Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w81 9/15 kur. 3-6
  • Tazama Mbele Kabisa Ukiwa Mkristo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Tazama Mbele Kabisa Ukiwa Mkristo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • TUNAYOONA TUKITAZAMA MBELE KABISA
  • JITIHADA INAHITAJIWA ILI KUANGALIA MBELE KABISA
  • SITAWISHA MAONI YANAYOFAA
  • SITAWISHA IMANI NA TUMAINI KUBWA ZAIDI
  • USIWE NA MAHANGAIKO
  • IMARISHA HALI YAKO YA KIROHO
  • TEMBEA NA MUNGU
  • KUTAZAMA MBELE KABISA KUNALETA ZAWADI BORA
  • Je, Jicho Lako Ni “Rahisi”?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Endelea Kutazama, Endelea Kusonga Mbele Pamoja na Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Toa Ushahidi kwa Ajili ya Yehova na Usichoke
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Jinufaishe na Uwanufaishe Wengine Kwa Kutumia Neno La Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
w81 9/15 kur. 3-6

Tazama Mbele Kabisa Ukiwa Mkristo

WAWINDAJI hao wa pomboo (mnyama wa barafuni) walikuwa wamepotea bila tumaini lo lote katika ulimwengu usiokuwa na cho chote isipokuwa barafu na pepo zenye theluji zenye kupofusha. Mambo yalipokuwa mabaya zaidi, mmoja wao alisema: “Sisadiki kwamba ye yote wetu ataokoka aeleze kisa hiki.” Hata hivyo, wanaume kadha walizidi kukataa kufa moyo. Mmoja wao, kiongozi wa kikundi kimoja, alikuwa anafikiria kwa shauku juu ya mpenzi wake aliyekuwa anatarajia kumwoa. Wakati wenzake waliokwisha nguvu walipotaka kufa moyo, wakati wote uso wake uliendelea kuwa mbele yake. Yeye hakutaka kufa, naye akawatia moyo wenzake wasilale juu ya barafu bali wazidi kusonga. Yeye pamoja na wanaume wengine kama 50 waliokoka msiba huo. Upendo aliokuwa nao kwa mpenzi wake, ambaye alimwoa baadaye, na kuwa na sura ya uso wake katika jicho la akili yake yote hayo yaliokoa wengi wasife.

Hadithi hii ya kweli inaonyesha maana ya kutokosa kuona wakati wo wote lengo letu katika shindano letu la Kikristo la uzima. Nyakati nyingine, kupigana kwa Mkristo asiiache njia ya haki kwaweza kuwa kugumu kama shindano la wawindaji hao wa pomboo waliokuwa wamekwisha nguvu. Kifo huja wakati mtu anapoacha “kupigana” na kushindwa na kishawishi kikubwa cha kulala na kusinzia. Ni wenye furaha kama nini wale wanaoweka mbele ya jicho la akili zao sura inayowatia moyo waendelee kutazama mbele kabisa na kutokufa moyo!

Hivyo ndivyo watu waaminifu wa nyakati za kale walivyofanya. Kwa mfano, mahali pa kuendelea na maisha akiwa mkuu katika baraza ya Farao wa Misri, Musa alichagua “kupata mateso pamoja na watu wa Mungu.” Na sababu gani alifanya uchaguzi huo? “Kwa kuwa aliyatazamia hayo malipo.” Ndiyo, Musa alitazama mbele na kuona si ile zawadi tu bali pia Yeye aliyetoa taraja la zawadi hiyo. Ilikuwa kana kwamba, Musa alimwona “Yeye asiyeonekana,” Mungu wake Yehova,—Ebr. 11:24-27.

Vilevile, Yesu Kristo hakufa moyo wakati wa kushindana kwenye uchungu ili aendeleze ukamilifu wake, hata ingawa alilazimika kufanya hivyo kwa “kulia sana machozi.” (Ebr. 5:7) Alijifunza kutii kutokana na mateso yaliyompata, naye akaendelea kutazama mbele kabisa kwenye zawadi ambayo Babaye, Yehova, alikuwa ameweka mbele yake.​—Ebr. 12:2.

TUNAYOONA TUKITAZAMA MBELE KABISA

Mungu Aliye Juu Zaidi anajifunua kwa wanadamu kupitia kwa jina lake Yehova na kupitia kwa upendo, rehema, uangalizi wa huruma na ukarimu wake. (Zab. 83:18; Matendo 14:17) Yehova amejionyesha kuwa amejaa sana sifa hizo hata kwamba, kama Ayubu mwaminifu wa nyakati za kale, twapaswa kusema hivi: “Nilikuwa nimesikia habari zako, kwa kusikia kwa masikio; bali sasa jicho langu linakuona.” (Ayubu 42:5) Vilevile kwa jicho la imani twamwona Yesu ameketi kwenye mkono wa kuume wa Mungu mbinguni. Ndiye aliyetoa maisha yake ili atuweke huru na utumwa wa dhambi na mauti. Ni jambo lenye kuvutia kama nini kulitazama!—Kol. 3:1, 2; linganisha Matendo 7:55, 56.

Zaidi ya hayo, kule-e-e kwenye upeo wa macho twaona, pia, kuangaza kwa kupambazuka kwa siku mpya. Siku ile ambayo ufalme wa Mungu utaanza kuifanya dunia paradiso imekaribia! Hatupaswi kuacha kuona mambo hayo ya hakika. Jicho letu lapaswa kuelekezwa vizuri kama vile kioo cha kamera nzuri, ili kwamba vitu vilivyoko mbele yetu vionekane vizuri rohoni na mioyoni mwetu.

“Taa ya mwili ni jicho,” akasema Yesu. “Basi jicho lako likiwa safi, mwili wako wote unao mwanga.” (Luka 11:34) Kwa jicho lenye kuona mambo kama yalivyo kumwelekea Yehova Mungu, Mwanawe na Ufalme, hata katika hali zilizo ngumu sana tutaweza kushinda maelekeo ya kuacha. Kwa hiyo tutaangalia zaidi shauri hili: “Kwa habari ya macho yako yanapaswa yatazame mbele kabisa, ndiyo, macho yako yenye kuangaza yanapaswa kuangalia mbele yako kabisa. Ifanye iwe laini njia ya mguu wako, nazo njia zako zote ziimarike.”​—Mit. 4:25, 26, NW.

JITIHADA INAHITAJIWA ILI KUANGALIA MBELE KABISA

Kutokana na hadithi hiyo ya maisha ya kweli iliyotolewa mwanzoni, ni wazi kwamba jitihada nyingi inahitajiwa ili kuendelea kusonga mbele katika hali ngumu sana. Maelekeo ni kuacha na kujitupa chini. Katika wakati huu wa historia ya ulimwengu tunaishi katika hali ngumu sana ambayo Paulo alituonya juu yake katika 2 Timotheo 3:1: “Lakini ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari.” Ingawa Wakristo wengi wanaweka mifano bora ya uendelevu, wengine wanaonyesha ishara za kuchoka na hata wengine wana maelekeo ya kuacha shindano. Inasaidia sana kujua baadhi ya sababu zinazomfanya Mkristo aanze kuonyesha ishara za kulegea na, zaidi ya yote, kujua yanayoweza kufanywa ili kuondoa jambo hilo. Mambo yafuatayo yamesaidia Wakristo fulani waendelee kutazama mbele kabisa wakati walipokuwa wamekufa moyo au walipokuwa karibu kuacha.

SITAWISHA MAONI YANAYOFAA

Kutiwa moyo ni nguvu kubwa katika kuendelea. (Matendo 27:33-36) Maoni yanayofaa yanahitajiwa ili kutiwa moyo, hali maoni yasiyofaa yana matokeo mabaya nayo yanavunja moyo. Je! unawajua watu wenye maoni yasiyofaa na ambao wanalaumu karibu kila kitu? Je! wao ni watu wenye furaha? Bila shaka, kulaumu kote si kubaya, maana kuna kulaumu kunakofaa pia. Walakini je! hukubali kwamba kulaumu kusikofaa kunamfanya mtu alegee nako kwaweza kumfanya akose furaha kabisa? Kwa sababu jambo hilo linahusiana kweli kweli na maoni, dawa ni kusitawisha maoni yanayofaa.

Sikuzote Yehova anatazama mema, hata katika watenda mabaya. Ijapokuwa kutenda mabaya kwa Mfalme Yehoshafati kulimletea ghadhabu ya Mungu, Yehova alimwambia hivi: “Walakini yameonekana mema ndani yako.” (2 Nya. 19:3) Kwa hiyo mbona usiwe kama Yehova kwa habari hiyo na kutazama mema katika watu wengine? Kwa mfano, ukiwa na maelekeo ya kulaumu mzee aliyewekwa katika kundi la Kikristo, je! lisingekuwa jambo la faida kufikiria mambo yake mengi mazuri—upendo wake kwa Yehova na kwa kundi, kazi yake ya bidii katika kutayarisha mikutano na nia yake ya kusaidia? Hiyo itasaidia kuondoa mawazo yasiyofaa akilini mwako. Na wakati wo wote unapoelekeana na hali mbaya, sababu gani usifikirie mema yatakayotokea ukitenda ifaavyo katika hali hizo? Tuna mfano bora wa Yesu, aliyeteseka mikononi mwa adui zake lakini “alijifunza kutii kwa mateso hayo yaliyompata.”​—Ebr. 5:8.

SITAWISHA IMANI NA TUMAINI KUBWA ZAIDI

Vilevile pengine umekwisha kutana na watu waliokubali washindwe na maoni ya kujiona kuwa wao si bora. Hata Wakristo wanaweza kushindwa na maoni hayo wajione kuwa hawafai kitu na hawastahili kuendelea katika njia ya Ukristo. Walakini hiyo ndiyo njia inayofaa katika kuangalia jambo hilo? Bila shaka sivyo. Watoto wa Yehova wa kidunia ni wenye thamani sana kwake. (Hag. 2:7) Hakuna ye yote anayejaribu kufanya yaliyo haki asiyekuwa bora machoni pake. Kwa hiyo tunachohitaji ni tumaini kubwa zaidi katika Yehova na imani kubwa zaidi katika uwezo wa Mungu wa kutufanya tuwe watumishi wanaostahili kupitia kwa roho yake.​—2 Kor. 3:5.

Mahali pa kujiruhusu tuvunjike moyo na kuacha, tukikumbuka mawazo haya yaliyotangulia tutatiwa moyo tuendelee kutazama mbele kabisa tukiwa na uhakika. Tutapata furaha katika kuendelea, maana “mwenye furaha ni yeye anayemtumaini Yehova.”​—Mit. 16:20, NW.

USIWE NA MAHANGAIKO

Kuhangaika kupita kiasi vilevile kunanyang’anya watu furaha ya maisha na kuwalegeza. Kwamba hilo ni jambo la maana wakati huu inaonyeshwa na maneno ya Yesu juu ya “wakati wa mwisho.” (Dan. 12:4) Alitaja kwamba ‘wanadamu watazimia moyo kwa sababu ya hofu na kutazamiwa kwa mambo yanayokuja juu ya dunia inayokaliwa na watu.’​—Luka 21:26, NW.

Sikuzote watu fulani wanazungumza juu ya nyakati zenye taabu, hali ngumu ya uchumi, infuleshoni iliyopanda juu, kuongezeka kwa uhalifu, kuvunjika kwa maisha ya jamaa, upweke na mambo mengine mengi yasiyopendeza. Kwa sababu ya hangaiko hilo hata Wakristo wengine wamepoteza nia ya kuendelea kutembea kuelekeana na taabu nao wamo katika hatari ya kupoteza maisha zao. Kwa hiyo kuna kila sababu ya kuwa na maoni tofauti kabisa. Hili ni shauri la Paulo lenye kuchochea: “Sikuzote [ndiyo, hata matatizo yanapotokea] furahini katika Bwana. Kwa mara nyingine nitasema, Furahini! . . . Msihangaikie cho chote, bali katika kila jambo kwa sala na kusihi pamoja na shukrani, Mungu na ajulishwe maombi yenu.” Matokeo yatakuwa nini? Ndipo “amani ya Mungu inayoshinda mawazo yote italinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kupitia kwa Kristo Yesu.” (Flp. 4:4-7, NW) Mtu wa namna hiyo hatakufa moyo.

IMARISHA HALI YAKO YA KIROHO

Ili kuendelea kusonga mbele katika upepo wenye theluji, nguvu nyingi sana zinahitajiwa. Nguvu zenye kupunguka mwilini lazima zirudishwe. Vivyo hivyo, Mkristo ambaye halishi kwa ukawaida akili na moyo wake kwa chakula cha kiroho atakosa furaha na kuchoka. Hali hiyo ikiendelea muda mrefu sana, hataendelea katika njia ya uzima.​—Mt. 4:4.

Mkazo unaotiliwa juu ya anasa siku hizi na vishawishi vinaweza kufanya hata waliokuwa Wakristo wenye nguvu wawe “wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu.” (2 Tim. 3:4) Hilo, nalo, lingewanyang’anya wakati wenye thamani unaohitajiwa kujilisha kiroho. Vilevile, kupenda mali, ‘kutaka kuwa na mali,’ kunachukua wakati mwingi wa mtu hata maelekeo yake ya kiroho yanaweza kuharibiwa. Maneno ya Paulo ya kuonya yanahusu nyakati zetu sana sana: “Wengine hali wakiitamani [fedha] wamefarakana na Imani.”​—1 Tim. 6:9, 10.

Mtu anayetaka kusimama imara katika nyakati hizi zenye msukosuko lazima aimarishe hali yake ya kiroho kwa kupanga wakati wa kila siku kujifunza Biblia na vitabu vya Kimaandiko. Naye lazima atafute kushirikiana kwa ukawaida na waamini wenzake. (2 Tim. 3:16, 17; Ebr. 10:24, 25) Hayo yatasaidia kuupatia moyo na akili yake nguvu zinazoelezwa katika Isaya 40:29-31: “[Yehova] huwapa nguvu wazimiao, humwongezea nguvu yeye asiyekuwa na uwezo. . . . wao wamngojeao [Yehova] . . . watapiga mbio, wala hawatachoka; watakwenda kwa miguu, wala hawatazimia.”

TEMBEA NA MUNGU

Mwenye furaha ni mtu asiyeenda peke yake bali anayekuwa na mwenzi njiani. Ndiyo, “afadhali kuwa wawili kuliko kuwa mmoja . . . Kwa maana wakianguka, mmoja wao atamwinua mwenzake.” (Mhu. 4:9, 10) Watu waaminifu wa kale kama Henoko na Noa walikuwa na mwenzi bora zaidi katika njia yao. Walitembea na Mungu wa kweli. (Mwa. 5:24; 6:9) Kutembea na Mungu kunampa mtu msaada unaohitajiwa ili kupita taabu mbaya sana. Mtu ataendelea kusimama akipashana habari kila siku na Yehova na akiwa na uhusiano wa kibinafsi wenye nguvu na Baba yake wa kimbinguni.

Kwa mfano, mtu akijiona kuwa mpweke kwa sababu ya kumpoteza mwenzi mpendwa wa ndoa au mtoto katika mauti, urafiki huo na Mungu utafanya hasara hiyo kubwa ivumilike. Mkristo anapoonewa, akitendewa isivyo haki, au hata anapokosewa sana na ndugu katika imani, uhusiano huo wa thamani pamoja na Yehova utamlinda asiache vita. Hata mtu akifanya dhambi nayo dhamiri yake imsumbue sana atubu, uhusiano wake pamoja na Yehova utamrudisha na, kupitia kwa dhabihu ya ukombozi ya Yesu Kristo, dhambi zake zitasamehewa. (1 Yohana 1:7) Ataendelea kutazama na kutembea mbele kabisa akiwa Mkristo.

KUTAZAMA MBELE KABISA KUNALETA ZAWADI BORA

Kama tulivyokwisha kuona, kuna uhitaji wa kuwa na maoni yanayofaa ili tuweze kushinda taabu kubwa za kibinafsi maishani mwetu. Licha ya hayo, huenda sisi binafsi tukalazimika kukabiliana na “dhiki kubwa,” “tufani” mbaya sana ya ulimwenguni pote ambayo itaharibu taratibu hii yote ya mambo. (Mt. 24:21, 22; Yer. 25:31, 32) Roho ya Mungu itatusaidia tushinde upepo huo mkali nasi tupatikane tukiwa hai utakapokwisha kabisa nalo jua liangaze juu ya dunia iliyosafishwa, ambayo itageuzwa iwe paradiso ya duniani pote.

Yehova Mungu hataki tuchoke wala tuache. Yeye anataka tuwe kati ya wale ambao mtume Paulo anasimulia katika Waebrania 6:11, 12: “Nasi twataka sana kila mmoja wenu aidhihirishe bidii ile ile, kwa utimilifu wa matumaini hata mwisho; ili msiwe wavivu, bali mkawe wafuasi wa hao wazirithio ahadi kwa imani na uvumilivu.” Hivyo, tusilegee, bali turuhusu uhusiano wetu pamoja na Yehova Mungu, imani yetu kwa dhabihu ya ukombozi ya Yesu na kuona kwa uangavu Taratibu Mpya yawe yenye kutia nguvu maishani mwetu. Kisha tutakuwa kama Musa, ambaye alimwona Yehova kwa imani, na kama Yesu, ambaye alitazama mbele kwenye furaha iliyowekwa mbele yake. Ndiyo, na kama mamia ya maelfu ya Wakristo kuzunguka dunia ambao wanatazama mbele kabisa na kusema hivi kwa uhakika: “Sisi hatumo miongoni mwao wasitao na kupotea, bali tumo miongoni mwa hao walio na imani ya kutuokoa [nafsi] zetu.”​—Ebr. 10:39.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki