Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 5/15 kur. 26-29
  • Jihadhari na Kuhesabia Nia Mbaya

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jihadhari na Kuhesabia Nia Mbaya
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Somo Kutoka Wakati Uliopita
  • Jinsi Tuwaonavyo Wazee
  • Hisia juu ya Wazazi
  • Mtazamo Wetu Kuelekea Wakristo Wenzetu
  • Chochewa na Upendo
  • Angalia Usiwatungie Wengine Nia Mbaya
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Upendo—“Njia Bora Zaidi”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Ni Nini Ufunguo wa Ukristo wa Kweli?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Tumeokolewa, Si Kupitia Matendo Tu, Bali Kupitia Fadhili Zisizostahiliwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 5/15 kur. 26-29

Jihadhari na Kuhesabia Nia Mbaya

MWENEZA evanjeli mashuhuri wa televisheni alitoa shutumu kali la hadharani dhidi ya mhubiri mwenzake kwa sababu ya kufanya uzinzi. Hata hivyo, baada ya mwaka mmoja, yule mwevanjeli mwenye kushtaki alifumaniwa akiwa pamoja na malaya.

Katika kisa kingine, serikali moja kuu ya ulimwengu ilituma wajumbe ili kuleta vikundi vyenye kupigana ili kujadiliana juu ya amani. Wakati huohuo, taifa lilelile lilituma kisiri wafanya-biashara walo wa silaha hadi mataifa ya kigeni kuuza silaha zenye thamani ya mabilioni ya dola.

Kwa kuwa unafiki mbaya umekuwa jambo la kawaida hivyo, je, inashangaza kwamba hali ya kushuku imechukua mahali pa itibari? Kwa wengi, kushuku nia za wengine kumekuwa zoea.

Tukiwa Wakristo, ni lazima tuwe waangalifu kutoruhusu mitazamo hiyo kuathiri uhusiano wetu pamoja na waamini wenzetu. Ijapokuwa Yesu Kristo alitusihi sana kuwa “wenye hadhari kama nyoka” tunapokuwa miongoni mwa adui zetu, hakusema kwamba twapaswa kuwa wenye kushuku wafuasi wake wa kweli. (Mathayo 10:16) Hivyo basi, hatari za kuhesabia wengine nia mbaya ni zipi? Ni katika maeneo gani lazima hasa tuwe waangalifu kuepuka mwelekeo huo? Na twawezaje kulinda salama uhusiano wetu wenye thamani pamoja na Wakristo wenzetu?

Somo Kutoka Wakati Uliopita

Kuhesabia wengine nia mbaya bila sababu hakika, ni sawa na kuwahukumu. Ni kana kwamba tunafanya hukumu kabla ya wakati kwamba maneno na vitendo vyao ni udanganyo unaoficha jambo fulani lenye vipengee na linalonuiwa kudhuru wengine. Mara nyingi kinachosababisha hilo tatizo ni maoni yenye makosa juu ya mambo, kama inavyoweza kuonekana katika simulizi la Biblia lipatikanalo kwenye Yoshua sura ya 22.

Waisraeli walikuwa wamekamilisha ushindi wao wa Bara Lililoahidiwa na walikuwa tu wamepokea maeneo yao ya kikabila. Makabila ya Reubeni na Gadi na nusu kabila la Manase yalijenga “madhabahu kubwa” kando ya Mto Yordani. Makabila yale mengine yalidhania kimakosa kwamba hilo lilikuwa tendo la uasi-imani. Ilidhaniwa kwamba hayo makabila matatu yangalitumia jengo hilo kubwa kwa ajili ya dhabihu badala ya kwenda kwenye hema la kukutania katika Shilo, mahali palipowekwa rasmi kwa ajili ya ibada. Mara moja, yale makabila yenye kushtaki yakafanya matayarisho kwa ajili ya hatua ya kijeshi.—Yoshua 22:10-12.

Ni jambo lililostahili sifa kwamba waliwasiliana na ndugu zao Waisraeli kwa kutuma ujumbe rasmi ulioongozwa na Finehasi. Waliposikia mashtaka ya kukosa uaminifu, uasi na uasi-imani dhidi ya Yehova, makabila yaliyodhaniwa kukosea yalieleza sababu yazo ya kujenga madhabahu hiyo kubwa mno. Badala ya kuwa madhabahu ya dhabihu, ilikuwa ni “ushahidi” wa muungano wa makabila ya Israeli katika kumwabudu Yehova. (Yoshua 22:26, 27) Hao wajumbe walirudi nyumbani wakiwa wameridhika kwamba ndugu zao hawakuwa na kosa lolote. Hivyo vita ya wenyewe kwa wenyewe na umwagikaji wa damu wenye kuogofya ziliepukwa.

Ni somo lililoje kwetu tusiwe kamwe wenye haraka ya kuhesabia wengine nia mbaya! Mara nyingi yale yaonekanayo kuwa kweli kwa maoni ya kijuu-juu tu yanapatikana kuwa tofauti kabisa yanapochunguzwa kwa uangalifu. Hilo ni kweli katika pande nyingi mbalimbali za maisha ya Mkristo.

Jinsi Tuwaonavyo Wazee

Katika kutekeleza madaraka yao “kulichunga kutaniko la Mungu,” nyakati nyingine wazee hulazimika kushauri watu mbalimbali kutanikoni. (Matendo 20:28) Mathalani, tunaitikiaje mzee akisema nasi juu ya watoto wetu juu ya mambo kama ushirika mbaya au mwenendo usiofaa pamoja na mtu wa jinsia tofauti? Je, tunakata kauli kwamba ana nia iliyofichwa na kujisemea, ‘Yeye hakupenda familia yetu kamwe’? Tukiruhusu hisia kama hizo ziwe na uvutano juu yetu, tungeweza kusikitika baadaye. Hali-njema ya kiroho ya watoto wetu yaweza kuwa hatarini, na twapaswa kuthamini shauri la Kimaandiko lenye kusaidia.—Mithali 12:15.

Mzee wa kutaniko anapotushauri, na tusitafute nia fulani iliyofichwa. Badala ya hivyo, na tujiulize wenyewe ikiwa kuna njia fulani ambayo tunaweza kunufaika na shauri lake lenye kutegemea Biblia. Mtume Paulo aliandika hivi: “Kwa kweli, hakuna nidhamu ionekanayo kwa wakati wa sasa kuwa yenye shangwe, bali yenye kihoro; lakini baadaye kwa wale ambao wamezoezwa nayo hiyo hutoa tunda lenye kufanya amani, yaani, uadilifu.” (Waebrania 12:11) Hivyo acheni tuwe wenye shukrani na tufikirie mambo kwa njia ya haki. Kumbuka kwamba mara nyingi ni vigumu kwa wazee kutoa shauri kama ilivyo kwetu kulipokea.

Hisia juu ya Wazazi

Wanapokabili vizuizi fulani kutoka kwa wazazi, vijana fulani hushuku nia za wazazi wao. Huenda vijana fulani wakasema hivi: ‘Kwa nini wazazi wangu wanafanyiza sheria nyingi hivyo? Ni lazima wawe hawataki nifurahie maisha.’ Hata hivyo, badala ya kufikia mkataa huo, wachanga wahitaji kuchanganua mambo kwa njia ya haki.

Wazazi wamewatunza watoto wao kwa miaka mingi. Hilo limefanywa kwa kujidhabihu sana kimwili na vinginevyo. Je, kuna sababu yoyote kufikia mkataa kwamba sasa wameazimia kufanya maisha ya watoto wao walio matineja kuwa yasiyo na furaha? Je, si jambo lifaalo zaidi kufikiria kwamba upendo ndio huwachochea wazazi hao kulinda watoto wao na kuwatunza? Je, upendo huohuo hauwezi kuwa ndio unaowachochea kuwawekea watoto wao vizuizi fulani, ambao sasa wanakabili magumu maishani? Jinsi lingekuwa jambo la kukosa fadhili na shukrani kuwahesabia nia mbaya wazazi wenye upendo!—Waefeso 6:1-3.

Mtazamo Wetu Kuelekea Wakristo Wenzetu

Wengi huelekea kuwahukumu wengine kimbele na kuwa na maoni yasiyofaa juu yao. Vipi ikiwa sisi wenyewe tumekuwa na mtazamo kama huo na kwa njia fulani tumekuwa tukiwashuku watu fulani? Je, mitazamo ya kilimwengu ingeweza kuwa na uvutano juu yetu katika habari hiyo?

Kwa kielelezo, tuseme kwamba mmojawapo wa ndugu zetu wa kiroho ana makao mazuri na gari la bei ghali. Je, tukate kauli moja kwa moja kwamba yeye ni mwenye kufuatia vitu vya kimwili ambaye haweki masilahi ya Ufalme kwanza maishani mwake? Huenda Wakristo wengine wakaweza kulipia vitu vizuri, lakini hilo halimaanishi kwamba wana nia mbaya au ‘hawatafuti kwanza ufalme.’ Huenda wakawa na shughuli nyingi katika utendaji mbalimbali wa kiroho, wakitumia mali zao za kimwili kuendeleza masilahi ya Ufalme, labda katika njia isiyo ya wazi.—Mathayo 6:1-4, 33.

Kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza lilifanyizwa na watu wa namna zote—matajiri na maskini. (Matendo 17:34; 1 Timotheo 2:3, 4; 6:17; Yakobo 2:5) Mungu hakadirii watu kwa msingi wa hali yao ya kifedha, nasi hatupaswi kufanya hivyo. Twapaswa kuwapenda waamini wenzetu waliotahiniwa na wenye uaminifu, “bila kufanya jambo lolote kulingana na mwelekeo wenye kuegemea upande.”—1 Timotheo 5:21.

Katika ulimwengu huu unaokaa katika nguvu za Shetani, kuwa na maoni yasiyofaa na kushuku hudhihirika katika njia mbalimbali. Kwa kielezo, huenda mtu akaonekana kuwa mjeuri au mwenye kufuatia vitu vya kimwili kwa sababu tu ya malezi yake. Hata hivyo, tukiwa Wakristo, ni lazima tukatae maoni hayo. Tengenezo la Yehova si mahali pa kuwa mshupavu na mwenye kushuku. Wakristo wote wa kweli wanahitaji kumwiga Yehova Mungu, ambaye ‘hana ukosefu wa uadilifu au ubaguzi.’—2 Mambo ya Nyakati 19:7, NW; Matendo 10:34, 35.

Chochewa na Upendo

Maandiko yasema waziwazi kwamba “wote wamefanya dhambi na hupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23) Hivyo tunahitaji kuwaona waabudu wenzetu kuwa wale wenye muungano pamoja nasi katika kujitahidi kumtolea Yehova utumishi unaokubalika. Ikiwa tumeruhusu kushuku au hisia nyingine zisizofaa kuathiri uhusiano wetu pamoja na ndugu au dada wa kiroho, na tusali kwa ajili ya msaada wa Mungu kupambana na mtazamo huo ili tusiwe windo la Shetani. (Mathayo 6:13) Yeye alimsadikisha Hawa kwamba Yehova alikuwa na nia mbaya, hakuhangaikia hali-njema yake, na alikuwa akimnyima uhuru mbalimbali ambao ungemfanya awe na furaha kwelikweli. (Mwanzo 3:1-5) Kuwahesabia ndugu zetu nia mbaya husaidia malengo ya Shetani.—2 Wakorintho 2:11; 1 Petro 5:8.

Tukipata kwamba tuna maelekeo ya kuwahesabia wengine nia mbaya, tufikirie kielelezo cha Yesu Kristo. Ingawa alikuwa Mwana wa Mungu aliye mkamilifu, yeye hakutafuta nia mbaya katika mitume wake. Badala ya hivyo, Yesu alitafuta sifa nzuri ndani yao. Mitume wake waliposhindania wadhifa wa umashuhuri, hakuwa na kauli kwamba walikuwa na nia mbaya na kuweka mitume 12 wapya mahali pao. (Marko 9:34, 35) Wakiwa ni wasio wakamilifu, huenda ikawa walikuwa na uvutano na utamaduni wa Dini ya Kiyahudi yenye kuasi-imani, pamoja na mkazo wayo juu ya kiburi na tofauti za kijamii. Yesu alijua kwamba kichocheo cha msingi cha wafuasi wake kilikuwa upendo kwa Yehova. Kwa kuonyesha upendo huo na kwa kushikamana na Yesu, walithawabishwa sana.—Luka 22:28-30.

Ikiwa tungewaangalia waamini wenzetu waaminifu kwa kuwashuku, hilo lingekuwa kama kuangalia vitu kwa kutumia kipande cha kioo kinachofanya vitu vionekane vyenye makosa au kuwa na umbo baya. Hakuna kitu kingeonekana kama vile kilivyo kwa kweli. Na tuwaangalie kupitia kioo cha upendo. Kuona uthibitisho mwingi kwamba Wakristo wenzetu wenye uaminifu-mshikamanifu wanatupenda na wanastahili ufikirio wetu wenye fadhili. (1 Wakorintho 13:4-8) Hivyo na tuwaonyeshe upendo na tujihadhari na kuwahesabia nia mbaya.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Wewe huwaonaje wengine wanaomwabudu Mungu kwa uaminifu?

[Picha katika ukurasa wa 27]

Itibari na staha zawafanya Mashahidi wa Yehova wawe familia moja yenye furaha

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki