“Israeli wa Mungu” na Mwisho wa Nyakati za Mataifa
1, 2. (a) Ni hali gani iliyo ndani ya kuta za mji wa Yerusalemu wa leo inayoonyesha kwamba Yehova hajarudia kutawala ulimwengu kwa kuutumia mji huo? (b) Lakini ni mji gani mwingine wenye jina hilo ambao sasa unazungumzwa?
MWEZI Desemba wa mwaka wa kati-kati wa vita, wa 1917, ndio wakati Waturuki walio wafuasi wa Muhamadi waliponyang’anywa Yerusalemu wa kidunia na askari wa Uingereza wakiongozwa na Jemadari Allenby. Wayahudi wa asili walilishangilia tukio hilo katika sehemu zote za dunia. Lakini mpaka leo hii hii kuwapo daima kwa jengo takatifu la wafuasi wa Muhamadi juu ya Mlima Moria ndani ya kuta za Yerusalemu kunazuia hekalu lo lote la ibada ya Wayahudi lisijengwe mahali hapo palipokuwa pamejengwa zamani hekalu la Mfalme Sulemani. Ni wazi kwamba Mungu aliyejengewa hekalu hilo na mwana wa kifalme wa Daudi hatawali ulimwengu kupitia Ufalme wake wa Kimasihi kwa kuutumia Yerusalemu wa kidunia wakati huu ambao “nyakati za Mataifa” zimekwisha kumalizika. Lakini namna gani ule Yerusalemu mwingine? Yerusalemu upi? Ule wenye kutajwa katika barua iliyoongozwa na Mungu wakaandikiwa wanafunzi wa Masihi Yesu katika jimbo la Galatia, miaka kadha baada ya yeye kutabiri uharibifu wa mji uliojengwa tena wa Yerusalemu, uharibifu ambao ulitokea mwaka wa 70 W.K. Humo katika Wagalatia sura ya 4, mistari 25, 26, tunasoma hivi:
2 “Maana Hajiri [kijakazi wa Abrahamu mzee wa ukoo aliyekuwa Mwebrania] ni kama mlima Sinai ulioko Arabuni, umelingana na Yerusalemu wa sasa; kwa kuwa anatumika pamoja na watoto [raia zake na wenye kutawalwa naye]. Bali Yerusalemu wa juu ni mwungwana [kama mke wa Abrahamu aliyekuwa mwungwana, Sara], naye ndiye mama yetu sisi.”
3, 4. (a) Paulo, pamoja na Wakristo Wagalatia, alimtambua nani kuwa “mama” yake wa kiroho? (b) Ni kwa njia gani taifa la Israeli lilikuwa limekuwa tengenezo la Mungu la ulimwengu mzima?
3 Mwenye kuandika maneno hayo alikuwa ni Sauli wa Tarso, Myahudi aliyeongolewa akawa mtume mchaguliwa wa Masihi Yesu. “Yerusalemu wa sasa” alioandika habari zake ulifukuzwa katika tengenezo la Mungu, sawa na vile Hajiri alivyofukuzwa katika jamaa ya Abrahamu, nao uliharibiwa mwaka wa 70 W.K. Paulo hakuutambua tena Yerusalemu huo wa kidunia kuwa mama yake. Yeye aliutambua “Yerusalemu wa juu,” yaani, Yerusalemu wa makao ya kiroho, kuwa mama yake wa kiroho. Akiwa pamoja na Wakristo hao Wagalatia, Paulo alikuwa mmoja wa “watoto” wake.
4 Kwenye Mlima Sinai, wakati Mungu alipoingiza watu wa Israeli katika uhusiano pamoja naye kupitia agano la Torati lililopatanishwa na Musa, hilo taifa la Israeli likawa sehemu inayoonekana ya tengenezo la Yehova la ulimwengu mzima. Taifa hilo likawa la tengenezo hilo sawa na vile kijakazi Hajiri alivyokuwa wa Sara, yule mke wa kwanza wa Abrahamu. Sara alikuwa kifananishi cha “Yerusalemu wa juu” ulio huru. Huo Yerusalemu wa juu ndio unaomzaa mzao aliyeahidiwa.
5. Kwa hiyo Yehova angeanza kutawala ulimwengu akiwa wapi mwishoni mwa Nyakati za Mataifa, na wakati ungekuwa umefika ajibu ulizo gani, na angelijibu kwa njia gani?
5 Kulingana na hayo, ni kuhusiana na huu “Yerusalemu wa juu” Yehova Mungu angeanza kutawala ulimwengu mwishoni mwa Nyakati za Mataifa katika mwaka wa 1914 wenye vita kali. Hapo ndipo ulipofika wakati wake wa kujibu kwa matendo lile ulizo lililotokezwa na Mfalme Daudi mwandikaji mwenye kuongozwa na Mungu, katika Zaburi 2:1-6:
“Mbona mataifa wanafanya ghasia, na makabila wanatafakari ubatili? Wafalme wa dunia wanajipanga, na wakuu wanafanya shauri pamoja, juu ya [Yehova], na juu ya masihi [mtiwa mafuta] wake, Na tuvipasue vifungo vyao, na kuzitupia mbali nasi kamba zao. Yeye aketiye mbinguni anacheka, [Yehova] anawafanyia dhihaka. Ndipo atakaposema nao kwa hasira yake, na kuwafadhaisha kwa ghadhabu yake. Nami nimemweka mfalme wangu juu ya Sayuni, mlima wangu mtakatifu.”—Ona pia Matendo 4:24-26.
6. (a) Kwa sababu gani kusimamishwa kwa Mfalme wa Kimasihi mwishoni mwa Nyakati za Mataifa hakukuonekana na watawala wa kidunia? (b) Ingawa watu walijulishwa mapema kwa muda wa makumi mengi ya miaka, watawala wa kilimwengu waliendelea kujitayarisha kufanya nini wakati huo wenye hatari?
6 Ndiyo, mwishoni mwa Nyakati za Mataifa mwaka wa 1914 ilifaa Yehova atimize maneno haya ya kiunabii yaliyoandikwa na Mfalme Daudi katika Zaburi 110:1, 2, NW: “Usemi wa Yehova kwa Bwana wangu ni: ‘Keti kwenye mkono wangu wa kuume mpaka mimi niweke adui zako kama kiti cha miguu yako.’ Fimbo ya nguvu zako Yehova ataituma toka Sayuni, akisema hivi: ‘Nenda uwe ukishinda katikati ya adui zako.’ “Mfalme wa Kimasihi alisimamishwa juu ya Mlima Sayuni wa kimbingu, na kwa hiyo tendo hilo halikuonekana na wafalme na wakuu walio katika serikali hapa duniani. Ingawa mwisho wa Nyakati za Mataifa ulikuwa umekwisha kutangazwa na Sosaiti makumi mengi ya miaka kuwa ungetukia mwaka wa 1914, watawala hao wa kidunia walikaza nia wampinge sana Masihi wa kimbingu asianze kutawala ulimwengu. Waliendelea kufanya matayarisho yaliyo ya hali ya juu zaidi kwa ajili ya vita ya kimataifa. Hata hivyo, kwa kuonekana kijuu-juu, mwaka wa 1914 ulianza ukiwa wenye amani. Halafu, Julai 28 mataifa yakajitumbukiza ndani ya vita.
7. Kusimamishwa kwa Masihi akiwa Mfalme mwishoni mwa Nyakati za Mataifa mwaka wa 1914 kulionyesha ameanza kuwa na uhusiano gani na dunia, na namna gani hivyo?
