“Mjawe na Furaha Milele”
1. (a) Ni nini “mji” unaotajwa na Waebrania 11:10? (b) Ni mpaka wakati gani “kundi kubwa” linapaswa kungojea “utimizo wa ile ahadi”?
KWA kweli, tunaweza kujawa sana na furaha kwamba Mfalme wa Kimasihi, Kristo Yesu, anatawala sasa katika “Yerusalemu” wa kimbingu. Huo ndio mji ‘wa mbinguni’ unaotajwa katika Waebrania sura ya 11, ambao kwa ajili yao Abrahamu, Isaka na Yakobo walijinyosha ‘waufikie.’ ‘Walikiri mbele ya watu kwamba walikuwa wageni, na wasafiri juu ya nchi’ ya Kanaani, kwa maana kwa bidii walikuwa wakiutafuta “mji wenye misingi ya kweli kweli, ambao mjenzi na mfanyi wao ni Mungu.” Lakini kama vile ilivyo kwa “kundi kubwa,” ambao leo wana tumaini la kupata uzima wa milele duniani, ni lazima “utimizo wa ile ahadi” kwa watu hao wa kale ungoje mpaka Wakristo waliotiwa mafuta wapokee urithi wao katika Ufalme wa kimbingu.—Waebrania 11:8-16, 39, 40; Ufunuo 7:9, NW.
“Yerusalemu wa mbinguni”
2. (a) Waebrania 12:1, 2 inaonyeshaje tumaini la Ufalme wa Kimasihi? (Zaburi 110:1, 2) (b) Kuja kwa Ufalme kulitangulia kufananishwaje huko Mlima Sinai?
2 Waebrania sura ya 12 inaendelea kuwatia moyo Wakristo waliotiwa mafuta wafaidike kutokana na mfano wa hao mashihidi waaminifu wa nyakati za kale, na pia ‘kumtazama sana yule Wakili Mkuu Zaidi na Mkamilishaji wa imani yetu, Yesu,’ ambaye, baada ya kuvumilia, ‘aliketi mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Mungu’ mpaka “majira ya Mataifa” ya malizike. (Waebrania 12:1, 2, NW) Halafu, akikazia tumaini la kupata Ufalme la Wakristo hao, Paulo anasimulia mawonyesho ya kuogopesha ya utukufu wa Yehova yaliyoonekana kwenye Mlima Sinai wakati wa kuanzishwa kwa agano la Torati pamoja na Israeli wa kimwili. Wakati huo ndipo Yehova alipowaambia Israeli hivi: “Ikiwa mtaitii sauti yangu kweli kweli, na kulishika agano langu, . . . mtakuwa kwangu ufalme wa makuhani, na taifa takatifu.”—Kutoka 19:5, 6.
3. Ni kwa njia gani Waisraeli wa kiroho ‘wamefikilia’ kitu cha kuogopesha zaidi?
3 Lakini, Waisraeli wa kiroho, yaani Wakristo wa leo waliotiwa mafuta, wamo katika “agano jipya.” (Waebrania 8:8-11) Na sasa ‘wamefikilia’ kitu chenye kuogopesha zaidi. Kitu gani? Paulo anajibu kwenye Waebrania 12:22: “Mmeufikilia mlima Sayuni, na mji wa Mungu aliye hai, Yerusalemu wa mbinguni.” Mfikilio huo ulikuwa umeanza na warithi wa Ufalme wa siku za Paulo, kwa kuwa walikuwa ‘wamejengwa wawe nyumba ya kiroho’ juu ya msingi, Kristo Yesu, ambao sasa ulikuwa umewekwa katika Sayuni. (1 Petro 2:4-9) Wakristo wengine watiwa mafuta wangeendelea kuufikilia Yerusalemu wa kimbingu mpaka wale 144,000 wote wakusanywe kwa Mwana-Kondoo, wasimame naye juu ya Mlima Sayuni wa kimbingu.—Ufunuo 14:1-5.
