Maswali kutoka kwa Wasomaji
● Kwa sababu gani Mashahidi wa Yehova hawasherehekei kukumbuka siku za kuzaliwa kwao?
Sababu ya msingi ni kwamba wao wanaliheshimu Neno la Mungu nao wanapendezwa sana na kuitikia uongozi wake.
Kusherehekea siku ya kuzaliwa ni jambo linalopendwa na watu wengi ulimwenguni pote na imekuwa hivyo katika muda wa miaka elfu nyingi. Mara nyingi kunakuwa na karamu na kutoleana zawadi. Walakini je! Biblia inasema lo lote juu ya siku za kuzaliwa?
Jambo la kwanza tunaloweza kusema ni kwamba Biblia haivunji watu moyo kutoa zawadi kwa ukarimu kwa mtu anayependwa. (Mwa. 33:10, 11; Luka 15:22; 2 Kor. 8:19) Wala haivunji watu moyo kufurahia karamu, kwa kuwa kula na kunywa kwa kiasi ni jambo linalopendekezwa kuwa jambo mojalapo la kufurahia maisha. (Mhu. 3:12, 13) Yesu alishiriki karamu ya arusi. Watoto wa Ayubu walifanya karamu ambazo huenda zilikuwa karamu za wakati wa mavuno zilizowapatia nafasi za kuwa pamoja. Ibrahimu alifanya karamu wakati Isaka alipoachishwa kunyonya. (Yohana 2:1, 2; Ayubu 1:4, 5, 13; Mwa. 21:8) Na ijapokuwa Wayahudi hawakuamriwa na Mungu wafanye hivyo, walikuwa na sikukuu ya kila mwaka katika tarehe ya kuzinduliwa kwa hekalu, naye Yesu alihudhuria karamu hiyo.—Yohana 10:22, 23.
Hata hivyo, Biblia inaonyesha kwamba uangalifu unahitajiwa, kwa kuwa haingefaa kushiriki katika sherehe yo yote pasipo kujali sababu au asili yake. (Kut. 32:1-6; 1 Pet. 4:3; 1 Kor. 10:20, 21) Namna gani juu ya kukumbuka na kusherehekea siku za kuzaliwa?
Kwa wazi, waabudu wengi wa kweli waliweka kumbukumbu la tarehe za kuzaliwa. Makuhani na wengine walijua umri wao. Jambo hilo halikufanywa kwa kukisia-kisia tu. (Hes. 1:2, 3; 4:3; 8:23-25) Walakini hakuna jambo lo lote katika Maandiko linaloelekea kuonyesha kwamba waabudu wa kweli walisherehekea siku za kuzaliwa kwao kila mwaka.
Biblia inatoa habari juu ya sherehe mbili tu za siku za kuzaliwa, na zote mbili zikiwa za watu wasio watumishi wa Mungu wa kweli.
Ya kwanza ni ile ya Farao wa Misri. Na katika wakati wa kuisherehekea, mkuu wa waokaji wa Farao aliyekuwa amefungwa pamoja na Yusufu, alitundikwa. (Mwa. 40:18-22) Akitoa maelezo juu ya Mwanzo 40:10, Dakt. Adam Clarke anasema hivi: “Kuadhimisha siku ya kuzaliwa kwa karamu inaonekana kutokana na mahali hapa kuwa desturi ya kale sana. Pengine ilitokana na wazo la kutokufa kwa nafsi, kwa kuwa mwanzo wa uhai waweza kuonwa kuwa na matokeo makubwa sana na mtu aliyeamini kwamba ataishi milele.”
Sherehe ya pili, iliyofanywa yapata miaka 1,800 baadaye, ilikuwa ya siku ya kuzaliwa ya Herode Antipa. Masimulizi katika Marko 6:21-24 yasomwa hivi:
“Hata ilipotokea siku ya kufaa, na Herode, sikukuu ya kuzaliwa kwake, alipowafanyia karamu wakubwa wake, na majemadari, na watu wenye cheo wa Galilaya; ndipo binti yake yule Herodia alipoingia, akacheza, akampendeza Herode na wale alioketi pamoja naye karamuni. Mfalme akamwambia yule kijana, Niombe lo lote utakalo, nitakupa. Akamwapia, Lo lote utakaloniomba nitakupa, hata nusu ya ufalme wangu. Basi akatoka, akamwuliza mamaye, Niombe nini? Naye akasema, Kichwa cha Yohana Mbatizaji.”—Angalia pia Mathayo 14:6-11.
Kwa habari ya masimulizi ya siku ya kuzaliwa ya Herode, Dakt. Richard Lenski anaeleza hivi: “Wayahudi walichukia kuadhimisha siku za kuzaliwa wakiziona kuwa desturi ya kipagani, walakini Waherode hata waliwapita Warumi katika kufanya sherehe hizo, hata kwamba ‘siku ya kuzaliwa ya Herode’ (Herodis dies) ukapata kuwa usemi wa mfano kumaanisha sikukuu yenye kufanywa kupita kiasi.”
Inatupasa kuzionaje sherehe hizo mbili za kukumbuka siku za kuzaliwa? Je! ni jambo lililotukia bila kukusudiwa kwamba zilitajwa na kwamba zote mbili zilikuwa za watu wasiokuwa na kibali ya Mungu? Au inaweza kuwa kwamba Yehova aliandikisha yote hayo katika Neno lake kwa kusudi, Neno ambalo yeye mwenyewe asema kuwa “lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza”? (2 Tim. 3:16) Jambo lililo na maana ndogo zaidi tunaloweza kusema ni kwamba masimulizi hayo mawili yaonyesha kwamba Biblia haikubali sherehe za kukumbuka siku za kuzaliwa, na kwamba ni zoea la watu waliotenganishwa na Mungu.
Vilevile, inapaswa kuangaliwa kwamba Mungu hakuandikisha tarehe yenyewe ya kuzaliwa kwa Yesu, ambayo kwa hakika ndiyo ingekuwa siku ya kuzaliwa ya maana zaidi ikiwa watumishi wa Mungu wangekuwa wakisherehekea siku za kuzaliwa. Badala yake, Biblia inaonyesha tarehe ya kifo cha Yesu nayo inawaagiza Wakristo waiadhimishe katika tarehe ile ile kila mwaka. (Luka 22:19; 1 Kor. 11:23-26) Jambo hilo linapatana na uhakika wa kwamba Biblia inasema kwamba siku ya kifo cha mtu ni ya maana zaidi kuliko siku ya kuzaliwa kwake ikiwa amejifanyia jina jema pamoja na Mungu katika wakati wa maisha yake.—Mhu. 7:1, 8.
Kupatana na yanayoonyeshwa na Maandiko, Wakristo wa kwanza hawakuadhimisha siku za kuzaliwa kwao.
“Wazo la sikukuu ya ukumbusho wa siku ya kuzaliwa lilikuwa mbali na mawazo ya Wakristo wa kipindi hiki kwa jumla.”—The History of the Christian Religion and Church During the First Three Centuries, cha Augustus Neander.
Wakati ulivyoendelea kupita, kukawa na ukafiri juu ya Ukristo ulio safi, jambo lililoanza kusherehekewa lilikuwa kifo, si kuzaliwa.
‘Heshima kubwa mno waliyopewa wafia-imani ilifanya mahali walipofia na siku ya kufa kwao viheshimiwe kupita kiasi. Kwa wazo la kufurahisha, siku ya kufa ya mfia-imani iliitwa siku ya kuzaliwa kwake. Mahali walipofia wafia-imani pakaja kuonwa kwa hofu takatifu. . . . Katika siku za tarehe ile ile ya kila mwaka ibada [makanisani] sana sana ilihusu kukumbuka utumishi wake na sifa zake. . . . Hata hivyo, yapaswa kukumbukwa kwamba ibada hizo za ukumbusho [za kila mwaka] hazikuwa sehemu ya utaratibu wa kawaida wa Kanisa.’—History of the Christian Church, cha Dakt. John F. Hurst, Kitabu cha Kwanza, kur. 350, 351.
Kwa hiyo, ijapokuwa Biblia haina katazo lililo wazi la kutosherehekea kukumbuka siku za kuzaliwa, Mashahidi wa Yehova wamefahamu kwa muda mrefu yanayoonyeshwa na Maandiko nao hawasherehekei siku za kuzaliwa kwao. Katika jambo hilo, wanapatana na mfano wa Wakristo wa kwanza kabisa.
Vilevile, ijapokuwa hakuna sababu ya Kibiblia ya kusherehekea kila mwaka siku ya kifo cha Mkristo, twaweza kukubali kwamba siku ya kifo ni bora kuliko siku ya kuzaliwa kwake. Kwa hiyo twaweza kukaza fikira zetu, si katika siku ya kuzaliwa bali katika kila siku kwa kumwiga Kristo na kwa kuonyesha mfano wa Mungu. Hivyo, tukifa, tutakuwa tumemtukuza Mungu kwa njia yetu ya maisha, naye bila shaka atatukumbuka.—Ebr. 5:9; 11:6; Flp. 3:8-11.