Ahadi ya Wakati Ujao Ulio Bora
NI MTU gani mwenye huruma ambaye hajapata kuumizwa sana kwa kushuhudia uonezi na kuteseka? Bila shaka kuna uhitaji wa kunyoshwa kwa mabaya mengi. Walakini je! kuna wakati wo wote tutakapoona kukoma kwa mambo yote yenye kutaabisha wakati wote jamii ya kibinadamu?
Zaidi ya karne 19 zilizopita mtu mmoja ambaye alijiruzuku kama mvuvi wa kawaida aliandika hivi: “Ziko mbingu mpya na dunia mpya ambazo sisi tunangojea kulingana na ahadi yake [Mungu], na katika hizi haki itakaa.” (2 Pet. 3:13, NW) Mtu huyo, mtume Petro, pamoja na watumishi wengine wengi wa Aliye Juu Zaidi katika karne zote, walitiwa moyo na ahadi hiyo. Kwa shauku wote hao walitazamia siku ile nzuri sana wakati uasi, uonezi na jeuri, vyote vitakapokoma nayo haki ya hukumu kusawazishwa. Lakini twaweza kuwaje na hakika kwamba ahadi hiyo ilitokana na Muumba wa mwanadamu na kwamba itatimizwa hakika? Je! kutimizwa kwayo kutaleta faida kwa wale tu walio hai katika wakati huo ujao? Na je! kuna jambo lo lote katika ahadi hiyo linalotoa tumaini lenye kutegemeka kwa mabilioni ya wanadamu wafu?
Inafaa kuangalia kwamba wakati Petro alipotaja “mbingu mpya na dunia mpya” hakuwa akianzisha ahadi ambayo Yehova Mungu alikuwa amefanya karibuni tu. Yapata miaka 800 mapema, Mwenye Nguvu Zote, kupitia kwa nabii wake Isaya, alikuwa ametangaza hivi: “Maana, tazama, mimi naumba mbingu mpya na [dunia] mpya, na mambo ya kwanza yatakumbukwa.” (Isa. 65:17) “Kama vile mbingu mpya na [dunia] mpya, nitakazofanya, zitakavyokaa mbele zangu, asema [Yehova], ndivyo uzao wenu na jina lenu litakavyokaa.”—Isa. 66:22.
USHUHUDA KAMILI
Ingawa maneno hayo yaliandikwa karne nyingi zilizopita, sisi leo tuna ushuhuda wenye kutegemeka kwamba chanzo chake ni Mungu. Biblia yenyewe inatoa njia ya kutambua chanzo cha unabii wa kweli. Mambo matatu makuu yanahusika: (1) Ujumbe wenyewe unapaswa kuendeleza ibada safi, (2) Nabii huyo anapaswa kusema katika jina la Yehova, na (3) Mambo yaliyotabiriwa yanapaswa kutimia. (Kum. 13:1-4; 18:20-22) Unabii wa Isaya unatimizaje matakwa hayo?
Uchunguzi wa kitabu cha Isaya unaonyesha kwamba wakati wote kinawasihi Waisraeli wauache mwendo wao mbaya na kumtumikia Muumba wakiwa na kusudi jema. Kwa habari zote maneno hayo yanatangazwa katika jina la Yehova. Kwa mfano, twasoma hivi:
“Jiosheni, jitakaseni; ondoeni uovu wa matendo yenu usiwe mbele za macho yangu; acheni kutenda mabaya; jifunzeni kutenda mema; takeni hukumu na haki; wasaidieni walioonewa; mpatieni yatima haki yake; mteteeni mjane. Kama mkikubali na kutii mtakula mema ya nchi; bali kama mkikataa na kuasi mtaangamizwa kwa upanga; maana kinywa cha [Yehova] kimenena haya.” (Isa. 1:16, 17, 19, 20)
“Mtafuteni [Yehova], maadamu anapatikana, Mwiteni, maadamu yu karibu; Mtu mbaya na aache njia yake, Na mtu asiye haki aache mawazo yake; Na amrudie [Yehova], Naye atamrehemu; Na arejee kwa Mungu wetu, Naye atamsamehe kabisa.” (Isa. 55:6, 7)
Kwa wazi, unabii wa Isaya unatimiza matakwa haya (1) kuongoza watu mmoja mmoja kwenye ibada safi na (2) ulisemwa katika jina la Yehova.
Walakini namna gani utimizo wenyewe—(3) kutimia kwa yaliyotabiriwa? Huenda mtu akasema hivi, ‘Tungali hatuoni “mbingu mpya na nchi mpya.” ‘ Walakini, inapaswa kuangaliwa kwamba kulikuwako utimizo wa mapema wa unabii huo ambao unaweza kuthibitishwa kupitia kwa historia.
Kwa sababu Waisraeli walikataa kusikiliza mwito wa kutubu uliotolewa kwa kurudiwa-rudiwa na manabii wao, Yehova Mungu aliwaacha watu hao wasiotii wakashindwa na maadui wao. Mji mkuu wa Yerusalemu na nchi ya Yuda vilifanywa mahame wakati Wababeli chini ya Nebukadreza walipomaliza mazingiwa yao. Ushuhuda wa wachimbuzi wa mambo ya kale unathibitisha jambo hilo la hakika. Kitabu The Archaeology of Palestine, kilichoandikwa na W. F. Albright kinasema hivi: “Hakuna kisa hata kimoja kinachojulikana ambapo mji wa Yuda wenyewe ulikaliwa kwa muda wenye kuendelea wakati wa kipindi cha kuhamishwa. Ili kuonyesha tofauti hiyo, Betheli, ambao ulikuwa kiunga katika mpaka wa kaskazini wa Yuda katika nyakati zilizotangulia kuhamishwa, haukuharibiwa wakati huo, bali wakati wote uliendelea kukaliwa mpaka sehemu ya mwisho ya karne ya sita.” (Uku. 142) Wakati nchi hiyo ilipokuwa ukiwa, Wayahudi wengi walikuwa uhamishoni katika Babeli.
Kulikuwako matumaini madogo kwamba wahamishwa Wayahudi wangeweza kurudi katika nchi ya kwao. Hayakuwa maongozi ya wafalme wa Babeli kuruhusu jambo hilo. (Isa. 14:16, 17) Hata hivyo unabii wa Isaya ulikuwa umeagiza kwamba mtawala mwenye kujulikana kama Koreshi angetoa ruhusa ya kujenga upya Yerusalemu na kuifanya nchi ya Yuda ikaliwe tena. (Isa. 44:25-45:2) Walakini jambo hilo lisingetokea mpaka kipindi cha miaka 70 kimalizike tangu kuanza kwa “ukiwa wa Yerusalemu” uliofanywa na Wababeli katika mwaka 607 K.W.K.—Dan. 9:2.
Badiliko lilitokea katika usiku wa Oktoba 5/6, 539 K.W.K., miaka 68 baada ya kuanza utumwa wa Yuda wa miaka 70 wa kutumikia Babeli. (Yer. 25:9-11) Wakijiona salama ndani ya Babeli uliofanywa boma imara, wakaaji wake walikuwa wakila karamu kwa fujo. Hawakufahamu uhakika wa kwamba kina cha maji ya Mto Frati ambao ulipitia katikati ya mji kilikuwa kikishuka haraka sana. Mto huo ulikuwa umepelekwa upande na majeshi yenye kufanya mazingiwa chini ya amri ya Koreshi Mwajemi. Wakati Wamedi na Waajemi walipopiga hatua juu ya sakafu ya mto huo, walifika kwa urahisi Babeli wakipitia malango yaliyokuwa kando ya mto huo. Wakipita haraka-haraka barabarani na kuwachinja wo wote waliopinga, watekaji hao waliteka jengo la mfalme na kumwua mtawala mkaaji Belshaza. Hivyo kwa usiku mmoja, pasipo kung’ang’ana sana, Babeli yenye nguvu ikaanguka.
Hayo yote yanahusianaje na ahadi ya “mbingu mpya na [dunia] mpya”? Kuna uhusiano wa moja kwa moja. Baada ya kuanza kusimulia ahadi ya “mbingu mpya na [dunia] mpya,” neno la Yehova kupitia kwa Isaya laendelea kusema hivi: “Furahini, mkashangilie daima, kwa ajili ya hivi niviumbavyo; maana, tazama, naumba Yerusalemu uwe shangwe, na watu wake wawe furaha. Nami nitaufurahia Yerusalemu, nitawaonea shangwe watu wangu; sauti ya kulia haitasikiwa ndani yake tena, wala sauti ya kuomboleza.”—Isa. 65:17-19
Baada ya kurudi kwa wahamishwa hao kwenye nchi ya Yuda na kumalizika kwa kazi ya kujenga upya, kwa hakika Yerusalemu ulipata kuwa “shangwe,” ukaacha kuwa mahali pa ukiwa wa kuombolezea. Sauti ya kulia yenye kutokana na misiba ya vita iliyokuwa imesikiwa barabarani mwa mji huo makumi ya miaka yaliyotangulia haikusikiwa tena. Katika mwaka 537 K.W.K., wakati nchi hiyo ilipoanza kukaliwa tena na Waisraeli waliorudishwa, ‘dunia mpya’ ilitokea. Hiyo ‘dunia’ ya Waisraeli waliorudishwa, ilitawalwa na “mbingu mpya,” kwa kuwa kupitia kwa Liwali Zerubabeli na Kuhani Mkuu Yoshua, Yehova Mungu aliongoza na kusimamia wahamishwa waliorudishwa.—Isa. 51:16; Hag. 1:1, 14.
Kwa sababu ya utimizo huo wa unabii wa Isaya, twaweza kusema kwamba unatokana na Mungu, unatimiza matakwa yote matatu ya unabii wa kweli. Kwa sababu chanzo cha ujumbe huo ni Mungu wa milele, Yehova, twaweza kuwa na hakika kwamba ahadi hiyo iliyotajwa tena ya “mbingu mpya na [dunia] mpya” itatimizwa kwa njia nzuri sana.
KUTIMIZWA KWA AHADI ILIYOTAJWA TENA
Kwa wazi, kwa kadiri taratibu ya mambo iliyopo itakavyoendelea, hatuwezi kutazamia haki iwepo kati ya wanadamu. Hivyo, taratibu iliyopo lazima ikome. Jambo hilo litatokea wakati Yehova Mungu, kupitia kwa Mwanawe, atakapochukua hatua juu ya wote wale wanaodumu katika mwendo unaoharibu amani na furaha ya jamii ya kibinadamu. Uhakika wa kwamba siku hiyo kuu ya hukumu ya kuua haijafika haupaswi kufahamika vibaya, kwa kuwa kupita kwa wakati kumekuwa na kusudi lenye kufaidi. Akieleza juu ya hilo, mtume Petro aliandika hivi: “[Yehova] hakawii kuitimiza ahadi yake, kama wengine wanavyokudhani kukawia, bali huvumilia kwenu, maana hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikie toba.”—2 Pet. 3:9, 10; 2 The. 1:6-10.
Kwa kutenda kwa hekima, hakuna ye yote wetu ambaye angetaka kuichukua subira ya Mungu vivi hivi. Siku ya kupambana inakaribia sana wakati wote. Tukio hilo likimpata mtu katika hali isiyokubalika mbele ya Muumba hiyo itamaanisha msiba. Ni kwa sababu hiyo Yesu Kristo alitoa onyo hili: “Jiangalieni, mioyo yenu isije ikalemewa na ulafi, na ulevi, na masumbufu ya maisha haya; siku ile ikawajia ghafula, kama mtego unasavyo; kwa kuwa ndivyo itakavyowajilia watu wote wakaao juu ya uso wa dunia nzima. Basi, kesheni ninyi kila wakati, mkiomba, ili mpate kuokoka katika hayo yote yatakayotokea, na kusimama mbele za Mwana wa Adamu.”—Luka 21:34-36.
Wale watakaosimama wamekubalika wataona kutimizwa kwa maneno yafuatayo baadaye: “[Mungu] atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.” (Ufu. 21:4) Lo! hiyo itakuwa faraja kubwa namna gani kwa wanadamu! Kuhuzunika kote kwa sababu ya uonezi, kuteseka na kunyanyaswa hakutakuwepo wakati huo. Maumivu yenye kutaabisha yatakuwa mambo ya wakati uliopita. Kifo hakitaua tena wapendwa wetu. Amani itakuwa kila mahali. Watu wote watachochewa na upendo wa kweli katika kunia, kunena na kutenda.
Hata wale waliokufa hawatakosa kuona kutimizwa kwa ahadi ya Mungu. Sababu gani hivyo? Biblia inajibu hivi: “Kutakuwa na ufufuo.” (Matendo 24:15) Yesu Kristo akiwa alifufuliwa kutoka kwa wafu—jambo la hakika ambalo lilishuhudiwa na zaidi ya mashahidi 500—anatoa msingi wa tumaini hilo.—1 Kor. 15: 3-6, 13, 16.
Hakika, ni habari bora zaidi kwamba ahadi ya Mungu ya ‘mbingu mpya na dunia mpya’ inaelekea kwa haraka kutimizwa. Hivyo, kuna uhitaji wenye uharaka kwetu kutafuta msimamo wenye kukubalika mbele ya Muumba wetu. Hivi ndivyo mtume Petro alivyowasihi waamini wenzake wafanye, akisema hivi: “Kwa kuwa mnatazamia mambo hayo, fanyeni bidii ili mwonekane katika amani kuwa hamna mawaa wala aibu mbele yake.” (2 Pet. 3:14) Je! hilo ndilo jambo unalojitahidi kufanya?
[Picha katika ukurasa wa 4]
Wakati Wayahudi waliohamishwa waliporudi kutoka Babeli, ‘dunia mpya’ ilisimamishwa
[Picha katika ukurasa wa 5]
Mpatieni yatima haki yake; mteteeni mjane.”—Isa. 1:17