Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 7/1 kur. 8-13
  • Ni Nani Awezaye Kuisoma “Ishara” Sawasawa?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ni Nani Awezaye Kuisoma “Ishara” Sawasawa?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Wakati Uliotiwa Alama ili “Ishara” Hiyo Itokee
  • Uwe Mwenye Shukrani—Ufalme wa Kimesiya wa Yehova Watawala
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • “Israeli wa Mungu” na Mwisho wa Nyakati za Mataifa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Lile Suala la Ufalme Lawekwa Mbele!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Mfalme Atawala!
    “Ufalme Wako Uje”
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 7/1 kur. 8-13

Ni Nani Awezaye Kuisoma “Ishara” Sawasawa?

“Enyi wanafiki, mwajua kuutambua uso wa nchi na mbingu; imekuwaje, basi, kuwa hamjui kutambua majira haya?”​—LUKA 12:56.

1, 2. Maadui wa Yesu wangaliweza kujua nini kwa kuangalia uso wa anga, lakini walishindwa kufahamu nini?

MABAHARIA wenye hekima wanajua jinsi ya kufasiri uso wa anga, na wanatii ishara zayo. Ni kama shairi moja linalojulikana sana linavyosema: “Anga jekundu usiku, ni furaha ya mabaharia,/ Anga jekundu asubuhi, enyi mabaharia jihadharini.”

2 Bwana Yesu Kristo alisema jambo kama hilo kwa njia yenye kutokeza zaidi alipokabiliwa na maadui wake. Kuhusu kabiliano hilo mwandikaji wa Injili Luka anaripoti hivi: “Akawaambia makutano pia, Kila mwonapo wingu likizuka pande za magharibi mara husema, Mvua inakuja; ikawa hivyo. Na kila ivumapo kaskazi, husema, Kutakuwa na joto; na ndivyo ilivyo. Enyi wanafiki, mwajua kutambua uso wa nchi na mbingu; imekuwaje, basi, kuwa hamjui kutambua majira haya?”​—Luka 12:54-56.

3. Ni “ishara” gani yenye kuthibitisha kwamba Yesu alikuwa Masihi ambayo maadui wake walishindwa kuifunika?

3 Maadui hao wenye kiburi wangeweza kutabiri hali ya hewa, lakini walikuwa wanafiki mno na wenye kukosa maarifa ya kiroho wasiweze kufahamu mambo yenye umaana mkubwa zaidi. Yesu alifanya ishara mbalimbali ambazo ziliwasaidia watu wenye mioyo minyofu wamwamini yeye. (Yohana 2:23) Lakini, hasa kifo chake Siku ya Kupitwa ya 33 W. K. na kufufuliwa kwake siku ya tatu ni mambo yaliyokuwa “ishara” yenye kuthibitisha kwamba alikuwa Masihi, au Kristo. (Mathayo 12:38-41; Luka 11:30) Kama ilivyo, maadui wa Yesu walijaribu kufunika “ishara” hiyo. (Mathayo 27:62–28:20; Matendo 4:1-4) Lakini kabla hajapaa kwenda mbinguni Wayahudi wenye kufikia 500 walipata kuwa mashahidi wa kufufuliwa kwake. (1 Wakorintho 15:3-6) Hali moja leo kuna “ishara” isiyoweza kufunikwa. Kuisoma sawasawa kunahusu uzima au kifo. Lakini “ishara” hiyo ni ipi? Na ni nani anayeweza kuisoma kwa usahihi?

Ishara” ya Siku Zetu

4. Leo, ni “ishara” gani inayoonekana, na baadhi ya sehemu zayo ni nini? (Mathayo 24:3)

4 Wanafunzi wa Yesu walikuwa wamemuuliza hivi: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” (NW) Katika kujibu, Kristo alitabiri mambo yafuatayo kwa kadiri isiyopata kuonekana tena: vita, upungufu wa chakula, matetemeko ya ardhi, na sehemu nyingine za “ishara” ya “kuwapo” kwake kusikoonekana katika uwezo wa Ufalme. Sehemu moja kuu ni kazi ya duniani pote ya kuuhubiri Ufalme ambayo sasa inafanywa katika nchi 203 na mashahidi wa Yehova zaidi ya 2,840,000. Vichapo vya Sosaiti yetu mara nyingi vimetaja jambo hilo na ushuhuda mwingine mwingi ambao sasa unatimiza “ishara” ya “kuwapo” kwa Yesu.​—Mathayo, sura za 24, 25; Marko, sura ya 13; Luka, sura ya 21.

5. Ni kwa sababu gani Yesu hakuwa akitilia chumvi kisa hicho alipowaita Wayahudi wa karne ya kwanza “kizazi kibaya na cha zinaa”?

5 Ni jambo lisiloweza kukanushika kwamba tangu kutokea kwa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza mwaka 1914 ushuhuda wa kutimizwa kwa “ishara” umekuwa ukiongezeka. Jambo hilo lapasa kuwa na umaana gani kwetu? Hatutaki kuwa kama Wayahudi wa karne 19 zilizopita ambao walikuwa watabiri wazuri wa hali ya hewa, lakini wakapuuza ushuhuda uliokuwa wazi machoni pao na hawakutaka kukata maneno kama ulivyoonyesha. Wakati mrefu kabla ya hapo, Mungu alikuwa amempa Musa uwezo wa kufanya ishara tatu za kuthibitisha mamlaka yake ya kimungu kwa Waisraeli waliokuwa wakiteseka. (Kutoka 4:1-31) Lakini wakiwa na ishara zinazozidi tatu, Wayahudi wa kizazi hicho cha karne ya kwanza hawakuwa na nia ya kukubali kuwa ndiye Masihi Yule aliye mkubwa zaidi ya Musa. (Yohana 4:54; Waebrania 2:2-4) Kwa hiyo Yesu hakuwa akiongezea chumvi kisa hicho alipowaita “kizazi kibaya na cha zinaa.”​—Mathayo 12:39.

6. Watu wenye maarifa wanasema nini sasa kuhusu hali za ulimwengu?

6 Watu wa kizazi hiki cha karne ya 20 wasiotaka au wasiosadiki kuja kwa pili kwa Yesu Kristo hawaisomi sawasawa “ishara” ya mwisho wa mfumo huu. Lakini hali za wakati huu si zenye kutia moyo hata kidogo, kama inavyoonyeshwa na mitajo ya habari ifuatayo:

“Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Javier-Perez de Cuellar amesema kwamba ulimwengu umeingia katika kipindi cha hatari sana katika matukio ya mambo ya kimataifa, na mwelekezo wa kuelekea kwenye utaratibu wa kimataifa wenye haki, amani na ulio imara yaonekana umedhoofishwa. . . . ‘Kule . . . kupungua kwa kutumainiana kati ya mataifa kunatokeza udongo wenye rutuba unaozalisha wasiwasi na ugomvi,’ akasema Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa.”​—Indian Express, Oktoba 22, 1983.

“Wengi wetu tumekuwa tukisema kwa miaka mingi kwamba vita ya nyukilia ingeua mamilioni za watu wasio na hatia na ingefanya sehemu kubwa za ulimwengu ziwe zisizokalika na watu . . . Kikundi kimoja cha wanasayansi wenye kuheshimiwa kimefikia mkataa wenye mabaya hata zaidi​—kwamba vita ya nyukilia, au hata mpambano mmoja mkubwa kati ya mataifa yenye nguvu zaidi, ungetokeza msiba wa hali ya hewa ulimwenguni pote ambao nao ungeua mabilioni wala si mamilioni na yawezekana ungekomesha uhai wa kibinadamu duniani. Uchunguzi huo wa miaka miwili ulitayarishwa kwa ajili ya Mkutano unaohusu Matokeo ya Muda Mrefu Yenye Kuhusu Viumbe Ulimwenguni Pote ya Vita ya Nyukilia. Maneno yake ya mkataa yalitiwa sahihi na wanasayansi zaidi ya 100 . . . Carl Sagan . . . alionyesha matokeo ya vita ya nyukilia kwa uwazi sana: ‘Kumalizwa kwa viumbe wa kibinadamu kungekuwa uwezekano halisi.’”​—The Express (Easton, Pa.), Novemba 3, 1983.

