Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w83 11/15 kur. 6-9
  • Yanayohitajiwa Ili Kuendelea Kujitenga na Ulimwengu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yanayohitajiwa Ili Kuendelea Kujitenga na Ulimwengu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Imani na Ushujaa ni Mambo Yanayohitajiwa
  • Uaminifu Katika Mambo Madogo
  • Unyenyekevu na Kujiweza
  • Kumwogopa Yehova na Upendo Usio na Choyo
  • Thawabu za Kuendelea Kujitenga
  • Kwa Sababu Gani Ni Lazima Wakristo Waendelee Kujitenga na Ulimwengu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Lazima Waokokaji Wawe “Si Sehemu ya Ulimwengu”
    Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
  • Wakristo Wanaodumisha Msimamo wa Kutokuwamo Katika Siku za Mwisho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Sifa za Kimungu za Upendo na Chuki
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
w83 11/15 kur. 6-9

Yanayohitajiwa Ili Kuendelea Kujitenga na Ulimwengu

BILA shaka, tukifahamu namna ulimwengu wa Shetani ulivyo mwovu na wenye ufisadi, tutasaidiwa tuendelee kujitenga nao. Ufahamu huo utafanya iwe vyepesi kwetu kuitii amri inayopatikana kwenye Zaburi 97:10: “Enyi mmpendao [Yehova], uchukieni uovu.” Ni lazima tuyachukie maovu kabisa kabisa kama vile mtume anavyoamuru, hata kama mambo hayo yanaupendeza na kuushawishi mwili wetu wenye dhambi namna gani. (Warumi 12:9, NW) Zaidi ya hilo, inatupasa tuwachukie wale ambao kwa makusudi wanajionyesha kuwa ni wachukia Yehova, wachukiao yaliyo mema. Ni kama vile Daudi wa kale alivyoeleza: “Je! [Yehova], nisiwachukie wanaokuchukia? Nisikirihike nao wakuasio? Nawachukia kwa ukomo wa chuki, wamekuwa adui [wakubwa sana] kwangu.” (Zaburi 139:21, 22) Sisi tunawachukia, si katika maana ya kutaka kuwaumiza au kuwatakia maumizo bali katika maana ya kuwaepuka kama vile tungeepuka sumu au nyoka mwenye sumu, kwa maana wao ni sumu kwetu kiroho. Ndiyo sababu tunaonywa hivi: “Msipotezwe. Mashirika mabaya yanaharibu mazoea mazuri.”​—1 Wakorintho 15:33, NW.

Na iangaliwe kwamba kukaa safi namna hiyo kwa kujitenga na waovu hakuhusu watu tunaoweza kukutana nao bila kutazamia tu au wale tunaopitana-pitana nao katika shughuli zetu za maisha ya kila siku, bali kunahusu pia wale tunaowachagua wawe washirika wetu katika mambo ya tafrija. Kumbuka kwamba tunaonywa hivi: “Uasherati usitajwe kwenu kamwe, wala uchafu wo wote wala kutamani, kama iwastahilivyo watakatifu; wala [mwenendo wa] aibu.” (Waefeso 5:3, 4) Hilo halimaanishi tuepuke kuyazungumza mambo hayo bali pia tuepuke kuyaacha yatajwe mbele yetu, kama kwa kutazama kipindi cha televisheni au kwenda sinema ambako mambo hayo ndiyo yanazungumzwa. Badala ya hivyo, na tujitahidi kusitawisha mashirika pamoja na waamini wenzetu ambao wamejitoa kwa ukamili, si kwenye kundi na katika utendaji wa shambani tu, bali kwa kuwa pamoja katika vikusanyiko vya kirafiki. Ndiyo, ili tuendelee kujitenga na ulimwengu ni lazima tuangalie washirika wetu; kwa upande mmoja, kuwaepuka wale wabaya na, kwa upande ule mwingine, kutia bidii kushirikiana na wale wasio sehemu ya ulimwengu sawasawa na sisi.

Imani na Ushujaa ni Mambo Yanayohitajiwa

Imani na ushujaa ni mambo yanayohitajiwa pia ili kuendelea kujitenga na ulimwengu. Ili tujenge imani yetu ni lazima tusitawishe hamu njema ya kiroho, kuujua uhitaji wetu wa kiroho nyakati zote. (Mathayo 5:3) Hiyo inatia ndani kuwa na mazoea ya kujifunza Biblia kibinafsi na kuhudhuria mikutano ya Kikristo pia kwa ukawaida. Katika upande huo wengi wa watu wa Yehova wanapungukiwa. Inampasa kila mmoja wetu aweke kando kwa ukawaida wakati wa kujifunza Biblia kibinafsi. Kukiwa na uhitaji, amka nusu-saa mapema kabla ya wakati wako wa kawaida. Wengi wanafanya hivyo, ili waweze kujifunza kwa njia hiyo. Tunataka kuthamini Neno la Mungu kama mtunga zaburi wakati alipokaza sauti akasema: “Sheria yako naipenda mno ajabu, ndiyo kutafakari kwangu mchana kutwa. Naifurahia ahadi yako, kama apataye mateka mengi.”​—Zaburi 119:97, 162.

Imani yenye nguvu ina sehemu kubwa katika kutusaidia tuendelee kujitenga na ulimwengu. Jambo hilo linaweza kuonekana kutokana na mfano wa wanaume waaminifu wa kale. Kwenye Waebrania sura ya 11 tunasoma kwamba hao walikuwa ni “watu ambao ulimwengu haukustahili kuwa nao.” Walikuwa wameweka matumaini yao juu ya Ufalme wa Mungu na ‘wakayaona mambo hayo tokea mbali na kuyashangilia, na kukiri kwamba walikuwa wageni na wasafiri’ katika ulimwengu huu.

Zaidi ya kuwa wonyesho wa imani yetu na kuwa jambo la kuitia nguvu, kwenda nyumba kwa nyumba kwa ushujaa tukiwa na habari njema za Ufalme wa Mungu ni msaada mkubwa katika kuendelea kwetu kujitenga na ulimwengu. Kufanya hivyo kunakazia akili zetu pengo kubwa sana lililo kati ya walimwengu na Wakristo; na tunapoona ubaridi, chuki zisizo na msingi na upinzani wa moja kwa moja kutoka kwa wengi wa wale tunaokuta, tunasaidiwa kupinga sana vishawishi vya kilimwengu. Ndivyo ilivyo pia kuhusu ushahidi wa vivi hivi. Kwa sababu ya kufanya hivyo, wengine waliokuwa mahipi (wazururaji wa ovyo-ovyo) hawaoni ugumu wa kujitenga na wale waliokuwa washirika wao zamani; washirika hao wa zamani wanajitenga mbali kwa sababu hawataki hawa waliokuwa rafiki zao wawahubirie.

Uaminifu Katika Mambo Madogo

Kuendelea kujitenga na ulimwengu kunatutaka tuwe waaminifu pia katika mambo madogo. Ni kama Yesu alivyosema: “Aliye mwaminifu katika lililo dogo sana, huwa mwaminifu katika lililo kubwa pia; na aliye dhalimu katika lililo dogo, huwa dhalimu katika lililo kubwa pia.” (Luka 16:10) Tukiwa waangalifu tusiufuate ulimwengu, tusivutwe nao katika mambo madogo, kama vile kuvaa na kujipamba kwa njia yenye kuamsha tamaa mbaya, kushughulikia mambo ya pesa kwa udanganyifu, kudanganya wakati wa kulipa kodi, kuwa magoigoi katika tabia za kikazi, au kujitia katika mambo yenye hatari bila sababu nzuri, kufuata mwenendo wa kutokujali tunapokuwa na wanawake au wanaume​—kutokufuata yote hayo kutatuepusha tusivunje sheria za Mungu katika mambo mazito zaidi.

Mfano wenye kuonyesha kanuni hiyo ni wale Waebrania wanne waliochukuliwa mateka mpaka Babuloni, kama ilivyoandikwa katika kitabu cha Danieli. Kwa sababu walikuwa waaminifu katika jambo lenye kuhusu chakula lililoonekana kama kitu kidogo tu, wao waliweza kushinda katika mambo yaliyohusu uzima na mauti, katika suala la kama wangetii Mungu au wanadamu.​—Danieli 1:1-17; 3:1-30; 6:4-23.

Unyenyekevu na Kujiweza

Unyenyekevu ni sifa nyingine itakayotusaidia sana tuendelee kujitenga na ulimwengu. Hiyo maana yake ni kujichukua wenyewe kwa njia ya kujishusha, si kufikiria sisi ni bora zaidi ya vile inavyofaa kufikiri. (Warumi 12:3) Wanaojifikiria kuwa bora sana wanaelekea kutegwa kwa wepesi na watu wa ulimwengu huu wenye kusifu-sifu wengine kwa uongo tu. Shetani alimtolea Hawa sababu iliyomsifu kwa uongo na hivyo akaweza kumdanganya. (Mwanzo 3:1-7) Kuwa wanyenyekevu kutatusaidia turidhike na baraka zetu za kiroho na za kimwili. Ikiwa sisi tuna utawa na uradhi tunaohimizwa tuwe nao kwenye 1 Timotheo 6:6, hatutafanya haraka-haraka ya kutamani anasa zinazokatazwa, wala mambo ya kusisimua yasiyofaa katika televisheni; hatutashawishwa tuwe wadanganyifu katika uhusiano wetu na wengine, wala kuwa na pupa ya kutaka faida ya kichoyo. Tukijichukua wenyewe kuwa watu wa hali ya chini, tutaridhishwa na wenzi wetu wa ndoa wala hatutakuwa na macho ya kutamani wengine ambao huenda wakaonekana kuwa na umbo la kupendeza zaidi, wenye kufurahisha zaidi au wenye hali nzuri zaidi ya urafiki.