7 Kusimamishwa kwa Masihi awe Mfalme mkono wa kuume wa Yehova katika mwaka huo huo kulionyesha mwanzo wa kuwapo kwake kusikoonekana kuhusiana na dunia yetu. Kwa sababu gani iwe hivyo? Kwa sababu akiwa ndiye Mfalme mpya aliyesimamishwa asimamie dunia ilimfaa aelekeze fikira zake juu ya makao ya kidunia, ambayo wakati huo yalikaliwa na adui zake, wenye tamaa nyingi ya kutawala ulimwengu ukiwa na makoloni yao. ‘Fimbo ya nguvu zake’ ilipelekwa kutoka “Yerusalemu wa juu,” kuelekea dunia yetu. Alipopewa amri na Yehova, alianza ‘kutawala katikati ya adui zake’ huku chini duniani. Pia ni huku duniani alikomvurumisha Ibilisi na mashetani wake kwa kuwaondoa mbinguni.—Ufunuo 12:7-17.
8. Mitume wa Yesu walimwomba awape “ishara” ya jambo gani, na mataifa yangekuwa katika hali gani kulingana na Zaburi 2:1?
8 “Ishara” ambayo Masihi Yesu aliisimulia kuwa ushuhuda wa “kuwapo” kwake kusikoonekana ilionekana mwishoni mwa Nyakati za Mataifa mwaka wa 1914. Muda mfupi kabla Yesu hajafa kifo cha kufia imani, mitume walimwuliza hivi: “Tuambie wakati mambo haya yatakuwa,—na ni nini ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa kizazi.” (Mathayo 24:3, The Emphasised Bible, iliyotayarishwa na J. Rotherham; The Emphatic Diaglott, iliyotayarishwa na Benjamin Wilson; Literal Translation ya Young; New World Translation) Kulingana na Zaburi 2:1, mataifa yangefanya ghasia wakati wa Mungu wa kumsimamisha Masihi Yesu awe Mfalme katika Yerusalemu wa makao ya kiroho, au Sayuni.
9. (a) Wakati wa karne ya kwanza, je! mitume wenye kuuliza ulizo walishuhudia dhiki kubwa ambayo haingekuwa na nyingine ya kulingana nayo mpaka milele? (b) Kwa hiyo kushuhudia kwao mambo yaliyotajwa na Yesu katika Mathayo 24:7-15 kulikuwa kama utimizo wa namna gani?
9 Sisi hatujui kama Yesu alikuwa akifikiria Zaburi 2:1 na pia Zaburi 110:1-4 alipokuwa akitoa jibu lake. Lakini vyo vyote iwavyo, jibu lake linalingana na ule unabii mbalimbali uliotolewa na Mfalme Daudi, ambao unavuta sana fikira tangu mwaka wa 1914 kuliko wakati wa ile miaka 37 iliyofuata baada ya mitume kuuliza ulizo lao na kutokea kwa uharibifu wa Yerusalemu ulioletwa na malejioni ya Kiroma mwaka wa 70 W.K. Ni jambo la hakika kwamba msiba huo wa Kiyahudi wenye kuogopesha sana haukuendelea kuwa bila mwingine wa kulingana nao. Kwa mfano, sio uliokuwa mbaya zaidi ya kuchinjwa-chinjwa kwa Wayahudi wanaosemekana kuwa walikuwa 6,000,000 katika utawala wa Hitler wa Nazi kabla ya Vita ya Ulimwengu ya Pili na wakati ilipokuwa ikiendelea. Uharibifu wa Yerusalemu haukuwa “dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe.” (Mathayo 24:21) Mambo yaliyoshuhudiwa na mitume mpaka mwisho wa karne ya kwanza W.K. yalikuwa utimizo mdogo tu wa unabii wa Yesu. Mambo hayo yalikuwa njaa kubwa-kubwa, matetemeko ya ardhi, magonjwa ya kipuku, vita na mateso, na pia kufagiliwa mbali kwa “Yerusalemu wa sasa.” Wao hawakuwa na uhitaji wa kupiga yowe kwa sababu ya tendo hilo, kwa sababu Yerusalemu wa makao ya kiroho ulibaki ukiwa umesimama.
10. Utimizo mkubwa wa unabii wa Yesu unatufanya tukate kauli gani?
10 Mambo yaliyotukia huko nyuma hayakujumlika na kuwa “ishara” yenye kuonyesha “kuwapo” kwake na “umalizio wa kizazi.” Kwa hiyo ili ukweli wa unabii wa Yesu utetewe, ilikuwa lazima kuwe na utimizo mkubwa wa maneno yake baadaye, wakati wa siku za washiriki wa mwisho wa “kundi dogo” lake la warithi wa Ufalme. (Luka 12:32) Utimizo huo ungetokea tangu kumalizika kwa Nyakati za Mataifa mpaka wakati wa sasa. Tunapotazama historia ya ulimwengu tangu tarehe hiyo, kwa msaada wa unabii wa Biblia, tunapata usadikisho wa wazi kwamba tunaishi katika “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 24:3, NW; Marko 13:4) Usadikisho huo unahakikishwa na utimizo wa Ufunuo 6:3-17, ulioandikwa zaidi ya robo-karne baada ya uharibifu wa Yerusalemu ukieleza habari za wale wapanda-farasi wanne wa Ufunuo, kama wanavyoitwa na watu.
11. Washiriki ambao wangali hai wa “kanisa la wazaliwa wa kwanza” wanakumbuka nini juu ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, na utimizo mbalimbali wa unabii wa Yesu wakati wa karne ya kwanza unalinganaje na matukio ya wakati huu?
11 Wengine wa mabaki ya “kanisa la wazaliwa wa kwanza walioandikwa mbinguni” wangali hai leo, nao wanaikumbuka sana homa kali ya Kispania. (Waebrania 12:23) Ugonjwa huo mbaya sana ulifagia halaiki ya watu duniani karibu na mwisho wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Ilikuwa moja la magonjwa ya kipuku yaliyotabiriwa, na iliua mamilioni mengi ya wanadamu kuliko yale yaliyouawa wakati wa ile miaka zaidi ya minne ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Washiriki wa mabaki ambao wangali hai wanayakumbuka pia mateso yaliyoletwa juu ya wanafunzi Wakristo wa Biblia waliokuwa wakijitahidi wasiwe na hatia ya damu ya ulimwengu. Wanakumbuka namna mateso hayo yalipofikia kilele wakati msimamizi (mwenye umri wa miaka 48), katibu-mweka-hazina (mwenye umri wa miaka 54), na washiriki wengine wa wafanya kazi wa makao makuu ya Sosaiti walipofungwa gerezani. Mashtaka waliyokuwa wamefanyiwa yalitupiliwa mbali na mahakama mwaka wa 1919. Kuhusiana na jambo hilo, vitabu vya Sosaiti vilipigwa marufuku katika Kanada na United States ya Amerika. Marufuku hiyo ilikuja kuondolewa baada tu ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Sasa basi, yaliyotukia nyakati za mitume wakati wa karne ya kwanza kwa utimizo wa unabii wa Yesu yanakuwa si kitu yanapolinganishwa na matukio yanayofanana na mambo hayo ambayo yametukia ulimwenguni pote wakati wa miaka ya 1914-1918 W.K.
Hatua ya Kutii ya “Israeli wa Mungu”
12. (a) Alipokuwa akijibu ulizo kuhusu “ishara” ya kuwapo kwake, alitaja mateso ya nani, na wale wa kwanza kati yao walikuwa wa taifa gani? (b) Ni nini kimechukua mahali pa “kile ambacho ni Israeli kwa njia ya kimwili”?
12 Alipokuwa akilijibu ulizo lililohusu “ishara” ya “kuwapo” kwake kusikoonekana, Yesu hakutaja kungetokea mateso yo yote juu ya “kile ambacho ni Israeli kwa njia ya kimwili.” (1 Wakorintho 10:18, NW) Alitabiri mateso ya wanafunzi wake, na ni wazi kwamba wa kwanza kati ya wanafunzi hao walikuwa Wayahudi na waongofu waliotahiriwa. Lakini wakati unabii wa Yoeli 2:28, 29 ulipotimizwa tangu siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. na kuendelea, wanafunzi wake wakawa Israeli mpya, Israeli wa kiroho. (Matendo 1:6–2:42) Karibu na katikati ya karne ya kwanza yule Myahudi aliyeongolewa, mtume Paulo, aliandikia Wakristo katika Galatia akaendelea kuwaambia: “Bali Yerusalemu wa juu ni [huru], naye ndiye mama yetu.” (Wagalatia 4:26) Na karibu na mwisho wa barua yake alieleza hivi: “Kwa sababu kutahiriwa si kitu, wala kutokutahiriwa, bali kiumbe kipya. Na wote watakaoenenda kwa kanuni hiyo, amani na iwe kwao na rehema, naam, kwa Israeli wa Mungu.”—Wagalatia 6:15, 16.
13. Mabaki na wenzi wao wanajitahidi wawe na ushiriki wa kibinafsi katika sehemu gani yenye kutokeza ya “ishara” ya “umalizio wa mfumo wa mambo,” na kufikia sasa matokeo yamekuwa nini?
13 Sasa, kwa kuwa mabaki ya “Israeli wa Mungu” wanaona “ishara” ya “umalizio wa mfumo wa mambo” ikiendelea kutimia, ni mwendo gani wanaopaswa kufuata kwa utii? Ni mwendo ule ambao wakiufuata watakuwa na ushiriki katika kutimizwa kwa ile sehemu yenye kutokeza ya “ishara” ambayo Yesu alitabiri, akisema: “Lakini yeye ambaye amevumilia [yale mateso] mpaka mwisho [Kigiriki: telos] ndiye atakayeokolewa. Na habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa [akina goyimu] yote; na ndipo ule mwisho [telos] utakapokuja.” (Mathayo 24:13, 14, NW; Marko 13:9, 10) Katika mwaka ulioifuata Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, mabaki waliobaki hai wa “Israeli wa Mungu” walianza kuitimiza amri hiyo ya kiunabii kwa utii. Matokeo yamekuwa kwamba, leo katika nchi 205 na katika lugha karibu 190, “habari njema hizi za ufalme” zinahubiriwa na mabaki ya Waisraeli wa kiroho na mashahidi wenzao wa Yehova. Wamefanya yote hayo ijapokuwa kumekuwako mateso na Vita ya Ulimwengu ya Pili.
14. Kwa kutoa ushuhuda huu wanajulisha watu kwamba ni “nyakati” gani zimeyamalizikia mataifa, na ni kwa njia gani imekuwa hivyo kweli kweli?
14 Kupitia ushuhuda huo usioweza kunyamazishwa unaotolewa juu ya Ufalme uliosimamishwa, akina goyimu, yaani Mataifa yasiyo ya Kiyahudi, wanafahamishwa kwamba “majira” yao, “nyakati saba” zao za kuukanyaga-kanyaga Yerusalemu, zilikwisha katika vuli ya mwaka wa 1914. (Luka 21:24) Yerusalemu unaohusika hapa si Yerusalemu wa kidunia ulio katika Mashariki ya Kati, bali ni Yerusalemu wa makao ya kiroho, kwa maana huko mbinguni ndiko Yehova Mungu alimketisha Masihi wake juu ya kiti cha ufalme, yule Mwana wake Yesu aliye mtiwa mafuta, wakati Nyakati za Mataifa zilipokwisha mwaka wa 1914. Kwa hiyo, kulingana na Ufunuo 11:1, 2, “mji mtakatifu” ambao Mataifa yasiyo ya Kiyahudi yangeukanyaga-kanyaga “miezi arobaini na miwili” si “Yerusalemu wa mbinguni” ambamo Masihi Yesu amekuwa akitawala tangu mwaka wa 1914. (Waebrania 12:22) Bali, mkanyago huo ulifanywa juu ya mabaki ya “Israeli wa Mungu” kwa muda wa miezi 42, au muda wa miaka mitatu na nusu inayohesabiwa kwa kutegemea mizunguko ya mwezi halisi. Mkanyago wenyewe ulikuwa mateso yaliyowapata wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Lakini kufikia wakati wa lile kusanyiko la pili la wanafunzi wa Biblia lililofanywa huko Cedar Point, Ohio, U.S.A., katika kiangazi cha mwaka wa 1922, wao walikuwa wamekwisha kupona kabisa kiroho. Kwa hiyo mateso ya mabaki wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza yalikuwa sehemu ya “ishara” ambayo ingeuonyesha uhakika wa kwamba Yesu alikuwapo katika Ufalme wake tangu mwaka wa 1914 akiwa katika Yerusalemu wa juu, asiweze kukanyagwa-kanyagwa kwa njia iwayo yote.—Mathayo 24:3, 9-13.
15. Wakati huo mabaki na wenzi wao walianza kufanya sana jambo gani kuliko nyakati zote zilizotangulia, na je! katika jambo hilo wamejiacha wakanyagwe-kanyagwe?
15 Huo ndio wakati mabaki ya “Israeli wa Mungu” walipojitokeza sana kuliko nyakati zo zote zilizotangulia ili ‘kumtangaza Mfalme na Ufalme.’ Kwa uneni wa kiroho, wao hawajalala chini wapate kukanyagwa-kanyagwa tena na Mataifa.—Ufunuo 11:7-15.
16. Tangu mwaka wa 1914, ni mfalme gani anayeendelea kuendesha farasi na kushinda katikati ya adui zake, na baada ya muda mfupi mambo yatabadilikaje katika lile tendo la kukanyagwa-kanyagwa?
16 Baada ya mambo kupata badiliko lenye kupendeza sana, Mfalme Yesu Kristo aliyeketishwa juu ya kiti cha ufalme amekuwa akitawala katika Yerusalemu wa makao ya kiroho tangu Nyakati za Mataifa zilipomalizika mwaka wa 1914 naye anaendelea kushinda katikati ya adui zake wa kidunia. Baada ya muda mfupi kupita, wakati ushuhuda wa Ufalme utakapokuwa umetolewa katika mataifa yote, mwisho wa “umalizio wa mfumo wa mambo” utakuja. Hayo Mataifa-adui yasiyo ya Kiyahudi yatakatwa yaanguke kama mzeituni uliojaa matunda. Ndipo atakapoyavurumisha ndani ya ‘shinikizo, kubwa la mvinyo la ghadhabu ya Mungu,’ kisha atayakanyaga-kanyaga humo barabara, ayavyoge-vyoge yatokwe na damu ya uhai wayo. (Ufunuo 14:18-20) “Naye atawachunga [mataifa] kwa fimbo ya chuma, naye anakanyaga shinikizo la mvinyo ya ghadhabu ya hasira ya Mungu Mwenyezi.”—Ufunuo 19:15.
17. Ni mfano gani ulio wa mwisho kutolewa katika unabii wa Yesu unaohusu “ishara,” na “ndugu” za kiroho za mtawala wanafanyiwaje mambo mema?
17 Utimizo wa mfano wa Yesu wa kondoo na mbuzi ulipasa kuwa sehemu ya “ishara” yenye kuonyesha “kuwapo” kwake kusikoonekana na “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 24:3, NW; 25:31-46) Kulingana na utabiri huo, mamilioni ya watu wamekwisha kukubali ushuhuda wa Ufalme unaotolewa na mabaki ya “Israeli wa Mungu.” Wameitikia kwa njia ya kuthamini. Hao “kondoo” waliotajwa katika mfano wanatendea mema hata aliye mdogo kabisa wa “ndugu” za kiroho za Mfalme anayetawala, Yesu Kristo. “Kondoo” wanashirikiana na “ndugu” zake hao, na ndio wanaoifanya ile sehemu kubwa zaidi ya mahubiri yaliyotabiriwa ya “habari njema hizi za ufalme” duniani pote ili kutoa ushuhuda wa mwisho.
18. Ni “ufalme” gani ambao kondoo za mfano wanataka kurithi, nao watapewaje ukaribishaji wa kufanya hivyo?
18 Hao “kondoo” waliotajwa katika mfano wanataka kurithi “ufalme [waliowekewa] tayari tangu kuumbwa ulimwengu.” (Mathayo 25:34) Watapokea ukaribishaji wa kuurithi kutoka kwa “Mwana wa Adamu” anayetawala wakati watakapokuwa wakiiingia “dhiki kubwa,” wakiwa na taraja la kuiokoka kwa kuwa chini ya ulinzi wa kimungu. Hiyo itatimiza maneno aliyoyasema Yesu kuumalizia mfano: “Na hao [mbuzi wa mfano wasiowatendea mema “ndugu” za Kristo] wataondoka waende kwenye kukatiliwa mbali kwa milele [katika kifo], bali wenye uadilifu [wale kondoo wa mfano] kwenye uzima wa milele.” (Mathayo 25:’46, NW) Hao ndio ule “mwili” utakaookolewa uipite moja kwa moja ile “dhiki kuu ya namna ambayo haijatukia tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, la, wala haitatukia tena.” Kwa ajili ya ‘wachaguliwa’ wa Mungu (mabaki ya “Israeli wa Mungu”) siku za hiyo dhiki iliyo kubwa kupita dhiki zote za kidunia zitakatishwa ziwe fupi.—Mathayo 24:21, 22, NW.
19. “Mkutano mkubwa” utatoka katika nini, na watafanya nini na makao ya “Ufalme” ambamo wataingizwa?
19 Hivyo “mkutano mkubwa” wa watu wenye mfano wa kondoo ‘utatoka katika dhiki ile iliyo kuu’ uingie ndani ya makao ya kidunia yatakayokuwa yamesafishwa, ya Mfalme Yesu Kristo. (Ufunuo 7:9-14) Tangu mwanzo wa mfumo mpya wa mambo watakuwa na ushiriki katika kugeuza makao haya ya Ufalme yawe Paradiso ya kidunia ulimwenguni pote kama Muumba alivyoyakusudia yawe alipowapa amri ya kimungu wazazi wa ulimwengu mzima wa wanadamu, Adamu na Hawa.—Mwanzo 1:27-31; 2:5-9.
20. Kwa wakati wa sasa, watu hao wenye mfano wa kondoo wanafanya nini pamoja na mabaki, na ni maana gani ya ile “ishara” wanayoendelea kufuata, moja kwa moja mpaka “mwisho”?
20 Wakati wa sasa, wanapongoja kusikia ukaribishaji wa “Mwana wa Adamu” anayetawala katika utukufu wa kimbingu wenye kusema: “Njoni, mliobarikiwa na Baba yangu, urithini ufalme mliowekewa tayari tangu kuumbwa ulimwengu,” waadilifu hao wenye mfano wa kondoo wanaendelea kufanya kazi bega kwa bega na “Israeli wa Mungu.” (Mathayo 25:34) Wao wako kama Waisraeli hao wa kiroho ambao hawaachi kuwa na imani katika kile kinachomaanishwa na kumalizika kwa Nyakati za Mataifa mwaka wa 1914. Kwa hiyo, wao hawajifanyi kama kwamba hawaioni “ishara” inayoendelea kung’aa ya kuonyesha “kuwapo” kwa Masihi Yesu akiwa Mfalme, bali wanaitukuza huduma yao wakiwa raia zake wa kidunia halafu wanasonga mbele kwa furaha nyingi, wakizihubiri “habari njema hizi za ufalme” duniani pote wakati ule “mwisho” unapoendelea kukaribia mbio-mbio.—Mathayo 24:14, NW.
—Kutoka w8/l/83.
Wewe Unaweza Kujibu?
□ Utimizo wa sehemu zote za “ishara” iliyotabiriwa unahakikisha nini?
□ “Israeli wa Mungu” na wenzi wao wanashiriki katika utendaji gani?
□ “Mji mtakatifu” uliokanyagwa-kanyagwa “miezi arobaini na miwili” ni nini, na ni “Yerusalemu” gani ambao haukukanyagwa-kanyagwa?
□ Wakati kutenganishwa kwa kondoo na mbuzi wa mfano kutakapokamilishwa, itakuwaje kwa kila kimoja cha vikundi hivyo?
[Picha katika ukurasa wa 15]
Ni shuhuda gani zenye kuonekana ambazo Yesu alitabiri ili wafuasi wake wajue kwamba Nyakati za Mataifa zimekwisha?