“Upendo Una Nguvu Kama Mauti”
“Upendo una nguvu kama mauti . . . mwako wake ni mwako wa moto, na miali yake ni miali ya Yahu.”—Wim. 8:6.
1, 2. Ndoa ya kwanza ilitokeaje, na ni kwa sababu gani mume na mke wangeambatana?
ILIKUWA siku yao ya arusi yenye furaha. Nayo ilifanywa katika paradiso. Ni jambo gani lingekuwa lenye furaha zaidi kuliko hilo? Yehova alikuwa amemfanya mwanamume wa kwanza, Adamu alale usingizi mzito sana. Kisha Mungu alikuwa ametoa ubavu mmoja wa mwanamume huyo, na kufunika mahali hapo, naye alikuwa ameutumia ubavu huo kama msingi wa kumfanyiza mwanamke wa kwanza.
2 Wakati msaidizi huyo na mkamilishaji wake mzuri alipoletwa kwa Adamu, alifurahi sana—walakini si kadiri ya kukosa maneno. Alifurahi sana hata kwamba maneno yake ya kwanza aliyatamka kwa namna ya kimashairi, akasema: “[Hatimaye] sasa huyu ni mfupa katika mifupa yangu, na nyama katika nyama yangu, basi ataitwa mwanamke, kwa maana ametwaliwa katika mwanamume.” (Mwa. 2:20-23) Hatujaambiwa namna mwanamke huyu alivyoona katika siku hiyo ya arusi yao, ijapokuwa baadaye ilisemwa hivi juu ya mke mwenye dhambi na asiyekamilika: “Tamaa yako itakuwa kwa mumeo.” (Mwa. 3:16) Hivyo, bila shaka alipokuwa mkamilifu, mwanamke wa kwanza, Hawa, lazima awe alimfurahia mwenzi wake. Kwa kuwa alikuwa ametwaliwa katika mwili wa mwanamume, wangeambatana pamoja. Kama alivyosema Mungu: “Kwa hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja.”—Mwa. 2:24; Mt. 19:4, 5.
3. Sababu gani ndoa haikuwa mpango wa kikawaida tu usio na maono ya moyoni?
3 Ndoa iliyoanzishwa na Muumba katika bustani ya Edeni, ilikusudiwa iwe kifungo cha umoja chenye kudumu. Ilitoa nafasi ya kuwa na ushirika na kusaidiana, pamoja na kusudi lake kubwa—kuzaa na kulea washiriki wa jamaa ya kibinadamu—jambo ambalo lilikuwa taraja lenye furaha. (Mwa. 1:27, 28; Mt. 19:6-9) Walakini ndoa haikukusudiwa iwe mpango wa kikawaida tu usiotoa nafasi za kuonyesha maono ya moyoni. Wanadamu waliumbwa wakiwa na uwezo wa kuonyesha upendo—kwa habari ya wale walio katika mpango wa ndoa, ni yale mapenzi kati ya mwanamume na mwanamke ambayo ni maono ya moyoni yanayochochea umoja wa ndoa, pamoja na kuoneana shauku kunakoimarisha jamaa.
4. Kwa sababu ya matatizo ya leo ya ndoa, ni maulizo gani yanayoweza kutokezwa juu ya upendo na ndoa?
4 Huenda leo ndoa katika paradiso ikaonwa kuwa jambo lenye kufaa. Kwani, katika jamii ya kibinadamu isiyokamilika ndoa nyingi zinavunjika. Mara nyingi sana ule upendo wa asili unaonekana ukipungua navyo vifungo vya ndoa vinakatika. Hivyo, huenda mtu akataka kujua, Je! inawezekana wale waliooana kuwa na upendo mwingi na wenye kudumu? Au je! ni ujinga kufikiri kwamba kupendana na kuheshimiana ni mambo yanayoweza kudumu?
“UPENDO UNA NGUVU KAMA MAUTI”
5. Kwa ufupi, ni mambo gani yaliyomo katika Wimbo wa Sulemani, nacho kitabu hicho cha Biblia kinafunua nini juu ya upendo kati ya mwanamume na mwanamke?
5 Upendo wa kweli kati ya mwanamume na mwanamke waweza kuwa wenye nguvu sana, imara, usioshindwa. Hilo lilionyeshwa vizuri kama nini katika kitabu cha kimashairi cha Maandiko Matakatifu, kilichotungwa na Mfalme Sulemani wa Israeli mwenye hekima miaka 3,000 iliyopita! Kikiitwa Wimbo Ulio Bora (Wimbo wa Sulemani), kinaeleza juu ya upendo usioweza kupotoshwa uliokuwako kati ya mchungaji mmoja na msichana wa mashambani kutoka katika kijiji cha Shunemu (Shulemu). Huu “wimbo ulio bora” wafunua vilevile kwamba, akiwa na uzuri na mali zake zote, mfalme huyo hakuweza kuvuta upendo wa msichana huyo mzuri wa Shulemu.—Wim. 1:1-14; 8:4.
6. Sababu gani Wimbo wa Sulemani ni kitia-moyo kwa washiriki wa ‘‘bibi-arusi” wa Yesu Kristo, au kundi lililozaliwa kwa roho?
6 Huu “wimbo ulio bora” unaonyesha uzuri wa upendo wenye kudumu na wenye kuendelea. Upendo kama huo usioweza kupotoshwa unaonyeshwa na uhusiano ulio kati ya Yesu Kristo na “bibi-arusi” wake, au kundi lililozaliwa kwa roho. (Efe. 5:25-32; Ufu. 21:2, 9) Hivyo, huo Wimbo wa Sulemani unaweza kuwatia moyo wale wanaodai kuwa washiriki wa “bibi-arusi” huyo waendelee kuwa waaminifu kwa Bwana-arusi wao wa kimbinguni. (2 Kor. 11:2) Hata hivyo kitabu hiki kilichoongozwa kwa roho ya Mungu kinasema mengi juu ya upendo ulio safi unaoweza kuwako kati ya mwanamume na mwanamke wanaomwogopa Mungu.
7. Watu ambao bado hawajaoa au kuolewa waliojitoa kwa Yehova wanapaswa kufikiria mambo gani wanapotafuta mwenzi wa ndoa?
7 Kutoa mfano: Wimbo wa Sulemani unaonyesha waziwazi kwamba haiwezekani kumpenda mtu ye yote kwa mapenzi ya mahaba. Kwa mfano, yule Mshulami hakuvutiwa na Mfalme Sulemani, naye alisema hivi: “Nawasihi, enyi binti za Yerusalemu, kwa paa na kwa ayala wa porini, msiyachochee mapenzi, wala kuyaamsha, hata yatakapoona vema yenyewe.” (Wim. 2:7; 3:5) Hivyo, basi, ni jambo lenye hekima kama nini kwamba mtu asiyeoa au kuolewa angojee kwa subira mpaka apatikane mtu anayeweza kumpenda kweli kweli! Na kwa habari ya wale waliojitoa kwa Yehova, huyo mwenzi mtarajiwa katika ndoa lazima awe mwanamume au mwanamke ambaye amejitoa vivyo hivyo kwa Yehova na ambaye ni mwaminifu Kwake. (Kum. 7:3, 4; Ezra 9:1-15; 1 Kor. 7:39) Ndipo ibada ya Yehova itakuwa jambo lenye maana zaidi kwa wenzi hao wawili. Wataweza kukabili maisha pamoja wakiwa na umoja katika ndoa na katika hali yao ya kiroho, bila hivyo kungekuwa na utupu wenye kuhuzunisha sana.
8. Yule Mshulami alijionyeshaje kuwa kama ukuta, wala si kama mlango?
8 Hata hivyo, kabla ya kumwoa mwamini mwenzako, ni lazima usafi udumishwe na mtu anayetamani kupata kibali ya Mungu. Ndugu za yule msichana Mshulami walihangaikia sana usafi wake, hata tangu alipokuwa mchanga sana. Katika miaka ya mapema, mmojawapo wa ndugu za msichana huyo alikuwa amesema hivi kuhusu msichana huyo: “Kwetu sisi tuna umbu [dada] mdogo, wala hana maziwa [matiti]; tumfanyieje umbu letu, siku atakapoposwa?” Ndugu mwingine alijibu hivi: “Kama akiwa ukuta, tumjengee buruji za fedha; na kama akiwa ni mlango, tumhifadhi kwa mbao za mierezi.” Mfalme Sulemani alijaribu kumfanya Mshulami huyo ampende, walakini yeye alijionyesha kuwa imara na safi katika upendo, wala si kama mlango wenye kufungukafunguka uliohitaji kufungwa kwa mbao ili kuuzuia usifunguke na kuingiza watu wasiotakikana au wasio safi. Yeye hakushindwa na vishawishi vya mfalme, bali alikuwa amesimama imara kama vile ukuta na kushinda vishawishi vyote vya mambo ya kimwili, alikuwa amejionyesha kuwa mtu mzima na sasa angeweza kukubaliwa kuwa mwanamke aliyekomaa mwenye kufuata kanuni njema. (Wim. 8:8-10) Mfano mzuri sana wa wanawake wa leo wenye kumwogopa Mungu ambao hawajaolewa!
9. Yule Mshulami alionwaje na mchungaji aliyempenda?
9 Mshulami huyo mnyenyekevu hakuwa mwenye kujikuza, walakini machoni pa mchungaji aliyempenda alikuwa mtu wa pekee. “Mimi ni ua la uwandani, ni nyinyoro ya mabondeni,” akasema. Walakini sivyo alivyokuwa kwa mchungaji, aliyejibu hivi: “Kama nyinyoro kati ya miiba, kadhalika mpenzi wangu kati ya binti.” (Wim. 2:1, 2) Huu haukuwa upendo wa kupumbazwa tu. Msichana huyo alimtumikia Yehova, alikuwa na uwezo wa kufanya mambo, alikuwa mzuri naye alikuwa na mambo mengi ya kumletea sifa. Je! jambo hili halionyeshi kwamba wasichana Wakristo wasioolewa wapaswa kujifunza kukubali madaraka ya wanawake, huku wakijitahidi kusitawisha hali yao ya kiroho?
10. Mshulami naye alimwonaje mchungaji?
10 Walakini angalia namna Mshulami huyo alivyomwona yule mchungaji. “Kama [mtofaa] kati ya miti ya msituni,” akajibu, “kadhalika mpendwa wangu kati ya vijana.” Yeye hakuwa tu mmojawapo wa miti mingi ya msituni. Mchungaji wake alikuwa amejitoa kwa Yehova, naye alikuwa na sifa na uwezo wenye kutamanika, na bila shaka lazima yeye awe alikuwa kijana mwenye kupenda mambo ya kiroho. (Linganisha 1 Kor. 2:6-16.) Ndiyo, kwake yeye Mshulami, alikuwa “kama [mtofaa] kati ya miti ya msituni.” Je! kijana wa kiume Mkristo asiyeoa bado hapaswi kujitahidi ili siku moja apate kuonwa kuwa namna hiyo na mpenzi wake?
11. Kupatana na maneno ya Mshulami, upendo wa kweli unalinganaje na mauti na kaburi?
11 Hakuna shaka kwamba huyo Mshulami na huyo mvulana walikuwa na upendo unaofaa kati yao. Kwa hakika msichana huyo aliyaeleza mambo kama vile yalivyokuwa kweli kweli alipomwambia mchungaji wake mpendwa hivi: “Nitie kama muhuri moyoni mwako, kama muhuri juu ya mkono wako; kwa maana upendo una nguvu kama mauti, na wivu ni mkali kama [kaburi]. Mwako wake ni mwako wa moto, na miali yake ni miali ya Yahu [Yehova]. Maji mengi hayawezi kuuzimisha upendo, wala mito haiwezi kuuzamisha; kama mtu [kama vile Sulemani] angetoa badala ya upendo mali yote ya nyumbani mwake, angedharauliwa kabisa.” (Wim. 8:6, 7) Ni kweli kama nini! Upendo hauwezi kununuliwa kwa mambo ya kimwili. Walakini upendo halisi una nguvu kama mauti, ambayo bila kushindwa huendelea kuwapata wanadamu waliohukumiwa. Ndiyo, na katika kusisitiza uwe wa mmoja tu, upendo kama huo unakuwa kama kaburi lisiloshindwa, ambalo huendelea kupokea miili ya wanadamu. Lakini namna gani juu ya “miali ya Yahu”? Mwanachuo mmoja wa Biblia alisema katika wakati mmoja kwamba, “miali ya upendo inayowaka katika mioyo ya wanadamu hutoka kwa Yehova,” Mungu wa upendo ambaye aliweka uwezo huu mzuri sana ndani ya wanadamu. (1 Yohana 4:8) Kwa hakika, upendo wa kweli haushindwi, ni mshikamanifu, ni wenye kudumu. (Linganisha 1 Wakorintho 13:8.) Ni jambo la hekima kama nini kwamba wale wanaofikiria ndoa wangojee na kusitawisha ‘upendo wenye nguvu kama mauti’!
NAMNA UPENDO UNAVYOKUA
12. Ni mambo gani yanayoonwa maishani yanayoweza kuufanya upendo ukue kati ya mume na mke wake?
12 Hata hivyo upendo unaweza kukua kadiri maisha ya mume na mke yanavyofungamana zaidi na zaidi. Akiwa na umri wa miaka 40 na kuwa amekomaa, Isaka hakuwa kijana aliyepumbazwa tu na mapenzi, alipomchukua, si msichana tu, bali “mwanamke kijana,” Rebeka awe mke wake. “Naye akampenda,” ndivyo tunavyoambiwa. (Mwa. 24:57-67, NW) Kadiri miaka inavyopita, wenzi wa ndoa wenye kumcha Mungu wanashiriki mambo ya kiroho pamoja. Wanakabili majaribu na matatizo ya maisha pamoja. Jitihada zao za pamoja zinasitawisha kumbukumbu zenye furaha zinazowaleta karibu zaidi. Hata mambo mepesi—pengine maongezi yenye kufurahisha wanapotembea pamoja msituni na mashambani—yanakumbukwa kwa muda mrefu. Kwani, yule Mshulami mzuri alitamani sana kwenda kutembea mashambani pamoja na mchungaji wake! (Wim. 2:8:14) Na bila shaka, walipokwisha kuoana, lazima wawe walifanya hivyo mara nyingi.
13. Ni kwa nini mume ana sababu nzuri za kumpenda “mke [mwenye uwezo]”?
13 Lakini, bila shaka, upendo unakua kwa sababu nyinginezo zinazofaa. “Mwanamke [mwenye uwezo] ni taji ya mumewe,” ambaye bila shaka huwa na sababu nzuri za kumpenda. (Mit. 12:4) Katika maneno ya Mfalme Lemueli (pengine yale ya Sulemani), “mwanamke [mwenye uwezo]” ni mwenye thamani kuliko mapambo yanayotamaniwa sana yenye kufanyizwa kwa marijani yenye rangi nyingi. Yeye anaaminika naye humthawabisha mume wake na “mema wala si mabaya, siku zote za maisha yake.” (Mit. 31:1, 10-12) Kwa kutumia mikono yake kwa nia yeye anafanya mavazi ya moto kwa ajili ya jamaa yake. (Mit. 31:13, 19, 21-24) Anahangaika hivyo hivyo aone kwamba watu wa nyumba yake wanapata chakula chenye kufaa. (Mist. 14, 15) Mambo yanayohusu sehemu nyingi za nyumbani kwake aweza kuaminishwa, kwa kuwa yeye anafanya kazi kwa bidii na ni mwenye kuweza mambo. (Mist. 16-18, 27) Mwanamke kama huyo anasema kwa fadhili, ni mkarimu na hata huwafanyia mema hata watu mmoja mmoja wa nje ya nyumbani kwake. (Mist. 20, 26) Hivyo, hata kama uzuri wa uso wa mke anayemwogopa Mungu unapunguka baada ya kupita miaka mingi, uzuri wake wa ndani unaendelea kukua nao humfanya apendwe sana na wapendwa wake. “Upendeleo hudanganya, na uzuri ni ubatili; bali mwanamke amchaye [Yehova], ndiye atakayesifiwa.”—Mit. 31:30; 1 Pet. 3:3, 4.
14. Ni sifa gani za mume anayemwogopa Mungu zinazomfanya mke Mkristo amheshimu sana?
14 Kwa upande mwingine, mume mwenye kumwogopa Mungu anatimiza madaraka yake kabisa kama kichwa cha jamaa, walakini si kwa kudhulumu. (Mwa. 3:16; Mal. 2:14-16; 1 Kor. 11:3) Yeye anaendelea kumpenda mke wake naye anaonyesha hivyo katika njia mbalimbali. Kwa mfano, yeye hamwonei uchungu wa hasira. (Kol. 3:19) Yeye anafanya kazi kwa bidii ili kutoa mahitaji ya kimwili na ya kiroho kwa mke wake na wengine anaowapenda. (1 Tim. 5:8) Kwa kweli, mume mwenye kumwogopa Mungu humwangalia mke wake kwa upendo namna ile ile Yesu Kristo anavyoliangalia kundi Lake. (Efe. 5:25-32) Ni mke gani Mkristo ambaye hangeheshimu mume kama huyo?
15. Kwa kuendeleza kanuni za Biblia za ndoa, mume na mke watafurahia uhusiano wa namna gani?
15 Jitihada zenye kuendelea zitahitajiwa ili kuendeleza kanuni ambazo zimekwisha kutajwa, kutumia Maandiko pamoja na kumtegemea Yehova kwa sala. Walakini katika hali ya ndoa ambayo imesitawishwa hivyo lazima upendo ukue. Haitakuwa lazima mume adai aheshimiwe. Litakuwa jambo la kawaida kuheshimiwa na mke anayetendwa vema na anayependezwa na mambo ya kiroho. Wala mke hatakuwa na lazima ya kulalamika, akisema, ‘Wewe hunipendi!’ Ni mume gani Mkristo asingempenda mke mwenye uwezo wa kufanya mambo na anayemwogopa Mungu? (Tofautisha Waamuzi 14:15-17 na Ruthu 3:11.) Katika nyumba ya namna hiyo, kila mmoja wa wenzi wa ndoa akitimiza daraka lake la Kimaandiko, haitakuwa vigumu kutii shauri la kimtume: “Kila mume lazima ampende mkewe kama nafsi yake mwenyewe, naye mke anapaswa kumstahi mumewe.”—Efe. 5:33, HNWW.
“UMFURAHIE MKE WA UJANA WAKO”
16. Mithali sura ya 5 inawatiaje moyo wale waliooana wawe waaminifu kwa wenzi wao wa ndoa?
16 Ndoa ilikusudiwa iwaletee wanadamu furaha. Walakini ili jambo hilo lipate kuwa hivyo nao upendo wa ndoa uendelee, lazima mtu awe mwaminifu kwa mwenzi wake wa ndoa. Katika usemi wa mfano, Maandiko yanatumia usemi “chemchemi” kuonyesha chanzo cha kutosheleza tamaa ya ngono, jambo ambalo halipaswi kutafutwa nje ya kifungo cha ndoa. Bila shaka, kwa kufaa, upendo kati ya mume na mke unatia ndani ngono, walakini wote walio nje ya kifungo cha ndoa hawawezi kuruhusiwa katika uhusiano huo wa karibu sana wa ngono. Kwa kufaa sana, mume anaambiwa hivi: “Unywe maji ya birika lako mwenyewe . . . Je! chemchemi zako zitawanyike mbali . . . ? Yawe yako mwenyewe peke yako, wala si ya wageni pamoja nawe. Chemchemi yako ibarikiwe; nawe umfurahie mke wa ujana wako. Ni ayala apendaye na paa apendezaye [pengine kuonyesha uzuri]. . . . Kwa upendo wake ushangilie daima.” —Mit. 5:15-23; 7:6-23.
17. Kufikiriana kwa upendo kwa wale waliounganishwa katika ndoa kutakuwa na matokeo gani?
17 Wale waliounganishwa katika ndoa wana wajibu wa Kimaandiko wa kuwapa wenzi wao haki za ndoa. Hiyo ni njia moja ya kuonyesha upendo mwingi, nayo yanapokuwa ni matokeo ya asili ya upendo utokao moyoni katika kifungo cha ndoa, yaweza kulinganishwa na mapambo mazuri sana. Hivyo, basi, ni jambo la maana kama nini kwamba wenzi wanaomwogopa Mungu waepuke kuharibu hali hiyo, na kwamba waepuke mazoea ambayo yangeweza kuchafua malazi ya ndoa! (Ebr. 13:4) Kufikiriana kwa upendo namna hiyo katika mambo hayo yenye uhusiano wa karibu sana kutasaidia kuzuia ndoa isivunjike na kuleta maumivu makali na vilevile kutawalinda wale walio katika kifungo cha ndoa wasiangukie katika kufanya uasherati.—1 Kor. 7:1-5.
18. Anapojitahidi kutosheleza mahitaji ya mke wake ya moyoni na mengine yanayohusiana nayo, mume anayemwogopa Mungu atakumbuka nini?
18 Kwa hiyo, mume anayemwogopa Mungu atajitahidi kutosheleza mahitaji ya mke wake ya moyoni na mengine yanayohusiana na hayo, walakini atafanya hivyo kwa kujizuia kama vile anavyofanya mtu aliye na roho ya Mungu na anayeonyesha tunda lake la kujiweza. (Gal. 5:22, 23 NW) Kwa kufikiria vizuizi vyake vya mwilini na vya maumbile, kama vile alivyofanya Yehova katika Sheria waliyopewa Israeli, mume Mkristo atatenda “kwa akili,” na kumpa mke wake “heshima, kama chombo kisicho na nguvu.”—Law. 18:19; 20:18; 1 Pet. 3:7.
19. (a) Ni baraka kulea watoto katika mazingira ya namna gani ya nyumbani? (b) Watoto wanahitaji adabu ya namna gani?
19 Baada ya muda kupita, huenda kifungo cha ndoa kikatokeza watoto, “urithi kutoka kwa Yehova.” (Zab. 127:3, NW) Inakuwa baraka wakati wanapolelewa katika mazingira ya nyumbani ambamo wazazi wanaonyeshana upendo wenye nguvu na ambamo mambo ya kiroho yanathaminiwa sana. Ni kweli kwamba, watoto watahitaji mashauri na kuonyeshwa makosa yao, “[lakini] yeye ampendaye [mtoto wake] humrudi mapema.” (Mit. 13:24) Kutakuwako faida kubwa wakati adabu ya wazazi yenye msingi wa Kibiblia inapotolewa katika njia ya upendo.
MWIGE YULE MSHULAMI KATIKA IBADA YA PEKEE
20. Ni kujitoa na upendo wa nani unaopita upendo wo wote ulio kati ya mwanamume na mwanamke wo wote?
20 Upendo wa yule Mshulami kwa mchungaji wake ulikuwa “una nguvu kama mauti,” nao upendo wa watu wenye kumwogopa Mungu waliounganishwa katika ndoa leo waweza kuwa mkubwa vivyo hivyo. Walakini msichana huyo alisema hivi: “Kwa kusisitizia ibada ya pekee ni mshupavu kama vile Sheol.” (Wim. 8:6, NW) Upendo wa Yesu kwa mwili wa wafuasi wake watiwa mafuta unapita upendo wo wote ulio kati ya mwanamume na mwanamke ye yote, nako kujitoa kwa kundi hilo kwa Kristo hakushindwi ni kama Sheol (kaburi). Hata hivyo kwa upendo Yesu alikufa si kwa ajili ya wale tu watakaokuwa “bibi-arusi” wake wa kimbinguni bali vilevile na kwa ajili ya “kondoo wengine” wake, ambao sasa wanawakilishwa na “mkutano mkubwa” ambao wana mataraja yenye baraka sana ya uzima wa milele duniani.—Yohana 10:16; Ufu. 7:9.
21. (a) Mshulami aliweka mfano gani unaostahili kuigwa? (b) Tunafaidikaje kwa kufikiria yale ambayo Yesu ametufanyia?
21 Kwa hawa watumishi wa Yehova, yule Mshulami aliwawekea mfano unaostahili kuigwa wa ibada ya pekee. Kwa kutafakari juu ya yale ambayo Yesu ametufanyia kupitia kwa dhabihu yake ya ukombozi, na kwa kufikiria maneno yake yenye upendo na ahadi zake, upendo wetu kwake unaongezeka. Hilo nalo, hutulinda tusifuatie mambo ya kichoyo, ya kimwili na yasiyo ya kiroho. Vilevile linatia nguvu uhusiano wetu na Yehova, Mungu aliyewawezesha wanadamu kuwa na ‘upendo wenye nguvu kama mauti.’
[Picha katika ukurasa wa 17]
“Naye akampenda”