Kujiweza kunahitajiwa pia ili kuendelea kujitenga na ulimwengu. Kujiweza kutafanya tuweze kuvumilia maumivu ili tusikubali kukana imani yetu tukiwa chini ya mateso makali, ikiwa nyakati zote tutamtegemea Yehova Mungu atupe nguvu tunazohitaji. Ndivyo ilivyo kuhusu vishawishi ambavyo ulimwengu wa Shetani au hali zinatuwekea njiani, yaani, vishawishi vya kutufanya tujiache tufuate kazi za mwili. (Wagalatia 5:19-21) Ikiwa tumesitawisha tunda la kujiweza, tutaweza kupinga sana vishawishi vyote hivyo, tufanye kama mtume Paulo: “Mimi naupiga-piga ngumi mwili wangu na kuufanya kama mtumwa, ili, nikiisha kuhubiria wengine, mimi mwenyewe nisije nikakataliwa kwa njia fulani.”​—1 Wakorintho 9:27, NW.

Kumwogopa Yehova na Upendo Usio na Choyo

Kumwogopa Yehova, ambako ndiko mwanzo wa hekima, kunahitajiwa pia ili kuendelea kujitenga na ulimwengu. (Zaburi 111:10) Woga wa kimungu wa kutotaka kuchukiza Baba yetu wa kimbingu utafanya tuendelee kujitenga na ulimwengu huu mwovu. Ulimwengu ni mwovu sana, na kumwogopa Yehova kunamaanisha kuchukia ubaya.

Lakini juu ya yote, upendo usio na choyo ndio unahitajiwa ili kuendelea kujitenga na ulimwengu. Ulimwengu unavuta tamaa ya watu ili wawe na uchoyo. Kwa kadiri ambayo sisi tutakuwa bila uchoyo, kwa kadiri iyo hiyo vishawishi vya ulimwengu vitashindwa kutuvuta. Ikiwa sisi tunampenda kikweli Yehova Mungu kwa moyo wetu wote na nafsi yote, kwa akili na nguvu zetu zote, tutakuwa washikamanifu kwake na hivyo hatutatumia wakati wetu tukiwa na adui zake. Hatutakosa kuwa na uaminifu kwake. Na ikiwa sisi tunapenda ndugu zetu Wakristo, tutaendelea kujitenga na ulimwengu, kwa maana tusipofanya hivyo huenda tukawakwaza, kwa sababu ya kuwawekea mfano mbaya. Ikiwa tunapenda jamaa zetu wenyewe, tutaendelea kujiepusha na vishawishi vyote vya kilimwengu vinavyoweza kutufanya tutake kuwa wasio washikamanifu kwa jamaa zetu katika wazo, neno na tendo.

Thawabu za Kuendelea Kujitenga

Ni nini thawabu za kuendelea kujitenga na ulimwengu? Kwanza, tunaweza kufurahia urafiki safi wa Yehova Mungu, wa Yesu Kristo na wa ndugu zetu Wakristo. Tena, kwa kuendelea kujitenga na ulimwengu, tutadumisha dhamiri safi na kuepuka matunda mabaya yanayotokana na kazi za mwili. (Wagalatia 6:7, 8) Kwa kuendelea kujitenga na Babuloni Mkuu, hatutashiriki hatia yake wala kupokea mapigo yake.​—Ufunuo 18:4.

Kuendelea kujitenga na mataifa ya kisiasa kuna thawabu zake pia. Ingawa kuendelea kujitenga na mapigano ya kutukuza taifa kumefanya mara kwa mara Wakristo wa kweli wapatwe na magumu, nyakati fulani-fulani kumewaletea faida pia. Katika nchi zenye kujawa sana na magombano makali kama Lebanoni na Irelandi ya kaskazini, msimamo wao wa kutokuwamo umewawezesha watembee huku na huku wakiwa na uhuru katika kazi yao ya kutoa ushahidi, tena hata umeokoa maisha yao.

Kisha kwa kuendelea kujitenga na ulimwengu tutaweza kujipatia faida kwa kutii amri inayopatikana kwenye Sefania 2:3: “Mtafuteni [Yehova], enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia, ninyi mliozitenda hukumu zake; itafuteni haki, utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya [Yehova].” Hivyo huenda tukaipita ile “dhiki kubwa” tukafurahie uzima wa milele katika taratibu mpya ya Mungu.​—Mathayo 24:21; 2 Petro 3:13.

Kwa hiyo Wakristo wote waliojiweka wakf kweli kweli na wakumbuke uhitaji wao wa kuendelea kujitenga na ulimwengu huu wenye kutawalwa na Shetani Ibilisi. Sikuzote na wazithamini sababu zile nyingi zinazowapa wajibu wa kufanya hivyo. Kisha na watie bidii kusitawisha sifa zile zinazohitajiwa ili kuendelea kujitenga na ulimwengu.

[Picha katika ukurasa wa 8]

CHUKIA MABAYA NA UYAEPUKE

JEURI

MAOVU

JENGA IMANI YENYE NGUVU KATIKA MUNGU

KUJIFUNZA

SALA

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki