi
Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli
wt sura 19 kur. 167-174

Sura Ya Kumi Na Tisa

Endelea Kuhubiri Neno la Mungu kwa Ujasiri

1. (a) Wanafunzi wa Yesu walihubiri habari gani njema, lakini baadhi ya Wayahudi walitendaje? (b) Ni maswali gani tunayoweza kuuliza?

MIAKA 2,000 hivi iliyopita, Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, alitiwa mafuta awe Mfalme wa dunia wakati ujao. Yesu aliuawa kwa sababu ya uchochezi wa maadui wa kidini, lakini Yehova akamfufua kutoka kwa wafu. Yesu alifungua njia ya kupata uhai wa milele. Hata hivyo, wanafunzi wa Yesu walianza kunyanyaswa walipohubiri habari njema waziwazi. Baadhi yao walitupwa gerezani, hata walipigwa viboko na kuamriwa wakome kutangaza habari za Yesu. (Matendo 4:1-3, 17; 5:17, 18, 40) Wangefanya nini? Wewe ungefanya nini? Je, ungeendelea kuhubiri kwa ujasiri?

2. (a) Ni habari gani njema inayohitaji kuhubiriwa siku zetu? (b) Ni nani walio na daraka la kuhubiri habari njema?

2 Yesu Kristo, Mfalme wa Ufalme wa Mungu alitawazwa mbinguni mwaka wa 1914 ili atawale ‘kati ya adui zake.’ (Zaburi 110:2) Kisha, Shetani na mashetani wake wakavurumishwa hadi duniani. (Ufunuo 12:1-5, 7-12) Siku za mwisho za ulimwengu huu mwovu zilikuwa zimeanza. Kipindi hiki kifikiapo mwisho, Mungu ataharibu ulimwengu wote wa Shetani. (Danieli 2:44; Mathayo 24:21) Wale watakaookoka watakuwa na tumaini la kuishi milele katika dunia itakayokuwa paradiso. Ikiwa umekubali habari hizi njema, una daraka la kuwaambia wengine. (Mathayo 24:14) Lakini wataitikiaje?

3. (a) Watu huitikiaje ujumbe wa Ufalme? (b) Ni lazima tufikirie swali gani?

3 Unapohubiri habari njema za Ufalme, huenda wengine wakakusikiliza, lakini wengi hawatapendezwa. (Mathayo 24:37-39) Huenda wengine wakakudhihaki au kukupinga. Yesu alionya kwamba huenda ukapingwa na watu wa ukoo wako. (Luka 21:16-19) Huenda ukapingwa pia kazini au shuleni. Katika nchi nyingine, Mashahidi wa Yehova hata wamepigwa marufuku na serikali. Unapokabili hali kama hizo, je, utaendelea kuhubiri neno la Mungu kwa ujasiri na ‘kusimama imara katika imani’?—1 Wakorintho 16:13.

Kutotegemea Nguvu Zetu Wenyewe

4. (a) Ni lazima tufanye nini ili tuwe watumishi waaminifu wa Mungu? (b) Kwa nini mikutano ya Kikristo ni muhimu sana?

4 Ili tuwe watumishi waaminifu wa Yehova ni lazima tutegemee maandalizi yake. Mojawapo ya maandalizi hayo ni mikutano ya kutaniko. Maandiko yanatuhimiza tusipuuze mikutano. (Waebrania 10:23-25) Wale ambao wameendelea kuwa Mashahidi waaminifu wa Yehova wamejitahidi sana kuhudhuria mikutano kwa ukawaida pamoja na waabudu wenzao. Ujuzi wetu wa Maandiko unaongezeka tunapohudhuria mikutano hiyo. Tunazidi pia kuthamini kweli za msingi, na kufahamu vyema zaidi jinsi ya kuzitumia. Tunakuwa na uhusiano mzuri zaidi na ndugu zetu Wakristo katika ibada yenye umoja, na tunaimarishwa kufanya mapenzi ya Mungu. Roho ya Yehova hutoa mwongozo kupitia kutaniko, na Yesu huwa kati yetu kupitia roho hiyo.—Mathayo 18:20; Ufunuo 3:6.

5. Mashahidi wa Yehova wanapopigwa marufuku, mikutano hufanywaje?

5 Je, unahudhuria mikutano yote kwa ukawaida, na je, unatumia yale unayojifunza mikutanoni? Nyakati nyingine, Mashahidi wa Yehova wanapopigwa marufuku, wanalazimika kukutana katika vikundi vidogo kwenye nyumba za watu. Nyakati nyingine, huenda mikutano ikafanywa mahali na saa tofauti-tofauti ambazo huenda zisikufae, mikutano mingine inaweza kufanywa usiku. Lakini ndugu na dada waaminifu hujitahidi sana kuhudhuria kila mkutano licha ya hatari au hali zisizofaa.

6. Tunaonyeshaje kwamba tunamtegemea Yehova, na kufanya hivyo kunaweza kutusaidiaje kuendelea kuhubiri kwa ujasiri?

6 Tunazidi kumtegemea Yehova tunaposali kwake kwa ukawaida kutoka moyoni, na tunapotambua kwamba tunahitaji msaada wake. Je, wewe hufanya hivyo? Yesu alisali mara nyingi wakati wa huduma yake duniani. (Luka 3:21; 6:12, 13; 22:39-44) Aliwasihi hivi wanafunzi wake usiku wa mwisho kabla ya kutundikwa mtini: “Fulizeni kulinda na kusali, ili msije kuingia katika kishawishi.” (Marko 14:38) Huenda tukashawishiwa kupunguza bidii yetu katika huduma watu wanapokataa kusikiliza ujumbe wetu wa Ufalme. Tunapodhihakiwa au kunyanyaswa tunaweza kuhisi kwamba ni afadhali kuacha kuhubiri ili kuepuka matatizo hayo. Lakini tukisali kwa bidii ili roho ya Mungu itusaidie kuendelea kuhubiri kwa ujasiri, hatutashindwa na majaribu hayo.—Luka 11:13; Waefeso 6:18-20.

Walihubiri kwa Ujasiri

7. (a) Kwa nini habari iliyo katika kitabu cha Matendo inatupendeza sana leo? (b) Jibu maswali yaliyo mwishoni mwa fungu hili, ukikazia jinsi habari hiyo inavyoweza kutufaidi.

7 Habari iliyo katika kitabu cha Matendo inatuhusu sana leo. Inasimulia jinsi mitume na wanafunzi wengine wa mapema—watu waliokuwa na hisia kama zetu—walivyoshinda vizuizi na kuwa mashahidi wa Yehova waaminifu na wenye ujasiri. Hebu tuchunguze sehemu fulani ya habari hiyo tukitumia maswali na maandiko yafuatayo. Tunapofanya hivyo, fikiria jinsi wewe binafsi unavyoweza kufaidika na mambo unayosoma.

Je, mitume walikuwa na elimu ya juu? Je, kwa asili walikuwa watu wajasiri katika hali yoyote ile? (Yohana 18:17, 25-27; 20:19; Matendo 4:13)

Ni nini kilichomwezesha Petro aseme kwa ujasiri mbele ya mahakama ya Kiyahudi ambayo ilikuwa imemhukumu Mwana wa Mungu mwenyewe? (Mathayo 10:19, 20; Matendo 4:8)

Mitume walikuwa wakifanya nini kabla ya kuletwa mbele ya Sanhedrini? (Matendo 1:14; 2:1, 42)

Watawala walipowaamuru mitume waache kuhubiri kwa msingi wa jina la Yesu, Petro na Yohana walijibuje? (Matendo 4:19, 20)

Baada ya kuachiliwa kwao, mitume walimwomba nani msaada? Je, walisali mnyanyaso ukome, au walisali juu ya nini? (Matendo 4:24-31)

Wapinzani walipojaribu kuzuia kazi ya kuhubiri, Yehova aliandaaje msaada? (Matendo 5:17-20)

Mitume walionyeshaje kwamba walifahamu sababu iliyofanya wakombolewe? (Matendo 5:21, 41, 42)

Hata wakati ambapo wengi wa wanafunzi walikuwa wametawanyika kwa sababu ya mnyanyaso, waliendelea kufanya nini? (Matendo 8:3, 4; 11:19-21)

8. Wanafunzi wa awali walipata matokeo gani yenye kutia moyo, nasi tunahusikaje?

8 Kazi ya kuhubiri habari njema haikuwa ya bure. Wanafunzi wapatao 3,000 walibatizwa siku ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K. “Waamini katika Bwana wakafuliza kuwa wakiongezwa, umati wa wanaume na pia wa wanawake.” (Matendo 2:41; 4:4; 5:14) Muda si muda, Sauli wa Tarso, aliyewatesa vikali watu wa Mungu, akawa Mkristo na akaanza kufundisha kweli kwa ujasiri. Alianza kuitwa mtume Paulo. (Wagalatia 1:22-24) Kazi ya kuhubiri iliyoanza katika karne ya kwanza haijakoma. Imepamba moto katika siku hizi za mwisho na imeenea kotekote duniani. Tuna pendeleo la kushiriki kazi hiyo, na tunapofanya hivyo, tunaweza kujifunza kutokana na mfano wa mashahidi waaminifu-washikamanifu waliomtumikia Yehova kabla yetu.

9. (a) Paulo alitumia nafasi gani kuhubiri? (b) Wewe huwahubiria wengine ujumbe wa Ufalme katika njia gani?

9 Paulo alifanya nini alipojifunza ukweli kumhusu Yesu Kristo? ‘Mara akaanza kuhubiri juu ya Yesu, kwamba Huyu ndiye Mwana wa Mungu.’ (Matendo 9:20) Alithamini fadhili zisizostahiliwa za Mungu ambazo alionyeshwa, naye alitambua kwamba kila mtu alihitaji kusikia habari njema alizokuwa amepokea. Paulo alikuwa Myahudi, naye alienda kuhubiri katika masinagogi kulingana na desturi ya siku hizo. Alihubiri pia nyumba kwa nyumba na kusababu na watu sokoni. Naye alikuwa tayari kuhamia maeneo mapya ili kuhubiri habari njema.—Matendo 17:17; 20:20; Waroma 15:23, 24.

10. (a) Paulo alionyeshaje kwamba ingawa alikuwa jasiri, alikuwa pia mwenye busara alipotoa ushahidi? (b) Tunawezaje kumwiga Paulo tunapowahubiria watu wa ukoo, wafanyakazi wenzetu, au wanashule wenzetu?

10 Paulo alikuwa jasiri lakini pia mwenye busara. Twapaswa kuwa na sifa hizo. Paulo aliwasihi Wayahudi akitumia ahadi za Mungu kwa babu zao. Aliwahubiria Wagiriki akitumia mambo ambayo walifahamu. Nyakati nyingine alitoa ushahidi kwa kutumia mambo yaliyompata yeye binafsi alipokuwa akijifunza kweli. Alisema hivi: “Nafanya mambo yote kwa ajili ya habari njema, ili nipate kuwa mshiriki wayo pamoja na wengine.”—1 Wakorintho 9:20-23; Matendo 22:3-21.

11. (a) Paulo alifanya nini ili kuepuka kukabiliana kila mara na wapinzani? (b) Tunaweza kumwiga Paulo tunapokabili hali gani, na jinsi gani? (c) Tunapata wapi nguvu za kuhubiri kwa ujasiri?

11 Upinzani ulipomlazimu Paulo kuhubiri eneo jingine kwa muda fulani, alifanya hivyo badala ya kukabiliana na wapinzani kila mara. (Matendo 14:5-7; 18:5-7; Waroma 12:18) Lakini hakuaibikia kamwe habari njema. (Waroma 1:16) Ingawa Paulo hakufurahia kutendewa kwa ufidhuli—hata kwa ujeuri—na wapinzani, ‘alijipa ujasiri kwa njia ya Mungu wetu’ ili kuendelea kuhubiri. Alisema hivi: “Bwana alisimama karibu nami na kutia nguvu ndani yangu, ili kupitia mimi kule kuhubiri kupate kutimizwa kikamili.” (1 Wathesalonike 2:2; 2 Timotheo 4:17) Yesu, Kichwa cha kutaniko la Kikristo, huendelea kututia nguvu tunazohitaji ili kufanya kazi aliyotabiri ifanywe siku zetu.—Marko 13:10.

12. Tunaonyeshaje kwamba tuna ujasiri wa Kikristo, na kwa nini tunaonyesha ujasiri?

12 Tuna kila sababu ya kuendelea kuhubiri neno la Mungu kwa ujasiri, kama Yesu na watumishi wengine waaminifu wa Mungu walivyofanya katika karne ya kwanza. Hilo halimaanishi kwamba tusijali masilahi ya watu au kwamba tujaribu kuwalazimisha wasikilize ujumbe wetu. Lakini hatuachi kuhubiri eti kwa sababu watu hawapendezwi; wala wapinzani hawatunyamazishi. Kama Yesu, tunawajulisha watu kwamba Ufalme wa Mungu ndiyo serikali yenye haki ya kuitawala dunia yote. Tunahubiri kwa ujasiri kwa sababu tunamwakilisha Yehova, Mwenye Haki ya Kuutawala Ulimwengu, na ndiye aliyetuagiza tuutangaze ujumbe huo. Tunapaswa kumsifu Yehova hasa kwa sababu tunampenda.—Wafilipi 1:27, 28; 1 Wathesalonike 2:13.

Mazungumzo ya Kurudia

• Kwa nini ni muhimu kuwahubiria watu wengi iwezekanavyo ujumbe wa Ufalme, lakini tunaweza kutarajia waitikieje?

• Tunaweza kuonyeshaje kwamba hatutegemei uwezo wetu wenyewe tunapomtumikia Yehova?

• Twajifunza mambo gani muhimu kutokana na kitabu cha Matendo?

[Picha katika ukurasa wa 173]

Watumishi wa Yehova wanahubiri neno la Mungu kwa ujasiri leo kama ilivyokuwa zamani

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki