Mashahidi Wajasiri wa Yehova Wafanya Vitendo!
Mpanuko wa Ukristo kama Unavyosimuliwa Katika Kitabu cha Matendo
YESU KRISTO alikuwa amezitangaza habari njema za ufalme wa Mungu kwa miaka kama mitatu na nusu. Alikuwa amehimiza wafuasi wake waache nuru yao iangaze. Lakini walikuwa wachache, na Yesu alikuwa ametabiri kwamba kazi ya kuhubiri ingefanywa ulimwenguni pote. (Mathayo 5:14-16; 24:14) Je! wanafunzi wake wangeweza wakati wo wote kutimiza huduma ya namna hiyo? Hata kama walitaka kuifanya, wangepata msaada gani?
Luka mwanafunzi mwaminifu, aliyekuwa tabibu mwenye elimu, alitoa majibu ya maulizo hayo na mengineyo katika kile kitabu kilichoongozwa na Mungu kinachoitwa “Matendo ya Mitume.” (Linganisha Luka 1:1-4; Matendo 1:1, 2.) Ushuhuda wa nje na wa ndani pia unaonyesha Luka kuwa ndiye mwandikaji wa Matendo.Inaelekea kwamba kitabu hicho kiliandikiwa huko Roma karibu na mwaka wa 61 W.K.-Wakolosai 4:14;2 Timotheo 4:11a
Kitabu cha Matendo kinaanza na kupaa kwa Yesu mbinguni na kumalizika na kufungwa gerezani kwa Paulo katika Roma. Kwa hiyo, kinazungumza mambo yaliyotendeka kwa muda wa miaka 28, tangu mwaka wa 33 mpaka wa 61 W.K. Katika kurudia kueleza Ukristo wa kwanza kwa upana, hayo kwa uhakika ni masimulizi yenye kusisimua juu ya mashahidi wajasiri wa Yehova wenye kufanya vitendo.
Kitabu cha Matendo kinaweza kutufaidi namna gani? Kati ya mambo mengine, kinaweza (1) kutuonyesha kwamba mkono wa Yehova uko pamoja na mashahidi wake waaminifu; (2) kutujulisha kwamba roho takatifu ina uwezo na kutuonyesha mavutano yake; (3) kututia nguvu katika uhakika wetu wa kuamini unabii ulioongozwa na Mungu; (4) kutusaidia tumweke Mungu kwanza wakati wa majaribu ya imani; (5) kututia moyo tuwe wajasiri katika kutoa ushuhuda kamili kabisa; (6) kutusaidia tuvumilie tunapokabiliwa na mateso; (7) kutuchochea tuwe wenye kujinyima katika utumishi wa Mungu; (8) kutuharakisha tuwe wanafunzi wenye bidii wa Neno la Mungu; na (9) kutia nguvu imani yetu katika tumaini zuri ajabu la Ufalme.
Petro—Shahidi Mjasiri na Mwenye Uaminifu
Kitabu cha Matendo kinapoanza, Yesu yuko karibu kuwaaga wanafunzi wake. Je! atarudishia Israeli ufalme wakati huu? Wanataka kujua. Lakini anawaambia kwamba ‘si kazi yao kujua nyakati wala majira, Baba aliyoyaweka katika mamlaka yake mwenyewe.’ Ingawa wakati huo wafuasi wa Yesu walikosa ufahamu kamili juu ya Ufalme, yeye anawaagiza wawe mashahidi wake katika Yerusalemu, Yudea na Samaria, kisha “kwenye sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.” Watawezaje kweli kuifanya kazi hii? Ni kwa uwezo wa roho takatifu!—Matendo 1:6-8, NW.
Siku ya Pentekoste wanafunzi wa Yesu karibu 120 wamekusanyika katika chumba cha juu katika Yerusalemu wakati wanapojazwa roho takatifu. Basi wanawezeshwa kutoa ushuhuda kwa ujasiri katika lugha mbalimbali za Wayahudi na waongofu ambao wametoka nchi za mbali kusherehekea Pentekoste huko Yerusalemu. Mtume Petro ndiye anayeongoza katika kutoa ushuhuda. Anaeleza kwamba kumiminwa kwa roho ni utimizo wa unabii wa Yoeli. (Matendo 2:14-21; Yoeli 2:28-32) Siku iyo hiyo nafsi 3,000 ‘wanalikumbatia lile neno kwa moyo na kubatizwa.’ (Matendo 2:41, NW) Ni wazi kwamba mkono wa Yehova uko juu ya mashahidi wake. Uwezo na mavutano ya roho takatifu yanaonekana wazi. Zaidi ya hilo, maneno ya Petro yanatia nguvu uhakika wetu wa kuamini kwamba unabii uliongozwa na Mungu utatimizwa.
Halafu, mtu kiwete anaponywa kwa mwujiza, na huo unakuwa ushuhuda zaidi wa kwamba roho takatifu ya Mungu ni yenye uwezo. Ndipo Petro na Yohana wanapotoa ushuhuda wa ujasiri kuhusu Yesu. Viongozi wa kidini wanakasirika sana, nao wanakamata hao mitume na kuwajaribu kesho yake. Petro na Yohana wanasema mambo wazi na kuonyesha kwamba wokovu unaweza kupatikana kupitia Yesu Kristo tu. Wanapoamriwa waache kuhubiri, wanakataa. Baada ya kutishwa na kufunguliwa wanakutana na waamini wenzao halafu wote wanaungana kumwomba Mungu awasaidie ‘kunena neno lake kwa ujasiri wote.’ Kwa hiyo, “wote wakajaa [roho takatifu], wakanena neno la Mungu kwa ujasiri.” Wanapoagizwa tena waache kuhubiri, wanajibu hivi bila kuogopa: “Imetupasa kumtii Mungu kuliko wanadamu.”—Matendo 4:19, 20, 29-31; 5:29.
Jambo hilo linapasa liwasaidie sana mashahidi wa kisasa wa Yehova wamweke Mungu kwanza wakati wa majaribu ya imani! Nalo linapasa kututia sana moyo tuwe wajasiri katika kutoa ushuhuda kwa ukamili kabisa, hata tunapoteswa!
Stefano, mmoja wa wanaume saba waliowekwa na roho takatifu wagawe chakula, anatoa pia ushuhuda wenye mkazo mwingi anapoletwa mbele ya Sanhedrini (mahakama kuu). Anapoonyesha wazi kwamba mahakimu wana hatia katika kifo cha Yesu, wanakasirika sana na kumpiga kwa mawe mpaka anakufa. Utulivu wa Stefano katika kisa chote hicho ni mfano mzuri, unaowatia moyo mashahidi wa kisasa wa Yehova wavumilie wanapokabiliwa na mateso.—Matendo 6:1–7:60; linganisha Wafilipi 4:6, 7, 13.
Mateso yanaongezeka, lakini hayawakomeshi wanafunzi. Bali, ko kote walikotawanyika wanaendelea ‘kuzitangaza habari njema’ (NW), wakiungwa mkono na Yehova na kubarikiwa naye. (Matendo 8:4-8) Baada ya muda mfupi, yule mtesi mkali Sauli wa Tarso anaongolewa wakati Yesu binafsi anapomtokea katika mwangaza wenye nguvu, naye Sauli anapofushwa na utukufu huo. Anania anamrudishia Sauli uwezo wa kuona, kisha mtu huyu aliyekuwa mtesi, ambaye baadaye anajulikana kuwa mtume Paulo, anakuwa shahidi mjasiri kwa ajili ya Mungu na Kristo.—Matendo 9:1-30; 22:6-11.
Sasa kundi ‘linaingia katika kipindi cha amani, likiwa linajengwa; nalo linapotembea katika kumwogopa Yehova na katika faraja ya roho takatifu linaendelea kuzidika.’ (Matendo 9:31, NW) Petro anamfufua Tabitha (Dorkasi) mpendwa kutoka kwa wafu. Baadaye, anapokea mwito wa kwenda Kaisaria, ambako anatangazia Kornelio na watu wa nyumba yake “habari njema.” Wao wanakuwa waamini na roho takatifu inamiminwa juu yao. Baada ya wao kujua kwamba “Mungu hana upendeleo; bali katika kila taifa mtu amchaye na kutenda haki hukubaliwa na yeye,” Petro anawabatiza—watu wa Mataifa yasiyotahiriwa walio wa kwanza kuwa wanafunzi wa Yesu.—Matendo 10:1-48.
Muda mfupi baada ya hapo, Herode Agripa wa Kwanza anamwua mtume Yakobo kisha anaagiza Petro akamatwe ili naye pia auawe. Lakini mtume anapata ukombozi wa kimalaika kwa kutolewa gerezani. Kuongezea hilo, kujapokuwa na magumu na mateso, mkono wa Yehova uko pamoja na mashahidi wake, basi ‘neno la Yehova linazidi na kuenea.’—Matendo 11:19-21; 12:24.
Safari Tatu za Paulo za Kueneza Evanjeli
Kwa roho takatifu, Barnaba na Sauli wanawekwa kando na kutumwa watoke Antiokia, Shamu. (Matendo 13:2, 3) Katika kisiwa cha Kipro watu wengi wanakuwa waamini, kutia na liwali Sergio Paulo. Mashahidi wa Ufalme wanalazimika mara nyingi kuhama-hama katika miji mingi kwa sababu ya mateso yenye jeuri. Kwa mfano, katika mji wa Listra Paulo hata anapigwa kwa mawe na kuachwa akidhaniwa amekufa. Lakini, wakati nguvu zinapomrudia, anarudia kazi yake ya kutoa ushuhuda kisha anawatia wengine moyo wabaki katika ile imani, akisema: “Imetupasa kuingia katika ufalme wa Mungu kwa njia ya dhiki nyingi.” (Matendo 14:22) Hayo yote yanawatia moyo sana mashahidi wa kisasa wa Yehova wavumilie wanapokabiliwa na mateso!
Mkutano wa mitume na wanaume wazee huko Yerusalemu unalitatua tatizo la tohara. (Matendo sura ya 15) Waongofu-Mataifa wasiwekewe takwa la kutahiri ndipo waingie katika Ukristo. Roho takatifu inashiriki kuamua jambo hilo, kwa maana, kwa ufupi, barua iliyopelekwa ikieleza mambo hayo inasema hivi: “Roho takatifu na sisi wenyewe tumependelea tusiongeze mzigo zaidi kwenu ninyi, isipokuwa mambo haya ya lazima, kuendelea kushika mwiko wa vitu vinavyotolewa dhabihu kwa sanamu na wa damu na wa vitu vinavyonyongwa na wa uasherati.”—Matendo 15:28, 29, NW.
Sila anaambatana na Paulo wakati wa safari yake ya pili ya kueneza evanjeli, na huko njiani Timotheo anajiunga nao. Katika njozi, Paulo anaombwa akanyage Makedonia akatoe msaada. Na kulingana na nia ya kujinyima ya mtume na washirika wenzake, wanauchukua huo kuwa mgawo wao katika utumishi wa Mungu. Je! sisi pia tunachochewa ivyo hivyo wakati tunapopewa nafasi ya kutia bidii katika utumishi wa Yehova?—Matendo 16:9, 10.
Huko Filipi, kutolea Ufalme ushuhuda kunatokeza ghasia nyingi, na Paulo na Sila wanafungwa gerezani. Tetemeko la ardhi linawaweka huru, lakini hawapigi mbio kuondoka hapo. Bali, wanamhubiri mtunza gereza na watu wa nyumba yake, kisha wote hao wanakuwa waamini waliobatizwa.—Matendo 16:11-34.
Halafu, wanasonga mbele mpaka Thesalonike, kisha Beroya. Waberoya ‘ni waungwana kuliko wale wa Thesalonike, kwa kuwa wanalipokea lile neno kwa uelekevu wa moyo, wakiyachunguza maandiko kila siku, waone kwamba mambo hayo ndivyo yalivyo.’ (Matendo 17:10, 11) Je! jambo hilo halipasi lituharakishe tuwe wanafunzi wenye bidii wa Neno la Mungu, tuwe Waberoya wa kisasa?
Anapofika Athene, Paulo anatoa ushuhuda kwa ujasiri katika eneo la soko kisha anapelekwa Areopago na wanafalsafa. Akiwa huko anatoa ushuhuda mkubwa wa kuonyesha uumba wa Yehova, umoja wa jamaa ya kibinadamu, na ufufuo wa Yesu Kristo. Matokeo yanakuwa nini? Wengine wanakuwa waamini wenzake. (Matendo 17:16-34) Wanaposonga mbele mpaka Korintho, mtume anakuta watu wakipendezwa sana na kweli ya Mungu hata anabaki huko muda wa miezi 18.—Matendo 18:1-17.
Baada ya kurudi Antiokia na kukaa muda fulani huko, Paulo anaanza safari yake ya tatu ya kueneza evanjeli. Katika Efeso anatoa ushuhuda kwa ujasiri, naye Mungu anaendelea kufanya maajabu ya uweza mwingi kupitia kwake. Huduma katika Efeso inakuwa yenye matunda, lakini inatokeza ghasia nyingi pia katika mji wenye kumiminika waabudu wa Artemi mungu-mke. Lakini mtume anaondoka huko bila kupatwa na madhara. Matendo 19:8–20:1.
Anapokuwa njiani kurudi Yerusalemu, Paulo anawaita waje pamoja wanaume wazee wa kundi la Efeso. Anawakumbusha habari za utumishi wake wa kujinyima alioufanya katikati yao. Alikuwa amekuwa mwenye shughuli nyingi akiwa mtangazaji wa Ufalme na angeweza kuwaonyesha kazi aliyoifanya ya ‘kufundisha waziwazi na nyumba kwa nyumba.’ Huo ni mfano mzuri sana kwa wale wanaochukua madaraka kati ya watu wa Yehova leo!—Matendo 20:17-35, NW.
Mateso Hayakomeshi Kutolea Ufalme Ushuhuda
Ingawa Paulo anaonywa asikanyage Yerusalemu, yeye harudi nyuma. (Matendo 21:10-14) Yakobo na wanaume wazee wengine wa kundi wanafurahi sana wakati Paulo anapowaeleza Mungu amebariki huduma yake kati ya mataifa. Lakini wakati mtume anapoonekana hekaluni, mambo yanakuwa mengine wee! Wayahudi wa kutoka mkoa wa Asia wanachochea fujo katika mji mzima ili ashambuliwe, nao askari Warumi wanamwokoa kabla hajamalizwa. Baadaye, katika mahakama yenye mgawanyiko ya Mafarisayo na Masadukayo, Paulo anatokeza ulizo la ufufuo, na hivyo anayapinganisha makundi hayo mawili. Mgawanyiko wao unapozidi kuwa na jeuri, askari Waroma wanamponyoa Paulo na kwenda naye. Anapelekwa siri kwa Gavana Feliki huko Kaisaria. Anajitetea mbele ya gavana kinyume cha washtaki wake. Lakini mtume anawekwa kizuizini kwa miaka miwili. Baadaye analetwa mbele ya Porkio Festo, anatoa ushuhuda wa ujasiri, na kuomba rufani kwa Kaisari. (Matendo 25:11) Tena baadaye, Paulo analetwa mbele ya Mfalme Herode Agripa wa Pili. Ingawa Agripa anatambua kwamba Paulo hana hatia, mtume ameomba rufani kwa Kaisari na basi anapelekwa Roma.
Safari ya kwenda Roma inakatizwa na tufani kali sana. Merikebu inapiga chini na kuvunjika-vunjika, lakini, sawa na vile malaika alivyokuwa amemhakikishia Paulo, wote waliokuwa ndani wanafaulu kufika ufuoni wakiwa salama, katika kisiwa cha Melita. Katika mji mkuu wa Kiroma, kwa muda wa miaka miwili Paulo anabaki ‘katika nyumba yake mwenyewe aliyokodi naye anawapokea kwa fadhili wale wanaomjia.’ Kwa kusudi gani? Ili aweze kuwapa ushuhuda, kwa maana tunaambiwa kwamba yeye alikuwa na shughuli nyingi ‘akiwahubiri ufalme wa Mungu na kuwafundisha mambo yanayomhusu Bwana Yesu Kristo kwa uhuru wa kusema ulio mkubwa zaidi sana, bila kipingamizi.’—Matendo 28:30, 31, NW.
Hivyo ndivyo kitabu cha Matendo kinavyomalizika kikiwa na masimulizi ya kutolea Ufalme ushuhuda kwa uaminifu, Ndiyo, kitabu cha Matendo kinalikazia tumaini zuri sana la Ufalme. Nayo masimulizi hayo yaliyoongozwa na Mungu yanapasa yachochee watumishi wa kisasa wa Mungu wawe kama Wakristo wenzao wa karne ya kwanza—mashahidi wajasiri wa Yehova wenye vitendo!
[Maelezo ya Chini]
a Kwa maelezo marefu, angalia kitabu Aid to Bible Understanding, ukurasa wa 32, na “All Scripture Is Inspired of God and Beneficial,” kurasa 198, 199. Vitabu vyote viwili vinachapishwa na Sosaiti.