Kuchagua Njia Bora Zaidi
“Nanyi mnalindwa na nguvu za Mungu kwa njia ya imani.”—1 Pet. 1:4, 5.
1, 2. Hali yetu sisi sote kabla ya kukubali “habari njema,” na kwa sababu gani twaweza kufurahi?
MTUME Paulo aliwaandikia Wakristo katika mji wa Kiasia wa Efeso hivi: “Wakati mmoja mlitembea kulingana na taratibu ya mambo ya ulimwengu huu . . . Naam, kati yao wakati mmoja sote tulijiendesha kwa kupatana na tamaa za mwili wetu, tukifanya mambo yanayotakiwa na mwili na fikira, nasi kwa asili tulikuwa watoto wa ghadhabu hata kama walivyo wengine. Walakini Mungu, mwenye wingi wa rehema, kwa ajili ya upendo wake mkuu ambao katika huo alitupenda, alitufanya tuwe hai pamoja na Kristo, hata tulipokuwa tumekufa katika dhambi—kwa fadhili zisizostahilika mmeokolewa”—Efe. 2:2-5, NW.
2 Sote leo, kabla hatujaijua kweli, tulijiendesha kwa kupatana na mwili. Hata hivyo, je! hatuna furaha kwa vile tumetumia uhuru wa uchaguzi aliotupa Mungu kwa fadhili zake? Na kwamba, kwa kufanya hivyo, tulichagua njia inayotuweka huru tusiwe katika utumwa, njia inayotuahidia uzima wa milele?
3. (a) Tunahitaji kufanya nini sisi wenyewe ili tuone tumaini letu lenye msingi wa Biblia likitimizwa? (b) Ni katika njia gani sisi tulifanya uchaguzi, nayo ni maulizo gani yanayotokea kwa habari ya sisi kushikamana nao mpaka mwisho?
3 Mtume Petro aliwaambia Wakristo wa karne ya kwanza kwamba Mungu alikuwa amewapa “tumaini lenye uzima.” (1 Pet. 1:3) Sisi, vilevile, tuna tumaini hakika katika mambo ya wakati ujao. Kwa kuwa tunayotumainia hayajafika bado—bado hatujaona tumaini likitimizwa—je! tutaacha? Mtume Paulo alisema: “Kama tunakitumaini kile ambacho hatujakiona bado, basi, tunakingojea kwa uvumilivu.” (Rom. 8:25, HNWW) Kwa hiyo, mambo yakielekea kukosa kutokea kama tunavyotarajia, kuna kila sababu ya kuonyesha uvumilivu na kutia nguvu tumaini. Hii maana yake ni kwamba, tukiwa tumekwisha kuchagua njia ya uzima ulio kweli kweli, ulio bora zaidi, na kwa hakika, njia ya pekee, ni lazima tushikamane na uchaguzi huo. Hatuwezi kuwa na uhakika kwamba tutaona tumaini hilo likitimizwa iwapo tunasitasita na kukosa uthabiti. (Yak. 1:6-9) Sisi tulifanya uchaguzi mkuu na wa kwanza, na kujitoa wakati tulipobatizwa, walakini kila siku sote twakabiliana na matatizo yanayotutaka kufanye maamuzi madogo zaidi na uchaguzi mdogo zaidi kwa kupatana na uamuzi ule mkubwa wa kwanza. Je! twaweza kila siku kuendelea kufanya uchaguzi ulio sahihi unaotudumisha katika njia ya uzima? Je! twaweza kuwa na hakika kwamba tutaona kutimizwa kamili kwa tumaini letu katika wakati ulio karibu?
SHIKILIA UCHAGUZI WAKO!
4. (a) Sababu gani hatupaswi kuachilia kukatisha tamaa kunakotokezwa na makosa kutuondoshe katika mwendo tuliouchagua? (b) Tamaa ya kuona tumaini lao likitimizwa imewaongoza Wakristo katika muda wote uliopita kwenye kosa gani?
4 Tukiendelea kuwa waaminifu, Mungu hatatuacha tufanye makosa yenye kuharibu. Walakini nyakati nyingine yeye anatuachilia tuingie katika makosa ili tuone uhitaji wa kumtegemea yeye wakati wote na Neno lake. Hii hutia nguvu uhusiano wetu naye na uvumilivu wetu huku tukingojea. Twajifunza kutokana na makosa yetu kwamba ni jambo la lazima kuwa waangalifu katika wakati ujao. Tamaa ya taratibu mpya ya mambo itakayochukua uongozi wa dunia wakati wote imekuwa yenye nguvu sana katika Wakristo katika karne zote zilizopita. Na kwa sababu ya muda wao mfupi wa kuishi, bila shaka waliitamani ije wakati wenyewe wa maisha yao. Zaidi ya pindi moja katika historia yote, wale ambao wamejaribu ‘kuukaribisha akilini’ wakati wa Mungu wa kuhukumu, wamekuwa wenye kutazamia kupita kiasi kufika kwa siku hiyo, wakijaribu kuharakisha katika akili zao kufika kwa matukio yenye kutamanika. (2 Pet. 3:12, NW) Kwa mfano, katika karne ya kwanza, mtume Paulo aliona lazima ya kuandikia Wathesalonike kwa jinsi hiyo, kama tunavyosoma katika 2 Wathesalonike 2:1-3, NW; “Walakini, ndugu, kwa habari ya kuwapo kwa Bwana wetu Yesu Kristo na kukusanywa kwetu pamoja kwake, twawaomba msiondoshwe haraka kutoka kwenye akili zenu wala kubabaishwa ama na usemi ulioongozwa na roho ama kupitia kwa ujumbe wa maneno tu ama kupitia kwa barua kama kwamba imetoka kwetu, ya kuwa siku ya Yehova imefika. Mtu ye yote asiwashawishi katika njia yo yote, kwa sababu haitakuja usipokuja kwanza ule ukafiri na yule mtu wa kuasi kufunuliwa, yule mwana wa uharibifu.”
5. (a) Mataraja yenye nguvu sana yalisitawije kuhusiana na mwaka wa 1975? (b) Ni kwa sababu gani maneno ya uangalifu yaliyochapishwa hayakuzuia kuhangaikia sana tarehe?
5 Katika nyakati za kisasa shauku kama hiyo, inayosifika, imeongoza kwenye majaribio ya kuweka tarehe ya kukombolewa kunakotamaniwa kutokana na mateso na kutaabika ambako ni fungu la watu wote katika dunia yote. Kitabu Uzima wa Milele—katika Uhuru wa Wana wa Mungu kilipotokea, pamoja na maelezo yake juu ya namna ambavyo lingekuwa jambo lenye kufaa utawala wa mileani (Miaka elfu) wa Kristo upatane na mileani ya saba ya kuwapo kwa wanadamu kutazamia kwingi mno kuliamshwa kuhusiana na mwaka 1975. Kulikuwako habari zilizotolewa wakati huo, na baada ya hapo, zilizokazia kwamba hilo lilikuwa jambo linaloelekea kutukia. Walakini, inasikitisha kwamba, pamoja na habari hizo zilizotolewa kwa uangalifu, kulikuwako habari nyingine zilizochapwa zilizodokeza kwamba kutimizwa kwa matumaini katika mwaka huo kulionekana kuwa jambo la hakika kuliko kuwa tu jambo linaloelekea kutukia.
6. Je! habari iliyochapishwa katika Mnara wa Mlinzi wa Desemba 15, 1976, ilijaribu kuweka daraka la hilo sana sana juu ya msomaji? Eleza.
6 Katika toleo lake la Desemba 1, 1976, Mnara wa Mlinzi, ukitoa maelezo juu ya kutofaa kuweka macho yetu juu ya tarehe fulani, ulisema hivi: “Ikiwa mtu fulani amekata tamaa kwa sababu ya kutowaza hivyo, sasa yampasa ajitahidi kurekebisha maoni yake, baada ya kuona kwamba si neno la Mungu lililomkatisha tamaa wala kumdanganya, bali kwamba ufahamu wake mwenyewe ulitegemea maoni mabaya.” Kwa kusema “mtu fulani,” Mnara wa Mlinzi ulitia ndani watu wote waliokata tamaa kati ya Mashahidi wa Yehova, hivyo ukitia ndani watu wenyewe waliohusika na uchapishaji wa habari hiyo ambayo ilitokeza matumaini makubwa juu ya tarehe hiyo.
7. (a) Makosa kama hayo ya kibinadamu yanapaswa kuwa na matokeo gani juu ya imani yetu katika ahadi ambazo Mungu mwenyewe ameahidi? (b) Kwa kweli, Neno la Mungu linakazia jambo gani kuwa la maana zaidi?
7 Hata hivyo, hakuna sababu ya kutuondoa sisi tusiziamini ahadi za Mungu. Mahali pake, kama matokeo, sote twasukumwa tufanye uchunguzi wa uangalifu zaidi wa Maandiko kuhusiana na jambo hilo la siku ya hukumu. Kwa kufanya hivyo, twapata kuona ya kuwa jambo la maana zaidi si siku hiyo. Lililo la maana ni kukumbuka wakati wote kwamba kuna siku kama hiyo—nayo inazidi kukaribia nasi sote tutahitajiwa kutoa hesabu. Petro alisema kwamba Wakristo wapaswa kwa kufaa ‘kungojea na kukaribisha akilini kuwapo kwa siku ya Yehova.’ (2 Pet. 3:12, NW) Siyo siku fulani katika tarehe ya wakati ujao, ni kuishi siku baada ya siku kwa Mkristo ndiko kwa maana. Yeye hapaswi kuishi siku yo yote moja bila ya kukumbuka kwamba yuko chini ya ulinzi wa upendo na uongozi wa Yehova naye apaswa kujitiisha chini yake, akikumbuka pia kwamba apaswa kutoa hesabu kwa vitendo vyake.
8. (a) Maneno ya Yesu na yale ya Paulo yanathibitishaje kufaa kwa maoni hayo? (b) Lazima tuvumilie mpaka mwisho; lakini “mwisho” huo ni lini, nasi tunaweza kujua jambo gani kuhusiana na wakati wa kufika kwake?
8 Yesu alitoa sababu yake hivi: “Kwa sababu Mwana wa Adamu atakuja katika utukufu wa Baba yake pamoja na malaika zake; ndipo atakapomlipa kila mtu kwa kadiri ya matendo yake.” (Mt.16:27) Mtume Paulo pia alitaja hivi: “Sisi sote tutasimama mbele ya kiti cha hukumu cha Mungu . . . Kwa hiyo, kila mmoja wetu atatoa [hesabu] yake mbele ya Mungu.” (Rum. 14:10-12, HNWW) Na, “Imetupasa sisi sote kudhihirishwa mbele ya kiti cha hukumu cha Kristo, ili kila mtu apokee ijara ya mambo aliyotenda kwa mwili, kadiri alivyotenda, kwamba ni mema au mabaya.” (2 Kor. 5:10) Tunao muda mrefu namna gani kabla ya kutoa hesabu? Yesu alisema: “Mwenye kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka.” (Mt. 24:13) “Mwisho” huo utakuwa wakati gani? Mwisho huo waweza kuja ama mwishoni mwa taratibu hii ya mambo ama wakati wa kufa kwa mtu mwenyewe kabla ya wakati huo. Kwa hiyo, kila mmoja wetu ana muda mrefu namna gani? Hakuna awezaye kuhesabu siku atakayokufa. Vivyo hivyo, Yesu aliwaambia mitume wake juu ya wakati wa kusimamishwa kwa ufalme wa Mungu hivi: “Nyakati na majira ya mambo hayo vimo chini ya mamlaka ya Baba yangu, wala si shauri lenu kujua yatakuwa lini.” (Matendo 1:7, HNWW) Ni jambo lisilowezekana kwetu kujua mwisho wa ulimwengu mapema.
UTIMIZO WA TUMAINI LETU
9. Ni maneno gani ya Petro yanayoweza kutupa uhakika ili tushikamane na uchaguzi wetu tuliofanya?
9 Iwapo mtu ye yote anaogopa kwamba, kwa sababu ya majaribu yawezayo kutokea, hatashikamana na Mungu na Kristo, na ayasikilize maneno ya mtume Petro. Mtume huyu anatuhakikishia kwamba tumaini letu ni hakika iwapo tutalishikilia kabisa kwa njia ya imani katika Mungu na ahadi zake hakika. Yeye asema hivi: “Nanyi mnalindwa na nguvu za Mungu kwa njia ya imani hata mpate wokovu ulio tayari kufunuliwa wakati wa mwisho.” (1 Pet. 1:3-5) Twajifunza nini kutokana na maneno hayo?
10, 11. (a) Ni nani anayepaswa kusifiwa kweli kweli kwa vile tulivyozikubali “habari njema,” na kwa sababu gani? (b) Mungu anawawezeshaje watu waikubali nuru ya kweli (c) Andiko la 1 Wakorintho 2:9 lasema nini juu ya uwezo wa wanadamu wa kuufahamu ukweli wa kimungu kwa uwezo wao wenyewe?
10 Basi, tulipozikubali kwanza na kuziamini “habari njema” tulizotangaziwa, je! kwa kufaa tungeweza kujisifu sisi wenyewe kuwa wenye akili nzuri ya kuona thamani zake na kuzifahamu mara hiyo? Hapana. “Tulipokuwa hatuna nguvu,” tukiwa hoi tusiweze kujiokoa wenyewe, “tulipokuwa tungali wenye dhambi,” naam, wakati tulipokuwa bado adui, “tulipatanishwa na Mungu kwa mauti ya Mwana wake.” (Rum. 5:6-10) Kwa hiyo, ni nani, tunayepaswa kumshukuru kwa sababu ya hali yenye upendeleo tuliyo nayo sasa? Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “hakuna mtu awezaye kuja kwangu Baba aliyenituma asipomvuta kwangu.” (Yohane 6:44, HNWW) Kwa kuchukua hatua yetu ya kwanza sisi wenyewe tusingeweza kamwe kupata maarifa ya Mungu. Hali yetu ya kibinadamu isiyokamilika, yenye dhambi, isingeturuhusu kamwe tufanye hivyo.
11 Hata hivyo, twaweza kumtafuta, kwa kuwa “hawi mbali na kila mmoja wetu.” (Matendo 17:27) Tukitazama au kupapasa-papasa tu ili kumpata Mungu, jambo hilo lampendeza. Kisha yeye anatukaribia. (Yak. 4:8) Mungu ajua tamaa ya ndani ya mtafutaji naye anatuma mtu kwake akiwa na “habari njema” au aweza kufanya mambo ili aweze kupata ujumbe wa Ufalme. Anapozisikia “habari njema” na kulichunguza Neno la Mungu, kwa msaada wa roho takatifu, ambayo Mungu hutoa, mtafutaji huamka kuiona hali yake. Kisha, akiamini yale anayosema Mungu, yeye anaweza kutoka gizani. Kwa habari ya uwezo wa mwanadamu, Biblia yasema hivi: “Jicho halijapata kuyaona wala sikio kuyasikia, mambo ambayo binadamu hajapata kuyafikiria moyoni, hayo ndiyo Mungu aliwatayarishia wale wampendao.” (1 Kor. 2:9, HNWW) Kupitia kwa fikira na tamaa zetu wenyewe za kibinadamu tusingeweza kusikia kamwe, na hakika tusingeifahamu kweli kama Mungu asingetuhurumia na kutusaidia sisi binafsi.
12. (a) Ili tuweze kushikamana na uchaguzi wetu wa kwanza ni nini tunalopaswa kukumbuka? (b) Mungu awezaje kutulinda na hatari ambazo katika hizo kutofahamu kwetu kwaweza kutuingiza?
12 Basi, kufahamu kwamba Mungu anaona hali yetu na kutusaidia tangu mwanzoni kabisa, twaweza kuthamini namna inavyowezekana kushikamana na uchaguzi wetu wa kwanza kadiri miaka inavyopita. Kwa kweli, Mungu aweza kutufanya tukue kiroho. Kama vile asemavyo Petro, twalindwa na uwezo wa Mungu. Twapaswa kutambua kwamba, mara baada ya kuwa Wakristo, hatuvumilii kwa kufaulu kwa nguvu zetu, hekima au ufahamu wetu—tusingeweza kufanya hivyo kwa uwezo wetu. Kwa mfano, mara nyingi hatutambui vyepesi. Nyakati nyingi tunapokuwa hatuna habari zo zote kabisa, tunaingia katika hali zinazohatirisha sana ukamilifu wetu wa Kikristo. (Gal. 6:1) Huenda tukawa twakaribia kuchukua hatua fulani inayoweza kutuongoza kwenye uharibifu. Walakini Mungu, akiwa anatazama, hutupenda na kutuhurumia akitimiza ahadi zake kwetu, na katika wakati unaofaa aweza kutuokoa katika hatari. Mfalme Daudi wa Israeli wa kale, baada ya ‘kulindwa’ hivyo na Mungu kwa uangalifu wake wa kukesha, alisema: “Umeniponya nafsi yangu na mauti; je! hukuizuia miguu yangu isianguke? Ili nienende mbele za Mungu katika nuru ya walio hai.”—Zab. 56:13.
TWALINDWA TUSIWE NA HATIA YA DAMU
13, 14. (a) Daudi alikaribiaje sana kumwaga damu isiyo na hatia? (b) Abigaili alitumiwaje amzuie katika mwendo wake huo mbaya?
13 Mfano unaoonyesha jinsi Mungu alivyomlinda na kumwokoa Daudi katika mawazo na vichocheo vyake visivyokamilika ni ue ulioandikwa katika 1 Samweli sura ya 25. Wakati Daudi alipokuwa akiishi kama mtoro, akiwa anawindwa ili auawe na Mfalme Sauli, Daudi na watu wake walikuwa wakisaidia, wakilinda na kuangalia watu wa Israeli po pote walipopata nafasi. Mtu mmoja waliyesaidia alikuwa Mwisraeli aliyekuwa tajiri sana, jina lake Nabali. Pindi moja wakati Daudi na watu wake walipokuwa wamepiga kambi katika ujirani wa wachungaji wa Nabali wakiwa na kondoo wao, watu wa Daudi walikuwa ukuta wenye kulinda juu ya wanyang’anyi, nao hawakuomba wala kuchukua cho chote kwa ajili ya utumishi wao. Baadaye, wakati watu wa Daudi walipokuwa wakihitaji chakula, Daudi alimwomba kwa fadhili Nabali, akiwa ndugu Mwisraeli, ampe msaada kidogo wa zawadi ya chakula. Badala ya kuonyesha shukrani na kutokuwa na choyo kama ilivyoamriwa na torati ya Musa, Nabali aliwatupia maneno ya kuwakemea na kuwatusi watu wa Daudi.
14 Tendo hilo la ukali, lisilo la shukrani lilimghadhibisha (lilimkasirisha) Daudi, hata akaondoka akiwa na watu 400 akalipize kisasi juu ya Nabali na nyumba yake. Walakini Abigaili mke wa Nabali, akapata kujua juu ya mwenendo mbaya wa mumewe, alifanya haraka kwenda kwa Daudi akiwa na zawadi kubwa ya chakula. Alimsihi Daudi kwa msingi wa uhusiano wake na Yehova aachane na kiasi alichokusudia, akisema: “Hili [lisiwe] kwako, wala chukizo la moyoni kwa bwana wangu, ama ya kuwa umemwaga damu bure, ama ya kuwa bwana wangu amejilipiza kisasi mwenyewe.” Daudi, akirudiwa na fahamu zake, alijibu hivi: “Na ahimidiwe [Yehova], Mungu wa Israeli, ambaye amekuleta hivi leo kunilaki; na ibarikiwe busara yako, na ubarikiwe wewe, uliyenizuia hivi leo nisimwage damu wala kujilipiza kisasi kwa mkono wangu mwenyewe.”—1 Sam. 25:31-33.
15, 16. (a) Ikiwa Daudi angeendelea katika mwendo wake huo, angekuwa na hatia ya makosa gani mawili, nalo ni jambo gani lililomwokoa? (b) Tunajifunza somo gani kutokana na jambo hilo, nalo lapaswa kuwa na matokeo gani kwetu sisi?
15 Kulingana na maoni ya kibinadamu, Daudi, alikuwa amejiona kuwa na haki alipoondoka kwenda kulipiza kisasi juu ya Nabali kwa ajili ya uovu wake, walakini iwapo angefanya hivyo angekuwa akijitegemea kwa kulipiza kisasi na kujitukuza, na angekuwa na hatia ya damu kwa kuwaua washiriki wasio na hatia wa nyumba ya Nabali. Ni nini kilichomwokoa Daudi? Yehova Mungu alikuwa akitazama, naye akamlinda asifanye dhambi hiyo mbaya.
16 Kutokana na mfano huo twaona kwamba hatuwezi kujitegemea tuendelee katika mwendo wenye kuleta wokovu, walakini twapaswa wakati wote kumtegemea Mungu, ambaye hutuangalia na kuhakikisha kwamba tumesalimika. Jambo hilo lapaswa kutupa hakika na vilevile kutufanya tuwe wanyenyekevu.
17. (a) Je! inatupasa kufikiri kwamba Mungu atakosa kumfanyia jambo kama hilo mtumishi wake mnyenyekevu leo? (b) Ni njia gani ambazo katika hizo Mungu aweza kutulinda tusifanye makosa mazito?
17 Hata hivyo, huenda mtu akasema, ‘Huyo alikuwa Mfalme Daudi mtiwa-mafuta wa Yehova, ambaye Mungu alikuwa amefanya naye agano la ufalme. Pengine hatatuangalia sisi sana.’ Je! kwa kweli twaweza kusema kwamba Mungu, aliyetununua kwa damu yenye thamani ya Mwana wake, hayalindi maisha yetu kwa wivu ule ule? Bila shaka anafanya hivyo. Kwa vile Mungu alivyomwokoa Daudi katika tendo la kutofikiri, kwa kumtumia Abigaili, bila shaka atatuokoa na sisi. Kama vile alivyomwongoza Abigaili amwokoe Daudi, huenda akatumia Neno lake Biblia, au malaika zake, au mshiriki Mkristo, au aweza kupanga hali kwa msaada wa kimungu zituzuie tusifanye jambo la upumbavu, iwapo tuna imani na twaendelea kufuatia mwendo ulio wa namna ya sala, na wa unyenyekevu, tukimtegemea kwa kila kitu.
18, 19. Kujua hivyo kwaweza kututiaje moyo tuendelee kuvumilia kwa uaminifu katika mwendo ambao tumechagua, nalo ni ulizo gani linalohitaji kujibiwa?
18 Lo! jinsi kufahamu mambo jinsi hiyo kunavyofariji na kutia moyo! Mungu hasemi, ‘Vema, sasa wajua namna ya kutenda na yote ni juu yako.’ Badala yake, kwa upendo yeye anapendezwa na wokovu wetu naye anatenda ili atulinde maadamu sisi tunaendeleza imani katika yeye na katika ukombozi alioutoa kupitia kwa Mwana wake. “Yeye anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi,” akijua kwamba, tukijitegemea sisi wenyewe, jitihada zetu wenyewe za kushikilia mwendo wa haki mpaka mwisho zaweza kushindwa.—Zab. 103:10-14, 17, 18; linganisha Zaburi 38:4, 22; 40:12, 13; 130:3, 4.
19 Je! hiyo maana yake ni kwamba hatuna sehemu yo yote kwa habari ya kuishi kwa uaminifu—kwamba yote ni juu ya Mungu? Hapana, kama vile mazungumzo haya yafuatayo ya Kimaandiko yanavyoonyesha waziwazi.