Yerusalemu—“Sababu ya Shangwe”
“Mimi ninaumba mbingu mpya na dunia mpya; na mambo ya zamani hayatakumbukwa, wala hayatainuka ndani ya moyo. Lakini shangilieni, enyi watu, na mjawe na furaha milele katika kila ninachoumba. Kwa maana mimi ninaumba Yerusalemu uwe sababu ya kujawa na furaha na watu wao wawe sababu ya shangwe. Nami nitajawa na furaha juu ya Yerusalemu na kushangilia juu ya watu wangu.”—Isaya 65:17-19, NW.
1. (a) Kwa sababu gani watu wa Mungu wanapaswa kusisimuliwa na maneno ya Zaburi 65:17-19? (b) Hata hivyo ni maulizo gani yanayotokezwa juu ya Yerusalemu?
MANENO hayo ya Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu ni yenye kusisimua, yakiwa yamesemwa kupitia nabii wake! Yanataja furaha tele. Je! wewe hutaki kuishiriki furaha hiyo? Hakika! Lakini labda utauliza Yerusalemu unaotajwa hapa ni nini? Je! una uhusiano wo wote na ule mji wa kisasa—ambapo ni mahali penye kujawa na mizozo yenye jeuri nyingi ya kidini na kisiasa? Je! wakati wo wote “Yerusalemu” utatimiza fungu la mji huo linalopatana na maana ya jina ulilo nalo—“Makao [au, Msingi] ya Amani Maradufu”? Zile “mbingu mpya na dunia mpya” zinahusianaje na Yerusalemu unaotajwa katika unabii huu? Tutaona.
Yerusalemu wa Kale
2. Historia ya kwanza ya eneo la Yerusalemu ilikuwa nini?
2 Eneo la Yerusalemu lina historia ndefu ya kuwa na upendeleo wa Yehova. Miaka zaidi ya 3,900 iliyopita, bila shaka hapo ndipo Melkizedeki kuhani-mfalme alipombarikia Abrahamu. Zaidi ya hilo, alimbariki Yehova kwa kumtaja kuwa “Mungu Aliye juu sana, Muumba mbingu na nchi.” (Mwanzo 14:18, 19) Lakini, baada ya muda fulani mji huo Salemu uliojengwa mlimani ukaja kuwa ngome ya Wayebusi waabudu-mashetani.
3. Ni mtajo gani unaofanywa juu ya Yerusalemu wakati wa Yoshua na baadaye?
3 Miaka zaidi ya 400 inapita, na katika Yoshua sura ya 10 tunaona mtajo wa kwanza wa “Yerusalemu” katika Biblia. Hapo tunasoma kwamba Mfalme Adonisedeki aliita wafalme wanne majirani waje wajiunge naye kufanya vita dhidi ya Israeli. Lakini Yehova akapigania Israeli. Hata jua na mwezi vikasimama ndi, Wakanaani wakaweza kutimuliwa mbio kabisa. Wale wafalme watano walichinjwa. Lakini, hapo hapasemi kwamba Yoshua aliuteka Yerusalemu. Kwa kweli, maandishi yanasema: “Katika habari ya Wayebusi, hao wenye kuketi Yerusalemu, wana wa Yuda [waliorithi eneo hilo] hawakuweza kuwatoa.”—Yoshua 10:1-27; 15:63; Waamuzi 1:21.
Yerusalemu wa Wafalme Daudi na Sulemani
4. Yerusalemu ulikuwaje na baraka siku za Daudi na Sulemani?
4 Yapata miaka 400 baadaye, Daudi akawa mfalme juu ya Israeli wote. Mwaka wa 1070 K.W.K. “Daudi akaitwaa ngome ya Sayuni; huu ndio mji wa Daudi,” katika Yerusalemu. Akaanza kutawala huko juu ya Mlima Sayuni akiwa mfalme mtiwa-mafuta wa Yehova. Sulemani mwanaye aliketi pia juu ya ‘kiti cha enzi cha Yehova, akiwa mfalme.’ Sulemani alijenga hekalu lenye utukufu juu ya Mlima Moria katika Yerusalemu wakati wa utawala wake wenye amani. Hekalu hilo likawa ndipo mahali pakuu pa ibada ya Yehova na kufunziwa Neno na Torati Yake.—1 Mambo ya Nyakati 11:5; 29:23; 2 Mambo ya Nyakati 7:12-16.
5. Kitabu cha Zaburi kinauelezaje Yerusalemu na “Mfalme mkuu” wa mji huo?
5 Zaburi nyingi zinasifu sana upendezi wa Sayuni na wa Yerusalemu. Wana wa Kora waliuimba mji huo wakiutaja kuwa “mji wa Mungu wetu, katika mlima wake mtakatifu.” Ndiyo, “kuinuka kwake ni mzuri sana, ni furaha ya dunia yote. Mlima Sayuni pande za kaskazini, mji wa Mfalme mkuu [Yehova Mungu].” Daudi mwenyewe aliueleza kwa maneno haya: “Miguu yetu [ilisimama] ndani ya malango yako, Ee Yerusalemu. Ee Yerusalemu uliyejengwa kama mji ulioshikamana, huko ndiko walikopanda kabila, kabila za [Yehova]; ushuhuda kwa Israeli, walishukuru jina la [Yehova].” Huyo “Mfalme mkuu” anasemwa kuwa ‘anakaa Yerusalemu’ na kuwa ndiye Mlindaji mwenye upendo wa watu wa mji huo. “Kama milima inavyouzunguka Yerusalemu, ndivyo [Yehova] anavyowazunguka watu wake, tangu sasa na hata milele.”—Zaburi 48:1, 2; 122:2-4; 135:21; 125:1, 2.
Kuharibiwa na Kurudishwa Katika Hali Yao
6. (a) Yerusalemu ulikuja kufananisha nini? (b) Ni hukumu gani iliyofikilizwa juu ya Yerusalemu, na kwa sababu gani?
6 Kwa kufaa, Yerusalemu na Mlima Sayuni ukaja kufananisha taifa la Israeli na watu walo. Lakini baadaye katika muda usiozidi miaka 500 taifa hilo likawa asi-imani, na wafalme waovu ‘waliujaza Yerusalemu damu zisizo na hatia.’ (2 Wafalme 24:4) Walikataa kutii onyo la manabii wa Mungu, mpaka mwishowe Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu akatangaza hukumu juu ya Sedekia, mfalme wa mwisho kutawala katika Yerusalemu, akisema: “Kiondoe kilemba . . . Nitakipindua, nitakipindua, nitakipindua; hiki nacho hakitakuwa tena, hata atakapokuja yeye ambaye ni haki yake; nami nitampa.” (Ezekieli 21:26, 27) Nebukadreza wa Babuloni aliharibu Yerusalemu na hekalu lao mwaka wa 607 K.W.K. na kupeleka waokokaji Babuloni wakiwa mateka.
7. (a) Ni kurudishwa gani kulikotukia, na kwa sababu gani hilo lilikuwa jambo la kustaajabisha? (b) Wakati huo Yerusalemu ulikuwaje tofauti, lakini kurudishwa kuliwezesha nini?
7 Lakini, manabii wa Yehova walikuwa wametabiri hatua yenye utukufu ya kuurudisha Yerusalemu katika hali yao, na Yeremia hata alitaja kwamba hiyo ingetukia mwishoni mwa miaka 70. (Isaya 44:24–45:7; Yeremia 25:11, 12; 29:10) Kwa njia ya kustaajabisha, na kwa utimizo wa unabii wa Yehova kupitia Isaya, Babuloni ulipinduliwa, naye Mfalme Koreshi wa Uajemi mwenye kuushinda akatoa amri iliyowezesha Wayahudi wenye kumcha Mungu warudi wakarudishe ibada ya Yehova Yerusalemu katika wakati barabara mwaka wa 537 K.W.K. Kama vile Isaya alivyokuwa ametabiri, ‘utukufu wa Yehova, ukuu wa Mungu wetu’ uling’aa tena katika Yuda na Yerusalemu. Safari hii hakuna mfalme aliyetawala katika Yerusalemu. Lakini kwa mara nyingine Yehova aliupa mji huo upendeleo kwa sababu jina lake lilikuwa limewekwa huko na kwa sababu ya uaminifu wa baki la watu wake. Tena, kufanya hivyo kulikuwa mfano wa mambo makubwa zaidi ya wakati ujao. Mji ulijengwa upya, ikafanya kule kutokea kwa Masihi huko kulikotabiriwa kuweze kutukia.—Isaya 35:2; 62:1-7.
Nyumba ya Yerusalemu Yaachwa Pekee
8. (a) Kwa sababu gani Yerusalemu haukumkaribisha Masihi? (b) Ni unabii gani wa Yesu uliotimizwa kuelekea Yerusalemu, na namna gani?
8 Miaka zaidi ya 500 baada ya kurudishwa kwa mji huo, kweli Masihi alijitokeza kwa Wayahudi katika Yerusalemu. Jambo hilo lilitukia pia katika wakati uliowekwa na Yehova, mwaka wa 33 W.K., likatimiza unabii wa Danieli sura ya 9 mistari 24-27. Lakini je! Yerusalemu ulimkaribisha Masihi? Hapana, kwa sababu ulikuwa umefanya tumaini lao litegemee msaada wa kisiasa. Yerusalemu ulikuwa umeasi imani kwa kuyaacha mafundisho ya Neno la Yehova, na watawala wa Wayahudi walitenda uhalifu usiosameheka wa kumwua Mwana wa Mungu mwenyewe! Siku tatu tu kabla Masihi, Yesu, hajagongomelewa misumari bila huruma kwenye mti wa mateso, yeye aliliambia hivi taifa hilo: “Ee Yerusalemu, Yerusalemu, uwauaye manabii, na kuwapiga kwa mawe wale waliotumwa kwako! Ni mara ngapi nimetaka kuwakusanya pamoja watoto wako, kama vile kuku avikusanyavyo pamoja vifaranga vyake chini ya mabawa yake, lakini hamkutaka! Angalieni, nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.” (Mathayo 23:37, 38) Yerusalemu wa kidunia ulihukumiwa na kutupiliwa mbali na Yehova mwaka huo wa 33 W.K. Mwaka wa 70 W.K. majeshi ya Kiroma yalifagilia mbali Yerusalemu na wengi wa wakaaji wa mji huo, wakaliharibu na hekalu, pamoja na maandishi yenye kuonyesha mfuatano wa vizazi na kumbukumbu nyingine zilizohusiana na mfumo wa mambo ya Kiyahudi.
9. Je! mji wa Yerusalemu wa kidunia umekuwa na matendo yanayolingana na jina lao?
9 Je! Yerusalemu wa kidunia uliojengwa upya umefurahia baraka yo yote kutoka kwa Mungu tangu wakati huo? Historia yao yenye msukosuko mwingi muda wa miaka 1,900 iliyopita inajibu. Na leo Yerusalemu unaendelea kuwa mji wenye mgawanyiko wa kidini. Hata kidogo huo si “makao ya amani maradufu,” wala hauna utukufu wa Yehova. Yerusalemu wa kidunia haufurahii tena nafasi ya kukubaliwa kuwa katika kusudi la kimungu.
Uasi-Imani Wafananishwa Mapema
10. (a) Yerusalemu wenye kuasi imani unafananisha nini vizuri? (b) Mathayo 7:20 inaweza kutumiwaje kuhusu huo “Yerusalemu” wa kisasa?