7. Wenye kupenda maisha katika ulimwengu bora wanapaswa kuangalia wapi wapewe uhakikisho?

7 Hayo ni maoni yasiyotumainisha ya waelezaji fulani wenye kutegemeka walio wajuzi. Mambo ni yenye kukatisha tamaa hasa kwa sababu hawawezi kuonyesha njia ya kutoka kwenye msiba huo wanaotangulia kuuona. Kwa uhakika, wenye kupenda uhai katika ulimwengu ulio bora wanataka habari yenye kutoa tumaini. Kwa furaha, kuna njia ya kutoka kwenye msiba huo wa ulimwengu unaokaribia, kwa maana kulikuwako waokokaji wa hatari ya dunia nzima iliyokuwa ikitisha jinsi iyo hiyo. Kama kusingalikuwako waokokaji wa Gharika katika siku za Noa, sasa dunia haingekuwa imejawa na wakaaji wa kibinadamu zaidi ya bilioni 4! Ni kitabu kimoja tu​—Biblia Takatifu​—kinachotupa masimulizi sahihi ya jinsi wanadamu wanane tu, pamoja na namna namna za wanyama, walivyookoka msiba huo wa dunia yote.

8. Tofauti na wengine, wanafunzi wa Yesu walipaswa kufanya nini wakati ukikaribia mfumo wa mambo wa sasa uondolewe?

8 Kwa kuwa kitabu icho hicho chenye kutegemeka kinatupa maelezo ya Yesu ya hali ambazo zingekuwako duniani wakati ambao mfumo wa mambo wa sasa unaoanguka ungeondolewa, je, hatupaswi kujaribu kusoma “ishara” hiyo sawasawa? Miaka 37 kabla Yerusalemu haujaharibiwa na majeshi ya Waroma mwaka wa 70 W.K., Yesu alitoa orodha hiyo ndefu ya sehemu za “ishara” yenye mambo mengi ambayo ingetangulia msiba wa duniani pote uliofananishwa na Gharika. Na kati ya mambo mengine, alisema: “Kutakuwako ishara katika jua na katika mwezi na katika nyota, na duniani huzuni kuu ya mataifa, wasijue njia ya kutokea kwa sababu ya uvumi wa bahari na msukosuko wake, huku wanadamu wakizimia moyo kwa sababu ya hofu na kwa kutazamia mambo yanayokuja juu ya dunia inayokaliwa na watu; kwa maana nguvu za mbingu zitatikiswa. Na kisha wataona Mwana wa mtu akija katika wingu na uwezo na utukufu mwingi. Lakini mambo hayo yaanzapo kutokea, jiinueni wima na kuinua vichwa vyenu juu, kwa sababu ukombozi wenu unakaribia.”​—Luka 21:25-28, NW.

9. Tangu 1895 mpaka 1931, mgawo wa gazeti hili ulionyeshwaje kwenye jalada lake la mbele?

9 Sehemu ya unabii huo ilitokea kwenye jalada la mbele la matoleo ya Mnara wa a Januari 1, 1895, hadi Oktoba 1, 1931. Juu ya mtajo huo wa Biblia kulikuwako mnara wa mlinzi wenye kutupa miale ya nuru, huku bahari iliyochafuka ikiupiga msingi wa mwamba ambao juu yake ulikuwa huo mnara wa mlinzi. Kwa hiyo gazeti hili lilionyesha mgawo walo katika kizazi ambacho washiriki wacho wangali hai na wangali wanasoma toleo ili hili la gazeti.

10. Tunaweza kuepukaje kuwa na woga walio nao viongozi wa kibinadamu leo?

10 Leo, wataalamu wa mambo yanayoendelea, ambao mioyo yao inazimia kwa woga, wanafafanua kivyao sehemu za “ishara” hiyo yenye mambo mengi. Lakini mfafanuzi wetu aliye bora zaidi ni Yesu Kristo, na tukikamatanisha “ishara” hiyo na umaana ambao aliipa, hatutapatwa na woga ulio kawaida ya viongozi wa kibinadamu ambao hawajui njia ya kutoka kwenye mvurugo wa ulimwengu uliopo wakati huu. Badala yake, tutafurahi kwa sababu ukombozi wetu katika mfumo huu mbovu unakaribia.

