Zaburi
Furaha ya Kushiriki Katika Ibada ya Kweli
KUSHIRIKI pamoja na wengine katika ibada ya kweli ni jambo lenye kuleta furaha isiyosemeka kwa watumishi wenye kujitoa kwa bidii nyingi wa Aliye Juu Zaidi. Uzito mwingi wa furaha yao unaonyeshwa katika Zaburi ya 122, na maneno yayo ya kwanza yanasema: “Nalifurahi waliponiambia, na twende nyumbani kwa [Yehova].” (Zb 122 Mst. 1) Wazo lenyewe tu la kwenda kwenye patakatifu pa Yehova lilimtia mtunga zaburi furaha na amani nyingi.
Maelezo yanayoitangulia Zaburi ya 122 utangulizi(NW) yanaonyesha yeye ndiye aliyeiandika. Walakini, tafsiri iitwayo Septuagint Version haiyaonyeshi maneno yanayosema “ya Daudi.” Jambo hilo na maneno fulani yanayotumiwa katika zaburi hii limefanya wanachuo wengi wakate maneno kwamba iliandikwa na mtu mwingine wala si na Daudi. Hata hivyo, Zaburi ya 122 inaweza kufahamika bila ugumu tukiyakubali maelezo yanayoitangulia yanayoonekana katika maandishi ya Kiebrania.
Daudi mwenye kumwogopa Mungu alipendezwa sana na kupanda aende kwenye nyumba ya Yehova ya ibada. Kadiri ya furaha yake inaonekana wazi kutokana na jambo alilofanya wakati lile sanduku takatifu lilipohamishwa likapelekwa kwenye Mlima Sayuni. Biblia inatuambia hivi: “Daudi akacheza [dansi, NW] mbele za [Yehova] kwa nguvu zake zote.” Yeye na “nyumba yote ya Israeli wakalileta sanduku la [Yehova] kwa shangwe.”—2 Sam. 6:14, 15.
Ingawa hivyo, kutokana na maneno yanayofuata inaonekana bila shaka kwamba Zaburi ya 122 ilikusudiwa ionyeshe misisimuko ya ndani ya mwabudu ye yote mwenye kupanda aende kwenye patakatifu pa Yehova. Tunasoma hivi: “Miguu yetu imesimama [ilisimama, NW] ndani ya malango yako, Ee Yerusalemu. Ee Yerusalemu uliyejengwa kama mji ulioshikamana, huko ndiko walikopanda kabila, kabila za [Yehova]; ushuhuda [ukumbushaji, NW] kwa Israeli, walishukuru jina la [Yehova].” (Zab. 122:2-4) Hivyo, zaburi hii inawaonyesha waabudu wakitoka nje na kuja Yerusalemu, kisha wanasimama mara tu baada ya kuingia na kuyapita malango ili wauone mji. Macho yao yanaona nini? Kwamba Yerusalemu ni mji “ulioshikamana” kwa umoja. Nyumba zilijengwa karibu-karibu pamoja, kama kwamba zilikuwa ‘zimeshikamanishwa’ kwa umoja. Huo ndio uliokuwa mpango wa kawaida kwa mji nyakati za kale. Ukiwa umekaribiana hivyo na kuzungukwa na maboma, ilikuwa vyepesi zaidi kuulinda mji wa namna hiyo kuliko kulinda mji mkubwa wenye nyumba zilizotapakaa huku na huku. Walinzi wa mji hawakuwa na lazima ya kulinda eneo kubwa sana, kwa njia hiyo wakiacha sehemu fulani fulani zikiwa katika hali ya kushambuliwa na adui kwa urahisi. Tena, Yerusalemu ulizungukwa na milima na mabonde ya mitelemko yenye kuinama sana upande wa mashariki, wa kusini na wa magharibi, na hivyo nafasi ya ujenzi ikapungua sana. Kwa kuwa wakaaji wa mji huo waliishi karibu-karibu na kutegemeana kwa msaada na ulinzi, kukaribiana huko kwa halisi kungeweza kuonyesha vizuri umoja wa kiroho wa taifa zima wakati makabila yote ya Israeli yalipokusanyika kwa ajili ya ibada. ‘Kulishukuru jina la Yehova’ kulimaanisha walimpigia asante Aliye Juu Zaidi, Yule mwenye kuwakilishwa na jina hilo.
Si kwamba Yerusalemu ulikuwa ndipo mahali pa kati tu pa ibada ya kweli bali mji huo ulikuwa ndio makao ya serikali pia. Mtunga zaburi anaendelea kusema: “Maana huko viliwekwa viti vya hukumu, viti vya enzi vya mbari ya Daudi.” (Zab. 122:5) Ukiwa ndio mji mkuu, Yerusalemu ulikuwa ndipo mahali pa kufanyia hukumu za mwisho. Mfalme Daudi ndiye aliyekuwa na cheo cha mwamuzi (hakimu) na vilevile wengine wa nyumba yake. Biblia inatoa habari hii: “Nao wana wa Daudi wakawa makuhani.” (2 Sam. 8:18) Kwa sababu wanaitwa “makuhani” inaonyesha kwamba walikuwa wahudumu wa serikali au maafisa, nao, wakiwa katika cheo hicho, bila shaka walifanya maamuzi (hukumu).
Kwa sababu ya ubora wa Yerusalemu, mtunga zaburi anaendelea kusema: “Utakieni Yerusalemu amani; na wafanikiwe wakupendao; amani na ikae ndani ya kuta zako, na kufanikiwa ndani ya majumba yako.” (Zab. 122:6, 7) Lingekuwa jambo la kufaa sana Waisraeli kuomba Yerusalemu uwe na amani au hali njema kwa maana ulikuwa ndio mji mkuu wa taifa na mahali pa kati pa ibada. Kuupenda mji kwa sababu ya ubora wao kungepatana na mapenzi ya Mungu. Kwa hiyo, wote walioupenda mji huo, yaani, wote waliopenda ibada ya kweli na haki ya hukumu, wangeweza kubaki wakiwa na uhakika wa kupata upendeleo wa kimungu nao wangefurahia usalama, ‘wafanikiwe’ [‘wawe na uhuru wa kutokuwa na hangaiko,’ NW]. Maneno ya sala ya mtunga zaburi yalisema kwamba ndani ya ukuta mkubwa wenye kinga au ndani ya maboma ya Yerusalemu kuwe na amani, kwamba hali njema ya mji iwe salama. Usalama huo ungetia ndani majumba [minara, NW] yaliyokaliwa na watu au makao ya kifalme yaliyowekewa kinga imara.
Hasa kwa sababu mji huo ulikuwa mahali pa kati pa ibada ya Yehova, kufurahia amani kwa mji huo kulikuwa jambo lenye kulifaa sana taifa lao. Kwa hiyo, Mwisraeli alipouombea Yerusalemu amani, alikuwa akiwatakia Waisraeli wenzake mambo yenye kuwafaidi. Jambo hilo linaonyeshwa wazi katika maneno yanayofuata ya Zaburi 122: “Kwa ajili ya ndugu zangu na rafiki zangu niseme sasa, Amani ikae nawe. Kwa ajili ya nyumba ya [Yehova], Mungu wetu, nikutafutie mema.”—Zb 122 Mist. 8, 9.
Siku hizi ibada ya kweli haishirikishwi tena na mji fulani wenye kutajwa wazi wala na mahali fulani duniani. Yesu Kristo alimwambia hivi mwanamke Msamaria: “Saa inakuja ambayo hamtamwabudu Baba katika mlima huu [wa Gerizimu], wala kule Yerusalemu. . . . Lakini saa inakuja, nayo sasa ipo, ambayo waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu.”—Yohana 4:21-23.
Kwa hiyo, badala ya kuombea (kusali kwa ajili ya) mahali fulani, watumishi wa Mungu kwa kufaa wanaombeana na kuombea amani ya kundi la Kikristo kwa ujumla, ambalo siku hizi ndilo linaloitukuza ibada ya kweli mbele ya wengine. Kwa habari ya mikutano ya kundi hilo je! misisimuko yako ya ndani iko kama ile ya mtunga zaburi? Je! wewe unafurahia kuwa pamoja na wengine wenye imani iliyo na thamani kubwa kama yako? Je! wewe pia unaihangaikia hali njema ya kundi kama mtunga zaburi alivyoihangaikia amani ya Yerusalemu? Ikiwa ndivyo unaishi kwa kupatana na roho (maana) ya Zaburi 122.