Neno la Mungu Li Hai
Abigaili—Mwanamke Mwenye Akili Nyingi Sana
ABIGAILI alikuwa na usawa mzuri sana wa uzuri wa mwili na ufahamu. Mwanamke huyo mwenye akili kutoka Karmeli akawa mke wa mwanamume tajiri wa kutoka Maoni uliokuwa jirani. Mume wake alikuwa mtu mkali, asiyejadilika aliyetenda kulingana na jina “Nabali,” linalomaanisha “mpumbavu,” au “mtu asiye na akili.”—1 Sam. 25:2, 3.
Hekima ya Abigaili inafunuliwa katika tendo lake lenye kukata shauri katika hali iliyomhusu Daudi. Hali hiyo ilikuwa yenye hatari sana hivi kwamba ingalimfanya Daudi awe na hatia ya damu mbele za Mungu tena ingalileta kifo juu ya kila mwanamume katika nyumba ya Nabali.
Katika kipindi kile alichokuwa ametangazwa kuwa haramia na Mfalme Sauli, Daudi aliendelea kutafuta faida ya Waisraeli wenzake. Kwa mfano, yeye pamoja na wanaume waliokuwa pamoja naye walilinda wachungaji pamoja na makundi ya Nabali wasishambuliwe na maharamia. Kwa sababu hiyo, Daudi aliona kwamba lilikuwa jambo linalofaa kumpa Nabali nafasi ya kuonyesha shukrani zake kwa sababu ya utumishi uliomsaidia sana afanikiwe. Wakati wa kunyoa kondoo ndio uliokuwa wakati unaofaa Nabali aonyeshe shukrani hizo. Wakati huo ulionwa kuwa sawasawa na wakati wa mavuno, kwa kuwa watu walifanya karamu.—1 Sam. 25:4-8.
Kwa hiyo, kutoka jangwa la Uyahudi, Daudi akatuma ujumbe wa watu 10 kwenda Karmeli, ukingoni mwa jangwa. Ndipo Nabali alipokuwa akifanya kazi ya kunyoa kondoo wake. Badala ya kuwapokea wanaume hao kwa fadhili, yeye aliwatupia maneno yenye kutukana. Daudi alipojua namna walivyopokelewa kwa ukatili, yeye, akiwa pamoja na wanaume kama 400 hivi wenye kuchukua upanga, aliazimia kumwua Nabali pamoja na wanaume wote wa nyumba yake.—1 Sam. 25:9-13.
Wachungaji wa Nabali walitambua kwamba namna bwana wao alivyoitikia ombi la wanaume wa Daudi kwa njia yenye chuki ingeweza tu kuwaletea taabu. Hiyo ndiyo sababu mmoja wao akamwambia Abigaili jambo lililokuwa limetukia. Mara hiyo akafahamu hatari ambayo Nabali alikuwa ameiletea nyumba yake. Akijua kwamba hangetumaini mume wake ajadilike, Abigaili akachukua hatua ya kwanza katika kushughulikia jambo hilo katika njia inayofaa. Kwake yeye, kukamatana na kanuni inayofaa lilikuwa jambo la maana zaidi kuliko kujaribu kumpendeza mwanadamu ambaye alikuwa ameipuza sheria ya kimungu kwa kulipa wema kwa uovu. Kutoka kwa chakula kingi cha karamu cha mumewe, Abigaili akachukua mikate 200, chupa mbili kubwa za divai, kondoo watano waliochunwa, pishi kama 16 hivi za nafaka iliyookwa, keki 100 za zabibu kavu na keki 200 za tini. Vyakula hivyo vikaletwa kwa Daudi kwa mikono ya watumishi vikiwa vinachukuliwa kwa punda. Abigaili mwenyewe akawa anawafuata.—1 Sam. 25:14-19.
Alipokutana na Daudi, akasujudu mbele yake akamsihi asilipe kisasi. Ombi lake lilitia ndani mambo haya ya msingi. Nabali alikuwa mpumbavu, “mtu asiyefaa [kitu].” Hiyo ilimaanisha kwamba yeye alikuwa chini ya laana ya kimungu naye Yehova angemchukulia hatua. Kwa kuonyeshwa mambo waziwazi namna hiyo mbele yake, Daudi alikuwa akizuiwa na Yehova “[a]simwage damu.” Tena lilikuwako ombi kwamba akubali vyakula kwa ajili ya wanaume wake.—1 Sam. 25:23-27.
Kisha, Abigaili akiwa na imani kabisa kwamba Yehova angemtumia Daudi, yeye aliendelea kusema hivi: “[Yehova] atamfanyia bwana wangu nyumba iliyo imara, kwa sababu bwana wangu anavipiga vita vya [Yehova]; tena uovu hautaonekana ndani yako siku zako zote. Na hata ijapokuwa binadamu angeinuka akuwinde, na kuitafuta nafsi yako, hiyo nafsi ya bwana wangu itafungwa katika furushi ya uhai pamoja na [Yehova], Mungu wako; na nafsi za adui zako ndizo atakazozitupa nje, kama kutoka kati ya teo. Tena itakuwa, hapo [Yehova] atakapokuwa amemtendea bwana wangu sawasawa na mema yote aliyoyanena juu yako na kukutawaza juu ya Israeli; hili halitakuwa kwazo, wala chukizo la moyoni kwa bwana wangu, ama ya kuwa umemwaga damu bure, ama ya kuwa bwana wangu amejilipiza kisasi mwenyewe; tena hapo [Yehova] atakapokuwa amemtendea bwana wangu mema, ndipo umkumbuke mjakazi wako.”—1 Sam. 25:28-31.
Hivyo, kwa sababu ya kumbukumbu ambalo Daudi alikuwa amejifanyia akiwa kama shujaa, Abigaili alitambua kwamba yeye alikuwa mtiwa-mafuta wa Yehova. Maneno yake yakawa namna ya unabii, yakataja juu ya wakati ambapo kungekuwako nyumba ya kifalme katika ukoo wa Daudi. Abigaili alikuwa na tumaini hakika kwamba Yehova angemlinda Daudi, akiuhifadhi uhai wake, au nafsi, kana kwamba katika “furushi” au mfuko ambao katika huo mtu angefungia kitu chenye thamani. Walakini, hiyo ingekuwa hivyo ikiwa tu Daudi hakutafuta kujiletea wokovu au ukombozi kwa mkono wake mwenyewe, pasipo kujali msaada wa kimungu. Yeye aliitikia, akakubali. —1 Sam. 25:32-35.
Wakati Abigaili aliporudi nyumbani, alimkuta Nabali akiwa mlevi. Asubuhi iliyofuata, alipokuwa amelevuka, Abigaili akamwambia mumewe yote yaliyokuwa yametendeka. “Moyo wake ukafa ndani yake,” maana ya hali hiyo yote kwa wazi ilimletea ugonjwa wa ghafula. Kama siku 10 hivi baadaye, inaelekea kwamba Nabali alipatwa na ugonjwa mwingine wa ghafula, uliomwua. —1 Sam. 25:36-38.
Baada ya hayo, Daudi akamposa Abigaili amwoe. Alipokuwa akikubali kuposwa huko, Abigaili akasema hivi katika unyenyekevu wote: “Tazama, mjakazi wako ni mtumwa wa kuwaosha miguu watumishi wa bwana wangu.” Hivyo, yeye alionyesha nia yake ya kutoa utumishi ulio wa chini kabisa. Akiwa pamoja na vijakazi vyake watano, akaanza kushiriki maisha yasiyotulia ya mwanamume ambaye alilazimika kuendelea kuishi kama haramia kwa sababu ya Mfalme Sauli. Kwa wakati fulani aliishi katika mji wa Gathi wa Kifilisti na baadaye katika Ziklagi. Mojalapo la magumu aliyovumilia lilikuwa kuchukuliwa mateka na maharamia Waamaleki. Hata hivyo, kwa furaha, aliokolewa pasipo dhara lo lote.—1 Sam. 25:39-42; 30:1-19.
Njia ya maisha ya Abigaili inaonyesha waziwazi jambo linalomfanya mtu kuwa mwenye akili machoni pa Mungu. Yeye alikuwa mnyenyekevu naye alitanguliza ushikamanifu kwa Mungu kuliko kuwa mshikamanaifu kwa mwanadamu. Kukubali uongozi wa kimungu ndiko kulikomfanya awe na hekima.
[Picha katika ukurasa wa 20]
ABIGAILI
NABALI
DAUDI