Wakati Uliotiwa Alama ili “Ishara” Hiyo Itokee

11. Yesu alionyeshaje kwamba matukio ya ulimwengu yenye kuonyesha mwisho yangetokea kwa wakati wake kabisa?

11 Matukio ya ulimwengu yanatokea kwa wakati wake kabisa. Jinsi gani hivyo? Kabla Yesu hajatoa unabii ulioandikwa katika Luka 21:25-28, alitabiri kuharibiwa kwa pili kwa Yerusalemu. Kwa kutimiza maneno yake, uharibifu ulitokea mwaka wa 70 W.K. Kwa habari ya Wayahudi waliookoka, Yesu alisema: “Wataanguka kwa makali ya upanga na kuchukuliwa mateka katika mataifa yote; na Yerusalemu utakanyagwa na mataifa, mpaka nyakati zilizowekwa za mataifa zitakapotimizwa.” (Luka 21:24, NW) Nyakati hizo zilimalizika wakati gani? Mengi zaidi yanahusika kuliko yale yaliyoupata Yerusalemu wa kidunia. Kwa hiyo tarehe ambayo Waisraeli wa kisasa walitwaa mji wa kale wenye kuta wa Yerusalemu, wala uhakika wa kwamba ndio mji mkuu wa taifa huru la kisasa la Israeli, silo jambo linaloamua. Orodha ya mambo ya Mungu ndiyo inayoamua!

12. Nyakati za Mataifa zilianza wakati gani, zilikuwa zenye urefu gani, na zilimalizika wakati gani?

12 Waroma walio watu wa mataifa walianza kuukanyaga Yerusalemu mwaka wa 63 K.W.K. Lakini kabla yao Mataifa: Wagiriki, Waajemi, na Wababuloni walikuwa wameukanyagia chini huo “mji wa Mfalme mkuu” Yehova. (Mathayo 5:34, 35) Wababuloni waliuharibu pamoja na hekalu lao mwaka wa 607 K.W.K. Tangu wakati huo kuendelea, kukanyaga kwa Mataifa juu ya kilichoufananisha Ufalme wa Mungu kulianza, na Nyakati za Mataifa zikaanza hasa. Nyakati za Mataifa hizo zingekuwa saba, kila wakati mmoja ukilingana na mwaka wa kiunabii wa siku 360. Kwa msingi wa “kila siku kuhesabiwa mwaka,” “nyakati saba” zote zingekuwa jumla ya miaka 2,520. (Danieli, sura ya 4; Hesabu 14:34; Ezekieli 4:6) Kuanzia na kufanywa ukiwa kwa Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K., zingemalizika mwaka wa 1914 W.K.

13. Ni tangu wakati gani wanafunzi wa Biblia walijua tarehe ya Nyakati za Mataifa kumalizika?

13 Mapema mwaka wa 1880, gazeti Mnara wa Mlinzi lilisema kwamba Nyakati za Mataifa zingeendelea mpaka mwaka wa 1914. Halafu kilipochapishwa kitabu The Time Is at Hand mwaka wa 1889, wanafunzi wa Biblia duniani pote walitahadharishwa zaidi juu ya uhakika wa kwamba Nyakati za Mataifa zingekwisha katika vuli ya 1914.

14. Yajapokuwa yaliyoupata Yerusalemu mwaka wa 1948, ni kwa sababu gani tunaweza kusema kwamba Nyakati za Mataifa zilimalizika mwaka wa 1914?

14 Basi, katika mwaka huo, je, Yerusalemu wa kale uliacha kukanyagwa na wasio Wayahudi, au Mataifa? Hapana, kwa maana mwaka wa 1914 mji huo wa kihistoria ulikuwa ungali mikononi mwa Milki ya Uturuki, rafiki ya Ujeremani ya kibepari. Katika Desemba 9, 1917, ulitwaliwa kutoka kwa Waturuki na majeshi ya Waingereza yakiongozwa na Jemadari Allenby. Yerusalemu uliendelea kuwa chini ya utawala wa Uingereza kwa amri ya Ushirika wa Mataifa mpaka mwaka wa 1948. Halafu Wayahudi wakaasi na kuteka sehemu ya magharibi ya Yerusalemu wa kisasa nje ya mji wa kale wenye kuta. Mji wenye kuta ulitwaliwa na wafuasi wa Muhamadi. Basi, tunawezaje kusema kwamba Nyakati za Mataifa zilimalizika mwaka wa 1914? Kwa sababu katika mwaka huo serikali ya Mfalme mkuu Yehova ilizaliwa mbinguni.