10 Yerusalemu ulioasi imani mara mbili, na ambao Yehova aliuadhibu kwa kufanya kwanza uvamiwe na Wababuloni na baadaye na malejioni (majeshi) ya Kiroma, unafananisha vizuri mfumo mwingine wenye kuasi imani—dini ya Jumuiya ya Wakristo iliyopangwa kwa namna ya tengenezo. Kama vile watawala wanafiki wa Yerusalemu walivyoitolea Torati ya Yehova ibada ya mdomo tu bila matendo, ndivyo viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo wanavyodai kwamba wananena kwa kumtetea yule Mungu wa Biblia. Lakini, asema Yesu Kristo, “kwa matunda yao mtawatambua.” (Mathayo 7:20) Na ni “matunda” ya namna gani ambayo Jumuiya ya Wakristo ya kisasa imezaa? Je! kwa njia yo yote yamekuwa “Msingi wa Amani Maradufu”? Wapi. Badala ya hivyo, kumekuwako matunda ya vita vya ulimwengu viwili vyenye kuogopesha sana, na vyote viwili vilitokea katika makao ya Jumuiya ya Wakristo na kupiganwa kwa kubarikiwa na viongozi wa kidini wa pande zote mbili. Kikweli, yale maneno ya kiunabii yaliyoelekezwa na Yehova kwa Yerusalemu wenye kuasi imani yanatumika hata zaidi kwa njia ya moja kwa moja kuwahusu viongozi wa Jumuiya ya Wakristo ya kidini: “Katika pindo za nguo zako imeonekana damu ya [nafsi] zao maskini wasio na hatia . . . juu ya hawa wote.”—Yeremia 2:34.
11. Jumuiya ya Wakristo imetimiza maneno ya Yesu kwenye Mathayo 24:11, 12 na Marko 7:6-8 kwa njia gani?
11 Katika Jumuiya ya Wakristo leo ndimo tunamopata mazao tele ya ufisadi, talaka, jamaa zilizogawanyika, matumizi mabaya ya dawa za kulevya na uhalifu wa kila namna. Dini ya Jumuiya ya Wakristo imekuwa hoi isiweze kuzuia ukuzi wa uasi-sheria. (Mathayo 24:11, 12) Kweli maneno ya Yesu yanawafaa sana viongozi wa kidini wa jumuiya hiyo! Yeye alitamka hivi: “Isaya alitabiri vema juu yenu ninyi wanafiki, kama ilivyoandikwa, Watu hawa huniheshimu kwa midomo ila mioyo yao iko mbali nami; nao waniabudu bure, wakifundisha mafundisho yaliyo maagizo ya wanadamu, ninyi mwaiacha amri ya Mungu, na kuyashika mapokeo ya wanadamu.” Hivyo Jumuiya ya Wakristo, ambayo ndiyo “Yerusalemu” wa kisasa mwasi-imani, inaelekeana na “dhiki” itakayotoka kwa Mungu wakati Bwana Yesu Kristo atakapofunuliwa kutoka mbinguni ili alete kisasi juu ya wasiotii.—Marko 7:6-8; 1 Yohana 2:18, 19; 2 Wathesalonike 1:6-9, NW.
Kuurudisha Ufalme
12. Ni kipindi gani cha ‘kukanyaga’ kilichotabiriwa katika Luka 21:24?
12 Lakini, je! Yesu hakuonyesha kwamba Yerusalemu wa kidunia ungerudishwa wakati aliposema hivi: “Yerusalemu utakanyagwa na Mataifa, hata majira ya Mataifa yatakapotimia”? (Luka 21:24) Ni kweli, Yerusalemu ulikuwa umekanyagwa-kanyagwa na Wababuloni mwaka wa 607 K.W.K., na kujapokuwako utukufu wa kurudishwa, hakuna mfalme wa ukoo wa Daudi aliyepata kutawala tena katika mji huo. Tena, katika karne ya kwanza, Yerusalemu ulikuwa ukikanyagwa na Waroma, ambao walikuwa watu wa kuchukiza sana kwa Wayahudi wenye akili za kufikiria mambo ya kisiasa. Mpaka leo hii, hakujawa na kurudishwa ko kote kwa ufalme wa kitheokrasi katika Yerusalemu wa kidunia. Wala hakutakuwako kamwe.
13. (a) Luka 21:7-11, 24-26 inatabiri nini kuhusu kumalizika kwa “majira ya Mataifa”? (b) Matukio ya tangu mwaka wa 1914 na kuendelea yalithibitisha nini?
13 Ah, lakini “majira ya Mataifa” yamekwisha kutimizwa! Habari zenyewe zinazouzunguka unabii wa Yesu kwenye Luka 21 ndizo zinazoonyesha kwamba bila shaka yametimizwa. Je! leo hatuoni katika pande zote zinazotuzunguka mambo yale yale ambayo Yesu aliyatabiri hapo—‘taifa kuondoka kupigana na taifa’ katika vita vya kutumia silaha na vya kutumia mdomo tu, ‘matetemeko ya nchi, tauni, njaa, mambo ya kutisha, dhiki ya mataifa wakishangaa, watu wakivunjika mioyo kwa hofu, na kwa kutazamia mambo yatakayoupata ulimwengu’? Ndiyo, kumalizika kwa “majira ya Mataifa” kumekamatana na matukio hayo yenye kuutikisa ulimwengu ambayo yamelipuka duniani tangu mwaka wa 1914 na kuendelea! (Luka 21:7-11, 24-26) Ufahamu ndio uliofanya watu wa Yehova wawe wakionyesha mapema habari za mwaka wa 1914 muda wote wa miaka 35 iliyoitangulia tarehe hiyo. Hilo si jambo lililojitokeza lenyewe tu halafu wakashtukia kuona kwamba maneno yao yalikuwa ya kweli. Wao walifahamu kwamba zile “nyakati saba” za unabii wa Danieli, sura ya 4, zingekwisha mwaka wa 1914, na hapo ndipo ungefika mwisho wa utawala wa mataifa yasio ya Kiyahudi juu ya dunia bila ya kukatizwa na Mungu.
14. Kwa sababu gani Luka 21:24 haiwezi kuwa inamaanisha Yerusalemu wa kidunia?
14 Kwa hiyo katika mwaka wa 1914 mataifa yalikuwa yamefikia wakati wa kuacha ‘kuukanyaga Yerusalemu.’ Ni “Yerusalemu” upi huo? Haungeweza kuwa ni Yerusalemu wa kidunia uliotekwa na Allenby jenerali Mwingereza katika mwaka wa 1917 kisha ukabaki chini ya amri ya utawala wa Waingereza mpaka mwaka wa 1948, wakati ilipozaliwa jamhuri ya Israeli, wala si ufalme wa Israeli. Basi, Yesu alimaanisha “Yerusalemu” upi?
15. Kwa sababu gani tungetazamia kwamba ‘mzao wa Daudi’ alitawazwa katika kiti cha enzi “Yerusalemu” mwaka wa 1914 W.K.?
15 Tunakumbuka kwamba Yehova alisimamisha ufalme wa kitheokrasi huko Yerusalemu, Daudi akiwa mfalme. Daudi ndiye aliyepewa huko ahadi hii na Yehova: “Neno moja nimeliapa kwa utakatifu wangu, hakika sitamwambia Daudi uongo, wazao [mzao, NW] wake watadumu milele, na kiti chake kitakuwa kama jua mbele zangu. Kitathibitika milele kama mwezi; shahidi aliye mbinguni mwaminifu.” (Zaburi 89:35-37) Yalipokwisha “majira ya Mataifa” yasiyo ya Kiyahudi mwaka wa 1914 W.K., ‘mzao wa Daudi’ mwenye haki ya kisheria alikuwa amefikia wakati wa kuanza tena kutawala katika “Yerusalemu,” au Sayuni. Lakini si katika Yerusalemu wa kidunia!
16. (a) Basi, ni wapi ambapo Masihi amekuwa akitawala tangu mwaka wa 1914? (b) Ni ushuhuda gani unaoonyesha kwamba Kristo ameanza kutawala?
16 Badala ya hivyo, sasa yeye anatawala katika Yerusalemu, au Sayuni, ambao kwa habari yao Yehova anasema hivi kwenye Zaburi 2:6: “Nami nimemweka mfalme wangu juu ya Sayuni, mlima wangu mtakatifu.” Huo ndio mji ambao Daudi anautaja kwenye Zaburi 110:1, 2, wakati anaposema kwa unabii juu ya Bwana Yesu Kristo hivi: “Neno la [Yehova] kwa Bwana wangu, Uketi mkono wangu wa kuume, hata niwafanyapo adui zako kuwa chini ya miguu yako. [Yehova] atainyosha toka Sayuni fimbo ya nguvu zako [akisema,] Uwe na enzi kati ya adui zako.” Ndiyo, Mfalme wa Kimasihi, Yesu Kristo, sasa amekwisha kutawazwa katika kiti cha enzi cha Mlima Sayuni wa kimbingu, au Yerusalemu, atawale katikati ya adui zake. Tayari amekwisha kumvurumisha chini yule adui aliye mkubwa wa wote, Shetani Ibilisi, kwenye ujirani wa dunia hii. Kwa kuwa anajua wakati wake ni mfupi, Shetani ameingiza mataifa katika “ghasia,” kama mwandikaji wa zaburi anavyosema kwa kufaa.—Zaburi 2:1; Ufunuo 12:7-12.
17. Kwa sababu gani inatupasa tutazamie kwamba “ghasia” za mataifa zitakwisha mapema?
17 Lakini, je! Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu atayaruhusu mataifa hayo yatokeze “ghasia” kwa wakati usiojulikana huku yakiupinga vibaya sana Ufalme wake ulio mikononi mwa Mwanaye? Kumbuka kwamba, Wakristo wa karne ya kwanza walishtakiwa kuwa ‘waliujaza Yerusalemu mafundisho yao’; na shughuli hiyo ya jitihada nyingi za kuhubiri peupe nyumba kwa nyumba ilipokwisha kutoa onyo, Yerusalemu wa kidunia ulifikiliziwa hukumu ya Yehova. (Matendo 5:28, 41, 42; 4:16) Vivyo hivyo leo, Mashahidi wa Yehova wametangaza siku Yake ya kisasi kote kote katika milki ya Jumuiya ya Wakristo.
18. Kwa sababu gani tunaungojea ushindi wa “kusudi la milele” la Yehova tukiwa na uhakika?
18 Je! sasa Yehova atashindwa kukamilisha utangazaji huo ulio mkubwa zaidi wa duniani pote unaoshinda mwingineo katika historia yote kwa kuleta pigo la kifo cha daima kwenye Har–Magedoni? Je! Yehova atashindwa “kuwaharibu hao waiharibuo nchi”? Haiwezi kuwa hivyo kamwe! Wale ambao wametia nanga ya matumaini yao katika ahadi za Mungu wanatazamia kwa uhakika kuona ushindi wa “kusudi la milele” lake. (Ufunuo 11:18; Waefeso 3:10-12) Kupitia Ufalme ulio mikononi mwa Masihi, ambaye sasa anatawala akiwa katika “Yerusalemu” wa kimbingu, “Mfalme mkuu” wetu, Yehova, atafanya Jina Kuu Zaidi lake liondolewe lawama. Halafu, kwa kurudishia wanadamu uzima wa milele katika ukamilifu juu ya dunia-Paradiso, Yehova ataonyesha kwamba yeye ‘ni Mungu wetu, milele na milele,’ na kwamba ‘hakuiumba dunia ukiwa.’—Zaburi 48:14; Isaya 45:18, 22-24; 46:9-11; 55:11; Yeremia 25:31.
Wewe ungeelezaje mambo yanayofuata:
□ Jina “Yerusalemu” lina maana gani?
◻ Je! matendo ya mji huo yamelingana na jina lao?
◻ Ni ulinganifu gani wa Yerusalemu usio mwaminifu unaoonekana leo?
◻ Luka 21:24-26 inaonyesha nini juu ya mwisho wa “majira ya Mataifa”?
◻ Basi ni “Yerusalemu” upi unaoacha ‘kukanyagwa’?