4. Kuhusiana na Ufalme wa Kimasihi, ni sehemu gani nyingine ambazo Wakristo watiwa mafuta ‘wamefikilia’?
4 Hapa katika Waebrania 12:22-24, Paulo anaeleza sehemu nyingine pia ambazo Wakristo ‘wamefikilia,’ na ambazo zina uhusiano na Ufalme wa Kimasihi na kusudi la Ufalme huo. Anataja kuwapo kwa “makumi elfu ya malaika” (NW), ambao Danieli 7:9-14 na hata Mathayo 25:31 inaonyesha wanakuwapo wakati Yule “aliye mfano wa mwanadamu” anapoupokea Ufalme. Pia Paulo anataja “kanisa la wazaliwa wa kwanza” wanaorithi Ufalme. Yeye anamtukuza Mungu kuwa “mwamuzi wa watu wote,” ambaye anawatangaza hao ‘wana wazaliwa wa kwanza’ kuwa wenye uadilifu au haki, ili waweze kuingizwa ndani ya agano jipya ambalo Yesu alipatanisha kupitia damu yake mwenyewe yenye thamani. (Waebrania 9:13-15; Warumi 5:1, 9) Paulo anataja pia ‘maisha za kiroho za hao waadilifu’ (NW), yaani warithi wa Ufalme, ambao sasa wanatembea katika “upya wa uzima.”—Warumi 6:4; 8:16.
5. (a) Waebrania 12:28, 29 inaonyeshaje wazi kwamba “Yerusalemu wa mbinguni” ndio Ufalme wa Kimasihi? (b) Ni kwa njia gani Waebrania 13:14, 15 inaonyesha kwamba “mji” huo bado haujafika?
5 Kwamba “Yerusalemu wa mbinguni” unaotajwa katika Waebrania 12:22 unamaanisha Ufalme wa Kimasihi ambao Wakristo ‘wameufikilia’ inazidi kuonyeshwa wazi na mistari inayofuata, 28 na 29, ambapo Paulo anawatia moyo hao, akisema: “Basi kwa kuwa tunapokea ufalme usioweza kutetemeshwa, na tuwe na neema, ambayo kwa hiyo tumtolee Mungu ibada ya kumpendeza, pamoja na unyenyekevu na kicho; maana Mungu wetu ni moto ulao.” Onyo hilo la upole linalowatia juhudi katika ‘kuufikilia’ Yerusalemu wa kimbingu, au Ufalme wa Kimasihi, linaendelea kutolewa mpaka mwisho wa barua ya Paulo, kama tunavyosoma katika sura ya mwisho, yaani, Waebrania 13:14: “Maana hapa hatuna mji udumuo, bali twautafuta ule ujao.” Sasa Ufalme huo umekuja—katika ule mwaka wa 1914 wenye kuanza kipindi kipya chenye badiliko! Basi inawapasa watiwa mafuta waliosalia duniani wawe na bidii nyingi sana katika ‘kuutafuta kwanza ufalme’ na kumtolea Yehova sikuzote “dhabihu ya sifa daima, yaani, tunda la midomo iliungamayo jina lake”!—Mathayo 6:33; Waebrania 13:15.
“Yerusalemu mpya”
6. (a) Kama inavyoelezwa katika Ufunuo, “Yerusalemu mpya” ni nini? (b) Kwa sababu gani “kundi kubwa” linapaswa kupendezwa sana na “Yerusalemu” huo?
6 Basi, namna gani juu ya “Yerusalemu mpya,” ambao kwa mara ya kwanza unatajwa kwenye Ufunuo 3:12? Hapo Yesu aliyetukuzwa anasema hivi juu ya “yeye ashindaye”: “Nitamfanya kuwa nguzo katika hekalu la Mungu wangu, . . . nami nitaandika juu yake jina la Mungu wangu, na jina la mji wa Mungu wangu, huo Yerusalemu mpya, ushukao kutoka mbinguni kwa Mungu wangu.” Baadaye, kwenye Ufunuo 21:1, 2 na 10, Yohana anawataja washindaji hao wakiwa katika “mbingu mpya” kisha anaeleza kwamba kikundi chao kilichojumlika katika jamii moja ni “mji ule mtakatifu, Yerusalemu mpya, ukishuka kutoka mbinguni kwa Mungu, umewekwa tayari, kama bibi-arusi aliyekwisha kupambwa kwa mumewe,” Kristo yule bwana-arusi. Yerusalemu Mpya huo ndicho chombo ambacho Mungu anatumia kutiririsha “maji ya uzima” yawafikie wanadamu watiifu, kwa kuwa wanaponywa na kufikishwa kwenye ukamilifu wa uzima hapa duniani. Hivyo Mungu, aliye Mwanzishi wa mpango bora sana huo, atatumia njia halisi ‘kufuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena.’ Hakika “kundi kubwa,” walio wenzi wa mabaki ya jamii ya “bibi-arusi,” wanashangilia sana taraja hilo!—Ufunuo 22:1, 2; 21:4.
7. “Yerusalemu mpya” unatofautianaje na “Yerusalemu wa mbinguni”?
7 Lakini, pana tofauti kidogo kati ya “Yerusalemu mpya” unaoelezwa katika Ufunuo na “Yerusalemu wa mbinguni” unaotajwa katia kitabu cha Waebrania kwa sababu “Yerusalemu mpya” ni wale 144,000 walioposwa kuwa mke wa bwana-arusi, hali “Yerusalemu wa mbinguni” ni 144,001, huyo “mmoja” aliyeongezeka kwenye hesabu hiyo akiwa ndiye Mfalme aliye bwana-arusi. Hivyo vitabu vya Biblia vya Waebrania na Ufunuo vinaonyesha ufanani unaokaribiana kati ya “Yerusalemu wa mbinguni” na “Yerusalemu mpya.”
“Yerusalemu wa juu”
8, 9. (a) “Yerusalemu wa juu” ni nani au nini? (b) Kwa kutaja maneno ya Isaya 54, Paulo anaelezaje utendaji kama wa mke wa mji huo?
8 Kwenye Wagalatia 4:26 tunasoma habari za “Yerusalemu” mwingine pia. Huo ndio “Yerusalemu wa juu.” Mji huo ni nani? Mtume Paulo anasema hivi juu yao: “Yerusalemu wa juu ni mwungwana [ni huru], naye ndiye mama yetu sisi.”—Linganisha Isaya 54:13.
9 Huyo “Yerusalemu wa juu” ni tengenezo la Yehova lililo kama mwanamke katika mbingu. Hilo lina makundi ya malaika washikamanifu, kutia ndani yule malaika mkubwa kupita wote ambaye sasa ametukuzwa, Yesu Kristo. (Ufunuo 12:7) Hao wanatumikia katika cheo cha “mke” kwa Bwana Mwenye Enzi Kuu wao. Kwa habari ya “mwanamke” (NW) huyo Paulo anaendelea kusema hivi: “Imeandikwa [yaani, kwenye Isaya 54:1], Furahi, wewe uliye tasa, usiyezaa; paza sauti, ulie, wewe usiye na utungu; maana watoto wake aliyeachwa pekee ni wengi kuliko wa huyo aliye na mume.”—Wagalatia 4:27.
10. “Yerusalemu wa juu” ulikujaje ‘kupaza sauti’ ya furaha?
10 Katika utimizo wa unabii huo, bila shaka “mke” wa Yehova, tengenezo kuu lake la kimbingu la viumbe vya kiroho, lilipaza sauti ya furaha kumwona Kristo Yesu akizaliwa kuwa “uzao” ulio mkuu wakati wa ubatizo wake mwaka wa 29 W.K. Bila shaka furaha hiyo ilifurika wakati Yesu mshika-ukamilifu alipoinuliwa kwa wafu mwaka wa 33 W.K. na kutukuzwa mpaka mkono wa kuume wa Mungu katika mbingu. Halafu, ikawa furaha gani kuuona “uzao” huo ukiongezeka kuwa na washiriki wengi kwa kuwa wanafunzi wa Yesu Kristo walitiwa ndani pia, wawe watoto wa kiroho wa mke huyo! Hayo yote yalitimiza ahadi ya Mungu kwa Abrahamu kwamba Yeye ‘angezidisha uzao wake’ ili ubariki mataifa yote ya dunia.—Mwanzo 22:15-18; Wagalatia 3:29.
11. Katika nyakati za kisasa, “Yerusalemu wa juu” umefurahishwaje?
11 Mwaka wa 1914 W.K., mbingu zilifurahi pia kuona “mwanamke” wa Mungu akizaa “mtoto mwanamume,” Ufalme wa Kristo. Na wakati Kristo yule Mfalme (anayeitwa Mikaeli pia, maana yake “Ni Nani Aliye Kama Mungu?”) alipoujibu mwito wa ushindani wa Shetani kwa kumvurumisha Ibilisi na malaika zake kutoka makao ya kimbingu, bila shaka kundi kubwa la malaika lilifurahi kweli kweli likishangilia ile “sauti kuu’ iliyotangaza hivi: “Kwa hiyo shangilieni, enyi mbingu, nanyi mkaao humo”! Walifurahi sana, pia, tangu mwaka wa 1919 na kuendelea, kuona “wana” waliosalia duniani wa “Yerusalemu wa juu” wakitenganishwa kabisa na dini ya Kibabuloni. (Ufunuo 12:1-12; 18:4, 5) Na sasa, wakati wakombolewa hao wanapofanya mfikilio wao wa mwisho kwenye “Yerusalemu wa mbinguni,” Ufalme wa Kimasihi, halaiki za malaika washikamanifu wa “Yerusalemu wa juu” wanafurahi weee!—Isaya 62:11; Ufunuo 19:7.
“Mbingu Mpya na Dunia Mpya”
12. (a) Ni “Yerusalemu” upi unaotajwa kwenye Isaya 65:17, 18? (b) “Yerusalemu mpya” unahusianaje na “mbingu mpya,” nao unafanya utumishi gani?
12 “Yerusalemu wa juu,” yaani, tengenezo la Mungu lililo kama mke wake, linashangilia yote ambayo mume walo Bwana Mwenye Enzi Kuu, Yehova, anatimiza, Lakini, acheni sasa tuchunguze Isaya 65:17-19 (NW). Hapo unabii unataja kwamba Yehova anaumba kitu kipya. Basi, bila shaka “Yerusalemu” huu ni ule “Yerusalemu mpya” ambao sasa unazaliwa ukiwa “binti Sayuni,” aliyeposwa kwa Mfalme-Bwana-Arusi, Yesu Kristo ili aolewe. (Isaya 62:11) Yehova anasema hivi juu ya “bibi-arusi” wake: “Mimi ninaumba Yerusalemu uwe sababu ya kujawa na furaha na watu wao wawe sababu ya shangwe.” Huyo “bibi-arusi” wa kimbingu anafurahi furaha kubwa kwa kutimiziwa washiriki wake wote 144,000, na kwa kuona pia Mungu akiumba “dunia mpya”—jamii ya kitheokrasi iliyoungana kati ya wanadamu.—Ufunuo 21:1-5.
13, 14. (a) Kwa sababu gani sasa mwaliko (ukaribishaji) wa ‘kushangilia’ unatokezwa? (b) Ni maono gani yenye utukufu yanayoonyeshwa kwenye Ufunuo 21:9-27? (c) Tuna sababu gani ya kuuchukua “Yerusalemu mpya” kuwa “sababu ya kujawa na furaha”?
13 Ni watu wote wa Mungu wanaopelekewa mwaliko huu: “Shangilieni, enyi watu, na mjawe na furaha milele katika kile ninachoumba.” Hakuna sababu ya kuwazuia wasishangilie! Kwa maana, baada ya muda mfupi, Yehova ataliondolea lawama jina lake maarufu kwa kuwaharibu wapinzani wote. (Zaburi 83:17, 18) Hapo ndipo zile “mbingu mpya” zitakapoushika usukani wote (zitaongoza mambo)! Halafu Ufunuo 21:9-27 unaonyesha maono yenye utukufu sana juu ya “ule mji mtakatifu, Yerusalemu [“bibi-arusi” wa Mwana-Kondoo, Yesu], ukishuka kutoka mbinguni kwa Mwenyezi Mungu; wenye utukufu.” Ukiwaka kwa kumeremeta kila namna ya kito cha thamani, kwa njia ya mfano, na kumulikwa na utukufu wa Mungu mwenyewe, huo Yerusalemu Mpya unatimiza vizuri sana wajibu wao wa kutolea “mataifa” ya wanadamu “maji ya uzima,” yanayotiririka kutoka “kiti cha enzi cha Mungu, na cha Mwana-Kondoo.”—Ufunuo 22:1, 2, 17.
14 Basi, limekuwa jambo lenye kufaa Yehova akasema hivi kuhusu “Bibi-arusi, mke wa Mwana-Kondoo,” ambaye anaingizwa pamoja na Kristo, bwana-arusi wake, ndani ya “mbingu mpya” za kiserikali: “Kwa maana mimi ninaumba Yerusalemu uwe sababu ya kujawa na furaha na watu wao wawe sababu ya shangwe.” (Isaya 65:18, NW) Lakini ile “dunia mpya” inaingiaje katika furaha hiyo?
“Dunia Mpya” Yafurahi Sana
15. Misingi ya “dunia mpya” imewekwaje?
15 Si katika mbingu pekee ambako Yehova ametokeza “sababu ya shangwe.” Amefanya hivyo hata papa hapa duniani. Hiyo ni kwa sababu ameweka misingi ya “dunia mpya,” jamii ya kimungu kati ya wanadamu ambayo itapanuka mpaka mwishowe ijae katika dunia nzima, na hapo sifa iwe kwa Yehova. (Isaya 11:9) Mwaka wa 1919 ndipo Yehova alipoufanya “Yerusalemu wa juu” ulio kama mke wake uzae “nchi”—eneo lenye ufanisi mwingi sana—ambamo aliwaingiza upesi wale waliosalia duniani wa Israeli wa kiroho wake. (Isaya 66:8, 10, 22) “Nchi” hiyo imekuwa paradiso ya kiroho, na hapo ndipo watu wa Yehova wamekusanyiwa wawe kiini (msingi) cha “dunia mpya.” Kumekuwa hakuna haja ya kungoja mpaka baada ya dhiki kubwa ili kuiingia hiyo paradiso ya kiroho. Tayari ipo!
16. Kumekuwako utimizo gani wenye utukufu kuhusu Isaya 62:1, 6, 7?
16 Kwa kuwa watu wa Yehova wamekwisha kuingizwa katika “nchi” hiyo yenye kuzaa sana, unabii mkubwa wa Isaya sura ya 62, unaohusu Sayuni, “Yerusalemu wa juu,” umetimizwa. ‘Haki yake inatokea kama mwangaza,’ nayo inamulika mataifa yote ya wanadamu kupitia watu wa mji huo, ambao Isaya anaeleza habari zao kwa maneno haya: “Nimeweka walinzi juu ya kuta zako, Ee Yerusalemu; hawatanyamaza mchana wala usiku; ninyi wenye [kumtaja Yehova], msiwe na kimya . . . mpaka atakapoufanya imara Yerusalemu, na kuufanya kuwa sifa duniani.” Kwa kweli, tengenezo la kimbingu la Yehova limekuwa “sifa duniani” wakati Mashahidi wake wanapohubiri kote kote duniani. Na sehemu iliyo kubwa zaidi ya sifa hiyo inafanywa sasa na wenzi wa “walinzi” watiwa mafuta, yaani, lile “kundi kubwa . . . kutoka mataifa yote,” ambao wamesimama mbele za kiti cha enzi cha Mungu, “wakimtolea yeye utumishi mtakatifu mchana na usiku.”—Isaya 62:1, 6, 7; Ufunuo 7:9, 14, 15, NW.
17. (a) Utumishi wa “mchana na usiku” umekuwaje sehemu ya Mashahidi wa Yehova? (b) Mwaka wa 1982 kulikuwako sababu gani ya kutokeza ya kujawa na furaha? (c) Furaha hiyo inafurika katika kipindi gani, na kwa sababu gani inafanya hivyo wakati unaofaa?
17 Huo utumishi wa “mchana na usiku” unaofanywa na “walinzi” na wenzi wao wa lile “kundi kubwa” unasonga mbele kwa kasi! Utumishi huo wa nafsi yote umekuwa sikuzote ndilo hangaikio la waangalizi wasafirio walio waaminifu na wake zao, wamisionari, mapainia wa kawaida na wa pekee na wafanya kazi wa Betheli. Katika nyakati za majuzi maelfu ya Mashahidi wenye juhudi, vijana na wazee, wamejinyima mambo fulani ili waushiriki utumishi wa painia msaidizi kwa mwezi mmoja au zaidi, wakutumia wastani ya saa zisizopungua mbili katika kazi ya nyumba kwa nyumba na kazi nyingine ya shambani kila siku. Wakati wa mwaka wa 1982 utendaji huo wa ulimwenguni pote ulifikia kilele kisichopata kuwako wakati mwingineo wote, kukawa na jumla kuu ya mapainia 305,778 wenye kuripoti utumishi wakijawa na furaha—wakiungwa mkono sana na mashahidi wengine washikamanifu wa Ufalme zaidi ya 2,000, 000. Kwa kweli, Yehova amekuwa ‘akiumba Yerusalemu uwe sababu ya kujawa na furaha na watu wao wawe sababu ya shangwe’—shangwe ambayo pia inafurika kila mwaka wakati wa kipindi cha kusherehekea Ukumbusho ulioamriwa na Bwana Yesu.—1 Wakorintho 11:23-26.
‘Hakutakuwa Tena na Sauti ya Kulia’
18. Yajapokuwako magumu, “kundi kubwa” limetimiziwa ahadi gani, na kwa njia gani?
18 Ingawa kutakuwako magumu na mateso maadamu Shetani anaruhusiwa kuleta ole kwenye dunia hii, “kundi kubwa” la waabudu wenye kujitoa kwa moyo hawahisi tena “joto lenye kuchoma” la kunyimwa upendeleo wa Mungu. Kwa kuwa wahubiri hao wa habari njema za Ufalme waliojiweka wakf na kubatizwa wameomba “dhamiri njema” kisha wakapewa, wanatumikia kwa kujawa na furaha huku Mwana-Kondoo, Kristo Yesu, akiwaongoza kwenye “chemchemi za maji ya uzima.” Tayari wao wamekwisha kutimiziwa katika paradiso ya kiroho ahadi hii: “Na Mungu atafutilia mbali kila chozi kutoka macho yao.”—1 Petro 3:21; Ufunuo 7:16, 17, NW.
19. (a) Kwa sababu gani “mlio wa huzuni” hauwezi kusikiwa katika “Yerusalemu”? (b) Isaya 65:21-25 inaonyesha nini kupatana na maana ya jina “Yerusalemu’’?
19 Yanayolingana sana na andiko hilo la mwisho ni maneno ya Yehova mwenyewe kwenye Isaya 65:19, NW: “Mimi nitajawa na furaha katika Yerusalemu na kushangilia katika watu wangu; na hakutasikiwa tena katika mji huo sauti ya kulia wala sauti ya mlio wa huzuni.” Wale waliosalia duniani ambao bado hawajafikia hatua ya kufufuliwa waingie ndani ya; “Yerusalemu mpya” wameiona furaha hiyo na sasa Yehova anamimina baraka za namna iyo hiyo juu ya “kundi kubwa” la “kondoo wengine.” (Yohana 10:16) Maneno yanayofuata katika Isaya 65:21-25 yanaisimulia vizuri sana hali ya kiparadiso ya “watu” wa Mungu ambao wamekusanywa wawe kiini (msingi) cha “dunia mpya”! Kwa uhakika, huu ni “Msingi wa Amani Madarufu,” yaani, amani ambayo sasa iko kati ya waabudu wa Yehova na itakayoendelea kuwapo mpaka ikaingie ndani ya Paradiso ya kimwili, wakati ambao mapenzi ya Mungu yatafanyika katika dunia yote.—Ufunuo 21:3-5; Mathayo 6:10.
20. Kwa kufaa, ni maulizo gani tunayoweza kujiuliza?
20 Je! Wewe unataka kumsifu Yehova kale na kale katika dunia-Paradiso kwa sababu ya mambo mazuri ajabu ambayo anatimiza kupitia “Yerusalemu wa juu,” tengenezo lenye kujitoa kwa moyo lililo kama mke wake? Je! wewe unataka kuuona “Yerusalemu wa mbinguni” ambao Mfalme wao ni Kristo, yule Daudi Mkubwa Zaidi, ukipata ushindi wenye shangwe juu ya mambo yote yasiyo ya uadilifu? Je! unataka kuuona “Yerusalemu mpya” ulio kama bibi-arusi ukinyosha maongozi yao yafike chini kutoka kwa Mungu na Kristo wake mbinguni, ili ufutilie mbali machozi yote ya wanadamu?
21.Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunathamini yote yanayofananishwa na Yerusalemu wenye uaminifu?
21 Ikiwa hiyo ndiyo tamaa yako, basi endelea kwa ushikamanifu kutoa “utumishi mtakatifu” uunge mkono mambo yote yaliyofananishwa na Yerusalemu wa kale wenye uaminifu, ule mji wa “Mfalme mkuu,” Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu. (Ufunuo 7:15, NW) Hivyo huenda wewe ukajiunga katika kuuimba ule wimbo wa hekaluni wenye kujaa furaha ulio katika Zaburi 87:3 (NW), na kuimba kwa shangwe hivi: “Mambo matukufu yanaendelea kunenwa juu yako, Ee mji wa Mungu wa kweli.”—Kutoka The Watchtower, March 15, 1983.
Baada ya kujifunza makala yote iliyoambatana na habari hii, unayafahamu maneno haya kuwa yana maana gani:
□ “Yerusalemu wa mbinguni”—Waebrania 12:22
◻ “Yerusalemu mpya”—Ufunuo 21:2
◻ “Yerusalemu wa juu”—Wagalatia 4:26
◻ “Mbingu mpya na dunia mpya”—Isaya 65:17, 18
[Picha katika ukurasa wa 12]
Yerusalemu Mpya—“sababu ya kujawa na furaha”