15, 16. (a) Yerusalemu wa kale uliacha kuwa “mji wa Mfalme mkuu” Yehova wakati gani, lakini kuna Yerusalemu gani uliokwezwa juu zaidi? (b) Basi, ni wapi ambapo Yehova angemtawaza Yesu Kristo kuwa Mfalme?

15 Yesu alipokuwa duniani, hekalu la Mungu lilikuwa katika Yerusalemu, na Yesu aliabudu huko. Kwa hiyo wakati huo Yerusalemu ungeweza kuitwa “mji wa Mfalme mkuu” Yehova. (Mathayo 5:34, 35) Lakini kwa uhakika wakati wa kuraruliwa kwa kimuujiza kwa pazia la hekalu la ndani kwenye kifo cha Yesu Siku ya Kupitwa ya mwaka 33 W. K., uliacha kuwa mji wa kifalme wa Yehova. Kuharibiwa kwa Yerusalemu na hekalu lake na Waroma walio Mataifa mwaka wa 70 W.K. kulithibitisha uhakika huo. Kwa furaha ya Wakristo Wayahudi wa wakati huo, na ya Wakristo wote tangu wakati huo, kuna Yerusalemu mwingine, uliokwezwa zaidi, “Yerusalemu wa mbinguni.”​—Waebrania 12:22.

16 Kwa kupatana na uhakika huo, unabii wa Yesu ulioandikwa katika Luka 21:24 ulianza kutimizwa juu ya Yerusalemu wa kidunia lakini ni lazima umalizike ukihusiana na “Yerusalemu wa mbinguni.” Ndiyo, kwa maana “Yerusalemu wa mbinguni” umechukua mahali pa Yerusalemu wa kidunia ukawa “mji wa Mfalme mkuu” Yehova Mungu. Huko, katika “mji” huo wa kimbingu, ndipo palipokuwa mahali pa “Mfalme mkuu” Yehova kumtawaza Mwanaye aliyetukuzwa Yesu Kristo mwishoni mwa Nyakati za Mataifa mwaka wa 1914.

17. Mwishoni mwa Nyakati za Mataifa, ni amri gani ya kimungu aliyopewa Mfalme Yesu Kristo aliyetawazwa, na ni nani waliojitoa wenyewe kwa moyo wa kupenda watumikie?

17 Huo ulikuwa ndio wakati uliowekwa wa kimungu wa Yehova kumpa Mwanaye aliyetawazwa Yesu Kristo amri iliyomo katika maneno ya Zaburi 110:2, 3, (NW): “Fimbo ya nguvu zako Yehova ataituma toka Sayuni, akisema: ‘Nenda hali ukitiisha katikati ya adui zako.’ Watu wako watajitoa wenyewe kwa moyo wa kupenda siku ya jeshi lako la vita. Katika fahari za utakatifu, kutoka tumbo la uzazi la mapambazuko, unalo shirika la wanaume vijana kama matone ya umande.” Kwa kutimiza unabii huo, “watu,” walio wakfu ambao walifuata hatua za Yesu na kutambua, mwisho wa Nyakati za Mataifa mwaka wa 1914 walijitoa kwa moyo wa kupenda ili watumike wakiwa watangazaji wa utawala uliotoka kuanza wa Yehova Mungu katika Sayuni wa kimbingu kupitia Bwana Yesu Kristo. Lakini yanayoitwa mataifa ya Kikristo hayakujitiisha kwa moyo wa kupenda kwa Mfalme aliyetoka kutawazwa wa Yehova. Kwa kweli, walithibitisha kuwa ni “adui” zake, kwa maana walishiriki katika vita ya ulimwengu ya kwanza ya historia ya kibinadamu kwa ajili ya suala la utawala wa ulimwengu. Ulimwenguni pote pia waliweka vikwazo kwa utangazaji wa Ufalme wa Mungu.

18. Katika mwaka wa 1918, kulikuwa na uthibitisho gani wa uadui dhidi ya Ufalme wa Mungu?

18 Uadui dhidi ya Ufalme wa Mungu ulionekana wazi hasa mwaka wa 1918. Katika Mei 8, 1918, mhariri wa gazeti Mnara wa Mlinzi na hesabu fulani ya wafanyi kazi wenzake walikamatwa wakati ambao vita ilikuwa ikiwaka sana. Baadaye, katika Juni 21, walihukumiwa miaka mingi ya kifungo katika gereza la taifa katika Atlanta, Georgia, U.S.A. Ni baada ya vita kumalizika tu na wakiwa wamekaa miezi tisa gerezani ndipo wahudumu hao wa Ufalme wa Mungu walipoachiliwa kwa dhamana. Baada ya muda, mashtaka yote ya uwongo waliyokuwa wamebandikwa yalitupiliwa mbali.

19. Baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, Muungano wa Baraza la makanisa ya Amerika ulichukua msimamo gani kuelekea Ushirika wa Mataifa?

19 Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilimalizika Novemba 11, 1918, na katika mwezi uliofuata Muungano wa Baraza la Makanisa ya Kristo katika Amerika ulitangaza waziwazi kwamba ulikuwa unaunga mkono Ushirika wa Mataifa uliopendekezwa wakati huo. Baraza hilo la kidini lilitangaza kwamba Ushirika ulikuwa ni “wonyesho wa kisiasa wa Ufalme wa Mungu duniani.” Ikipuuza pendekezo hilo la kidini, kwa ajili ya sababu za kisiasa United States ya Amerika ilikataa kujiunga na Ushirika huo, ikajiunga tu na Mahakama ya Ulimwengu. Hata hivyo Ushirika huo ulianza kutenda mwanzoni mwa 1920, na washiriki wa Muungano wa Baraza la Makanisa ukaubariki na kuuunga mkono.

20. Watu wa Yehova walichukua msimamo gani kuuelekea Ushirika huo, nao walianza kutangaza nini?

20 Kwa upande mwingine, gazeti Mnara wa Mlinzi na watu wa Yehova wenye kulieneza walikataa kutambua Ushirika wa Mataifa kuwa kitu cha kisiasa kilicho badala ya Ufalme wa Mungu. Hawakuutambua kamwe kuwa ndio utimizo wa sala ya kielelezo aliyofundisha Yesu Kristo: “Ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.” (Mathayo 6:9, 10) Hawakujitoa watumikie kitu hicho kilichofanywa na wanadamu kiwe badala ya Ufalme wa Mungu, kisingizio! Badala yake, walitoa utii wao kamili kwa Ufalme wa Mungu wa halisi mikononi mwa Yesu Kristo katika “Yerusalemu wa mbinguni.” Kwa msaada wa Mungu walikuwa wamesoma sawasawa “ishara” ya “kuwapo” kwa Yesu na “umalizio wa mfumo wa mambo.” Kwa hiyo wakatoka watangaze Ufalme ulimwenguni pote.

Jibu Lako Ni Nini?

◻ Ni “ishara” gani inayoonekana leo, na ni zipi baadhi ya sehemu zayo?

◻ Tunaweza kuepukaje woga walio nao sasa viongozi wa kibinadamu wenye ujuzi?

◻ Nyakati za Mataifa zilianza wakati gani na zilikwisha wakati gani?

◻ Yehova amemtawaza Yesu Kristo awe Mfalme katika “Yerusalemu” gani?

◻ Watu wa Yehova walikuwa na maoni gani juu ya Ushirika wa Mataifa?

[Chati katika ukurasa wa 11]

Oktoba, 607 B.C.E. — Oktoba, 1 K.W.K. = miaka 606

Oktoba, 1 B.C.E. — Oktoba, 1914 C.E. = miaka 1,914

NYAKATI SABA ZA MATAIFA = miaka 2,520

[Picha katika ukurasa wa 10]

Wale wanaoisoma “ishara” sawasawa wanaweza kuokoka mwisho wa huu mfumo, sawa na watu wanane walivyookoka Gharika

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki