Ni Nini Ufunguo wa Ukristo wa Kweli?
LEO, watu walio wengi hudai kuwa Wakristo kuliko kikundi kingine chochote cha kidini. Lakini imani za hao wanaojiita wenyewe Wakristo hupingana, hawana umoja, na nyakati nyingine wao hata huuana. Kwa wazi, wengi si Wakristo wa kweli. Yesu alisema kwamba katika siku yetu, wengi wangemwambia, “Bwana, Bwana,” yaani, wangedai kuwa Wakristo, hata hivyo angewaambia hivi: “Sikuwajua ninyi kamwe; ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu.” (Mathayo 7:21-23) Kwa hakika, hakuna yeyote kati yetu ambaye angetaka kuwa miongoni mwa hao! Kwa hiyo tunaweza kujuaje kama sisi ni Wakristo wa kweli?
Hakika ni kwamba, mambo mengi yanahitajiwa ili kuwa Mkristo wa kweli. Mkristo wa kweli apaswa kuwa na imani yenye nguvu kwa sababu “pasipo imani haiwezekani kumpendeza [Mungu].” (Waebrania 11:6) Imani hiyo yenye nguvu yahitaji kuandamana na vitendo vinavyofaa. Mwanafunzi Yakobo alionya kwamba “imani pasipo matendo imekufa.” (Yakobo 2:6) Isitoshe, Mkristo apaswa atambue mamlaka ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” (Mathayo 24:45-47) Lakini ufunguo wa Ukristo wa kweli ni jambo jingine tofauti na hayo.
Ufunguo ni nini? Mtume Paulo alieleza hivi katika barua yake ya kwanza kwa Wakorintho: “Nijaposema kwa lugha za wanadamu na za malaika, kama sina upendo, nimekuwa shaba iliayo na upatu uvumao. Tena nijapokuwa na unabii, na kujua siri zote na maarifa yote, nijapokuwa na imani timilifu kiasi cha kuweza kuhamisha milima, kama sina upendo, si kitu mimi. Tena nikitoa mali zangu zote kuwalisha maskini, tena nikijitoa mwili wangu niungue moto, kama sina upendo, hainifaidii kitu.”—1 Wakorintho 13:1-3.
Kwa hiyo upendo ndio ufunguo wa Ukristo wa kweli. Imani, matendo, na ushirika unaofaa ni vya muhimu, vya lazima. Lakini bila upendo, thamani yavyo haitimizwi. Kwa sababu gani?
Kwa msingi, ni kwa sababu ya aina ya Mungu tunayemwabudu. Mtume Yohana alieleza kuhusu Yehova, Mungu wa Ukristo wa kweli, katika maneno haya: “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Yehova Mungu ana sifa nyingine nyingi, kama vile uweza, haki, na hekima, lakini kwa kuwa yeye kwa dhahiri ni Mungu wa upendo, angetaka waabudu wake wawe watu wa aina gani? Bila shaka, watu wanaomwiga na kusitawisha upendo.—Mathayo 5:44, 45; 22:37-39.
Kusudi Linalofaa
Naam, upendo unafanya Wakristo wawe kama Mungu wanayeabudu. Inamaanisha kwamba makusudi yao yanafanana na makusudi ya Mungu. Ni kusudi gani sana-sana lililomsukuma Yehova Mungu amtume Yesu duniani ili atupe nafasi ya kupata uhai wa milele? Upendo. Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Basi, ni kusudi gani linalopasa kutusukuma tufanye mapenzi ya Mungu? Tena, ni upendo. “Huku ndiko kumpenda Mungu, kwamba tuzishike amri zake; wala amri zake si nzito.”—1 Yohana 5:3.
Je, inawezekana kumtumikia Mungu bila kusudi zuri? Ndiyo. Paulo alitaja wengine katika siku yake waliokuwa wakitumikia kwa ajili ya kijicho na fitina. (Wafilipi 1:15-17) Hilo laweza kutukia kwetu. Ulimwengu huu ni wenye ushindani sana, na roho hiyo yaweza kutuvuta. Huenda tukawa na kiburi na kufikiri kwamba sisi ni wasemaji walio bora zaidi au twaweza kuangusha vichapo vingi kuliko wengine. Huenda tukalinganisha mapendeleo yetu ya utumishi na yale yanayoonewa shangwe na mtu mwingine na kuwa wenye kujifikiri wakuu—au wenye kijicho. Mzee huenda akawa na wivu kwa ajili ya cheo chake cha mamlaka, hata afikie hatua ya kumzuia mwanamume kijana mwenye uwezo asifanye maendeleo. Tamaa ya faida ya kibinafsi huenda ikatusukuma tusitawishe urafiki wa Wakristo walio matajiri zaidi hali tukiwapuuza walio maskini zaidi.
Mambo hayo yaweza kutukia kwa sababu sisi si wakamilifu. Hata hivyo, ikiwa—kama Yehova—tunafanya upendo uwe kusudi letu kuu, tutapiga vita juu ya mielekeo kama hiyo. Ubinafsi, tamaa ya kujitukuza, au kiburi cha kimbelembele vyaweza kusukuma nje upendo, hivi kwamba ‘haitatufaidi kitu.’—Mithali 11:2; 1 Wakorintho 13:3.
Upendo Katika Ulimwengu Wenye Ubinafsi
Yesu alisema kwamba wafuasi wake wasingekuwa “sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:14, NW) Twaweza kuepukaje kuelemewa na uvutano wa ulimwengu unaotuzunguka? Upendo utasaidia. Kwa mfano, leo watu huwa “wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu.” (2 Timotheo 3:4) Yohana alituonya tusiwe hivyo. Alisema hivi: “Msiipende dunia, wala mambo yaliyomo katika dunia. Mtu akiipenda dunia, kumpenda Baba hakumo ndani yake. Maana kila kilichomo duniani, yaani, tamaa ya mwili, na tamaa ya macho, na kiburi cha uzima, havitokani na Baba, bali vyatokana na dunia.”—1 Yohana 2:15, 16.
Hata hivyo, si rahisi kukataa katakata “tamaa ya mwili” na “tamaa ya macho.” Mambo hayo yanapendwa hasa kwa sababu yanavutia mnofu wetu. Isitoshe, kuna anasa nyingi tofautitofauti zipatikanazo leo kuliko zile zilizokuwako siku ya Yohana, kwa hiyo kama tamaa ya macho ilikuwa tatizo wakati huo, ni tatizo hata zaidi sasa.
Jambo la kupendeza ni kwamba, anasa nyingi za kisasa zinazotolewa na ulimwengu si mbaya zenyewe. Hakuna kosa lolote kuwa na nyumba kubwa, gari zuri, televisheni, au rekodiplea aina ya stereo. Wala haivunji sheria yoyote ya Kibiblia kwenda safari ndefu, zenye kupendeza na kuwa na likizo zenye kusisimua. Jambo kuu la onyo la Yohana ni nini, basi? Kwanza, vitu kama hivyo vikiwa vyenye maana sana kwetu, vinasitawisha ndani yetu roho ya ubinafsi, ya kupenda mambo ya kimwili sana, na ya kiburi. Na jitihada ya kuchuma pesa za kuvipata yaweza kutatiza utumishi wetu kwa Yehova. Hata kuvifurahia vitu hivyo kunachukua wakati, na ingawa kiasi fulani cha pumziko huleta burudisho wakati wetu si mwingi, kwa sababu ya wajibu wetu wa kujifunza Biblia, kukutana na Wakristo wenzetu kwa ajili ya ibada, na kuhubiri habari njema ya Ufalme.—Zaburi 1:1-3; Mathayo 24:14; 28:19, 20; Waebrania 10:24, 25.
Katika enzi hii ya kupenda vitu vya kimwili sana, kupiga moyo konde kunahitajiwa ili ‘kutanguliza Ufalme wa Mungu’ na kujizuia ‘tusiutumie ulimwengu sana.’ (Mathayo 6:33, NW; 1 Wakrintho 7:31) Imani yenye nguvu itasaidia. Lakini, upendo wa kweli kwa Yehova na kwa majirani wetu ndio hasa utakaotuimarisha tupinge mavutano ambayo, ingawa si mabaya yenyewe, huenda yakatuzuia ‘tusitimilize huduma yetu.’ (2 Timotheo 4:5) Bila upendo kama huo, thamani ya huduma yetu yaweza kupunguka iwe jitihada ya kijuujuu tu.
Upendo Katika Kundi
Yesu alikazia maana ya upendo aliposema hivi: “Hivyo watu watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.” (Yohana 13:35) Je! wazee wangetumia wakati mwingi sana wakichunga na kusaidia Wakristo wenzao ikiwa hawawapendi? Je! watu wa kundi wangevumilia udhaifu mbalimbali wa wenzao—kutia na wa wazee—ikiwa si kwa sababu ya upendo? Upendo unawasukuma Wakristo wasaidiane katika njia ya kimwili wanaposikia kwamba wengine wana uhitaji. (Matendo 2:44, 45) Pindi za mnyanyaso, Wakristo hulindana na hata hufiana. Kwa nini? Kwa sababu ya upendo.—Yohana 15:13.
Nyakati nyingine mathibitisho makubwa zaidi ya upendo huonekana katika mambo madogo. Mzee, ambaye tayari anabanwa na kazi nyingi, huenda akakaribiwa na Mkristo mwenzake anayetokeza tena lalamiko lisiloonekana kuwa la muhimu kwa mzee huyo. Je, mzee apaswa akasirike? Badala ya kuruhusu hilo liwe sababu ya mtengano, anashughulika na ndugu yake kwa saburi na kwa fadhili. Wanazungumzia jambo hilo pamoja, na hilo laimarisha urafiki wao pia. (Mathayo 5:23, 24; 18:15-17) Badala ya kila mtu kusisitizia haki zake, wote wapaswa kujaribu kusitawisha moyo mkubwa uliopendekezwa na Yesu, kwa kuwa tayari kusamehe ndugu zao “saba mara sabini.” (Mathayo 18:21, 22) Hivyo, Wakristo hujibidiisha sana kujivika upendo, “ndio kifungo cha ukamilifu.”—Wakolosai 3:14.
Kuzidisha Upendo Wetu kwa Mmoja na Mwenzake
Naam, upendo ni kusudi linalofaa la kumtumikia Yehova. Upendo utatuimarisha tuendelee kujitenga na ulimwengu, na upendo utahakikisha kwamba kundi litaendelea kuwa la Kikristo kwelikweli. Utasaidia wale wenye mamlaka wasiwe wenye kufuatia sana mafanikio hivi kwamba wanasahau fadhili na upole katika kushughulika na wengine, wakati ule ule upendo hautaachilia mafanikio. Upendo unasaidia sisi sote ‘tuwatii wenye kutuongoza, na kuwanyenyekea.’—Waebrania 13:17.
Mtume Petro alituhimiza tuwe na “upendo mwingi sana” kwa mmoja na mwenzake kwa sababu “upendo unafunika wingi wa dhambi.” (1 Petro 4:8, NW) Twaweza kufanyaje hivyo? Mwanadamu aliumbwa kwa mfano wa Mungu na hivyo ana uwezo wa kiasili wa kupenda. Lakini aina ya upendo tunayozungumzia inahitaji jambo fulani zaidi. Kwa kweli, huo ni tunda kuu la roho ya Mungu. (Wagalatia 5:22) Hivyo, ili kusitawisha upendo, ni lazima tujiweke katika hali ya kuweza kupata roho ya Mungu. Jinsi gani? Kwa kujifunza Biblia, iliyopuliziwa roho ya Yehova. (2 Timotheo 3:16) Kwa kusali tupate roho ya Yehova ili kujenga upendo wetu kwa Yehova na kwa ndugu zetu. Na kwa kushirikiana na kundi la Kikristo, ambamo roho hutiririka bila kizuizi.
Pia tunahitaji kujichunguza wenyewe ili kuona vitendo au mawazo yoyote yasio ya upendo. Kumbuka, upendo ni sifa ya moyoni, na “moyo huwa mdanganyifu kuliko vitu vyote, una ugonjwa na kufisha.” (Yeremia 17:9) Ujapokuwa msaada wote ambao Yehova hutoa, nyakati nyingine tutatenda katika njia isiyo ya upendo. Huenda tukasema na Mkristo mwenzetu tukiwa na ukali usiohitajiwa, au huenda tukakasirika na kuudhiwa na jambo linalosemwa. Kwa hiyo, twafanya vema kurudia sala ya Daudi: “Ee Mungu, unichunguze, uujue moyo wangu, unijaribu, uyajue mawazo yangu; uone kama iko njia iletayo majuto ndani yangu, ukaniongoze katika njia ya milele.”—Zaburi 139:23, 24.
Kama vile Biblia husema, “upendo haupungui neno wakati wo wote.” (1 Wakorintho 13:8) Tukizoea kupendana, hatutapatikana na kasoro yoyote katika nyakati za kujaribiwa. Upendo uliomo miongoni mwa watu wa Mungu unachangia sana paradiso ya kiroho iliyopo leo. Wale tu wanaopendana sana kutoka moyoni ndio watakaopata furaha ya kuishi katika ulimwengu mpya. Kwa hiyo, mwige Yehova kwa kuonyesha upendo kama huo na hivyo kuimarisha kifungo cha umoja. Sitawisha upendo, uwe na ule ufunguo wa Ukristo wa kweli.