Wanawahitaji Rafiki Zao
WAKATI wa kazi yake ya kila siku Mkristo moja alijibu simu. Aliyeipiga alikuwa mke wa Mkristo mwenzake: “Ee, ndugu, daktari kaniambia mume wangu yuna miezi mitatu tu ya kuishi. Sijui namna ya kumwambia. Mara moja nikakufikiria wewe. Tafadhali, ungependa kuzungumza naye?” Baada ya nukta chache jibu hili likaja: “Bila shaka. Natumaini kumwona kesho asubuhi.”
Asubuhi iliyofuata, wanaume hao wawili waliamkuana kwa uchangamfu. Baada ya kunywa kikombe cha kahawa mgeni huyo alimwuliza rafiki yake mgonjwa namna alivyokuwa akijisikia. “Vyema kabisa. Upasuaji ulifanikiwa. Sasa libakilo ni kupata nguvu tena.”
“Hiyo inatia moyo. Inaonyesha kwamba wewe unajipa moyo. Ukiwa mtumishi wa Mungu unaweza kuwa mchangamfu wakati wote, hata ikiwa kupata kwako nafuu kunachelewa, pengine kwa muda mrefu zaidi kuliko unavyodhania sasa. Walakini vyo vyote iwavyo, twaweza kuvumilia mambo yote katika uwezo wa Baba yetu wa kimbinguni, sivyo?”
Mgonjwa huyo, mwanamume aliyekomaa maishani pia, alitazama sana macho ya rafikiye. “Ewe! Unafahamu jambo fulani juu yangu nisilolifahamu mimi mwenyewe?” Mgeni wake akajibu kwa utulivu: “Ndiyo, hakika. Daktari alizungumza na mke wako, nalo alilosema ni jambo zito. Yeye anadhani kwamba maisha yako yamo hatarini. Bila shaka, yeye ndiye daktari wa kwanza kutoa maoni yake, walakini jambo hilo linaonyesha kwamba twapaswa kufanya jambo fulani. Je! lisingekuwa jambo la busara kumwona daktari mwingine ambaye anaweza kukusaidia kwa namna nyingine ya utabibu. Wagonjwa wengine kama wewe wameishi muda mrefu zaidi kuliko walivyotabiri madaktari. Lakini je! isingekuwa afadhali kuangalia mambo sasa, iwapo maradhi yako yataongezeka? Mimi niko tayari kusaidia katika njia yo yote utakayoniomba.”
Mazungumzo hayo yaliendelea kwa muda mrefu zaidi, lakini tumekwisha kusikia ya kutosha kuweza kuona vizuri namna yalivyokuwa ya unyofu na yenye kusaidia. Wagonjwa wana haki ya kujua kweli juu ya hali yao, sana sana wanapouliza.
SABABU GANI NYAKATI NYINGINE TUNASITA-SITA?
Pengine tunasita kumtembelea mtu ambaye maisha yake yatakoma karibuni. Twauona uwezo wenye kuharibu wa kifo ukiwa karibu, nao unatuogopesha. (Ebr. 2:14, 15) Lakini, tafadhali—kama ilivyo katika visa vyote ambavyo rafiki zako wamo katika magumu makubwa—usijifikirie mwenyewe ukiwa katika hali hizo. Mithali 17, mstari wa 17, halisemi bure: “Rafiki [wa kweli] hupenda sikuzote; na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu.” Kwa kuwa, ukiwa mshiriki wa kundi la Kikristo, ndugu au dada yako anakuhitaji sasa zaidi kuliko wakati mwingine wo wote. Usiruhusu hali yenye kutaabisha ya rafiki yako mgonjwa ikufanye uongozwe na maono ya ndani kuliko kuhangaikia mahitaji yake ya kweli. Yafikirie mapendezi yake makubwa, nawe uwe rafiki mzuri. Jambo hilo litaondoa mkazo ulio nao, nayo furaha nyingi ya kutumikia wengine itatuliza huzuni yako.
MAMBO YA KUSEMA
Unapomtembelea mtu aliye mgonjwa sana, jambo zuri zaidi la kufahamu ni kwamba yeye hatasaidiwa na uchangamfu wa kujifanya. Ulizo hili la fadhili “Ungependa niketi pamoja nawe kwa muda mfupi?” laweza kukupa utangulizi mzuri. Maulizo kama “Unajisikiaje?” au “Naweza kukufanyia jambo lo lote?” yanaweza kukuonyesha mambo ambayo mgonjwa huyo anataka kuzungumza juu yake. Iwapo anaogopa mambo yanayokuja yasiyojulikana, itakuwa vigumu sana kwake kuzungumza juu yake. Mtu hawezi kusema kwa urahisi mambo yanayoendelea katika akili na moyo wake. Walakini iwapo mgonjwa huyo atazungumza juu ya taraja lisilo na tumaini la maradhi yake, usikatize kwa semi zisizokuwa za kweli kama: “O, usifikiri juu ya hilo! Utapata nafuu.” Kubaliana naye kwa unyofu kwamba mambo yanaweza kuwa mabaya zaidi, lakini kwamba hata hivyo anaweza kuweka mambo yote katika mikono yenye uwezo ya Baba yake wa kimbinguni.—Flp. 4:6, 7.
Unaweza kusema hivi: ‘Je! ungependa nikusomee maneno mazuri katika Biblia?’ Maneno hayo yenye kufariji yatakuwa na matokeo yenye kutia nguvu imani. Wagonjwa hupenda Zaburi kwa sababu maono ya ndani ya mtu aliye katika taabu na kilio chake cha msaada kwa Yehova yanafunuliwa kwa njia nzuri sana ndani yake.
Watu walio wagonjwa mahututi wakati mwingi wanakuwa wamechoka na hawana nguvu za kuendelea na mazungumzo. Kwa hiyo hakuna uhitaji wa kusema sana katika hali hizo. Kuketi kwa unyamavu kando ya kitanda cha mtu huyo na kushika mkono wake kwaweza kuwa chanzo cha faraja. Hata ingawa hawaombi sala itolewe, rafiki zetu wanaoelekea kufa watathamini sana iwapo Wakristo wenzao wanatafuta nafasi ya kushirikiana katika sala. Iwapo unaweza kupata maneno ya kuonyesha kwamba unaamini kabisa kwamba Yehova ana nia na uwezo wa kumtegemeza rafiki yako katika hali hiyo ngumu, nyote wawili mtakuwa na wakati mzuri sana wa umoja katika roho.
Ijapokuwa hatupaswi kamwe kumkaza mtu aliye mgonjwa sana afanye mipango kwa ajili ya wakati ambao hatakuwa hai, ni vema kuangalia nafasi ambayo angependa kuzungumza juu ya jambo hilo. Atafarijika sana ikiwa rafiki zake Wakristo wataahidi kuangalia mambo yote baada ya yeye kulala katika mauti—sana sana mke na watoto wake, au, kwa habari ya mwanamke, mume wake. Pengine ni lazima kuandika kitu ikiwa ulinzi unapaswa kupangwa au mali kuhamishwa kwa mwingine. Kushauriana na wakili kunatoa uhakikisho mzuri zaidi kwamba mapendezi ya mwisho yatafikilizwa.
Bila shaka, ziara zetu hazipaswi kuwa zenye hali ya uzito wakati wote kama vile tumesimulia sasa hivi. Inategemea hali ambayo unampata rafiki yako mgonjwa akiwa nayo. Mara nyingi wagonjwa hupenda kukumbukwa kama vile walivyokuwa katika nyakati zenye furaha maishani mwao. Je! unafahamu jambo linalopendeza mliloshirikiana naye? Lisimulie, nawe unaweza kuwa na hakika kwamba baada ya wewe kuondoka, mgonjwa huyo atafikiria kumbukumbu hizo zenye kuchangamsha. Unaweza kuleta furaha nyingi sana moyoni mwa mtumishi mwenye juhudi wa Yehova ambaye hawezi kufanya lo lote katika kazi ya kuhubiri ‘“habari njema.” Mkumbushe yote aliyofanya katika kazi hiyo wakati uliopita. Wasifu wagonjwa kwa shauku kwa ajili ya ustahimilivu wao na mfano bora wanaoweka wanapovumilia taabu zao kwa imani na uchangamfu.—Ebr. 6:10.
USHINDE WOGA WAKO
Utakubali kwamba wale ambao wamekubali uwezekano wa ugonjwa au msiba kukomesha maisha yetu wamo katika hali nzuri zaidi ya kusaidia wengine ambao wanalazimika kuelekeana na kifo kinachoelekea kutokea upesi. Ni wonyesho wa kukomaa kutokukataa mambo ya kweli ambayo huenda sote tukalazimika kuelekeana nayo.
Walakini iwapo woga wa kifo unatusumbua, twaweza kufanya nini ili kushinda maono mabaya hayo ya ndani na mawazo yasiyo na tumaini? Kwanza kabisa, usijaribu kupuza woga wako. Chukua wakati kutafakari juu ya mashaka ya uzima huu na suluhisho ambalo Mungu anatoa. Rafiki za Mungu, Chanzo cha uhai cha kimbinguni, wanaweza kufikiria jambo hilo katika njia ya kweli na iliyosawazika. Wao wanafahamu kifo ni nini hasa: usingizi usiokuwa na ufahamu usio na maumivu au maogofyo. (Yohana 11-14) Yesu alifundisha waziwazi kwamba wafu watafufuliwa, kwa kusema hivi: “Msistaajabie maneno hayo; kwa maana saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake. Nao watatoka.” (Yohana 5:28, 29) Ijapokuwa Yesu aliuawa na wapinzani wake, alifufuliwa kwenye uzima na Baba yake wa kimbinguni. Baada ya mwujiza huo, mtume Paulo anaandika hivi, “aliwatokea ndugu zaidi ya mia tano pamoja; katika hao wengi wanaishi hata sasa.” (1 Kor. 15:3-8) Ndiyo, hakika, kulikuwako ushuhuda mwingi wa kufufuliwa kwa Kristo.
