Angalia Usiwatungie Wengine Nia Mbaya
“NIAMBIE. Hukunisalimu barabarani juzi, sababu gani? Una ubaya gani nami?”
“Tulikutana? Ala, sikumbuki!”
“Sivyo kabisa! Tulikutana na hata ukanitazama machoni, bali hukunisalimu! Ewe una ubaya gani nami?”
Je! umepata kuona au kushuhudia hali inayofanana na kisa hicho cha kweli? Pengine umekwisha kuona kisa kizito hata zaidi wakati mtu alipotungiwa nia mbaya. Kutilia shaka na kutotumainia pasipo msingi hakumpendezi Mungu. Jambo hilo linaonyeshwa wazi na matokeo mabaya yanayoweza kutokezwa na tabia hizo. Yafikirie yale yaliyotukia katika nyakati za Kibiblia kwa taifa la Israeli.
Baada ya kushinda Nchi ya Ahadi, makabila mawili na nusu ya Kiisraeli yalitwaa maeneo yao waliyogawiwa katika ng’ambo ile nyingine ya Mto Yordani. Hapo walijenga madhabahu, si ya kutoa matoleo na dhabihu bali ya kuwa ushuhuda kwamba wao na watoto wao hawakuwa wameiacha ibada ya kweli. Walakini yale makabila mengine yaliwatungia nia mbaya, wakiwashuku (wakitilia shaka) Waisraeli hao kuwa walikuwa wameachana na ibada ya Yehova, na hivyo yakaamua kupigana nao. Ni jambo la furaha kwamba hali hiyo ilielezwa wazi vizuri na tendo la kijeshi lililokuwa likifikiriwa halikutekelezwa.—Yos. sura 22.
Pindi moja Mfalme Daudi alituma watumishi wake wakamfariji Mfalme Hanuni wa Amoni baada ya kifo cha babaye. Walakini Waamoni walimshuku Daudi isivyofaa kuwa alikuwa ametuma wanaume hao kama wapelelezi, na kwa hiyo akawaaibisha sana. Jambo hilo hata likaongoza kwenye vita, ambavyo katika hivyo Waamoni na Washami walishindwa vibaya sana. Yalikuwa matokeo mabaya kama nini ya kutungia wengine nia mbaya!—2 Sam. sura 10.
NIA NJEMA ZINAPOTILIWA SHAKA
Katika pindi fulani, katika siku za Wakristo wa kwanza, watu walitungiwa nia mbaya. Kwa mfano, jambo hilo lilimpata mtume Paulo. Kwa hiyo, akalazimika kuandika hivi: “Sikuwalemea. Hata hivyo, mwasema, nilikuwa ‘mwenye hila’ nami niliwapata kwa ‘ujanja.’ “Ndiyo, waamini wenzi fulani katika Korintho walibisha isivyofaa kwamba Paulo hakuwa akitenda kwa sababu ya upendo. Walimtungia isivyofaa mtume huyo mwaminifu nia mbaya.—2 Kor. 12:16, NW.
Mfano wenye kutokeza ni kisa cha Mwana wa Mungu. Yeye alikuja duniani akiwa na nia iliyo njema zaidi, wakati wote akijitahidi kutukuza na kuondolea lawama Yehova Mungu. Hata hivyo, kwa uongo alishtakiwa kukufuru. (Mt. 26:64, 65) Matokeo yenye msiba yaliwapata wale waliomtungia Mwana wa Mungu nia mbaya kwa makusudi, wakawa wenye hatia ya kuuawa kwake na kujitahidi kuzuia njia ya wokovu ya watu wengi.—Mt. 23:29-39.
Hata Yehova Mungu ametungiwa nia mbaya. Shetani na mashetani wake anashikilia kwamba Mungu hatawali kwa sababu ya upendo. Mahali pake, Ibilisi anashikilia kwamba Yehova akijifikiria mwenyewe tu huwanyima wanadamu jambo fulani zuri kwa kuweka adili na wema wa kuwazuia. Zaidi ya hayo, Shetani anashikilia kwamba Mungu hutoa malipo ili watu wamtii. (Ayubu 2:3-5) Vivyo hivyo, nia njema za watumishi wa Mungu hutiliwa shaka na Shetani. We, Ibilisi ‘amewashtaki mchana na usiku mbele ya Mungu!’ (Ufu. 12:10) Bila shaka, watu watawa wasingependa kamwe kumwiga Shetani kwa kutungia wengine nia mbaya.
JIHADHARI NA KUTOFAHAMU VEMA
Wakristo wanaweza kujifunza jambo gani kutokana na maandishi ya Biblia? Jambo moja ni kwamba inawezekana kufahamu vibaya maoni na nia za wengine. Ndivyo walivyofanya Waamoni wakati Daudi alipotuma wanaume fulani wakamfariji Mfalme Hanuni. Leo, mtu anaweza kuwa mwenye haya na mnyamavu. Pengine vilevile ana sura ya ukali. Huenda wengine wakakata kauli isivyofaa kwamba yeye ni mwenye ubaridi, kiburi na asiye na upendo, ingawa huenda isiwe hivyo kabisa.
Nyakati nyingine watu huwatungia wengine uvivu kwa makosa. Walakini yule ambaye wanamwona kuwa mvivu huenda akawa anafanya yote awezayo. Huenda asiweze kufanya zaidi au kufanya kazi kwa haraka zaidi kwa sababu ya udhaifu fulani wa kimwili au tatizo la afya. Kwa hiyo ni vizuri kufahamu kwamba kwa sababu nyingi nyingi, si watu wote walio na matokeo na ustadi unaolingana.
Nyakati nyingine, wale ambao wamejaribu kuhangaikia wengine kwa upendo wametungiwa nia mbaya. Kwa mfano, katika afisi fulani watu kadha hupeana zamu ya kujibu simu hata baada ya saa za kawaida za kazi. Si lazima waketi mahali ilipo simu wakingojea ilie, bali wanaweza kufanya jambo jingine katika chumba kilicho karibu. Siku moja, mtu mwenye madaraka ambaye hakuwa kazini alikuwa karibu kabisa na simu wakati ilipolia. Kwa huruma, aliijibu ili kwamba mtu yule aliyekuwa kazini asikatishe utendaji aliokuwa akiendelea nao katika chumba kilichokuwa karibu. Hata hivyo, inasikitisha kwamba yule aliyekuwa kazini alitunga nia mbaya mahali pa kumshukuru mtu huyo mwenye huruma kwa ajili ya msaada wake wa upendo. Je! ni kajambo kadogo? Ndiyo, walakini kanaonyesha uhitaji wa kujihadhari na kutofahamu vema wakati wa kuchanganua maoni na nia za wengine.
KUWASADIKI WENGINE
Kwa kuyaona matokeo yenye kusikitisha ya kutungia wengine nia mbaya, bila shaka tungependa kuepuka kufanya hivyo. Wakristo wanatenda kwa hekima kwa kuwasadiki wengine. Jambo hilo linapatana na kanuni ya kimungu iliyoelezwa na mtume Paulo, ambaye alisema kwamba upendo “huamini yote.” (1 Kor. 13:7) Kushikamana na kanuni hiyo kwa hakika kunamaanisha kutumaini Mkristo mwenzako kunapokuwa na mashaka, mahali pa kumshuku isivyofaa.
Kufahamiana vema zaidi na wengine kwaweza kutusaidia kuepuka kutungia wengine nia mbaya. Wakati mwingine jambo hilo linachukua miezi mingi, au hata miaka. Walakini katika visa vingi, kwa kadiri tulivyo na habari nyingi zaidi, ndivyo hatari ya kuwatungia wengine mabaya inavyopungua.
NIA ZETU ZINAPOTILIWA SHAKA
Lakini namna gani ikiwa sisi ndio tunaotungiwa nia mbaya? Twapaswa kutendaje? Ni vizuri kutokasirika, kwa kuwa Mhubiri 7:9 lasema hivi: “Usifanye haraka kukasirika rohoni mwako.” Muda upitapo, huenda mtu yule mwingine akakufahamu vizuri zaidi naye huenda akarekebisha maoni yake. Akiisha kuthamini kwamba alikosea, atakupenda hata zaidi, sana sana iwapo hukutenda kwa hasira. Bila shaka, Wakristo wanataka kumwiga Mungu, ambaye huonyesha kujiweza anaposhtakiwa. Vilevile, Yehova anazifahamu nia zetu, naye atatufariji. Tutapata furaha iwapo tutaendelea ‘kutumaini [Yehova] na kutenda mema.’ Iwapo yeye ataka kutuondolea lawama katika jambo fulani, aweza kufanya hivyo wakati ufaao.—Zab. 37:3-8; Matendo 15:8; 2 Kor. 7:6.
Sana sana hali ngumu sana inatokea wakati mtu anapopata shauri kutoka kwa mtu anayefahamu vibaya nia zake. Jambo liwalo lote likisemwa katika kujitetea laweza kuonwa kuwa ni kujionyesha kuwa mwenye haki. Hata hivyo, kwa hakika, huenda shauri hilo lisihusu kwa sababu mambo yote hayakufikiriwa. Huenda bado washauri fulani wenye kusudi jema wakatilia shaka nia zako ukijaribu kuonyesha hali ilivyo kabisa. Hivyo, suala lenyewe likiwa halina maana sana, unaweza kuchagua kutosema zaidi ili kusahihisha maoni ya mshauri huyo, mradi hakuna matokeo mabaya yanayoweza kutazamiwa kwa ajili ya kunyamaza. Walakini nyakati zote haitakiwi kwamba usiseme hata kidogo iwapo msimamo wako au nia zako zimefahamika vibaya. Bila shaka, kwa adili lingekuwa jambo baya kukubali uongo uwepo pasipo kupingwa. Kuna visa vinavyofaa kueleza msimamo au maoni yako kwa utulivu, ili kwamba dhamiri yako itulie kwa sababu unafahamu kwamba ulijaribu kueleza wazi mambo mahali pa kuwa na hatia ya kukubali shtaka la uongo bila upinzani wo wote. Kwa njia hiyo mshauri huyo anaweza kufaidika pia, sana sana kwa habari ya kusitawisha usawa katika kutoa shauri.
Mithali ya Kijeremani husema hivi, “Mtu akisema uongo mara moja, hataaminiwa tena, hata akisema kweli.” Lakini jambo hilo halipaswi kuwa hivyo kati ya Wakristo. Mtu akitenda kosa ambalo linakuja kujulikana na wengine, na kisha tukio la baadaye liwakumbushe watu fulani juu ya kosa hilo la wakati uliopita, je! hawapaswi kumshuku mtu huyo aliyekosa katika wakati uliopita? Kwa lazima sivyo, kwa kuwa upendo haufanyi haraka kumhukumu mtu. Iwapo sisi, ingawa hatuna hatia, tunashukiwa jambo fulani kwa sababu tu tulitenda jambo kama hilo wakati uliopita, je! tusingeumizwa na kutokututumaini wanakoonyesha wengine? Bila shaka ingekuwa hivyo, kwa kuwa chini ya uongozi wa roho takatifu ya Mungu, watu wamefanya mabadiliko makubwa na kuwa bora. Vilevile ni jambo zuri kukumbuka kwamba “upendo . . . hauhesabu mabaya.”—1 Kor. 6:9-11; 13:4, 5.
UHITAJI WA KUJIHADHARI NA KUWA NA USAWA
Tunapojitahidi kufuata kanuni ya kutotungia wengine nia mbaya na ya kuwa na usawa makusudi yetu wenyewe yakifahamika vibaya, twapaswa kukumbuka kwamba kuna uhitaji wa kujihadhari. Kwa mfano, wakati Wakristo wanapoishi chini ya utawala unaowatesa watumishi wa kweli wa Mungu, wakuu fulani wanaweza kutumia hila ili wawafanye wasaliti waamini wenzao. Katika visa hivyo, mtu anawezaje kuamini kila usemi au ahadi inayotolewa na watesi hao? Kanuni ifuatayo ya Neno la Mungu inahusu katika hali hiyo: “Mjinga huamini kila neno; bali mwenye busara huangalia sana aendavyo.” Naye Yesu Kristo aliwaambia wafuasi wake ‘wawe na busara kama nyoka.’—Mit. 14:15; Mt. 10:16.
Hata hivyo, Wakristo wanapaswa kutumaini na kuamini waabudu wenzao wa Mungu maadamu hakuna ushuhuda hakika wa kukosa ushikamanifu. Twafanya vema kukumbuka maneno yaliyoongozwa kwa roho: “Wewe u nani unayemhukumu mtumishi wa mwingine?” “Mtoa sheria na mwenye kuhukumu ni mmoja tu, ndiye awezaye kuokoa na kuangamiza. U nani wewe umhukumuye mtu mwingine?”—Rum. 14:4; Yak. 4:12.
Je! unakumbuka kisa kile kilichotajwa mwanzoni? Mtu mmoja alikuwa amemtungia nia mbaya mwingine ambaye alikosa kumsalimu. Haya, katika mazungumzo ya baadaye ilionekana kwamba mwanamume huyo alikuwa akifikiria naye hakumtambua mwanamke huyo. Hiyo ndiyo sababu tu iliyomfanya akose kumsalimu. Ni jambo zuri kwamba mwanamke huyo alizungumza na mwanamume huyo juu ya maoni yake naye hakumwekea kinyongo huku akinyamaza. Walakini suluhisho lililo hata bora zaidi la tatizo hilo lingekuwa kuwazia tangu mwanzoni kwamba mtu yule mwingine alikosa kumwona tu.
Hakika, kuna uhitaji wa kuwa na usawa katika kuchanganua nia za wengine. Ni jambo la furaha kwamba kutakuwako wakati ambapo hakuna mtu ye yote duniani atakayetilia shaka maneno au matendo ya wanadamu wenzake. Mwishowe, hivyo ndivyo itakavyokuwa katika taratibu mpya ya mambo chini ya utawala wa ufalme. Wakati huo kila mtu ataonyesha upendo naye ataona sifa njema za wengine. Hakutakuwako tena sababu za kukasirika, kuumwa moyo, uchungu wa moyoni au kuvunjika moyo. Mpaka wakati huo, twapaswa kuangalia tusitungie wengine nia mbaya isivyofaa.