Wakristo wanafahamu kwamba maisha wanayofurahia sasa si ndilo jambo la muhimu zaidi. Kuwa na kibali ya kimungu ni jambo la thamani zaidi, kwa kuwa kunayo “ahadi ya uzima wa sasa, na ya ule utakaokuwapo baadaye.” (1 Tim. 4:8) Na uwe na hakika kwamba Yehova atatupa nguvu za kuelekeana na kifo wakati ule tunapozihitaji kweli kweli.—Zab. 46:1.
“BALI HATUACHWI BILA MSAADA”
Ukiona kwamba maradhi uliyo nayo sasa hayana tumaini, basi kwa kweli ni jambo la lazima udumishe usawa wako wa kiroho. Pengine maulizo kama vile: ‘Lakini sababu gani mimi?’ yanajaa akilini mwako. Woga na maono mengi ya ndani ya kuachwa huenda yakakusumbua. Pigana nayo. Uwe mwenye kutawala mawazo yako na uyaongoze. Ungali hai naye Yehova yu karibu. Tambua kwamba Ibilisi angependa kutumia udhaifu wako ili kujaribu kudhoofisha imani yako katika Mungu na ahadi yake. Walakini hupigani vita peke yako. Yehova ‘hatakuacha bila msaada.’—2 Kor. 4:9, HNWW.
Tafuta rafiki wakusaidie, sana sana wale ambao tayari wamekwisha kushinda magumu mengi katika uwezo wa Yehova. Shikilia imani yako kabisa katika ahadi zote za Mungu. Tazamia mbele katika wakati ambao utarudi kwenye uzima na kuziona baraka zote za Yehova. Utakuwa Wakati mzuri kama nini! Kuishi milele pasipo maumivu na huzuni, pamoja na rafiki wa kweli. Yehova Mungu anatutaka sote tuishi milele. Yesu alisema hivi: “Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi.”—Yohana 11:25.
WAKUMBUKE RAFIKI ZAKO WENYE KUOMBOLEZA
Ndugu au dada Mkristo akilala katika mauti, usiwasahau watu wake wa ukoo wa karibu. Huo ndio wakati wa kujiweka mwenyewe katika hali yao. Je! unaweza kuwazia namna wanavyojisikia baada ya kufiwa? Wanapaswa kuendelea na maisha yao ya kawaida ya kila siku, walakini wangali na uchungu mwingi. Sasa ndio wakati wanapohitaji rafiki zao—lakini, rafiki wanaoweza kusikiliza. Kuwa na mtu akisikiliza tena masimulizi juu ya yale ambayo mume, mke au mtoto alisema au kufanya kwaweza kuwa jambo la kutuliza na kufariji. Ni jambo lisilowezekana kwao kusahau mara moja wapendwa wao waliokufa. Wakati huo, unaweza kuwasaidia kuendelea na maisha yao tena.
Unaweza kufanya mengi sana kwa rafiki zako wenye kuomboleza. Yanayoweza kufanywa ni kupiga simu au mwaliko kwenye chakula usiotazamiwa. Je! unaweza kuwa nao katika funzo lako la pekee la Biblia? Je! mpango wa mambo ya kisheria na yanayohusu fedha umekwisha fanywa? Je! wana fedha za kutosha kujiruzuku, na ikiwa sivyo, je! tuna nia ya kuwasaidia kwa baadhi ya yale ambayo Yehova ametupa?
Inakuwa wazi wakati rafiki zetu wanapotuhitaji katika njia ya pekee—katika nyakati za huzuni, mahangaiko na hata woga. Yesu alitoa mfano wake juu ya Msamaria mwema kwa ajili ya faida yetu katika nyakati kama hizo pia. Na isiandikwe kamwe juu yetu hivi: Yeye “alipita kando,” kama vile walivyofanya kuhani na Mlawi katika hadithi ya Yesu. (Luka 10:29-37) Twafahamu vizuri zaidi sasa yaliyoandikwa katika Mhubiri, sura ya 7, mstari wa 2: “Heri kuiendea nyumba ya matanga, kuliko kuiendea nyumba ya karamu.” Naye Yakobo aliandika hivi: “[Ibada] iliyo safi, isiyo na taka mbele za Mungu Baba ni hii, Kwenda kuwatazama yatima na wajane katika dhiki yao, na kujilinda na dunia pasipo mawaa.” (Yak. 1:27) Yehova na atubariki kwa kufanya jambo hilo!